Showing posts sorted by relevance for query mohamed awadh chico. Sort by date Show all posts
Showing posts sorted by relevance for query mohamed awadh chico. Sort by date Show all posts

Thursday, 2 February 2017



Baada ya kusoma taazia ya Abdallah Tambaza sina nguvu ya kuandika chochote kuhusu rafiki yangu Mohamed Awadh maarufu kwa jina la Chico. Taazia ya Abdallah mimi imenitia simanzi kiasi ya machozi kunilengalenga kila ninapopita sentensi moja kwenda nyingine sababu ni kuwa Abdallah alikuwa ananitajia mambo na watu niliokuwa nawafahamu na wengine tayari wameshatangulia mbele ya haki. Nikawa kama vile watu hawa nawaona tena. Miezi kama miwili hivi nilikutana na Chico Masaki akiwa amekaa na wajukuu zake ndani ya gari. Tulisalimiana kwa bashasha sana na wala haukunipikitikia kuwa ile ndiyo itakuwa mara yetu ya mwisho kuonana. Mazikoni Kisutu nimekutana na Abdallah kisha nikamuona na ndugu yake Mwinyikhamisi yeye ni mkubwa kwangu kwa umri na aliponiona tu Mwinyikhamisi anahangaika kusimama maana alikuwa kakaa chini miguu inampa tabu. Kila nikimzuia kunisimamia yeye ndiyo anashikilia kushika mkono wangu asimame tusalimiane. Namwambia, ‘’Ka Mwinyi starehe, starehe…’’ Wapi hanisikii anailazimisha miguu yake isimame anisalimie mimi  mdogo wake. Mapenzi na heshima iliyoje mkubwa kumsimamia mdogo. Hivi ndivyo wazee wetu walivyotufunza. Allah awarehemu.

Kulia ni Mwinyikhamis, Abdallah Tambaza na Ibrahim wote hawa ni ndugu
wakiwa katika khitma ya Dar es Salaam Saigon Club
Niko katika, ''keyboard,'' sasa naandika. Msiba wa Chico umetugusa wengi khawa vijana wa Dar es Salaam. Mwinyikhamis alikuwa mchezaji mpira wa sifa katika New Port Club wakati wa ujana wake. Leo Mwinyi hawezi kusimama. Inanijia mechi moja ambayo naamini iko katika kumbukumbu ya wenzangu wengi wa wakti ule. New Port imepangiwa kucheza na Brazil, timu ya wababe watu wakorofi wa sifa mji mzima unawafahamu kwa shari yao ingawa walikuwa na mpira mzuri wa wachezaji wa kusifika. New Port, club ya vijana waungwana, wastaarabu wanaocheza soka la kupendeza. Mashabiki wanajiuliza itakuwaje mpira huu leo na wahuni wale? 

Saa kumi jangwani pamefurika. Hii ni mechi ya kikombe mfano wa ''league,'' kwa sasa. Wakati ule vilabu vya mtaani villikuwa na nguvu na uongozi thabiti wa kuweza kuchezesha mechi nzuri zilizojaza watazamaji na kuibua gumzo mji mzima. Brazili kuna Kitwana (Victor Mature) mbabe wa sifa, Mrisho (Wanted) mbabe wa sifa, Abdallah Mkwanda (Inger Johannsson), mbabe pia, Suleiman Jongo (Rory Calhoun) mchezaji mpole na muungwana sana lakini anacheza timu ya wababe, Mohamed Ndava. Shamte Kobe (Bingwa wa Mieleka na ngumi), Hamisi (Marlon Brando), Sadiki Ngwira (Kitonsa), Salum Hussein (Livingstone Madegwa) mtoto wa Sheikh Hussein Juma ana boli safi sana.  Wengi katika hawa wametangulia mbele ya haki Allah awarehemu. New Port wanajua kuwa leo wanacheza meshi muhimu na watu washari na wababe wa mji. 

New Port, akina Mwinyikhamis na wenzake wametandaza boli staili ya TPC mpira unatembea kwenye majani na wanakwepa hila zote za ubabe hakuna kukunjana mashati. Brazil imefedheheka kwa sababu mechi imeishia sare na wababe hawakuweza kutamba. Hata hivyo New Port wametoka kwenye mechi ile hoi kama wamepigana round 15 na Muhammad Ali. Brazil usiku ule ule wamewafata New Port club kwao kudai wapewe siku ya mechi ya marudiano. Wamefika New Port wamepanda baiskeli zao na kuziegesha kwa vishindo. Wanatafuta shari ile waliyoikosa uwanjani.

Uongozi wa New Port walifanya kikao cha haraka na uamuzi ukawa hawataki kurudiana na Brazil, wahuni wale na wapewe ushindi. Asubuhi taarifa zimeenea Kariakoo nzima na pembezoni kuwa ile mechi ya marudiano haitakuwapo New Port wamekataa kucheza na wametoa ushindi. Brazil wakautangazia mji kuwa New Port wamejisalimisha. Hii ilikuwa 1965 au 1966 maana nakumbuka mimi nilikuwa niko shule ya msingi.

Msomaji nimekuletea kisa hiki kirefu upate kujua Dar es Salaam aliyokulia Chico na sisi sote wa uzao ule ilikuwaje.

Chico alikuwa mmoja wa wacheazaji wa Everton Club iliyokuwa Mtaa wa Narung’ombe si mbali sana na nyumbani kwao Mtaa wa Tandamti mtaa aliokuwa akiishi Mzee Mshume Kiyate rafiki mkubwa wa Mwalimu Nyerere na mmoja katika wazee wa Baraza la Wazee wa TANU lililoongoza harakati za kupigania uhuru wa Tanganyika. Mtaa huu umebadilishwa jina na kuitwa Mshume Kiyate lakini sasa takriban mwaka wa ishirini kibao cha jina la Mshume Kiyate hakijawekwa kwa sababu ambazi si tabu kuzifahamu. Sasa hii Everton baada ya mtafaruku ndiyo ilikuja kuundwa Saigon na baada ya muda na uhasama wa muda mfupi Everton ilikufa na wote wakajiunga na Dar es  Salaam Saigon hii tuijuayo hivi sasa. Turudi kwa Chico. 

Chico alikuwa akicheza kama mlinzi na namkumbuka Chico kwa uchezaji wake wa ukakamavu, staili ikiitwa ''kikiri,'' Chico akicheza, ''halfback,'' na alikuwa, ‘’hard tackler’’ mchezaji aliyekuwa akiingia kufata, ''loose ball,'' anakumba mpira na mguu wako. Navikumbuka viatu vyake vya mpira alivyokuwa akivaa – ''Adidas Admire.'' Kulikuwa siku zile na aina mbili za viatu vya Adidas, ''Adidas Admire,'' na ''Adidas La Plata.'' Maarufu ambavyo wengi tukivaa ilikuwa ni ''La Plata.'' Hivi vilikuwa na njumu yaani, ‘’studs,’’ unyayo mzima wakati, ''Admire,'' njumu zilikuwa chache na zilikuwa za kufunga na ‘’spanner.’’ Chico alikuwa kijana, ‘’special.’’ Simkumbuki kijana yoyote katika timu zetu za mitaani aliyekuwa akivaa, ''Admire.''

Ndani ya uwanja Chico alikuwa nahodha mzuri. Yuko nyuma na mbele marehemu Jumanne Masimenti, Jalala, Oshaka (Mazola), Mashaka (Alfredo Di Stefano), Juma Abeid, Ali Kodo, Maufi wanashambulia sauti ya Chico itasikika akihamasisha kwa Kiingereza kisafi kilichonyooka mpira upelekwe goli la adui. Utasikia akipiga kelele, ‘’Push the ball forward,’’ ‘’Score,’’ au ‘’On him,’’ yaani asiachiwe mpira adui. Inawezekana hapo anamuhimiza Ahmada Digila (Danny Blachflour) au Khalid Fadhil (George Young) wapeleke mpira mbele. Chico uongozi na ukamanda alianza toka utoto hakuanzia katika Jeshi la Polisi. Kwa kweli tulikuwa tukisikia sauti hii mori ulikuwa unapanda na hakika tukiongeza juhudi katika kushambulia au kulinda goli. Huyu Ahmada alikuwa umri wangu. Yeye ni mtoto wa Sheikh Digila wa Mtaa wa Nyamwezi nyumba yake ilikuwa karibu na msikiti wa Makonde. Ahmada alipata elimu kubwa sana ya dini. Ahmada alikuwa na kasi ya ajabu katika kusoma Qur’an. Kwenye khitma yeye anawea kukumalizia juzuu hata tatu wewe moja hujakamilisha. Alikuwa ''midfielder,'' hodari katika vijana wa Saigon pamoja na Hassan (Gilbert Mahinya). Hassan Gilbert baadae alikuwa kuwa mtaalamu wa, ''Systems,'' katika moja ya mashirika ya umma na siku tulipokutana Mlimani City akiwa na mabinti zake wakubwa waliojipamba kwa hijab alinifahamisha kuwa amestaafu kazi baada ya kufikisha miaka 60. Nilpomfahamisha kuwa nami nami pia nishapumzika akanambia taarifa zangu anazo kwani alikuwa akinifuatilia huko Tanga nilipokuwa nafanyakazi. Nilifarajika kusikia hayo kuwa hata baada ya miaka ya kutengana wana Saigon walikuwa wakitaka kujua nani yuko wapi na anafanya nini.

Hivi ninavyoandika ni kama vile najiona niko Mnazi Mmoja tunafanya mazoezi na wakati mwingine tukijifunza kuachiana pasi za haraka za kuwazuga maadui. Namuona Ghalib Hamza, maarufu kwa jina la Guy. Chico juu ya ushujaa wake wa kuwakumba washambuliaji hathubutu kumfata Guy akiwa na mpira. Guy alikuwa hana kimo, mfupi lakini ana maungo kiasi. Kilichokuwa kikitutisha kwa Guy ni ile, ‘’ball control,’’ yake na ‘’dribbling skills,’’ angeweza kumzunguka Chico na hata kumtia harusi, yaani kupitisha mpira katikati ya miguu yake. Kulikuwa na Mohamed Ramadhani Kondo (Garincha), Rashid Vava mchezaji rafu club nzima tukimuogopa.  Wote wenzetu hawa wametangulia mbele ya haki. Naamini wasomaji vijana watapata tabu sana kuelewa haya majina niliyoyataja, hizi ''nicknames za akina Mazola, Di Stefano, Blanchflour. Hawa walikuwa katika wakati wetu wa miaka ya 1960 ndiyo wachezaji mpira maarufu wa vilabu tofauti vya Ulaya.

Chico alikuwa na baiskeli yake, ‘’sports’’ nyuma aliiandika, ‘’Thunderbird’’ na mwenyewe akiita baiskeli yake kwa jina hilo. Alikuwa anaipanda kwenda shule kavaa vizuri sana na kichwani kavaa, ‘’baseball cap.’’ Amechomekea shati lake jeupe alilolivalia T Shirt nyeupe ndani ndani na kiunoni amevaa, ‘’army belt.’’ Hii ilikuwa mikanda myeupe ya ‘’canvass,’’ yenye, ''buckle,'' ya fedha  au ''gold,'' inayong’aa. Mmarekani amekwishakazi. Vijana wote tuliokuwa tukijiona, ‘’fashionable,’’ tukivaa hivyo lakini Chico mwenzetu alitushinda kwa kuwa ilikuwa kama vile mambo yale yako katika damu yake. 

Nakikumbuka vyema chumba chake pale kwao. Kilikuwa nadhifu na alikuwa na ‘’record player,’’ yake na sahani za santuri nyingi za nyimbo mbalimbali za wanamuziki wa zama zile. Sasa hapo ndipo utakapotambua kuwa Chico alikuwa, ‘’special.’’ Mimi nilikuwa na ‘’record player,’’ yangu, ‘’Dansette,’’ imetengenezwa Uingereza, Sussex, nakumbuka ile label. Chico santuri zake zilikuwa ni Nat King Cole, Ray Charles, Dean Martin na wanamuziki mfano wa hao kama Sammy Davis na wengine. Muziki mgeni kwa wengi kwa wakati ule. Nyimbo alizokuwa akizipenda na akaniambukiza na mimi kuzipenda ni, ‘’Ramblin Rose,’’ na ‘’The Good Times,’’  zote za Nat King Cole. Hadi leo kila nikizisikia nyimbo hizi huwa nakumbuka utoto wetu katika mitaa ya Kariakoo.



Kushoto mstari wa mbele Hussein Shebe, Henin Seif, kulia wa pili ni Raymond Chihota, Hussein,
(pass) Mbaraka ''Bata'' picha ilipigwa mapema 1960

Miaka ya 1960 ilikuwa miaka ya patashika si Dar es Salaam tu bali dunia nzima na ndiyo maana Waingereza wakaipa jina miaka hiyo kuwa ni, ‘’Roaring 60s.’’ Dar es Salaam ilikuwa na mastaa wake wakivuma kama Hussein Shebe, Raymond Chihota na Henin Seif kuwataja wachache  katika Chipukizi Club, timu ya waimbaji vijana wakipigiwa muziki na The Blue Diamonds,  ''band,'' ya vikana wa Kigoa. Kulikuwa na Sammy Davis Jr Salim Hirizi akiimba nyimbo maarufu, ''Summer Time,'' kwa umahiri mkubwa.  Katika hawa waimbaji kubwa lao alikuwa Sal Davis. Siku Sal Davis alipokuja na Hussein Shebe Mtaa wa Tandamti kuwaamkia wazee wake Hussein nyumbani kwa kina Mohamed Jaggan ilikuwa gumzo la mtaa mzima na sisi ambao hatukuwapo kumuona Sal Davis tulisikitika sana. Uhuru wa Tanganyika uliingiza katika nchi mambo mengi kutoka Ulaya yaliyotuvutia sisi vijana. Huu ulikuwa wakati wa wazimu wa mambo mengi sana kutoka Marekani na Ulaya. Sote tukisukumwa na ujana tulikumbwa na wimbi hili. Haya ndiyo yalikuwa maisha ya sisi vijana katika Dar es Salaam ya miaka ile ya 1960 na Chico hakuweza kuliepuka wimbi hili kama vijana wengi walivyoshindwa.


Salum ''Sammy Davis Jr'' Hirizi kama alivyo hivi sasa

Sal Davis Katika Onyesho Ujerumani 1960s

Ilikuwa Chico ndiyo, ‘’alinijulisha,’’ mimi kwa Sidney Poitier na nikaanza kuingia kila senema yake ilipokuja mjini. Sidney Poitier katika miaka ile hakuwa maarufu kwa vijana wengi wa Dar es Salaam. Wengi wetu tulikuwa na John Wayne, Richard Widmark, Alan Ladd, Victor Mature, Marlon Brando na mfano wa hao na wala haikutupitikia kuwa tunaweza kwenda senema Empire, Avalon, Empress au Chox kuangalia senema, ‘’actor,’’ Mnegro kama Sidney Poitier au Jim Brown. Chico alikuwa, ‘’special,’’ yeye akimjua Sidney Poitier, Eartha Kitt na wengineo siku nyingi sana. Kuanzia hapo na mimi nikabadilika. Nakumbuka senema za Sidney Poitier alizokuwa akipenda kunihadithia kama ni kama ''Lilies of the Fied,’’ ‘’A Patch of Blue,’’ na nyingine nyingi.

Image result


Ujana haukawii kukimbia. Haukupita muda tukakua na ikawa lazima tukubali kuwa wakati wa mchezo umepita tunaingia ukubwani. Chico alitushangaza wengi alipojiunga na Jeshi la Polisi kwani si katika kazi ambazo, ‘’watoto wa mjini,’’ tulizipenda na kubwa ni kuwa kazi ya jeshi ilikuwa inahitaji kufanyakazi nje ya Dar es Salaam na wengi wakiona dhiki kuondoka mjini. Sasa hapa ndipo ninapotaka kuhitimisha kuwa Chico alikuwa, kwa kweli na kwa hakika kabisa alikuwa ‘’special.’’ 

Chico alijiunga na Jeshi la Polisi na aliitumikia nchi yake kwa uadilifu mkubwa. Alifanyakazi takriban kila mahali na kuacha jina lililotukuka. MIaka mingi baada ya sisi kutoweka hapa duniani, itakapokujaandikwa historia ya watoto wa Dar es Salaam na nini wamefanya katika taifa hili nina hakika Kamanda Chico jina lake litakuwa juu. 

Allah amlaze pema ndugu yetu Mohamed Awadh Saiwaad maarufu kwa jina la Chico aliloishi nalo utotoni hadi ukubwani. 

Mwandishi akiwa Viwanja Vya Mnazi Mmoja ambako Everton na kisha Saigon
walikokuwa wakicheza mpira. Nyuma ni barabara iliykuja kupewa jina la Bi. Titi 
Mohamed na ukivuka barabara hiyo ni Soko la Kisutu maarufu kwa jina la Soko 
Mjinga. Picha ilipigwa 1966

Wednesday, 1 February 2017

Buriani Alhaaj Kamanda Chico
Na Alhaaj Abdallah Tambaza

JUA limekuchwa baada ya sala ya alasiri jijini Dar.

Waombolezaji mamia kwa mamia, wamejibanza chini ya vivuli vya miti ya miarobani iliyotapakaa kila upande wa makaburi haya ya Kisutu jirani kabisa na mabweni ya Chuo cha Biashara- CBE.

Kwenye vipaza sauti, ilisikika surat Yaasin, ikisomwa kwa pamoja na waumini wa dini ya Kiislamu; ikafuatiwa na tarumbeta pamoja na milio ya bunduki yenye kupasua roho kwa mshindo wake mkubwa—puu…puu…puu!! 

Hivyo ndivyo alivyozikwa, Jumapili ya Januari 22, mwaka huu, kipenzi chetu, ndugu yetu, rafiki yetu, kamanda wetu na mwana Dar es Salaam kindakindaki; (mstaafu) Kamishna wa Polisi Msaidizi Mwandamizi (SACP), Alhaaj Dk. Mohammed Chico.

Kamanda Chico alifariki saa 7:00 usiku wa Jumamosi, Januari 21, 2017 na mara kulipokucha habari za msiba zikatapakaa kote nchini kwa kasi ya ajabu kabisa.

Wa kwanza kunishitua alikuwa ni Mzee Shamas Akil, kutoka maeneo ya Kigamboni aliyenipigia simu saa 12:00 asubuhi kabla hakujapambazuka sawasawa na kunipa kile alichokiita, ‘habari za mjini’.

“Abdallah eh! Ndugu yetu Chico ametutoka… sikuweza kulala tena tokea nipate habari hizi saa 8:00 usiku jana… tutafahamishana mipango ya mazishi In Shaa Allah,” alisema Ali Kobe (Kocha) rafiki wa karibu wa hayati Kamanda Chico.

Mussa Shaggow, ni Mweka Hazina wa Klabu ya Saigon, klabu ambayo hayati Dk. Chico pia ni mwanachama. Naye Nilipompigia simu kufahamu taratibu za mazishi alisema:

“…Nimefadhaishwa sana na kifo hiki… ni juzi tu mimi na wenzangu tulikwenda kumjulia hali baada ya kuwa kitandani kwa muda mrefu sana…msiba uko kwake Kijitonyama lakini sala ya jeneza itafanyika Msikiti wa Manyema kabla ya alasiri leo,”alinifahamisha.

Alhaaj Kamanda Chico, kama ilivyo kwangu mimi, alizaliwa na kukulia jijini Dar es Salaam maeneo ya Kariakoo na kupata elimu yake ya awali pale AgaKhan School, Upanga (sasa Shule ya Msingi Muhimbili).

Baadaye alijiunga kwa masomo ya Sekondari ya Shaaban Robert ya jijini Dar es Salaam pia. Alijiunga kwa mara ya kwanza na Jeshi la Polisi kitengo cha Marine kule Kigamboni akianzia ngazi za chini kabisa. Alijiendeleza mpaka kuwa na degree ya uzamivu (Phd) akiwa kwenye utumishi polisi.

Nimemfahamu almarhum Kamanda Chico yapata nusu karne sasa, tokea tulipojuana mara ya kwanza kwenye madrassa ya Maalim Mzinga & Sons pale kona ya Mafia na Sikukuu, Dsm tulikopelekwa na wazazi wetu kuanza kusoma elimu ya msingi ya Dini ya Kiislamu tukiwa vijana wadogo chekechea.

Chuo Cha Maalim Mzinga kama kilivyo hivi sasa Mtaa wa Mafia na Sikukuu
Haraka haraka, Chico na mimi tukawa marafiki kwa sababu sote tulikuwa tukienda pale madrassani tukiwa na baiskeli zetu ambazo tulikuwa tukiendesha kwa pamoja kwenye mitaa ya Kariakoo wakati wa kutoka chuoni, tukikimbizana na kufurahi pamoja tukila embe mbichi zenye pilipili tulizonunua kwa mzee maarufu wakati huo Mzee Melabon.

Kutokana na utundu na ubunifu wake aliouonyesha kutoka utotoni, Kamanda Chico, akiwa na umri mdogo sana aliweza kuandika kwa ustadi mkubwa jina lake M.A. Saiwaad, pembezoni mwa baiskeli yake kuonyesha umiliki wake.

Nilivutiwa sana na maandishi yale, nami harakaharaka nikamwomba aniandike jina langu A. Mohammed, kwenye baskeli ya kwangu ili twende sawa. 

 Mohammed Awadh Saiwaad, ndiyo jina halisi la almarhum Dk. Chico. Ili kumjua vizuri makuzi yake ni lazima msomaji uwe na uelewa mzuri kwanza wa Jiji la Dsm.

Wakati huo, mji wa Dsm ulijengeka kutoka Gerezani; Mission Qrts (maeneo ambayo watu wa dini ya Kikristo walipenda kuishi); Kariakoo, Kisutu, Mwembetogwa – sasa Faya –; Ilala na Magomeni Mapipa.

Watu wa wakati huo walikuwa wakipenda mpira, muziki, senema, siasa na mambo ya namna hiyo. Wale waliopenda sana kucheza mpira walijipachika majina ya wachezaji mashuhuri wa wakati huo (role models) wa hapa nyumbani ama nje. Majina yao hayo ya kujipachika (nicknames) au kupewa na marafiki, yamebaki kuwa sehemu ya utambulisho wao mpaka leo.

Kwenye siasa, yupo mzee wetu Mzee Kissinger pale mtaa wa Kongo, ambaye jina lake hasa ni Mzee Shekue, lakini watu hawalijui jina hilo ila wamelizoea lile alilopewa la waziri wa zamani wa Mambo ya Nchi za Nje wa Marekani Dk. Henry Kissinger, lilotokana na umahiri wake wa kujenga hoja.
Mzee Kissinger
Jina halisi Shekue

Kwenye soka, walikuwapo waliojiita kina Peter Oronge kutoka Kenya (Mwinyi Mussa), Springet golikipa wa England (Kitwana Juma), Mnyika wa Tabora (Rashid Mohammed), Dennis Law England (Jamil Hizam), Mussa Shaggow kutoka Unguja (Alhaaj Mussa Mohammed Khamis wa Saigon).

Klabu ya Sunderland (sasa Simba) wakati huo alikuwapo winga machachari akiitwa Salim Ali ‘Jinni’. Alipewa jina hili kutokana na uwezo wake mkubwa wa kuruka juu kupiga vichwa mipira ya kona. Kwa ustadi ule watu walimfananisha na jinni.

Hayati Kamanda Chico, yeye tokea udogo wake akipenda sana ukakamavu na ubabe  wa Kimarekani. ‘Miondoko’ na mavazi yake kwa jumla yaliendana na mila na desturi za kimarekani.
Hiyo, ukichanganya na Kimombo kizuri alichokuwa akizungumza, alikuwa amekamilika. Jina likawa limetua mahala pake hasa. Ilikuwa ni kutokana na Wamarekani wa Kihispaniola (Spanish Americans), ndani ya senema zile za kizungu, majina ya Chico ndiko yakisikika.

Sheikh Hamid Jongo, ni Kadhi wa Mkoa wa Dsm na Imam Mkuu wa Msikiti wa Manyema hapa jijini. Akitoa wasifu kabla ya sala ya jeneza siku ile ya Jumapili ya msiba, alimwelezea marehemu kama mmoja wa watu wanaounda kikundi cha Ashabi L’yamini, kilichosheheni waumini wa Msikiti wa Manyema.
Sheikh Hamid Jongo
Picha ya 1988
Alimwelezea  Alhaaj Dk. Mohammed Chico namna alivyoweza kuishi, kusaidia, kujichanganya, kujumuika na kutoa michango mbalimbali katika jamii alimoishi kila alipokwenda kikazi na hapa Dsm kwao.

“…kila watu wana vijiwe vyao; Kamanda Chico naye alikuwa na cha kwake kilichojulikana kama Ashabi L’yamini ambacho kilikuwa na kawaida ya kufanya dua na kuombeana kheri pale nyumbani kwangu Tandika wiki mara moja…

“ Kwa mapenzi yake Kamanda Chico alipendekeza mkusanyiko ule uwe unahamahama kwenda nyumba nyingine pia na basi ikawa hivyo…mara nyingi ikawa inafanyika kwake Kijitonyama, ”Sheikh Jongo alisema.

Kwa hiyo msomaji, ili kufahamu vizuri hali ya maisha ya watu wa Dsm zama hizo ni lazima kwanza uelewe mazingira yake na vitu vilivyokuwa vinawaunganisha wakazi hata wakawa wakijuana na kupendana tofauti na ilivyo sasa—jirani yako nyumba ya pili humjui!

Eneo la Kisutu ndiko mwandishi huyu alikozaliwa na kwamba ndiko kulikokuwa na kitovu cha Dsm na watu wake. Kisutu kulikuwa na barabara moja tu kuu ikijulikana kama Wadigo street.
Nyumba yetu sisi ilikuwa hapo. Pamoja na watu wengine mashuhuri walioishi Digo street ni mpigania Uhuru maarufu Mzee Haidar Mwinyimvua. Huyu ndiye baba mzazi wa Sheikh Ahmed Haidar, Imam Mkuu wa Masjid Mwinyikheir pale, Kisutu Akiba.

Wengine ni babu yake marehemu Chiko Mzee Mohammed Mshihiri, aliyekuwa anaishi nyumba ya nne hivi kutoka kwetu yeye na mmoja wa wake zake, Bibi bint Said. Mzee Mohammed Mshihiri alimiliki (landlord) nyumba kadhaa jijini Dsm.

Wadigo street ilikuwa mita kama 10 hivi kutoka uzio wa makaburi ya Kisutu eneo ambalo lilizungukwa na miti mingi ya mivinje. Mwisho wa barabara kulikuwa na madrassa maarufu ya Sheikh Goma walikosoma wengi wa wakazi wa eneo hilo.

Watoto wa Mzee Mohammed Saiwaad (Mshihiri) ni Awadh, Said, Hemed na Abeid. Awadh Mohammed (babake  Chico), huyu alikuwa akifanya kazi sokoni Kariakoo akiwa agent mkubwa wa samaki wabichi kutoka Bagamoyo, Kunduchi, Mbweni, Ununio na Kigamboni.

Biashara hiyo ilimpa umaarufu na kumfanya awe na uwezo mkubwa kifedha akimiliki, pamoja na mambo mengine, nyumba kadhaa maeneo mbalimbali jijini.

Mzee Issa Aussi, yeye  ni mmoja wa wazee wakongwe wa jiji la kwetu la Dar es Salaam. Nilikutana naye na kuongozana naye kutoka makaburi ya Kisutu baada ya mazishi ya Dk. Chico. Nikataka kujua alimjuaje babake marehemu Mzee Awadh Mohammed?

“… Ah! Sipati kukwambia… alikuwa mtu mwema na mkarimu sana kupita kiasi…

“ Kwa kweli alinifanya niache kwenda kwake kununua samaki pale sokoni Kariakoo … kwa sababu kila mara alikuwa akinipa samaki bure… alikataa pesa kutoka kwangu;

“…Kutokana na namna watu walivyojuana na kupendana mzee yule alikuwa akiona picha ya babaangu mbele yake hivyo akawa anashindwa kuchukua pesa zile…

“…Sasa nikaona nitakuwa namtia hasara hivyo nikawa siendi kununua samaki kwake, badala yake nikituma mtu,”alisema kwa mshangao mkubwa Mzee Issa.

Kulia: Ally Sykes, Issa Ausi, Sheikh Ayub na Juma ''Spencer'' Abeid

Mzee Awadh Mohammed, alimudu kumsomesha mtoto wake Chico katika shule ya AgaKhan Dsm. Wakati ule wa ukoloni shule hiyo wakisoma watoto wa watu wenye uwezo, kipato na majina makubwa (elites) hasa wahindi wenyewe na Waarabu.

Kamanda Chico alisomea huko na hivyo kuwa na uwezo mkubwa sana wa kuzungumza lugha ya Kiingereza kwa ufasaha na madoido mingi tokea utotoni; tofauti kabisa na zile shule zetu sisi za ‘Kikayumbakayumba’ za Mchikichini na Mnazi Mmoja.

Sasa, kila mara ninapokumbuka (retrospect) hali hii, siachi kuichukia serikali dhalimu ya Kifalme ya Uingereza iliyokuja hapa kwa kisingizio cha kueneza umissionari kupitia kanisa lao la Ki-Anglikana (Mfalme wa Uingereza ndiye mkuu wa Kanisa la Anglikana duniani), ikawa imefanya ubaguzi wa namna ile katika utoaji huduma muhimu, ikiwamo elimu, afya na makazi.

Msomaji hebu zingatia, hapakuwapo na hospitali yoyote jijini Dsm kwa watu weusi (Muhimbili ilijengwa 1957) hadi pale zilipojengwa hospitali ndogo tatu (Magomeni, Ilala, Mnazi Mmoja) kwa msaada kutoka Ireland. Wazungu wakitibiwa European Hospital (sasa Ocean Road); wahindi Hindu Mandal, Burhani na AgaKhan Hospital.

Waafrika walitibiwa kwenye hospitali ndogo na mbaya tu; iliyojengwa na mhindi  mmoja Khoja kutoka Bagamoyo aliyekuwa karibu na waafrika. Sewa Haji Hospital, ilikuwa pale karibu na Kituo cha Kati cha Polisi (Central). Tiba hapo sana sana ni kufunga vidonda, kucheki kifua kikuu (msiwaambukize watawala) nk. Magonjwa mengine yote ni kufa huku unajiona.

Kuhusu elimu, shukrani nyingi ziwaendee walimu wale wa madrassa ya Maalim Mzinga & Sons na Al Hasnain Muslim School ya kina marehemu baba zake Sheikh Yahaya, Sheikh Hassan na Hussein Juma ndugu wawili mapacha kwa jitihada kubwa walizozichukua madrassani kwao, kurekebisha ile tofauti kwa kutoa elimu ya ziada ya kisekula katika masomo ya hesabu, kuandika na kusoma Kiingereza.

Kushoto Sheikh Hassan Juma na kulia ni pacha mwenzake Sheikh Hussein Juma

Elimu hii ya ziada ikatufanya sisi tuliokuwa tunasoma Mnazi Mmoja na Mchikichini kuwa na uwezo sawa au zaidi na wale wenzetu wengine na hivyo kufaulu katika viwango vya juu katika elimu na kwenye ajira, wakati na baada ya Mwingereza kuondoka.

Mtoto wa pili wa (Babu Chico) Mzee Mshihiri ni Said Saiwaad. Mzee Said Saiwaad alipata elimu yake pamoja na hayati babangu Mzee Mohammed Swaleh Tambaza katika Kitchwele Govt. School jijini Dsm, na baadaye wawili hao walijiunga na Shirika la Reli la Afrika Mashariki.

Ingawa babangu alikuja kuacha kazi Railways mapema, baada ya kutukanana na mzungu wakati huo wa ukoloni, Said Saiwaad yeye aliendelea hadi kufikia ngazi za juu kabisa katika shirika hilo kubwa la treni katika Afrika Mashariki.

Mwandishi huyu wakati akijiunga na Chuo Cha Usafiri na Usalama wa Anga (East African School of Aviation,  pale Wilson Airport, Nairobi, mwaka 1973, alimkuta marehemu Mzee Said Saiwaad akiwa na cheo cha Afisa Mkuu Ugavi wa Shirika la Reli Afrika Mashariki Ukanda wa Kenya (District Supplies Officer Railways -Kenya Region). Wakati ule tukiwa badobado kielimu; cheo kama hicho ni cha wazungu tu.

Mzee Said Saiwaad na mkewe Bi. Ajuza pamoja na watoto wao Abdallah, Omar, Safia, Nuru na Eshe walikuwa wakiishi eneo mashuhuri kabisa kule Lavington, Nairobi. Kila mara, nafasi ilipopatikana mwishoni mwa juma niliwatembelea kwao tukala na kunywa pamoja tukikumbuka nyumbani.

Baba mwingine mdogo wa Alhaaj Kamanda Chiko ni Hemed Saiwaad, aliyekuwa agent wa soda na muuza barafu kwa wingi jijini Dsm na vitongoji vyake; na wa mwisho Mzee Abeid yeye alikuwa msanii wa michezo ya kuigiza kwenye runinga na redio nyumba yake ilikuwa pale mtaa Rufiji Kariakoo karibu na hospitali ya Dk. Juma Mambo.

Tarika ya Dandarawi (kikundi cha kufanya dua za pamoja, dhikri mbalimbali na kumwomba Mwenyezi Mungu ina makao yake pale Msikiti wa Ijumaa Kitumbini, Dsm. Hii ni moja ya tarika kongwe jijini iliyoongozwa kwa kipindi kirefu na Almarhum Sherrif Juneid Imam Mkuu wakati ule.

Hayati Dk. Chico alikuwamo humu akifuata nyayo za waliomtangulia kwenye familia yao ambao wote walikuwamo kwenye Dandarawi. Kwa namna moja ama nyengine, tarika hii inafanana na ile ya Shaddhilly ya Sheikh Nurdin Hussein. 

Familia nyingine ambayo ni wafuasi wazuri wa Dandarawi ni ile ya Hayati Abdulwahid na Ali Sykes. Wengine ni Sheikh Muharram Swaleh Kitembe (babake Sheikh Mahdi) na Sheikh Haidar Mwinyimvua wa Kisutu na wanawe wote.

Kwa makusudi nimeelezea habari hizi za tarika ya dandarawi na Ashabi Lyamini, katika muktadha huu wa maisha ya Kamanda Chico ili kuonyesha ni kwa kiasi gani zimeweza kumbadilisha na kumjenga kiroho na kuwa mtu bora wa namna yake. Kule polisi Kamanda Chico alianzia ngazi ya kuruta wa kawaida jeshini hadi kuweza kufikia ngazi za juu kabisa za uongozi.

Kuelezea maisha na nyakati za Almarhum Dk. Chico ni safari ndefu. Huwezi hata ukijitahidi vipi kuyamaliza na kuyaelezea kwa ukamilifu wake yale mwanajamii huyu aliyoyaishi katika uhai wake – ni mengi mno!

Katika safari yake ya kikazi alipata kushika wadhifa wa RPC –Kamanda wa Polisi wa mikoa ya Kilimanjaro na Morogoro kwa muda mrefu. Kote huko alikopita ameacha athari ya uongozi uliotukuka. 

Marehemu Kamanda Chico alikuwepo kama mwanachama pale kwenye klabu maarufu ya Saigon tokea miaka ya mwanzo ya 60 hivi akitokea klabu yake ya mtaani ya Everton alikokuwa akicheza mpira pamoja na watoto wenzake akina Suleiman Jongo (mchezaji wa zamani wa Yanga), Jumanne Macimenti (Simba) na Ahmada Digilla.

Almarhum Chico amefanya mambo mengi katika kudumisha udugu wa wana Saigon hata pale alipokuwa nje ya Dsm kwenye transfer za kikazi, basi roho na akili yake ilikuwa pamoja na wenziwe.

Daima, kila palipofanyika hafla pale klabu utamwona hayati Chico—akiwa na kofia yake ya tarbush kichwani— akiwa mstari wa mbele akifanya hili ama lile, iwe kwenye kufuturisha ama Khitma za kurehemu waliotangulia, na bila shaka yeyote, kama ilivyo ada, jina la Dk. Mohammed Chico litakuwa miongoni mwa watakaorehemewa mwaka huu. 

Saigon ni kiungo muhimu kwa wakazi na wenyeji wa Dsm ikiwa haitofautishi dini, siasa ama Simba au Yanga. Pale utakuta watu wakijinasibisha na U-daresalama wao tu. Hali iliyofanya kuwa kimbilio la walio wengi.

Daima tutakukumbuka shujaa wetu na kamanda wetu, sisi nduguzo wazawa wa Dar es Salaam kwa kuonyesha mfano wa kuigwa kwa kujitoa muhanga kuchagua kulitumikia Jeshi la Polisi wakati vijana wengi wakiwa hawapendi kufanya kazi hivyo.

Msomaji hebu fikiri kama watu wote wangekataa kuwa mapolisi hali ya usalama kwa raia ingekuwaje? Ni kazi ya wito ambayo wale tu wenye moyo wa uzalendo wa kweli hupenda kuifanya ili amani na utulivu upatikane kwa watu wengine.

Kule Ulaya na Marekani, kama kijana atajitolea kuwa jeshini, basi familia anayotoka na jamii anamoishi kwa ujumla hujivunia mtu huyo. Picha zake akiwa kwenye uniform zake daima huwa zinaning’inia kwenye kuta za sebule kwenye nyumba za jamaa zake.

Kamanda Chico alikuwa na fursa nzuri ya kujiunga na biashara kutokana na uwezo wa kifedha ambao familia yake imeuonyesha tokea awali; ukiongeza na elimu yake aliyokuwa nayo angeweza kuwa mtu yeyote yule mwengine lakini alichagua kufanya hii kazi ya kijamii pamoja na misukosuko yake.

Kamanda Chiko amemwacha mkewe Bi. Barke, watoto wanne na wajukuu watano. Mtoto wake mkubwa SP Awadhi Chico, amefuata nyayo za babake, kwani amekuwako Jeshini Polisi siku nyingi na sasa ni Deputy Regional Crimes Officer Ilala Region.   

Tunamwomba Allah (sw) amghufirie madhambi yake na pepo ya firdaus iwe makazi yake.
Inna Lillah Waina Illayhi Rajiuun!
Simu: 0715808864/ 0628985862
Kushoto: Sheikh Manzi, Chico, Sheikh Ali


Kulia Mwinyikhamisi, Abdallah Mohamed Tambaza na Ibrahim



Sunday, 26 March 2017


Sheikh Mtoro tupoe sote kwa kuondokewa. Binafsi miezi mitatu hii nimeondokewa na watu wangu wa karibu watatu ambao tumekuwa na kucheza pamoja, wawili - Eyshe Abbas Max na Mohamed Awadh Chico, Mohammed Ali Muhsin huyu tumejuana tuko vijana. 
Elvis Presley. ..

Kaka kwa wale wa miaka ile wanajua Eid ilikuwaje Dar es Salaam kuanzia Mnazi Mmoja kwa ''Karagosi Kalewa Tembo,'' hadi kwenye ''theatres'' mjini. Chips pale sasa Mbowe nk nk.
Nilikuwa na miaka 12 mwaka wa 1964.

NIkaingia Empire kumuona Elvis katika ‘’Blue Hawaii.

Kuanzia siku ile hatukuachana hadi alipofariki 1977.

Nikiimba nyimbo zake nyingi. Nakumbuka siku ya pili nakunywa chai na marehemu baba yangu siku hizo tukikaa Lindi Street mkabala nyumba yetu na International Hotel inakaribia Nkrumah Street.

Mtaa huu ndipo marejemu Ally Sykes alikujwa na ofisi yake na Peter Colmore High Fidelity (Makao Makuu yakiwa Government Road Nairobi) na ndipo nilipomjua Peter Colmore kwa karibu.

Basi nampa mzee stori za Elvis na ‘’Blue Hawaii.’’ Yeye ananisikiliza tu.

Mwisho akanambia kuwa wao enzi zao mjanja wao alikuwa Bing Crosby.

2011 nimekaribishwa kusomesha darasa la ‘’Undergraduates,’’ University of Iowa Marekani  mwenyeji wangu ni Prof. James Giblin alinambia kabla, Waamerika hupenda kumjua mtu ''backgroud'' yake kabla hawajaingiliananae.

Mkewe na yeye ni ''lecturer,'' pia akanambia hilo darasa hao wanafunzi ni watoto wa ''millionaires'' nisishangae nikiwoana hawana adabu.

Ananambia wazee wao wametutupia sie walimu ulezi wa watoto wao maana karibu wote ni watoto vigego yaani hawasikii.

Basi nimetayarisha ''slide.''

Slide ya kwanza kwenye ''screen,'' ‘’poster,’’ ya Blue Hawaii wanashangaa vipi huyu Mwafrika na Elvis wapi na wapi?

Nawaambia, ''It was Elvis and this movie which made me pick up the guitar.''

Mshangao unaendelea na ''curiosity.'' Picha ya pili mimi mwenyewe ''on stage with ''The Rifters...1969...

'' Sir that's you with tha band?''

Sote sasa tuko ''relaxed,'' wanafunzi wanaona ala huyu kumbe ''crazy,'' mwenzetu...''

Lecture ikaanza, ''Islam and Politics in Tanzania The Struggle for Independence.''
Empire kaka movie nyingi tumeona pale hasa ''Westerns,'' enzi za Gemma, Django nk. nk.

Rafiki yangu Abdallah Mkwanda (Ingemar Johansson) alikuwa heshi kunikumbusha ''All The Young Men'' aliocheza Allan Lade movie aliyoiona Empire Theatre.

Siku zimepita.

Monday, 27 February 2017

Waliokaa kwenye viti nyuma ni Omari Mahita na Said Mwema wote IGP
Wastaafu
Sheikh Abbas Ramadhani Abbas na kushoto kwake ni Sheikh Uwesu

Kulia Iddi Abdallah Chaurembo na Abdallah Mohamed Saleh au
Abdallah Tambaza

Kulia Henin Seif, Mwandishi na Hussein Shebe
Kulia ni mtoto mkubwa wa Chico Awadh akifuatia na mdogo wake na mjukuu
wakiwa na Hussein Shebe na Iddi Chaurembo. Hussein alikuwa akiishi jirani na
Chico katika utoto wao na Iddi alikuwa mlinda mlango wa Cuba Rovers timu
akicheza Chico na rafiki yake Ishaka Marande
Kulia ni Hussein Shebe akizungumza na viongozi wa Saigon Club kulia
kwake ni Mussa Shagoo na anaetazamana na Hussein ni Boi Juma Risasi
Kaka Shomari

Wednesday, 6 December 2017

Buriani ‘Kaka Kleist’
Na Alhaji Abdallah Tambaza

Mwandishi wa makala Abdallah Tambaza ni huyo wa kwanza kushoto, Bubby Bokhari, Kleist Sykes, Yusuf  Zialror, Mohamed Said, waliochutama kushoto ni Kaisi, Wendo Mwapachu na Abdul Mtemvu, 1968

AWALI ya yote napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Allah (SW) na kumtakia rehma Mtume wetu Muhammad (SAW) kwa kuniwezesha kukaa mbele ya kompyuta na kuandika taazia hii ngumu na nzito ya marehemu kaka yangu; ndugu yangu; sahib yangu; na rafiki yangu kipenzi kabisa kupata kutokea, Kleist Abdulwahid Abdallah Sykes – Inna Lillah Waina Ilayhi Rajiun.

Mwezi Januari mwaka huu nilimwandikia rafiki yangu mwengine, SACP Mohammed Chico, taazia nzito kama hii iliyonitoa jasho na machozi pale ilipokamilika. Sikudhani hata kidogo kama hautapita muda mrefu nitarudi kuandika tena taazia nyengine kwa mtu anayefanana na yeye ­­– wote ni watu wa kwetu Dar es Salaam niliowajua vilivyo. Wazungu wa kule Ulaya Ingereza na Marekani, wanapofikwa na msiba wa ukubwa kama huu, husema kwamba umekuja ‘untimely’ (haukutarajiwa kwa wakati ule, wakati sio ule na labda ungesubiri baadaye hivi). Wanasema ‘untimely’, kwa sababu bado wasingependa kuachana na mpendwa wao kwa wakati ule; wanasema ‘untimely’ kwa sababu wanajua uchungu wa kuondokewa; na wanasema ‘untimely’ kwa sababu kwa anayeondokewa hategemei tena kupata mbadala wake! Kwa kiasi fulani wako sahihi, kwani yu wapi leo ‘Kaka Kleist’ mwengine? Marehemu ‘Kaka Kleist’, alifariki dunia alfajiri ya kuamkia Jumatano, Novemba 22, mwaka huu, katika Chumba cha Watu Wenye Kuhitaji Uangalizi Maalumu (ICU), pale katika spitali ya Agakhan ya hapa Dar alikokuwa amelazwa jana yake.

Mara baada ya kifo kutokea, dadake, Misky Sykes, ambaye alikesha kucha pale spitali kufuatilia hali ya mgonjwa wake, akanipigia simu kunipa habari za msiba ule mzito huku akilia na kuomboleza: “…Kaka Abdallah eh …nadhani Kaka Kleist amefariki sasa hivi, naona madaktari na manesi wanahangaika pale… nafikiri ametutoka kwani hawasemi kitu… Ooh! Ooh! Ooh!” alikatiza Misky mazungumzo na kutoweka na kilio chake. Kleist alizikwa siku ya Alhamisi jioni katika makaburi ya Kisutu, katika mazishi yaliyoongozwa na aliyepata kuwa Rais wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, Jaji Joseph Warioba na Jaji Mkuu (mstaafu) Mohammed Chande Othman. Wengine ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Hussein Mwinyi, na Waziri wa Ujenzi na Miundombinu, Makame Mbarawa, ambaye ndiye aliyemwakilisha Rais JPM. Alikuwapo pia Prof. Haruna Lipumba wa CUF, Mbunge Mussa Azzan Zungu na Iddi Azzan zamani Mbunge pale Kinondoni, pamoja na mameya na madiwani mbalimbali wa jiji hili la Dar es Salaam. Walikuwapo pia vijana wengi wa Dar es Salaam wa kizamani ambao pengine wamesoma au kucheza pamoja na marehemu katika maeneo mbalimbali ya jiji hili.Walikuwapo pia watoto wa marafiki wa Kleist ambao waliongozana na wazee wao kuja kumsindikiza katika safari yake ya mwisho mwana wa jiji mwenzao ambaye habari zake na ukarimu wake pengine walikuwa wakisimuliwa na wazee wao kwenye sebule zao.

Jaji Chande Othman, pamoja na kwamba alikuwa pale kwenye turubai lilowakinga viongozi, sidhani kwamba moyoni mwake alikuwa akihisi kuwa pale alipo alikuwa akihudhuria mazishi ya mtu wa kiserekali tu, kwani siku zile za utotoni kwake, si tu alisoma pamoja na Kaka Kleist, lakini pia yeye pamoja na kakake mkubwa Prof. Othman Chande, walikuwa kundi moja la Boys Scouts tawi la Saint Joseph’s Convent School, Forodhani. Mohammed Chande na Kleist pia walisoma wakati mmoja pale H.H. AgaKhan Secondary School (1964-1967).Hawa kina Chande wawili, waliungana na vijana wengine wa pale Shule ya Mtakatifu Joseph, Forodhani wakaunda kikundi cha vijana kilichojulikana kama The Scorpions, madhumuni yake yakiwa ni kupendana, kusaidiana na kutembea pamoja pale inapobidi.

Scorpions wengine waliokuwapo pale siku ile ni Hassan Ndumballo, Abdallah Mgambo, Abdul Mtemvu, Wendo Mwapachu, Yusuf Zialor, Christopher Faraji, Kamili Mussa, Bhobby Bokhari pamoja na mimi mwandishi wa makala haya. Nilimwona pia Mbunge Mussa Azzan ‘Zungu’ pale makaburini. Zungu hakuwa anamwakilisha Spika Ndugai pale. Kwa vyovyote vile alikuwapo kwa ajili ya kuwa amecheza na Kleist utotoni kwenye mitaa ya Kariakoo na Gerezani ambako wote ndiko walikokulia. Mzee Warioba, pamoja na nasaba yake ya Musoma, alikuwa mtu wa hapa mjini siku nyingi. Kabla hata hajajiunga na Chuo Kikuu, pale Mlimani alikuwa akionekana akivinjari mitaa ya New Street, Gerezani na Mission Kota, siku nyingi sana na hivyo akawa amezoeana vilivyo na vijana wengi wa jiji hili akiwamo marehemu Kleist Sykes. Isitoshe, mke wa Jaji Warioba ni mwenyeji wa Dar mwenye uhusiano wa karibu sana na kina Sykes.




Mwingine ni Mzee Kikwete. Huyu hakuwapo pale kumzika kada mwenziwe wa CCM tu. Kikwete naye Dar es Salaam ni yake na vijana kama Kleist ni rika lake, hivyo wakigongana hapa na pale kwenye kumbi za starehe na burudani hasa miziki ya ‘’Buggy,’’ na kwenye viwanja vya mpira. Kikwete alipotea njia kidogo akawa anapenda Yanga, wakati Kleist ni Simba wa kutupwa. Mapema, katika nasaha zake kwa waombolezaji mara baada ya sala ya jeneza pale Msikiti wa Maamur, Upanga, Imam Mkuu Sheikh Issa aliwataka waumini kujiandaa na kile alichokiita ‘certainty of mortality,’ akiimaanisha kwamba kifo kimedhihiri na kwa hakika kitamfika kila mmoja; kwa hiyo hapana budi watu kukifanyia maandalizi yake kabla. “Katika maisha yetu ni vizuri basi watu wakakaa mbali na yale yote ambayo Allah (SW) ameyakataza na kuyafanya kwa wingi (kuyakimbilia) yale ambayo Allah (SW) ameyaamrisha kwayo,”amesema Sheikh Issa.  


Nyuma kulia ni Rais Mstaafu Jakaya Kikwete
Sasa wakati nikiyatafakari maneno yale adhimu ya msomi yule pale msikitini, nilijihisi kama vile alikuwa akiniambia mimi au labda alikuwa akijua namna marehemu alivyokuwa mtu wa kheri, hasa katika utoaji wa sadaka na mambo kama hayo. Kaka Kleist, alipenda sana kusaidia wengine na wala hakusubiri kufuatwa kwa shida ndiyo afanye hivyo. Kuna wakati unaweza kukutana naye tu iwe ofisini au sehemu yeyote na ghafla atakurushia swali: “Vipi wewe uko vizuri mifukoni?” Kabla hujajibu tayari atakuwa amekwishatoa pochi lake na kukuvurumushia pesa ukafanyie jambo lolote. Kwa watu wazima na vikongwe hapo tena ndio usiseme. Hivyo ndivyo alivyoishi katika jamii inayomzunguka na kwenye makundi ya marafiki zake. Sasa wakati Sheikh Issa akitoa nasaha zile ikaja taswira fulani hivi ya kwamba rafiki yangu yule, njia yake ya kuelekea kwa Mola wake ilikuwa kwa kiasi fulani imesafishika tayari.

Siku moja wakati ugonjwa umeshamtopea kwelikweli na figo hazipatikani, nilifika kumwona pale kwake Mbezi Beach. Tulitazamana machoni na yeye akagundua kwamba mimi nimehuzunika sana. Alinitazama na akaniambia: “Sikiliza we ‘timbwa’ wala usihuzunike mimi tayari nimewasomesha watoto wangu wote vizuri sana …sina kinyongo hata kama Mwenyezi Mungu atanichukua leo… niko tayari kwa hilo,”alisema. Yale yalikuwa ni maneno mazito kuyasema mtu aliyekuwa kwenye hali kama yake. Palepale nilijua ile ilikuwa ni kama ananiaga kiaina, kwani tayari alikwishahisi dalili kuwa safari yake haiko mbali. Kamwe, hakuwa mtu wa kukata tamaa kirahisi, kwani aliujua vizuri ugonjwa wa kisukari na madhara yake ikafikia hata wakati mwengine kupendekeza tiba mwenyewe kwa madaktari wake. Katika juhudi zake za kupambana na maradhi, marehemu kwa nyakati tofauti alikwenda sehemu mbalimbali duniani kutafuta tiba. Juhudi za kila aina zilifanyika kupata figo mbadala (transplants), lakini ilishindikana kwa sababu mbalimbali ikiwemo ya umri mkubwa n.k. Na hapa napenda kumfariji shemeji yangu Stella Mallya ambaye alijitolea sana kuhakikisha mume wake anapona kwa namna yeyote ile.

Kwa upendo na hali ya kawaida, tulikuwa tukipenda kumwita ‘Kaka Kleist’, hata kwa wale ambao hawakuwa wadogo zake wa damu. Sababu ni kwamba wadogo zake walikuwa marafiki pia, na hivyo kwa kawaida huchanganyika na watu wengine kutembea na kustarehe pamoja. Sasa, inakuja katika mazungumzo, majadiliano ya hoja au kutaniana kwa aina yeyote, watu wengine walikuwa wakimwita Kleist kavukavu hivihivi; wakati wadogoze (akiwamo Abraham, Ayoub, Mussa, Misky, Omar (sasa marehemu), Adam (sasa marehemu), Ebby (sasa marehemu) ilikuwa inawashinda; kwani kila mara ni lazima waanze na kitu ‘kaka’. Hivyo tamko ‘Kaka Kleist’ likawa linaleta ladha fulani kulisikia; maana nduguze hawakumwita mtu mwengine yeyote kaka zaidi ya Kleist, hata kama ni mkubwa kama huyo kaka yao. Wengine waliitwa tu, kwa majina yao ya utani na mzaha (nicknames) kama kawaida.

Katika miaka hiyo, mwandishi huyu, kwa marafiki zake alikuwa akipachikwa majina mengi ya masikhara na utani kama vile ‘Nene’ au ‘Timbwa’, kutokana na wingi wa kilo mwilini. Lakini kamwe sikusikia mtu akiniita ‘Kaka Nene’. Tamko hilo lilikuwa ni makhsusi kwa marehemu Kleist peke yake. Sababu nyengine ya kuitwa kaka ni kwamba, alikuwa ni mtu wa upatanishi na usuluhishi panapotokea sintofahamu baina ya marafiki zake. Alikuwa na kipaji, uwezo na akili nyingi sana za kuweza kuleta suluhu au ushawishi katika kujenga hoja kwenye vikao mbalimbali. Mambo hayo ni miongoni mwa sifa zilizomfanya watu wamwite, ‘Kaka Kleist’.

Mara ya kwanza kabisa kukutana na Kleist, ilikuwa pale kwenye Shule ya Aljamiatul-Islamiya fi Tanganyika, mtaa wa New Street (sasa Lumumba) kwenye miaka ya 50s, tulikopelekwa na wazee wetu kupata elimu ya dini ya Kiislamu. Hapa Kleist alikuwa akijulikana sana maana shule haikuwa mbali na kwao. Pia waasisi wa mwanzo wa taasisi ile pamoja na mchango mkubwa  wa jengo zima ilikuwa kutoka kwa familia ya Sykes, hasa babu Mzee Kleist Abdallah Sykes ambaye alijitolea hali na mali kuhakikisha Uislamu na Waislamu hawaachwi nyuma. Walimu mashuhuri pale kwa siku zile nakumbuka alikuwa Maalim Simba, Maalim Mataar, Maalim Adam Issa na Sheikh Abdallah Iddi Chaurembo ndiye aliyekuwa Mwalimu Mkuu wa taasisi ile. Palikuwepo pia na walimu wanawake kama vile mwalimu Sakina Arab na mwalimu Tahia. Namkumbuka huyu mwalimu Tahia kwa sababu alikuwa pia ni mke wa Mzee Juma Mwinyimkuu rafiki mkubwa wa marehemu babangu wakicheza mpira pamoja timu ya Morning Star iliyokuwa timu ya pili ya Sunderland wakati huo (sasa Simba). Mwalimu Sakina yeye alikuwa ni mwanamke mmoja maarufu sana katika harakati za wanawake hapa kwetu, kwani alifikia hadhi ya kuwa na kiti cha kudumu cha udiwani katika Manispaa ya Dar es Salaam siku hizo za ukoloni wa Kingereza. Habari za Al Jamiatul Islamiyya fi Tanganyika ni ndefu mno na mchango wa Mzee Sykes pamoja na watoto wake Abdul, Ally na Abbas katika jamii ya Kiislamu na ukombozi wa nchi hii kwa ujumla, zimeelezwa kwa kina na mwanahistoria maarufu nchini ndugu yangu Sheikh Mohammed Said, katika kitabu chake mashuhuri, “The Life and Times of Abdulwahid Sykes 1968 The Untold Story of the Muslim Struggle Against British Colonialism in Tanganyika,’’ kinachosambazwa na Ibn Hazm Media Centre ya Dar es Salaam. Ndani ya kitabu hicho, Mohammed ameuelezea mchango mkubwa wa familia ya Sykes katika kuanzisha chama cha TAA kabla ya TANU na namna walivyoweza kupambana na Waingereza kwa namna mbalimbali mpaka pale uhuru ukapatikana. Msomaji ikutoshe tu kusema hata pale TANU ilipoanzishwa, akina Sykes walikuwa na kadi namba za mwanzo mwanzo kabisa ambazo zilibuniwa na kugharimiwa na Mzee Ally Sykes (sasa marehemu).

Rafiki yangu, marehemu ‘Kaka Kleist, alizaliwa jijini Dar-es-Salaam miaka 68 iliyopita akiwa mtoto wa pili kwa baba Abdulwahid na mama Mwamvua Mrisho Mashu (maarufu mama Daisy). Watoto wengine ni dada Aisha-Daisy Buruku, ambaye alizaliwa mwanzo kabla ya Kleist, wakafuatia Adam na Omar ambao tayari wameshatangulia mbele ya haki. Adam alikufa yapata nusu mwaka sasa. Anao pia nduguze wa mama mwengine, kwa sababu mzee Abdulwahid alioa mara tatu. Huku utamkuta Ebby (sasa marehemu), Elyassar (anayeishi Canada) na wanawake Misky na Mariamu (sasa marehemu). Hakukuwa na mtoto yoyote kutoka kwa yule mke wa tatu ambaye alikuwa naye baada ya kuwa ameshaachana na mama Daisy na mama Ebby.

Baada ya kupata elimu ya dini pale Aljamiatul, ‘kaka’ Kleist, kama ilivyokuwa kwa kina Sykes wote wakati huo, alijiunga na shule ya H.H. The Aga Khan (sasa Tambaza High School na Muhimbili primary) pale Upanga Dar es Salaam, shule ambazo zilikuwa mahsusi kwa watoto wa jamii ya Kihindi wakati huo wa elimu ya kibaguzi ya utawala wa Kiingereza. Kina Sykes, walipata hadhi hiyo nadra wakati huo, kutokana na heshima kubwa iliyokuwa imepewa familia yao kwa sababu ya mchango wa Babu Mzee Sykes katika jamii. Na kwa heshima hiyo hiyo Mzee Abdulwahid Sykes (babake ‘kaka’ Kleist) aliingizwa katika Bodi ya Aga Khan Schools, na kwa hivyo ikawa ni rahisi ‘ujiko’ kwa kina Sykes wote kupata elimu pale. Kaka Kleist, alisoma pale kuanzia chekechea mpaka Form IV alipomaliza mwaka 1967. Baadaye akachaguliwa kujiunga na Chuo cha Kilimo kule Ukiriguru, Mwanza. Kufuatia kifo cha ghafla cha marehemu babake, mnamo mwaka 1968, kijana Kleist Sykes, ilibidi akatize masomo yake Mwanza na kusafiri kwenda kwa babake mdogo Abbas Sykes aliyekuwa Balozi wa Tanzania kule Canada kwa ajili ya malezi na masomo mapya.

Nakumbuka kama vile jana, nikiwa bado kijana mdogo nilihudhuria mazishi ya mzee Abdul pale mtaa wa Lindi, Gerezani, jijini yaliyofurika watu wengi— wengi kwelikweli— akiwemo Mwalimu Julius Nyerere, rais wa kwanza wa taifa hili. Tofauti na marais Kikwete, Mwinyi na Mkapa, katika uongozi wake, Mwalimu hakuhudhuria mazishini mara kwa mara. Ukiacha mazishi haya, mazishi mengine aliyohudhuria Mwalimu ni ya Sheikh Kaluta Amri Abeid, aliyekuwa waziri wake wa Sheria na Katiba wakati huo, aliyefia nchini Ujerumani mwanzoni mwa miaka ya 1960s na mwili kuletwa nyumbani kwa mazishi, akiwa kiongozi wa kwanza mwandamizi kufariki akiwa kazini. Alishiriki pia mazishi ya makamu wake wa rais Abeid Amani Karume kule Zanzibar na yale ya waziri wake mkuu Edward Moringe Sokoine, kule Monduli Juu, Arusha.

Katika mazishi ya Mzee Abdul Sykes, mwandishi huyu, alimshuhudia Nyerere akiwa kwenye majamvi pale mtaani Lindi na baadaye kulisindikiza nyuma jeneza mpaka Msikiti wa Ijumaa, Kitumbini. Katika hali isiyo ya kawaida, Nyerere alisubiri nje mwili uswaliwe swala ya jeneza na ulipotoka, aliusindikiza kwa miguu mpaka makaburini Kisutu pasi na kutaka asaidiwe usafiri. Kufuatia kifo kile, serikali ya Nyerere ilitangaza kujitwika mzigo wa kuwasomesha na kuwaangalia watoto wa marehemu rafiki yake yule, ambaye ndiye aliyempokea katika harakati za kugombania uhuru wetu akawa anakula na kulala kwake baada ya kuacha kazi ya ualimu Pugu ili ajiunge na harakati za kudai uhuru.

Katika maisha yake ya kule Canada, Kleist alihitimu shahada yake ya kwanza na ya  pili (uzamili) kwenye masuala ya Ustawi wa Jamii. Aliweza pia kupata ajira kwenye taasisi iliyojulikana kama Canadian University Students Organisation (CUSO). Kazi kubwa za shirika hilo ni kama lile la kule Marekani la American Peace Corps, lenye malengo na madhumuni ya kutoa misaada ya kimaendeleo kwa nchi changa duniani.  Sasa baada ya miaka kadhaa pale kazini, nafasi ikatokea ya kuja kuwa Mkurugenzi (Director of CUSO –Tanzania). Wakati huo Kleist alikuwa tayari ameoa kulekule Canada na kubahatika kupata mtoto wake wa kwanza Latifa. Kwa sababu ambazo hazikuelezwa, mamake Latifa alikataa katukatu kuongozana na mumewe kuja Tanzania, akihofia labda pengine wasingerudi tena Canada. Kwa mapenzi ya nchi yake na nduguze, Kleist aliondoka akaja yeye akiwa amembeba mtoto wake mdogo Latifa, wakati huo akiwa na umri takriban miaka mitatu hivi. Kwa kweli ilikuwa ni nderemo na hoi hoi kwenye ukoo wa Sykes kwa ujio wa Latifa. Bibi yake, marehemu mama Daisy, alishereheka sana kupata mjukuu yule kwa mtoto wake wa kiume. Latifa alikuwa juu juu—mara Upanga, mara Temeke, mara Mbezi Beach kwa babu Ally Sykes.


Kushoto: Mama Daiy mbele kulia Bi. Titi Mohamed
Mamake hayati Kleist Bi. Mwamvua Mrisho Mashu, alikuwa ni mwanaharakati mkuu wa masuala yanayohusu maendeleo ya wanawake hapa nchini. Katika uhai wake anatajwa kwamba alikuwa ni mmoja wa waasisi wakuu wa Chama Cha Wazazi nchi (TAPA), siku nyingi kabla uhuru wa nchi haujapatikana. Bi. Mwamvua anatajwa pia mmoja wa watu walioshirikiana kwa karibu na kina Bibi Titi kuanzisha UWT, ambako yeye alidumu kuwa mwenyekiti wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa kipindi kirefu akishinda chaguzi mbalimbali. Mama Daisy pia alikuwa Mwenyekiti wa TANU/CCM tawi la Miburani pale Wailes, Temeke kwa miaka kadhaa. Mwandishi huyu mara nyingi alimshuhudia Kleist akiwa na mamake wakipanga na kupangua mipango ya siasa, hasa zile zilizomhusu Kleist, kwani Bi. Mwamvua alikuwa na hazina kubwa ya uongozi wa nchi hii kichwani mwake kutokana na kule kuwa mke wa Mzee Abdul Sykes. Bila shaka yeyote ile, nguvu kubwa na uwezo aliokuwanao Kleist ulitokana na maelekezo na mafunzo kutoka nyumbani kwa mama yake baada ya kuwa babake aliaga dunia mapema.   

Sasa, mnamo miaka ya 1970 mwishoni, ili kuziba ombwe la kukosekana mama wa kumlea mtoto Latifa, Kleist aliamua kumchumbia Stella Mallya aliyekuwa akiishi jirani na nyumbani kwake pale mbele ya Shule ya Tambaza. Mzee Mallya ambaye ndiye baba wa bibi harusi hakuwa ameridhia kabisa binti yake kuolewa nje ya Uchagani kwao Moshi.  Baada ya tafakuri ndefu, wawili wale, bwana na bibi harusi wakaamua kuwa ndoa lazima ifungwe ‘iwe jua iwe mvua’, itakiwe isitakiwe. Ndoa ikafungwa kwa siri kwa DC pale Ilala na hapakuwa na sherehe wala mialiko yeyote. Mimi nikawa ndiyo mpambe ‘best man’ wa Bwana harusi, wakati Bi Bernadetta Majebelle akawa mpambe wa Bibi harusi. Baada ya shughuli ile pale bomani, tuliondoka mahala pale tukaenda peke yetu maeneo fulani kule Sea View tukajipongeza kwa vinywaji na vyakula kidogo mpaka usiku ulipoingia tukaagana.

Siku kadhaa baadaye, na kutokana na mapenzi aliyokuwa nayo kwa binti yake, mzee Mallya alirudi matawi ya chini akawa tayari kumpokea tena binti yake. Aliwatembelea nyumbani pale Upanga akakaribishwa kwa vyakula na vinywaji, ambapo mwandishi huyu alimshuhudia Mzee Mallya akiwa mwenye furaha kwelikweli baada ya kuwa amepata ‘kinywaji moto’ na ‘kinywaji baridi’. Ndoa ile imedumu kwa miongo zaidi ya mitatu na ikaajaliwa kupata watoto watatu ambao ni watu wazima sasa; Aisha, Abdulwahid, Ally na Latifa akawa dada yao mkubwa.

Uzoefu, uaminifu na utumishi uliotukuka pale CUSO, ulimpatia sifa Kleist za kuchaguliwa kujiunga na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) ambapo alifanya kazi kule Geneva, Switzerland na Zambia kama mwakilishi mkazi. Baada ya kuwa ametumikia UNHCR muda mrefu, ‘Kaka Kleist’ alirejea nyumbani na kujikita kwenye biashara mbalimbali ikiwemo kuanzisha kampuni yake ya kuhudumia meli iitwayo Prevention and Indemnity (P&I), ofisi zake mpaka leo zikiwapo pale mtaa wa Mkwepu jijini Dar es Salaam.

Kwa kutumia uzoefu wake wa biashara, utawala na nidhamu ya kazi, na kwa ushawishi mkubwa kutoka kwa marafiki zake wa utotoni (akina Yusuf Zialor na Wendo Mwapachu), ambao nao ni mabingwa katika masuala ya biashara, wakaanzisha kampuni iliyojulikana kama Business Center International (BCI) iliyokuwa na ofisi zake pale kwenye jumba la Bushtracker kwenye makutano ya Bibi Titi na Ali Hassan Mwinyi.  Marafiki wengine waliokuwa pamoja utotoni kwenye kundi la Scorpions ndio waliokuwa maofisa mbalimbali pale Bushtracker. Alikuwapo dada Mariam Zialor, Abdul Mtemvu, Booby Bhokari, Hassan Ndumballo, Abdallah Mgambo na Ramadhani Madabida. Business Center International (BCI) ilikuwa na kampuni tanzu kadha wa kadha ikiwamo ofisi mashuhuri ya safari za ndege ya KEARSLEY LTD pale Barabara ya Samora jijini na kiwanda kikubwa cha uchapishaji cha PRINTFAST kule Nyerere Road.

Kwenye jamii, Kleist alikuwa mwanachama mwandamizi wa Klabu maarufu ya Saigon ya Dar es Salaam, kama ilivyokuwa kwa wanafamilia wengine wa ukoo wa Sykes. Michango ya kina Sykes kwenye klabu hii haisemeki—wako mstari wa mbele kila pale wanapohitajika.
Kila mmoja aliwashuhudia vijana kutoka klabu ya Saigon walivyokuwa mstari wa mbele siku ya maziko kuanzia uhudumu wa chakula kwa wageni pale nyumbani mpaka makaburini Kisutu, kuhakikisha kila kitu kinakwenda sawasawa kwenye mazishi ya mpendwa wao. Alikuwa mwanachama pia wa klabu mashuhuri ya viongozi pale Leaders Club, iliyoko mbele ya Klabu ya Usiku ya Bilicanas, kwenye barabara ya Ali Hassan Mwinyi. Mwanachama mwandamizi kutoka Leaders Club, Zainul Dossa, ndiye aliyeratibu shughuli zote za mazishi ya Kleist kuanzia chakula nyumbani mpaka makaburini Kisutu akihakikisha kila kitu kimekwenda kama kilivyopangwa.

Katika upande wa siasa, marehemu Kaka Kleist alikuwa kada mzuri wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) akifuata nyayo za familia yake katika harakati za siasa. Alipata kuwa mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama chake chini ya uongozi wa Jakaya Mrisho Kikwete. Akiwa diwani wa Kata ya Kivukoni, marehemu Kleist aligombania na kuchaguliwa kuwa Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam kwenye miaka ya 1990, na moja ya mafanikio makubwa ambayo amekufa akijivunia ni kuweza kutatua tatizo la msongamano wa magari jijini Dar es Salaam, kwa kubuni na kusimamia mradi mkubwa wa Usafiri wa Mabasi ya Mwendo Kasi (Dar Rapid Transit). Aliweza kuwashawisha maofisa wa Benki ya Dunia, akiwamo rais wake, ambao awali walikuwa wamepanga kupeleka mradi ule kwenye moja ya nchi za kule Afrika Magharibi, kubadili mawazo na kuleta mradi ule mkubwa hapa kwetu, mradi ambao umeiweka Tanzania katika ramani ya dunia kwa kuwa na mradi mkubwa ambao, si tu utakidhi haja, lakini pia imekuwa ni fursa nyingine kwenye ajira na hivyo kupeleka mbele maendeleo ya nchi kwa jumla. Wawakilishi kutoka sehemu mbalimbali ulimwengu wamekuwa wakimiminika kuja kujifunza namna Tanzania ilivyofanikiwa kwenye hili. Akizungumza kabla jeneza la marehemu Kleist Sykes halijaondoka nyumbani kwa ajili ya kwenda kuzikwa, mwakilishi aliyetumwa na shirika la UDART, ambalo ndilo linatoa huduma za mabasi ya mwendo kasi jijini, alisema daima marehemu atakumbukwa kwa kubuni, kupanga na kukamilisha  hatua zote za utekelezaji wa miradi yote sita ya mpango mzima wa mabasi ya mwendo kasi.“...mpaka sasa tayari phase moja tu imekamilika yaani kutoka Kivukoni mpaka Kimara na kwamba mradi mzima una phase 6 ikiwamo Kariakoo – Mbagala; Morocco—Tegetta; na Kariakoo—Gongo la Mboto,...pale phase zote zitakapomalizika nchi itakuwa imepiga hatua kubwa …” amesema.

Mpaka umauti unamfika, marehemu Kleist, alikuwa amewekeza nguvu zake kwenye biashara ya kilimo cha mkonge kwani tayari alishanunua mashamba makubwa kule Kibaranga, wilayani Muheza, akiongozwa kitaalamu na mtaalamu bobezi wa Kilimo cha Mkonge nchini, Abdallah Mussa Kamili. Kwenye kazi hiyo, tayari alikuwa akishirikiana kwa karibu na wanawe katika uendeshaji na utawala wa shughuli hiyo. Sidhani kama kutatokea ugumu wowote, maana katika kipindi kirefu ambacho amekuwa akiugua ni watoto haohao ndio waliokuwa wakifanya shughuli hizo. InshaAllah kwa uwezo wa Mungu watajiunga pamoja na mama yao kumalizia pale ambapo baba amekomea. 


Sheikh Abdallah Awadh alipata kumbeba Kleist akiwa mtoto akisoma dua kwenye kaburi
Kushoto ni Kleist Abdul Sykes na kulia ni Abdallah Tambaza na katikati ni Mussa Abbas Sykes

INNA LILLAH WAINA ILLAYHI
RAJIUUN
simu: 0715808864