Mkakati wa
Tanga Kupambana na Wapinzani wa Kura Tatu, 1958
Mwaka 1958
serikali ya kikoloni iliandaa uchaguzi wa Baraza la Kutunga Sheria ambao viti
vilikuwa vishindaniwe kwa misingi ya utaifa. Kulikuwa na viti kwa ajili ya
Wazungu, Wahindi na Waafrika. Masharti mengine ya kumwezesha Mwafrika kupiga
kura yalimtaka awe na kipato cha paundi mia nne za Kiingereza kwa mwaka, awe na
kiwango cha elimu ya darasa la kumi na mbili na awe ameajiriwa katika kazi
maalum. Haya yalikuwa masharti magumu na yaliyoonekana kama hayataweza
kukubalika na TANU. TANU ilifanya mkutano wake mkuu wa mwaka wa 1958 mjini
Tabora kuanzia tarehe 21-26 Januari kujadili miongoni mwa mambo mengine ikiwa
ishiriki katika uchaguzi chini ya masharti haya ya kibaguzi yaliyowekwa au
wasuse. Mkutano ule ulitishia kuigawa TANU katika kambi mbili hasimu. Kambi
moja ni ile ya wenye siasa za wastani waliopendelea kushiriki katika uchaguzi
na ile ya pili ni ile ya wenye msimamo mkali waliotaka uchaguzi ususiwe kabisa.
TANU ilinusurika na kile ambacho kingeweza kuwa mgogoro ndani ya chama ambao
ungewafanya wale wenye msimamo mkali kama Sheikh Suleiman Takadir, Mwenyekiti
wa Baraza la Wazee wa TANU katika makao makuu, na Zuberi Mtemvu, wakati huo
katibu mwenezi wa TANU, kufanya mapinduzi ambayo yangekigawa chama kama
isingelikuwa busara ya Julius Nyerere, Rais wa TANU.
Lakini ili
kuzielewa hisia za wanachama wa TANU, fikra za uongozi wake na nguvu zilizokuwa
zikidhibiti siasa Tanganyika wakati ule wa ukoloni, na ili kuelewa kwa nini
kura tatu ilileta mgogoro na kutoelewana katika uongozi, inatubidi turudi nyuma
tufuatilie mwanzo wa siasa mjini Tabora, mahala ambapo TANU ilifanya uamuzi
wake ya kihistoria na kuwanasa Waingereza katika mtego wao wenyewe. Tunahitaji
kuyatazama mambo kwanza kuanzia Tanga mahali ambapo Nyerere na uongozi wa TANU
pale Tanga walikutana kwa siri kuweka mikakati ya mkutano wa Tabora. Baada ya
kufanya hivyo tufichue jambo moja baada ya jingine katika ule mkutano ambao
wajumbe wa TANU walikutana katika ukumbi wa Parish wa Kanisa Katoliki, Tabora.
Hii itatuwezesha kujua kwa nini mkutano mkuu huu ulikuwa muhimu na kwa nini
kutokana na mkutano huu Waislam ambao walijitoa mhanga sana katika kudai uhuru,
mara tu baada ya uchaguzi huo walianza kupoteza nguvu yao katika siasa hatimaye
kutupwa nje na katu hawakuweza kurejesha tena nguvu hiyo hadi hivi sasa. Akiiandikia Fabian Colonial Bureau,
katibu mwenezi wa TANU, Zuberi Mtemvu ambae alikuwa amelichambua jambo hili la
utatanishi aliandika:
‘’Katika nchi kama
Tanganyika, utajiri na elimu vimo mikononi mwa wageni. Mwafrika ni maskini na
hana elimu. Upigaji kura wenye masharti magumu yaliyoegemezwa kwenye mali na
elimu utawaathiri Waafrika peke yao bila kuwagusa Wazungu na Waasia hata
kidogo.’’
TANU kwa hakika
kilikuwa chama cha Waislam; kwa hiyo ilikuwa ni dhahiri kuwa kuyakubali
masharti yale ya kibaguzi ya upigaji kura ilikuwa sawasawa na kuwasukuma
Waislam ambao ndiyo walikuwa wafuasi wakubwa wa chama nje ya wigo wa siasa.
Nimtz ameandika kwa ufupi hali ya Waafrika katika uchaguzi wa mwaka wa 1958 na
1959 katika mji wa Bagamoyo, mji ambao ni wa Waislam:
‘’...kutokana na sifa za
wapiga kura na masharti magumu ambayo serikali ya kikoloni iliweka, upigaji
kura ulibakia kwa asilimia ndogo sana ya Waafrika ambao ndiyo waliokuwa wengi.
Katika Wilaya ya Bagamoyo ambako uchaguzi ulifanyika mnamo Septemba, 1958, watu
630 tu, katika idadi ya watu 89,000, ndiyo waliyojiandikisha. ‘’
Ujumbe wa
Nyerere mwenyewe kutoka makao makuu ulikuwa na watu wengi ambao wasingeweza
hata kidogo kusimama kama wagombea katika uchaguzi chini ya masharti yale.
Makao makuu ya TANU yalikuwa yanawakilishwa kwenye mkutano mkuu na Julius
Nyerere, Sheikh Suleiman Takadir, Bibi Titi Mohamed, John Rupia, Elias
Kissenge, Dossa Aziz, Julius Mwasanyangi, Michael Lugazia, Ramadhani Chaurembo,
Hussein Mbaruk, Clement Mtamila, Idd Tulio, Mzee Salum, Idd Faiz Mafongo, Idd
Tosiri, Haidari Mwinyimvua na Rajabu Diwani. Hii ilikuwa na maana uongozi wa
Waislam kule Dar es Salaam, Tanga, Tabora, Dodoma na mahala pengine nchini
Tanganyika usingeweza kusimama kama wagombea uchaguzi ili wachaguliwe kuingia
katika Baraza la Kutunga Sheria wala wasingeweza kuwapigia kura wagombea
wanaowataka. Kwa hiyo ilikuwa ni jambo la wazi kabisa kuwa TANU ingesusia
uchaguzi. Serikali ya kikoloni, ikishirikiana na wamishionari, walikuwa
wamewanyima Waislam elimu, sharti lile lile ambalo sasa linawekwa kuwazuia
Waislam kushiriki katika siasa. Mkutano wa Tabora ulikuwa uamue ikiwa TANU
itashiriki katika uchaguzi na kushindana na UTP au ingesusia uchaguzi huo na
hivyo kumpa mshindani wake mkubwa na hasimu wake ushindi wa bure.
Hakuna
kumbukumbu zozote zinazoeleza mawazo ya Nyerere katika suala la kura tatu wala
hakuna nyaraka inayoweza kueleza kuwa alipata hata kuzungumza suala hili kwa
faragha pale makao makuu na viongozi wenzake kama Sheikh Suleiman Takadir,
Zuberi Mtemvu, Rajab Diwani, Idd Faiz, Haidar Mwinyimvua, Dossa Aziz au Bibi
Titi Mohamed. Kwa ajili hii ni vigumu kuweza kujua ni kwa kiasi gani Nyerere
alikuwa amejizatiti katika msimamo wa TANU kuingia katika kura tatu chini ya
masharti yale. Lakini ikiwa utafanya tathmini kutokana na hali ya hewa ya siasa
kama ilivyokuwa katika miezi ya mwisho ya mwaka 1958, si vigumu kuona kwa nini
Nyerere ilibidi afiche msimamo wake katika suala la kura tatu kama TANU
lilivyotwishwa na serikali. Nyerere alikuwa anafahamu hatari iliyokuwa
ikinyemelea TANU kutokana na kura tatu. Alijua wazi ili kukinusuru chama na
mgawanyiko kulikuwa na haja kubwa ya yeye kufanya uamuzi haraka na kwa makini
kabla ya kuenda kwenye mkutano Tabora.
Siku kadhaa
kabla ya kusafiri kwenda Tabora kwenye ule mkutano mkuu wa mwaka wa TANU,
Nyerere na Amos Kissenge, Kaimu Katibu Mwenezi wa TANU, walisafiri kwenda Tanga
kushauriana na uongozi wa Kamati Kuu ya Taifa ya TANU Tanga kuhusu matatizo
yaliyoletwa na uchaguzi wa kura tatu. Mkutano huu baina ya Nyerere, Kissenge na
ule uongozi wa Tanga ulikuwa wa siri sana. Tanga iliwakilishwa na Hamisi Heri,
Mwalimu Kihere, Abdallah Rashid Sembe, NgĂanzi Mohamed, Mustafa Shauri na
Abdallah Makatta. Nyerere alizungumza waziwazi na kwa ithibati ya moyo wake.
Nyerere alikiambia kikao kile kuwa amekuja Tanga kuomba wamuunge mkono kwa
sababu ilikuwa ni matakwa yake TANU lazima ishiriki katika ule uchaguzi wa kura
tatu uliokuwa unakaribia hata masharti yakiwaje. Nyerere aliuambia uongozi wa
Tanga uliokuwa ukimsikiliza kwa makini kuwa alikuwa amekuja kwao kwa sababu
watu wa Tanga wanajulikana kwa ufasaha wa lugha na kwa uwezo wao wa kuzungumza
vizuri. Nyerere alisema angehitaji hiki kipaji adimu cha watu wa Tanga kuunga
mkono msimamo wake huko Tabora. Nyerere alitoa hoja kwamba TANU lazima iingie
katika uchaguzi kwa sababu kuususia ni sawasawa na kukipa chama hasimu, UTP
ushindi bila jasho kuingia katika Baraza la Kutunga Sheria. TANU ingedhoofika
na hivyo ingekosa sauti katika maamuzi yatakayotolewa na serikali katika siku
zijazo.
Kufichuka kwa
msimamo wa Nyerere wa kutaka TANU iingie kaatika kura tatu kulishtua uongozi wa
Tanga. Majadiliano makali yalifuata uongozi wa Tanga ukionyesha upinzani wao
kwa msimamo wa Nyerere. Baada ya majadiliano ya muda mrefu Nyerere alifanikiwa
kuwashawishi wote wawili, Hamisi Heri na Mwalimu Kihere ambao ndiyo walikuwa
wapinzani wakubwa wa msimamo wa Nyerere na uchaguzi wa kura tatu. Nyerere
aliutahadharisha uongozi wa Tanga kuwa agenda ya kura tatu itakapokuja
anatabiri kupata upinzani mkali kutoka katika majimbo. Huko Tanga kwenyewe,
TANU ilikuwa ikikabiliwa na upinzani mkali kutoka UTP na serikali.
Matawi kadhaa
yalikuwa yamepigwa marufuku. [1] UTP ilikuwa na nguvu Tanga kwa
sababu wanachama wake wengi walikuwa wakimiliki mashamba ya mkonge katika jimbo
hilo. Kwa ajili hii chama kilikuwa kinaelemewa na mashambulizi kutoka wa
wapinzani. Wakati huo Tanga ilikuwa imetoa viongozi wenye uwezo lakini wote
walikuwa wamehamishiwa makao makuu mjini Dar es Salaam. Wapangaji mikakati
wazuri kama Peter Mhando alikuwa amehamishiwa Dar es Salaam na kutoka hapo
alipelekwa Tabora ambako si muda mrefu akafa. Elias Kissenge vilevile
alihamishiwa makao makuu kushika nafasi ya Katibu Mkuu wa TANU baada ya Oscar
Kambona aliyekuwa ameshika nafasi hiyo kwenda Uingereza kwa ajili ya masomo.
Uongozi wa TANU Tanga hata baada ya kujadili mbinu waliyopanga na huku Nyerere
akielekeza mikakati ambayo Mwalimu Kihere na Abdallah Rashid Sembe
wataitekeleza Tabora, bado uongozi ule ulikuwa na wasiwasi wa mafanikio ya
mpango huo. Kwa ajili ya wasiwasi huu, viongozi wa TANU wa Tanga walimuomba
Nyerere wawe pamoja ili ifanywe tawaswil waombe msaada wa Allah awape ushindi
dhidi yaa vitimbi vya Waingereza.
Maili tatu
kutoka Tanga kipo kijiji cha Mnyanjani ambako kulikuwako na tawi la TANU
lililokuwa na nguvu sana likiongozwa na Mmaka Omari kama mwenyekiti na Akida
Boramimi bin Dai akiwa katibu. Mmaka alikuwa kijana aliyekuwa akiendesha
mgahawa pale kijijini na Akida bin Dai alikuwa mwashi. Akida aliongoza tawi la
vijana wa TANU ambalo baadae lilikuja kujulikana kama Tanga Volunteer Corps
(TVC). TVC ilikuwa sawasawa na Bantu Group, ambayo wakati huo ilikuwa
imekwishaanzishwa huko Dar es Salaam na Tabora. Vikundi hivi mbali na kufanya
shughuli za propaganda na kuhamasisha wananchi halikadhalika viliifanyia TANU
ujasusi. Nyerere na Kissenge walichukuliwa hadi Mnyanjani na tawaswil ikasomwa.
Waliohudhuria kisomo hicho walikuwa Abdallah Rashid Sembe, Sheikh
Dhikr bin Said, Mzee Zonga, Hemed Anzwan, Salehe Kibwana aliyekuwa mshairi
maarufu, Akida Boramimi bin Dai na Mmaka Omari. Aliyechaguliwa kusoma Quran
Tukufu alikuwa mjomba wa Mwalimu Kihere, Sheikh Ali Kombora.
No comments:
Post a Comment