SHUJAA WA KURA TATU
Utangulizi
Nilikwenda
kumuona Mzee Yusuf Olotu nyumbani kwake Moshi nyakati za jioni baada ya L’ Asr.
Nilimkuta
Mzee Olotu ndani amelala kwa kuwa hali yake ya afya haikuwa njema sana.
Baada
ya ujitambulisha alichangamka kwani nilipomtajia wazazi wangu wote akawa anawafahamu
ingawa ni miaka mingi hawajaonana.
Mtoto
wa Mzee Olotu Ahmed ni makamo yangu na tulicheza pamoja utotoni kwa kuwa nyumba
zetu zilikuwa jirani Moshi Mtaa Chini.
Mzee
Olotu alifurahi kusikia naandika kitabu cha historia yao wapigania uhuru wa
Tanganyika. Akanieleza kuwa walipita watu kwake miaka michache iliyopita
wakitokea CCM na wakachukua nyarakza zake zote na picha wakidai kuwa
wanakusanya nyaraka hizo na picha kwa ajili ya kuandika historia ya TANU na pia
kutoa kifuta jasho kwa wale waliokuwa mstari wa mbele kupigania uhuru wa
Tanganyika.
Kwa
masikitiko alinieleza kuwa hakuna kilichofanyika na hata alipokwenda ofisi ya
CCM kuomba angalau wamrudishie nyaraka na picha zake aliishia kuzungushwa.
Tukaanza
mazungumzo huku kinasa sauti change kikizunguka taratibu.
Mzee
Olotu alikuwa anasumbuliwa na kikohozi lakini alianza kuzungumza kwa utaratibu
baada ya kuwaambia watoto wake waliokuwa nje kuwa ana mgeni muhimu na hataki
kusumbuliwa.
Hatukufika
mbali katika mazungumzo mvua kubwa ikaanza kunyesha ikasindikizwa na radi…
Kwa
miaka mingi kila nilipokuwa namsikiza Mzee Olotu katika kinasa sauti changu na
nikisikia vile akinyamaza kuzungumza kwa ajili ya kikohozi kisha akireja
kueleza historia ya uhuru sauti yake ikiingiliana na radi nilikuwa najiuliza –
ile radi ilikuwa inaashiria nini?
Nilikuwa
Arusha baada ya miaka kupita ndipo nilipopata taarifa kuwa Mzee Olotu amefariki
na kazikwa jana yake.
Niliondoka
siku ya pili yake kwenda Moshi kuhani.
Nasikitika
kuwa Mzee Olotu hakukiona kitabu ambacho kimemtaja yeye na wenzake katika kuunda
TANU Kilimanjaro, mwaka wa 1955 na kupigania uhuru wa Tanganyika.
MS
MS
Historia ya harakati za kudai uhuru wa Tanganyika kama
walivyoshiriki wananchi wa Kilimanjaro haiwezi kamwe kukamilika bila ya kutaja
jina la Yusuf Ngozi achilia mbali mchango wake katika kuipa TANU ushindi katika
uchaguzi wa kura tatu. Jina hili la Ngozi alilipata kwa kuwa alikuwa akifanya
kazi katika kampuni ya kuuza ngozi. Uchagga ilikuwa chini ya utawala wa machifu
waliokuwa wakijulikana kama Mangi. Baadhi ya machifu hawa walikuwa katika
Baraza la Kutunga Sheria na kwa ujumla wao walikuwa karibu na serikali ya
kikoloni kuliko walivyokuwa na wananchi wanaowaongoza. Hali ya siasa katika
Jimbo la Kaskazini ilikuwa ngumu na ya kukatisha tamaa. Wakati TANU inakabiliwa
na Kura Tatu mgogoro wa ardhi ya Wameru ulikuwa umekwisha kwa wananchi
kudhulumiwa haki yao. Japhet Kirilo alikuwa tayari amerudi mikono mitupu kutoka
Umoja wa Mataifa alikopeleka madai ya Wameru.
![]() |
| Chief Marealle, Chief Maruma na Chief Shangali |
Kirilo hakuwa na chochote cha kuwaonyesha
Watanganyika. Ilikuwa Yusuf Ngozi ndiye aliyeweza kuifanya TANU iingie
kwanza Moshi mjini kwa vishindo na kutoka hapo akaieneza vijijini. Kupitia
kumbukumbu za Mzee Yusuf Ngozi ndipo unapokutana na historia za awali kabisa za
wanasiasa maarufu waliopata majina na vyeo na wengine kuwa mawaziri katika
Tanganyika huru. Mfano wao ni Lucy Lameck, Enesmo Eliufoo na wengineo. Ilikuwa
ni Yusuf Ngozi pamoja na wazalendo wengine walioifanya TANU ishinde uchaguzi wa
kura tatu mwaka 1958. Kupitia kumbukumbu zake halikadhalika ndipo kwa huzuni
kubwa utakapokutana na mashujaa waliosahaulika kama yeye mwenyewe, mashujaa wa
kike na wa kiume na wazalendo kama marehemu Mama Bint Maalim, Amina Kinabo,
Halima Selengia, Juma Ngoma, Melkezedek Simon, Gabrieli Malaika na wengineo.
Hawa ndiyo mashujaa ambao kwa muda waliamua wasahau nguvu na utawala wa machifu
wao na kujiweka chini ya TANU.
Habari za kuenea kwa TANU Kilimanjaro na matatizo ya Kura Tatu
zimeelezwa na Yusuf Olotu katika mahojiano aliyofanya na mwandishi nyumbani
kwake Moshi tarehe 21 Januari, 1989. Yusuf Ngozi alimfahamisha mwandishi kuwa
ofisi ya CCM Wilaya, miaka michache iliyopita walimuandikia barua kumuomba
awape nyaraka zake zote za mwanzo kuhusu TANU na awaandikie historia ya jinsi
chama kilivyoenezwa Kilimanjaro na mchango wake binafsi. Kazi hii aliifanya na
akakabidhi nyaraka hizo kwa CCM. Yusuf Ngozi alimfahamisha mwandishi kuwa
alidokezwa kuwa nia ya zoezi hilo ilikuwa ni kuweka kumbukumbu za mashujaa wa
harakati za uhuru ili wapate kuenziwa na taifa na wale ambao hali zao za
kimaisha si nzuri wasaidiwe na chama. Yusuf Olotu alifariki dunia tarehe 3 Juni,
1997 akiwa na umri wa miaka sabini.
Yusuf Ngozi hakuwa na elimu bali alikuwa mwananchi wa kawaida
aliyethamini utu wa Mwafrika na mtu aliyechukia dhulma na fedheha ya
kutawaliwa. Kilimanjaro ilikuwa inasifika kwa kuwa na Waafrika waliokuwa na
elimu ya juu kabisa katika Tanganyika. Lakini wasomi hao walishughulishwa zaidi
na maslahi yao binafsi. Wengi wao walikuja kujitokeza na kuingia chama cha TANU
mwaka 1958 katika uchaguzi wa kura tatu. Wakati huo mambo yalikuwa shwari na
Waingereza walikuwa wamesalimu amri. Yusuf Ngozi labda kwa kuelewa mazingira ya
Kilimanjaro alianza kujenga msingi wa TANU si kwa wanaume bali kutoka kwa akina
mama. Hiki ni kitu azizi sana katika historia ya kupigania uhuru. Katika
historia ya TANU sehemu ambazo chama kilipata nguvu kubwa sana ni zile sehemu
ambazo kulikuwa na utamaduni wa Kiswahili wa vyama vya akina mama kama hapo
Moshi mjini, Dar es Salaam, Tanga, Lindi na kwingineko.
Joseph Kimalando aliogopa kuitumikia TANU lakini alijiona
amesalimika kuifanyia kazi United Tanganyika Party (UTP) – chama cha Wazungu
kilichoundwa kuipinga TANU. Kimalando alikuwa katibu wa UTP Moshi na Mohamed
Kishikio Badi alikuwa mwenyekiti wake. Yusuf Ngozi aliwahamasisha wanawake wa
Moshi chini ya Mama bint Maalim kuipiga vita UTP hadi ikafa. Wanawake wale
walikuwa wakizikusanya kadi za UTP na kumpelekea Mzee Yusuf Ngozi kwenye ofisi
ya TANU. Yeye kama njia ya kuwakatisha tamaa na kuwapiga vita vya kisaikolojia
UTP alikuwa akichukua marundo kwa marundo ya kadi za UTP na kumpelekea rais
wake Mohamed Badi kumhakikishia kuwa wananchi walikuwa hawakitaki chama chake
cha vibaraka.
Yale masharti ya Kura Tatu yaani kipato, elimu na kazi ya maana,
kwa wapiga kura na wagombea hayakuwasumbua Wachagga wengi kwani wao kama
tulivyoona walikuwa ni watu waliokuwa na elimu na vipato vya kutosha. Kwa
maneno mengine sheria ile (ambayo kwa sehemu nyengine kama vile Bagamoyo
ilikuwa ngumu) kwa Wachagga ilikuwa nyepesi na hivyo kuruhusika kupiga kura
pasi na pingamizi. Lakini kwa bahati mbaya sana iliingia fikra kuwa masharti
yale ya kupiga kura na hasa kile kipengele cha kipato ilikuwa njama ya serikali
ya wakoloni kutengeneza orodha ya Wachagga ili wawatoze kodi ya mapato. Wachagga
ni wafanya biashara na wenye bidii katika kilimo.
Hiki kipengele cha kipato kiliwaweka wana - TANU wa Uchaggani –
wafanyabiashara, wafugaji na wakulima wa kahawa katika hofu kubwa. Hulka ya
kuthamini mali ilikuwa imefifilisha umuhimu mzima wa watu wa Kilimanjaro kupiga
kura ili TANU ichukue viti katika Baraza la Kutunga Sheria. Tatizo la Uchaggani
sasa likawa ni la kipekee. Kazi kubwa hapa ilikuwa ni kubadilisha fikra za watu
na kuwatoa hofu ya kulipa kodi kwa mali zao na kuwafanya kuona ukweli na umuhimu
wa kuishinda UTP na kumng’oa Mwingereza Tanganyika. Hili lilikuwa tatizo ambalo
TANU hawakukutana nalo mahali popote katika Tanganyika. Hata katika mkutano wa
Tabora kujadili juu ya Kura Tatu hakuna kumbukumbu yoyote inayoonyesha kuwa
kuna Waafrika ambao watashindwa kutumia haki yao ya kupiga kura kwa kuwa na
fedha nyingi. Tatizo ilikuwa ni kinyume chake. Tatizo la TANU katika majimbo
mengine lilikuwa ni kuwafanya watu wakubaliane na masharti yale magumu ya
kibaguzi katika kupiga kura ili chama kiingie katika uchaguzi.
Katika hali ya kawaida mtu angalitegemea kuwa watakaosimama ni
wale wasomi wa Makerere kuwaeleza wananchi hali ya mambo na mwelekeo wa nchi.
Katu hao hawakusimama. Alikuwa Yusuf Ngozi aliyehamasisha. Alitembea
Kilimanjaro nzima na kuwaeleza watu kuwa kama hawatajiandikisha kuipigia kura
TANU na kumuunga mkono Mwalimu Nyerere katika vita dhidi ya Waingereza basi
wajue kuwa UTP itashinda na Waingereza wataendelea kuitawala nchi hii. Sehemu
nyingine alikuwa akiwafahamisha Waafrika wenye biashara ndogondogo kuwa wao
vilevile wana kazi na kipato kinachokidhi masharti ya upigaji kura kwani hesabu
zao za mwaka zilikuwa zinapita kile kiwango cha pauni mia nne (400). Aliikuta
hali hii kwa mafundi cherehani huko Kahe – kijiji kidogo nje ya Moshi. Mafundi
hawa walijihesabu hawana kazi ya maana wala kipato cha pauni 400 kwa mwaka.
Mzee Yusuf Ngozi aliwasomesha na kuwaonesha kuwa walikuwa na kazi ya maana na
kipato cha kutosha. Hivyo aliwanasihi wasiache kujiandikisha na kuipigia kura
TANU. Sehemu nyingine Yusuf Ngozi alikuwa na propaganda yake ya kutisha.
Alikuwa akiwauliza wananchi kama wao walikuwa wako tayari kuishi katika nchi
yenye bendera tatu. Katika Jimbo la Kaskazini TANU ilimsimamisha Enesmo Elufoo.
![]() |
| Sophia Mustafa |
Eliufoo kwa kiti cha Moshi na Sophia Mustapha alisimamishwa
Arusha. Yusuf Ngozi aliifanyia kampeni TANU kwa ufanisi mkubwa na TANU iliweza
kushinda kwa kura nyingi sana na wajumbe wake kuingia katika Baraza la Kutunga
Sheria.TANU ilishinda ule uchaguzi wa kura tatu. UTP ambayo ilikuwa na nguvu
sana huko Tanga ilikiri kushindwa. David Emmanuel mwenyekiti wa UTP akitambua
ukweli kuwa hakukuwa na mategemeo yoyote kwa chama hicho pale Tanga na kama
ishara ya pekee kabisa ya ukarimu na moyo wa kutaka maelewano mema, alikusanya
samani yote iliyokuwa ndani ya ofisi ya UTP na kuitunukia TANU.
NB
Kwa maelezo kamili kuhusu Uchaguzi wa Kura Tatu
angalia The Tanganyika Gazette Vol. XXXIV No. 48 26 September, 1958. Vilevile
Sauti ya TANU No. 25 Septemba, Uchaguzi wa mwaka 1958 ulifuatiwa na uchaguzi
mwingine mwaka 1959 ambao TANU ilishinda.



No comments:
Post a Comment