Utangulizi
![]() |
| Waumini wakiwa nje ya msikiti palipofanyika mauaji |
Yaliyotokea Mwanza jana katika sala ya Isha ni kitendo ambacho hakijapatapo kutokea Afrika ya Mashariki nzima. Waislam waliokuwa wakiswali sala ya Isha walivamiwa katika sijda na watu walioficha nyuso zao wakapigwa mapanga. Watu watatu wameuawa hapo hapo ndani ya msikiti. Tumepokea mikono mingi ya taazia katika ukumbi huu kuanzia jana hadi hii leo. Mmoja katika ndugu zetu katuletea taazia ya aina yake. Kafungamanisha katika mkono wake wa pole na makala hii ambayo Sheikh Ali Muhsin Barwani aliandika kama indhar kwa umma wetu huu kuhusu khatari za farka.
Nami naziweka hapa nasaa za marehemu Sheikh Ali Muhsin:
Nami naziweka hapa nasaa za marehemu Sheikh Ali Muhsin:
“Na mwenye kumuuwa
Muumini kwa kukusudia, basi malipo yake ni Jahannamu humo atadumu, na Mwnyezi
Mungu amemlaani, na amemuandalia adhabu kubwa.”
(Annisaai: 93).
Ole
wao walioingia kuwauwa ndugu zao Waislamu kwa makusudi na bila ya kosa lolote.
Watu
kuzidi kuelimika na kuchanganyika kwa kila yao, wanafahamu ya kwamba kwa hakika
hakuna chenye kutafautisha hivyo baina ya Sunni na Ibadhi. Ilivyo katika
Usuul-l-Fiqh, Ibadhi inafundisha na kufuata zilezile zilizomo katika kitabu
cha Imam Shaafii, Arrisala. Mufti wa Oman, Sheikh Ahmed
bin Muhammad Al Khalili; ameeleza ya kwamba hakuna moja lenye kufuatwa na
Ibadhi ambalo halifuatwi na moja kati ya madhehebu manne ya Sunni. Oman na pia
Zanzibar Sunni na Ibadhi wanasali msikiti mmoja, wanaowana na wanashirikiana
kwa kila lao bila ya kuhisi taabu na bila ya ubaguzi wowote ule. Unaweza
kuingia msikitini na ukamfuata Imam katika Salaa na kumaliza na bila ya kujuwa
ni wa Madhehebu gani. Sio sivyo ukisema ya kwamba Ibadhi sawa na Sunni, ni Ahli
Sunnah, kwa sababu Hadithi za Mtume wetu mpenzi s.a.w. ndio marejeo ya pekee
baada ya Qur’ani Tukufu kwa Waumini wote. Hili neno Sunni halikuwa
likitumika isipokuwa mnamo karne ya saba baada ya Hijra, hivi ni muda mrefu
kupita baada ya Maimamu wote wanne wa Sunni kufariki, yaani Imam Hanafi, Imam Malik,
Imam Shafii na Imam Hambal. Wote hawa wakati wa
uhai wao, na pia Maimamu wa Kiibadhi, Jabir bin Zayd, na Abdulla
bin Ibadh, walikuwa wakijuulikana kwa jina la Imam Muslimiina (Imam
wa Waislamu). Hivi hivi ndivyo hali ilivyokuwa kwa Maimam wakubwa wa
Kishia, Imam Muhammad Al Baqir, Jaafer Assadiq, na Zayd
bin Ali. Waislamu wote walikuwa wakiwaendea Maimamu wote hawa kwa uwongozi
wao na kusoma kwao.
Ni
hakika ya kwamba utaratibu wa mtu kujifungia katika fikra zake na upungufu wa
ilimu ulisababisha kuwepo vizingiti kuzuia watu kufahamu yaliomo katika
madhehebu mbalimbali, haya ndivyo yalivyokuwa Zanzibar na Oman pia. Hali hii
ilikuwa zaidi sehemu za ndani sana huko Oman kuliko ilivyokuwa visiwani
Zanzibar. Mwenyezi Mungu Mtukufu amjazi kheri kwa kazi yake ya faida sana
alioifanya mwanazuoni maarufu wa Kiibadhi wa Algeria, Sheikh Muhammad
bin Yusuf Al It’feish, kwa yale maelezo yake katika Qur’ani katika kitabu
chake Sharh Nnil, kitabu cha Fiqh, kwa kazi zake adhimu hizi mengi
yaliokuwa yakisababisha mfarakano baina ya madhehebu yaliweza kubainishwa
hakika yake na kuondolewa. Kazi hii hivi leo inaendelezwa na Mufti wa Oman,
Sheikh Ahmed bin Muhammad Al-Khalili. Khatua kubwa na ya
kishujaa aliichukuwa Sultan Qaboos pale alipotowa amri yake ya
kusaliwa Salaa ya Ijumaa Oman. Kwa karne, Ibadhi wa Oman na hata waliokuweko katika
Afrika Mashariki walikataa kusali Salaa ya Ijumaa kwa kuwa ati ni aibu kwao.
Wakifanya hivi kutekeleza fikra za baadhi ya wanazuoni wao ambao walishindwa
kutambuwa maamrisho ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kama yalivyo ndani ya Qur’ani
Tukufu. Hakuna Salaa iliotajwa kwa uwazi kabisa katika Qur’ani kuliko Salaa ya
Ijumaa. Sura nzima imepewa jina la “Surat Al-Jum’a”:
“Enyi mlio amini! Ikiadhiniwa
Sala siku ya Ijumaa, nendeni upesi kwenye dhikri ya Mwenyezi Mungu, na wacheni
biashara. Hayo ni bora kwenu, lau kama mnajua”.
(Al-Juma’: 9)
(Al-Juma’: 9)
Kwa
hii amri yake Sultan Qaboos ya kuwataka Ibadhi wasali Sala ya Ijumaa iling’oa
kisingizio kilichokuwa hakikuwa na msingi na kuwaweka Maabidhi sawa na ndugu
zao wa madhehebi yote katika kutekeleza maamrisho ya Mwenyezi Mungu Mtukufu,
khasa hii Sala ya Ijumaa. Hivi leo Ibadhi hajioni kuwa ni tafauti na mwenziwe
yeyote yule au haoni kuwa sivyo kusali na asiekuwa Ibadhi mwenziwe. Ibadhi hivi
leo wameweza kufuta kabisa zile tuhuma ambazo hazikuwa na ukweli wowote ule
kuwa ati Ibadhi inatokana na Khawaarij. Alhamdulillah, leo sio tu ya kwamba
wanasali pamoja Sala ya Ijumaa bali Sala zote tano katika wiki nzima wanasali
pamoja bila ya tafauti yoyote ile. Kwa upande wao, Masunni na wao wanazidi
kutambuwa ya kwamba hakuna tafauti yoyote ile ya kimsingi baina ya Ibadhi na
Sunni. Kwa hakika hata hizo tafauti ziliopo baina ya Sunni na Shia, sio tafuti
katika mambo ya misingi ya dini. Nyingi ya tafauti hizi asili yake ni mambo ya
kisiasa na taarikh ya kale, leo hayana tena pahala katika Waumini. Wenye busara
miongoni mwa wanazuoni wa madhehebu mbalimbali wanasisitiza ya kwamba umefika
wakati Waumini tujivue hizi pingu za mfarakano katika dini yetu zilizo
sabibishwa na mambo ya kisiasa na taarikh ya kale ambayo hayana msingi wowote ule.
Wanazuoni maarufu wenye busara na maarifa wameandika kukhusu juhudi za kuondoa
mfarakano wa madhehebu katika Uislamu, tafadhali tusome kitabu cha Dr. Mustafa
Shak’a: “Islamu Bilaa Madhaahib” (Uislamu
Bila ya Madhehebu), vilevile tusome kitabu cha Dr. Moosa Al I’sawy: “Ash-shiia
wa Ttas-hih”, kitabu cha Sheikh Shaltout: Al-Islam
A’qidatah wa Sharia’h” (Uislamu A’qida na Sharia).
Katika Qur’ani mumejaa Aya zenye kuhimiza umoja wa Waumini na kukataza
mfarakano wa aina yoyote ile, khasa wa madhehebu. Ametueleza Mwenyezi Mungu
Mtukufu:
“Hakika walio igawa Dini yao na wakawa makundi makundi,
huna ukhusiano nao wowote. Bila ya shaka shauri yao iko kwa Mwenyezi Mungu;
kisha atawaambia yale waliokuwa wakiyatenda.”
(Al-Ana’am: 159)
Kisha
akatueleza Mwenyezi Mungu Mtukufu uovu wa wale wenye kuigawa dini makundi
makundi na vile kuwa kila kikundi hufurahia yale yalio yao:
“Muwe wenye kutubia kwake, na mcheni
Yeye, na shikeni Sala, na wala msiwe katika washirikina. Katika wale ambao
kwamba wameigawanya dini yao, na wakawa makundi makundi, kila kikundi
kinafurahia kilicho nacho.”
(Ar-ruum: 31-32)
Ikiwa
kuna Bid’a iliyotoka nje kabisa na maarisho ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, basi ni
vile kuzusha mfarakano; hata ikiwa mfarakano huo umekuja kwa kile kisingizio
cha kupigana na Bid’a.
Kwa hakika Mwenyezi Mungu Mtukufu anatakaza mfarakano katika dini - wacha baina
ya madhehebu, kama vile dini ya Kibudi, Ukiristo na Uislamu, zote hizi kwa vile
asili yake ni kitu kimoja. Ametueleza Mola wetu Mlezi:
“Amekuamrisheni Dini ile ile aliyo
muusia Nuhu na tuliyo kufunulia wewe, na tuliyo wausia Ibrahim na Musa na Isa,
kwamba shikeni Dini wala msifarikiane kwayo...” (Ash-shura: 13).
Inasikitisha
kuona ya kwamba mpaka hii leo wako baadhi ya watu wenye fikra potofu ambao
wanavuka mipaka katika kushindana na kugombana kwa ajili ya kuthibitisha
tafauti za kimadhehebu na kuzifanya kama kwamba ni zenye muhimu katika dini,
hufanya hivyo hata kufika kutumia Qur’an na Hadithi za Mtume (SAW). kwa kutaka
kuthibitishia mawazo yao. Hivyo ndivyo walivyokuwa Wafarisayo (wanafik wa
Kiyahudi) miongoni mwa Mayahudi, Sayyidna Isa a.s. moja kwa moja
alikataza vitendo vyao hivyo. Kwa hakika wenye kufanya hivyo ilivyo khasa ni
kwamba bila ya wao kutambuwa wanaleta uharibifu katika Uislamu kwa jumla na kwa
hayo madhehebu wanayo jinasibisha nayo. Wenye ilimu na maarifa miongoni mwetu
ni busara kutowaachilia watu wenye fikra potofu kama hao kuvunja juhudi
zinazofanywa katika kujenga na kuimarisha mafahamiano mema baina ya binadamu,
ikiwa ni katika dini au baina ya madhehebu.
Kuweko
misikiti ya zamani sana, kama ile ilioko Kilwa Kisiwani katika
Tanganyika, Ndagoni Pemba, Kizimkazi na Tumbatu
Zanzibar, na Gedi katika Kenya, ni ushahidi wa kutosha
kuthibitisha ya kwamba Uislamu umefika katika Afrika Mashariki kwa karne na
karne nyuma. Sisi tulikwisha kuwa Waislamu hata kabla ya mtindo wa
kujigawa Waislamu vikundi vikundi na kuingizwa kwa madhehebu katika
dini. Waislamu badala ya kujinasibisha kuwa ni Waislamu na kufuata Uislamu kama
ulivyokuja, wameona ni ndivyo kuwania na kujinasibisha na madhehebu. Kwa karne
nyuma watu wa Afrika Mashariki walisalimika na hii balaa ya mfarakano wa
madhehebu ambao umekuwa kwa muda sasa unabomowa umoja wa Waislamu katika sehemu
nyingi za ulimwengu.
Yalikuweko
katika Zanzibar madhehebu mbalimbali, hakukuweko mivutano au mashindano ya
kimadhehebu. Japokuwa sehemu kubwa ya wakaazi wa sehemu hizi walikuwa “Sunni”,
na kwa muda wa miaka mia mbili waliokuwa wakihukumu ni Ibadhi. Wakihukumu
kutoka Zanzibar na kwa nufudhu kubwa ilioenea Afrika Mashariki na ya Kati, na
wakiwemo sehemu ndogo kabisa ya wakaazi wa Kishia, wengi wenye asili ya Kiasia.
Juuyayote haya, hapakuwepo ubaguzi wowote wala mvutano wowote baina yao kwa
sababu ya hivi kuwa wa madhehebu mbalimbali.
Katika
Afrika Mashariki mingi ya misikiti imejengwa na Ibadhi, ambao pia walijenga
vyuo na kuwasaidia kimaisha wengi wa walimu wa vyuo hivyo. Yote haya wakitenda
kwa ajili ya manufaa ya watu wote, wengi wao wakiwa ni Sunni. Haikupata kutokea
kuwa madhehebu yoyote yale kutaka kumgeuza Muislamu yeyote yule kutoka
madhehebu na kuingia madhehebu mengine. Haikutendwa hivyo kwa nguvu, au
kwa kulaghai kama vile kwa kuwarubuni kwa vyeo, au vijizawadi, au kwa kuwapa
fursa za safari za nje.
Mmoja
wa wazee wangu ndie alieanzisha mji na bandari ya Lindi, alianzisha
mji na bandari hii kwa kufyeka pori na kukata mikoko. Wakaazi wa sehemu hizi, Wamakonde walioonesha
imani yao ya kuwa Waislamu, yeye mzee wangu ambae alikuwa ni Ibadhi alikwenda
kumleta Sheikh Omar Stambuli kutoka Malindi Kenya ili
aje awafundishe Wamakonde Uislamu na Sharia zake. Sheikh Omar alikuwa ni
mwanazuoni wa Kisunni. Haikumpitikia mzee wangu huyo kuwa ni muhimu amlete
mwanazuoni wa Kiibadhi kwa wajibu huu. Kama angelitaka kufanya hivyo, basi
angeliweza kupata mwanazuoni huyo kutoka Zanzibar au hata kutoka Oman na
kueneza Uibadhi. Lililokuwa muhimu kwake sio madhehebu yake, bali ni dini yake. Uislamu
unapinga mfarakano wa kimadhehebu. Kwa kuzidi Mwenyezi Mungu Mtukufu
kutukataza mfarakano na kutuhimiza juu ya dharura ya kushikana sote pamoja na
kuepusha mfarakano, ametwambia Mola wetu Mlezi, Subhaanahu wa Ta'aala:
“Na shikamaneni kwa Kamba ya Mwenyezi
Mungu nyote pamoja, wala msifarikiane. Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu iliyo
juu yenu: vile mlivyo kuwa nyinyi kwa nyinyi maadui naye akaziunganisha nyoyo
zenu; kwa neema yake mkawa ndugu. Na mlikuwa ukingoni mwa shimo la Moto, naye
akakuokoeni nalo. Namna hivi Mwenyezi Mungu anakubainishieni Ishara zake ili
mpate kuongoka.”
(Al ‘Imraan: 103).
Na
akaendelea Mwenyezi Mungu Mtukufu kutueleza katika Sura hii hii juu ya haja na
dharura ya watu kuwa wamoja na kuepukana na mfarakano na waweko miongoni mwetu
wenye kuamrisha kutenda mema na kukataza kutenda uwovu:
“Na uwe kutokana na nyinyi umma
unao lingania kheri na unao amrisha mema na unakataza maovu. Na hao ndio walio
fanikiwa. Wala msiwe kama wale walio farikiana na kukhitalifiana baada ya
kuwafikia hoja zilizo wazi. Na hao ndio watakao kuwa na adhabu kubwa”.
(Al ‘Imraan: 104-105).
“Kulingania
kheri”, maana yake ni
kulingania binadamu wawe wamoja, sio kufariqiana vikundi vikundi na madhehebu
madhehebu; sio kufariqiana baina ya ndugu - Waumini. Kulingania kheri sio
kutukanana, wala sio kutuhumiana wenyewe kwa wenyewe. Kulingania kheri muhimu
na kukuu kwenye kuhitajika ni kwamba sote tuwe kitu kimoja bila ya mfarakano wa
aina yoyote ule. “Kukatazana maovu”, ni kukatazana kila lile
ambalo ni ovu kwa binadamu, na ambalo linaondoa mafahamiano mema baina ya
viumbe. Kama tunavyoona hapo juu, adhabu kubwa itawafikia wale wenye
kufariqiana na kukhitalifiana baada ya kuwa ushawafikia uwongofu na maamrisho
ya Mwenyezi Mungu Mtukufu ya kutakiwa wawe wamoja. Adhabu ya Mwenyezi Mungu
Mtukufu huanza kuwafika viumbe vyake tangu hapa ulimwenguni. Ni wajibu wetu
tujihisabu kabla ya kuhisabiwa, hivi ili tuweze kujuwa makosa yetu ili tupate
kujisahihisha, na kutenda mema. Wema hufuta uwovu:
“Mambo mazuri na mabaya hayawi sawa.
Ondosha (ubaya unaofanyiwa)
kwa mema; tahamaki yule ambaye baina yako na baina yake kuna uadui atakuwa kama
ni jamaa (yako) mwenye kukufia uchungu. Lakini (jambo hili) hawatapewa ila wale
wanaosubiri, wala hawatapewa ila wenye hadhi kubwa (kwa Mwenyezi Mungu).” (Fusilat: 34 –35).
Uislamu
sio dini mpya, Uislamu ni mchanganyiko wa dini zote alizoziteremsha Mwenyezi
Mungu Mtukufu kwa viumbe vyake; mchanganyiko wa dini zote ili viumbe vyote wawe
ni kitu kimoja. Uislamu unakataza hata kuwatukania makafiri waungu wao, ili
kuepusha na wao kwa ujinga wao kumtukana Mwenyezi Mungu Mtukufu:
“Wala
msiwatukane hao wanao waomba badala ya Mwenyezi Mungu, wasije na wao
wakamtukana Mwenyezi Mungu kwa jeuri bila ya kujua. Namna hivyo tumewapambia
kila umma vitendo vyao. Kisha marejeo yao yatakuwa kwa Mola wao Mlezi, naye
atawaambia waliyo kuwa wakiyatenda”.
(Al
An-‘aam: 108).
Leo
imefika kuwa baadhi ya Waislamu wanawatukana Maimamu wa wenziwao, bali wamefika
hata kuwatukana baadhi ya Masahaba wa Mtume wetu mpenzi s.a.w. Huu sio Uislamu.
Tafadhali isome Qur’ani kama vile imeteremshwa kwako weye khaasa. Isome Qur’ani
na izingatie vyema maana yake. Tuisome Qur’ani na tujitahidi kuifuata na
kutekeleza maarisho yake na kujiepusha na yale tunayokatazwa kama tunavyoweza. Ni
ndivyo kuongozwa waliokosea Njia, lakini sio kwa kutukanana. Kuongozana ni kwa
njia ya upole, maarifa, busara na kustahamiliana, ametwambia Mola wetu Mlezi:
“Waite waelekee kwenye Njia ya
Mola wako Mlezi kwa hikima na mawaidha mema, na ujadiliane nao kwa namna iliyo
bora....”.
(Annahal: 125).
Hao
waliofarikiana na kugawana vikundi vikundi, hao ndio sisi tulivyo hii leo.
Natija yake imekuwa tumejidhuru wenyewe na kujifanya kuwa ni dhaaifu baada ya
kuwa tumeletewa Uwongofu. Uislamu haujaja kwetu jana. Tangu ulipoteremshwa sisi
tulikuwa Waislamu. Juuyahivyo imekuwa leo sisi ndio wenye kufarikiana na
kuzozana juu ya mambo ambayo sio ya kimsingi wala yenye faida yoyote katika
dini yetu. Mambo ambayo yameletwa kwetu na watu ambao ni hii leo tu ndio
wamekuwa Waislamu. Wametuletea sababu hizi za kufariqiana kwa maslaha yao wao
wenyewe binafsi au kwa maslaha ya fikra zao dhaifu za kikabila au kimadhehebu.
Kwa ajili ya kutekeleza na kuendeleza maslaha yao hayo ndio wanasababisha
mfarakano baina yetu. Wao wanachotaka ni wafuasi na wahami wa fikra na vitendo
vyao miongoni mwetu sisi. Wao hawataki kueneza Dini ya Mwenyezi Mungu Mtukufu
Lillahi Ta’ala. Ni wajibu wetu tutahadhari na Siku itakapofika na Mwenyezi
Mungu Mtukufu kutuuliza: “Je! Mlikufuru baada ya kuamini kwenu?”
Mlikhitalifiana baada ya kukufikieni Uwongofu kutoka Kwangu?
Inatupasa
tutahadhari na wale ambao - japokuwa ni wachache - wanataka kutubabaisha fikra
zetu kwa njia hii au nyengine na kuleta mfarakano baina ya Waislamu wa Afrika
Mashariki. Mwenyezi Mungu Mtukufu
atujaalie tuwe wenye kushikamana kwa Kamba Yake ili tupate kumqabili Siku ya
Hisabu na hali yakuwa nyuso zetu ni zenye kung’ara kwa Rehema Zake – Aamyn!
Sisi
ambao tulikuwa wenye kupigiwa mfano kwa jinsi tulivyo shikamana na kuwa wamoja.
Wamoja kwa kila njia na maana, leo na sisi tume jitumbukiza katika hii balaa ya
mfarakano. Leo tumekuwa huyu anamtukana huyu kwa kisingizio cha “Bid’a” na yule
anamtukana yule na kufika kumwita ni kafiri. Huu sio Uislamu, wala sivyo
ulivyofundisha Uislamu. Kukhitilafiana rai Maimamu katika mambo ya Fiqh isiwe
ndio sababu ya sisi kuleta mfarakano baina yetu na kufika kuwacha tabia yetu ya
ustahamilivu na kuchukuliana. Kukhitilafiana rai katika mambo madogo madogo
(ambayo sio ya misingi) hakutaacha kuwepo. Kwa hikika hivyo ni rehema kwa
Waumini, madhali hatutoki katika misingi ya Dini yetu. Khitilafu katika Fiqhi
au katika kuifahamu taarikh kusiwe ndio sababu ya bughdha na kujenga mfarakano,
mvutano na adawa baina yetu.
Hebu
natuizingatie hali ya Zanzibar ilivyokuwa kabla ya nchi yetu kuvamiwa na kumezwa
na kufisidiwa kila kitu. Mfalme alikuwa ni Ibadhi. Sehemu kubwa ya Umma
walikuwa ni Sunni. Sehemu ndogo walikuwa ni Shia. Juuyahivyo, katika kalenda ya
Serikali kuliwekwa siku mbili kuwa ni siku za kufungwa kazi serikalini, mwezi
21 Ramadhani, siku aliouliwa Imam Ali r.a. na mwezi kumi Muharam,
siku aliouliwa Imam Hussein r.a. Nchi ngapi ambazo zinafanya hivi kwa
kuhishimu wananchi wao ambao ni sehemu ndogo kabisa ya wananchi. Hatuoni hayo
kufanyika hata katika zile nchi ambazo Shia ni nusu ya wananchi wa nchi hizo.
Watu
wa Afrika Mashariki wamepata faida kubwa kutokana na ukarimu wa aila ya Karimjee
Jivanjee, Bwana ambae ametujengea hospitali, nyumba za wazee waliokuwa
hawana njia za kujisaidia, mwahala mwa kujumlikia na klabu mbalimbali. Aila
ya Karimjee inatokana na Mabohora ambao ni Shia. Ukarimu wao umewafaa kila
mtu, sio basi Waislamu. Kwani kuna Mabohora wangapi katika Afrika Mashariki
hata iwe ukarimu wao huo wanakusudiwa wao tu? Hata huko Zanzibar Mabohora ni
wachache kabisa.
Siwa
Hajee, ni Shia wa Kismailia,
wao ndio wafuasi wa Aga Khan, yeye ndie aliejenga hospitali ya mwanzo
Zanzibar na akajenga nyengine huko Dar es Salaam. Ismaili mwengine, Tharia
Topan, yeye aliwacha Wakfu ambao ndio ukaasisiwa Madrasa katika Msikiti Barza,
wa Sunni; na misikiti mingine mingi ilijengwa kutoka na mali yake
alioiwacha kwa makusudio hayo. Kwa bahati yeye Bwana Tharia Topan alikuwa ni
waziri wa Sayyid Barghash. Watu wasiofadhila wamefika hata kufuta majina ya hao
mabwana waliofanya kheri hizo juu ya majengo walioyajenga, kama vile jina la Karimjee kwenye
hospital ya Mnazimoja. Hospitali aliwajengea wananchi wa Zanzibar, badala yake
wavamizi wakaiita hospitali hio kwa jina la V. I. Lenin, mtu ambae sisi hatuna
makhusiano nae hata chembe. Kuzidisha msumari wa moto juu ya kidonda kwa bwana
karimu huyu, Sir Tayabali Karimjee, wavamizi wakamnyang’anya nyumba
yake ambayo ndiyo aliokuwa akiishi yeye na aila yake na ndiyo aliokusudia aishi
humo katika utuuzimani mwake na kumalizia uhai wake. Kwa kufikishwa katika
idhlaali ya hali hii, yaani kunyang’anywa nyumba yake na kuachwa hana pakukaa,
ilimlazimu aihame nchi yake - Zanzibar - na kwenda kuishi ugenini, Pakistani na
kufia huko. Yeye Bwana Tayabali alikuwa ni mzaliwa wa tano wa
Kizanzibari. Hivi ndivyo sisi tunavyowalipa wale wanaotutendea kheri. Na hivi
ndivyo tulivyo mpaka hii leo. Huu ndio uungwana wetu. Mwenyezi Mungu Mtukufu
ametwambia ya kwamba tukimshukuru atatuzidishi neema zake, na tukimkufuru basi
adhabu yake ni kali:
“Na alipo tangaza Mola wenu
Mlezi: Mkishukuru nitakuzidishieni; na mkikufuru, basi adhabu yangu ni kali.”
(Ibrahim: 7).
Asieweza
kumshukuru binadamu mwenziwe basi huyo hamshukuru hata Mwenyezi Mungu Mtukufu.

No comments:
Post a Comment