Thursday, 13 February 2014

BAKWATA SEHEMU YA SITA

BAKWATA
Sehemu ya Sita
Wakati Tume ya Waislam inasubiri mawazo ya Waislam sasa kundi la Adam Nasibu wakijionesha wazi kuwa serikali na TANU ilikuwa nyuma yao, lilikutana kwa ajili ya kile walichokiita Mkutano wa Waislam wa Taifa ulioanza tarehe 13 Desemba, 1968. Serikali ikifanya kazi nyuma ya pazia ilijitahidi sana kuhakikisha kuwa mkutano ule unafanikiwa. Serikali ndiyo iliyotoa fedha za kufanyia mkutano ule, ukatoa vyombo vyake vya habari kwa ajili ya kuutangaza vizuri na ukatoa ulinzi kwa wajumbe wote.

Wajumbe waliohudhuria mkutano ule walikuwa kama mia mbili. Mkutano huu ulihudhuriwa na Waislam waliokuwa na vyeo katika serikali na TANU, Waislam waliokuwa wakuu wa wilaya na mikoa na Waislam wenyeviti wa TANU. Waislam wote wenye majina walialikwa, pamoja na Waislam waliokuwa katika halmashauri kuu ya TANU na baadhi ya wajumbe wa mkutano walitoka Zanzibar. Ulikuwa mkutano wa wanasiasa Waislam ambao ukitoa majina yao walikuwa hawana chochote katika harakati za Uislam isipokuwa majina yao. Lakini uzito wa mkutano huu ulitokana hasa na kuwa ulikuwa mkutano ambao ulitawaliwa na Waislam waliokuwa hawapendezi mbele ya macho ya umma wa Kiislam. Ni ukweli usioweza kupingika kuwa kama mkutano ule ungelikuwa hasa umetayarishwa kwa ajili ya kumtumikia Allah, ni wazi ungehudhuriwa na Waislam wa kweli na wenye historia ya unyenyekevu na mapenzi kwa dini yao. Waislam wa sifa hizi hawakuwepo katika mkutano ule ukimtoa Sheikh Mohamed Ramia wa Bagamoyo na wengine wachache ambao kwa kutotambua mambo waliitika mwito. Mkutano ulifunguliwa na Karume na kufungwa na Kawawa. Katika hotuba yake ya ufunguzi Karume alisema maneno haya:

Dini haiwezi kuwa nje ya siasa kwa sababu siasa ndiyo damu inayoipa jamii uhai wake. Wakati wa ukoloni wananchi na daini zao zilikuwa chini ya utawala wa wageni. Hivi sasa watu wamevua mabaki ya ukoloni pamoja na kutawaliwa kwa misingi ya dini. Kuanzaia sasa uongozi wa dini lazima ukwe chini ya wananchi wenyewe bila ya kuongozwa na kiongozi kutoka nje.

Mkutano wa Iringa ulipitisha katiba ya jumuiya mpya ya Waislam, katiba ambayo ilikuwa sawasawa na katiba ya TANU. Hivi ndivyo BAKWATA ilivyoundwa. BAKWATA ikamchagua Saleh Masasi, Muislam tajiri na ambae alikuwa kama mwenyekiti wa mkutano ule kuwa Mwenyekiti wa Taifa na Adam Nasibu akawa Katibu Msaidizi. Nafasi zote za juu katika BAKWATA kama ilivyotegemewa zilichukuliwa na kundi la Adam Nasibu, kundi ambalo toka mwanzo lilikuwa likidai kuvunjwa kwa EAMWS. Uongozi wa BAKWATA uliomba serikali itambue jumuiya hiyo mara moja na ipige marufuku EAMWS kama jumuiya isiyo halali na mali zake zizuiwe. BAKWATA ilitoa maazimio kadha lakini azimio namba nne ndilo hasa linafaa kuelezwa. Azimio hilo liliomba serikali, TANU na ASP kuwatazama na kufanya uchunguzi wa kina kwa viongozi wote wa EAMWS, hasa Rais, Makamo wa Rais, Katibu wao na baadhi ya viongozi wa mikoa na wilaya ambao wana chuki na hii jumuiya mpya. Uongozi wa BAKWATA katika ushindi wao hawakutaka salama na mawaelewano na Waislam wenzao katika EAMWS wala kuwaonea huruma kama Uislam unavyofundisha, bali ulitaka chama na serikali uwaandame, hasa wale waliokuwa viongozi.

Baada ya kuundwa BAKWATA, ili kuondoa wasiwasi na kuwarudishia imani Waislam, Katibu wa Tume ya Waislam, Mussa Kwikima alitoa taarifa iliyosema:

Hakuna anaeweza kutishia kuwepo kwa EAMWS isipokuwa wanachama wake, sheria na serikali, lakini si watu binafsi hata ikiwa mikoa yote kumi na saba ikijitoa haitamaananisha kuwa jumiya imekufa kwa kuwa kuwepo kwake hakutokani na kuwepo kwa mikoa hiyo kama wanachama isipokuwa kuwepo kwa wanachama wake, Waislam.

Wakati ilipotoka taarifa hii BAKWATA ilikuwa bado haijaandikishwa rasmi na Msajili wa Vyama. Kisheria ilikuwa haiwezekani kwa kundi la Adam Nasibu kuunda jumiya mpya iliyokuwa na malengo sawa na jumuiya ambayo tayari ishaandikishwa. Kwa muda wa siku tatu BAKWATA na EAMWS zikawepo kwa wakati mmoja. Ilionekana kama kwamba EAMWS itashinda vitimbi vya serikali na vya kundi la Adam Nasibu.

Tarehe 19 Desemba, 1968 serikali kama vile imegutushwa na taarifa ya Kwikima, iliipa BAKWATA Cerificate of Exemption na kuifungia EAMWS.  Waziri wa Mambo ya Ndani Said Ali Maswanya kwa niaba ya serikali alitoa taarifa fupi:

Waziri wa Mambo ya Ndani kwa kuamriwa na Rais anatangaza kuwa tawi la Tanzania la East African Muslim Welfare Society na Baraza la Tanzania la la East African Muslim Welfare Society ni jumuiya zisizotambulika kisheria chini ya kifungu 6 (i) cha Sheria ya Vyama.

Kwa tangazo hilo la Rais wa Tanzania, Julus Nyerere, Waislam walinyimwa nafasi ya kukutana na kuzungumza kuhusu tatizo ambalo kwa kweli liliwahisu Waislam peke yao. Kwa ajili hii basi Waislam walinyimwa nafasi ya kujadili na kulitolea uamuzi tatizo hilo.

Viongozi wa EAMWS waliitwa mbele ya Kabidhi Wasii ambae ndiye alikuwa amekabidhiwa na serikali jukumu la kusimamia shughuli za kufunga rasmi shughuli za EAMWS. Viongozi walifahamishwa kuwa chini ya sheria ya vyama mali zote za EAMWS zitauzwa na madeni yatalipwa kutokana na fedha hizo na fedha zitakazobaki watapewa wanachama. Serikali ilikuwa haiwezi kufanya kama sheria ilivyokuwa imeelekeza. Ilikuwa jambo zito sana kwa serikali ya Nyerere kuonekana anasimamia kuuzwa kwa mali za Waislam. Viongozi wa EAMWS walipoitwa kwa Kabidhi Wasii mara ya pili walifahamishwa kuwa serikali imebadilisha mawazo yake kutekeleza amri kama sheria inavyosema kwa ajili hiyo basi imefanya mabadiliko ya sheria ya vyama ambayo yanaiwezesha sasa kutoa mali ya EAMWS na kukabidhi BAKWATA. Hivi ndivyo mali za EAMWS zilivyochukuliwa na kupewa BAKWATA bila ya ridhaa ya Waislam wenyewe. Hivi ndivyo shule zote zilizojengwa na EAMWS pamoja na mradi wa Chuo Kikuu cha Kiislam kilipoanguka katika mikono ya kundi la Adam Nasibu. BAKWATA haikuwa na uwezo wa kuendesha mipango yoyote na taratibu shule na miradi yote ya elimu ikafifia na mwishowe kufa kabisa. Hivi ndivyo halikadhalika moto wa Waislam uliowashwa kwa kupatikana kwa uhuru waliopigania hadi ukapatikana ulivyokufa. Moto huu ulikuja ukawaka tena, lakini hiki ni kisa kingine. Insha Allah Mwenyezi Mungu akipenda tutakuja kukieleza.

Huu ndiyo ukawa mwisho wa kile kilichokuwa kikijulikana kama mgogoro wa Waislam ulivyomalizika. Mgogoro ambao ulianza pale mwalimu wa shule ya msingi asiyefahamika na yeyote alipofanya maandamano katika mitaa ya Bukoba akimuunga mkono Julius Nyerere na Azimio lake la Arusha na ukaishia kwa mwalimu huyu akiwa na nafasi juu katika jumuiya ya Kiislam ambayo ilikuwa ikichukiza machoni mwa Waislam. Mwalimu huyu ambae sasa amekuwa Makamu Katibu Mkuu wa BAKWATA alianza kazi yake kwa kuwashutua Waislam. Katika mkutano wa waandishi wa habari Adam Nasibu aliiomba TANU na ASP kujikinga na watu wanaohujumu umoja wa nchi kupitia dini. Akaendelea na kusema kuwa BAKWATA ni sawa na Baraza la Kikristo la Tanzania.  Kwa kuwa Waislam walinyimwa fursa ya kujadili ìmgogoroí hivi sasa kilichobaki na dhana tu, kuwa nini kingelitokea endapo wangeliruhusiwa kufanya mkutano ule ulioitishwa na EAMWS. Waislam wa Bukoba ambao ilitaarifiwa kuwa walifanya maandamano kuunga mkono Azimio la Arusha hawakutayarisha maandamano ya kuunga mkono BAKWATA. Dar es Salaam na katika miji mingi ya Tanzania, neno BAKWATA halina tofauti na tusi. Kumuita Muislam kuwa yeye ni mwanachama wa BAKWATA ni sawa na kumuita Mkristo mfuasi wa Yuda Iscariot, aliyemsaliti Yesu kwa vipande thelathini vya fedha.

Mjumbe mmoja wa Tume ya Waislam inastahili kuelezwa habari zake ni Mussa Kwikima. Mussa Kwikima mwaka 1968 alikuwa ameteuliwa kuwa jaji na Rais Nyerere. Yeye ndiye hasa alikuwa nguvu kuu katika tume ya Waislam. Wakati alipojitolea kuisaidia tume katika kupambana na kundi la Adam Nasibu, Waikela alimuonya kuhusu hatari ambayo itamkabili yeye mwenyewe binafsi na kazi yake. Kwikima alijibu kuwa umoja wa Waislam ni muhimu kuliko maslahi yake binafsi. Ilipoundwa BAKWATA na hapo kuwa ndiyo mwisho wa ''mgogoro,'' Kwikima alihamishwa kutoka Dar es Salaam na kupelekwa Mwanza kama Hakimu Mkazai na Rais Nyerere akamvua madaraka ya ujaji wake. 

No comments: