TANU Ilivyovunja Ngome
ya Kanisa Katoliki Jimbo la Kusini, 1955
Sehemu ya Kwanza
![]() |
| Waasisi wa TANU, New Street, Dar es Salaam 7 Julai, 1954 |
TAA mjini Lindi ilikuwa chini ya uongozi wa Suleiman Masudi Mnonji aliyekuwa Rais na Katibu wake alikuwa Mohamed Waziri. Mnonji alikuwa fundi cherahani na Waziri alikuwa mchoraji wa ramani za nyumba. TAA ilichelewa kuanza mjini Lindi. TAA ilianzishwa Lindi mwaka 1953 wakati uongozi wa TAA mjini Dar es Salaam si tu ulikuwa unaigeuza TAA kuwa chama cha siasa bali ulikuwa ukifanya mipango kumpeleka mjumbe wake Umoja wa Mataifa kudai uhuru. Masudi Mnonji alikuwa na uzoefu wa kutosha katika siasa. Baada ya Vita Kuu ya Pili alikuwa amejaribu kuanzisha vyama vya wafanyakazi katika mashamba mbalimbali ya mkonge kusini mwa Tanganyika. Vilevile aliwakusanya wapishi na madobi mjini Lindi waanzishe umoja wao. Ilikuwa kupitia juhudi zake binafsi TAA ijapokuwa ilichelewa, ilikuja kuanzishwa mjini Lindi na Mnonji alijitolea nyumba yake katika mtaa wa Makonde kama ofisi ya chama. Mnonji kwa kutambua umuhimu wa kuwa na uongozi ulioelimika vizuri, alimleta Nangwanda Lawi Sijaona kutoka Nachingwea aje aishauri TAA jinsi ya kufanya mambo kwa utaalamu.
Wakati
huo mjini Lindi kulikuwa na chama cha wafanyakazi bandarini Dockworkersí Union
chini ya uongozi wa Mussa Athumani Lukundu, chama ambacho kwa kiasi chake
kilianzisha vuguvugu la siasa za vyama vya wafanyakazi. Ingawa vyama hivi
viwili, yaani TAA na Dockworkersí Union vilikuwepo katika mji mmoja, siasa za
hiki chama cha pili cha wafanyakazi bandarini hazikupitia TAA kama ilivyokuwa mjini
Dar es Salaam. Hii kidogo ilidhoofisha mwamamko wa siasa kwa wananchi. Jimbo la
Kusini lilikuwa katika usingizi mzito wakati sehemu nyingine Tanganyika
zilikuwa zikipiga hatua kwenda mbele zikiandaa vita dhidi ya utawala wa
kikoloni. Chanzo cha usingizi huu mzito huko kusini ulikuwa na asili yake
katika historia ya Tanganyika.
Vita
vya Maji Maji vilipoanza kusini ya Tanganyika mwaka 1905 kwa nia ya kuwafukuza
Wajerumani kutoka Tanganyika, zile sehemu zenye Wakristo wengi zilikataa
kujiunga na vita na badala yake wakajiunga na majeshi ya Wajerumani na kupigana
bega kwa bega dhidi ya wazalendo. Hii ilitokana na sababu ya kuwa uasi dhidi
ya dhulma wa Wajerumani ulianza katika maeneo yenye Waislam wengi na vita
vikachukua sura ya vita vya Kiislamu dhidi ya Wazungu ambao dini yao ni
Ukristo. Kwa kuwa wamishonari walikuwa washirika wa wakoloni, walichukuliwa
kama maadui na hivyo ikawa vituo vyao vinashambuliwa na wapiganaji wa Maji
Maji. Kutokana mashambulizi haya, Wakristo walivichukua Vita Vya Maji Maji kama
vita dhidi ya Ukristo. Harakati za Maji Maji zilishindwa na Wajerumani
walifanya fisadi kubwa dhidi ya wananchi na viongozi wao. Jambo hili liliacha
kovu kubwa katika fikra za wananchi na kwa upande wa Wakristo ambao
walinusurika na ghadhabu ya Wajerumani, wengi wao wakajiweka mbali na aina
yoyote ya kupinga ukoloni.
| Selemani Mamba Shujaa wa Vita vya Maji Maji Aliyenyongwa na Wajerumani. Selemani Mamba alikuwa Kiongozi wa Wamwera. Viongozi Wengine Walionyongwa walikuwa Kinjikitile Ngwale Kiongozi wa Wamatumbi, Abdallah Chiami Kiongozi wa Wangindo, Mataka Ambuje Kiongozi wa Wayao na Songea Rauf Mbano Kiongozi wa Wangoni |
Kufuatia
historia hii Waafrika waliokuwa kusini ya Tanganyika sasa wakiwa chini ya
utawala wa Waingereza na kuwa chini ya himaya ya wamishonari walipumbazwa kiasi
kiasi kwamba waliogopa siasa. Baada ya Waafrika kushindwa vita kwa silaha kali
za Wazungu sasa Kanisa likaona ndani ya fadhaa ile fursa yao kutawala sehemu
hiyo kwa kutoa vishawishi kama vile shule na hospitali. Kwa hiyo Wamishionari
na Waingereza walionekana kama mabwana wema wenye kuwajali raia zao kinyume na
serikali katili na ya kidhalimu ya
Wajerumani. Vuguvugu la siasa kama ilivyokuwa Vita vya Maji Maji, lilianza
katika maeneo ya Waislam kufuatia mfumo ule ule kama ilivyokuwa katika upinzani
wa ukoloni wa Wajerumani. Wakristo katika Jimbo la Kusini waliiona TANU kama
walivyoviona Vita Vya Maji Maji, kama harakati nyingine za Waislam zilizowa
zinakuja tena kwa mara ya pili kuvuruga amani na utulivu. TANU ilipoanza ikawa
inavuma kuwa safari hii Waislam walikuwa wamemua kuanzisha vita dhidi ya
Waingereza kama walivyoanzisha vita na Wajerumani.
TANU
ilipoanzishwa mjini Dar es Salaam na hisia za utaifa zilipokuwa zikipanda pole pole katika fikra
za wananchi katika sehemu nyingi za Tanganyika, Jimbo la Kusini lilikuwa bado
usingizini likiishi katika zama za kale.
Mnonji na Waziri, kwa sababu ya utu uzima wao, daraja yao katika jamii na hasa
kutokana na kuhusika kwao katika siasa za pale mjini, walikuwa na nguvu kubwa
katika TAA. Wakati TANU imeshachukua nafasi ya TAA, uongozi wa TAA Lindi
haukutaka kufungua tawi la TANU. Mtu wa kwanza kuutanabaisha uongozi wa TAA
mjini Lindi juu ya mageuzi yaliyokuwa yakitokea Tanganyika na kuanzishwa kwa
chama kipya cha siasa mjini Dar es Salaam alikuwa Abdallah Juma Makopa, kijana
kutoka Tanga akifanya kazi ya ukarani Posta ya Lindi. Makopa aliwaendea Mnonji
na Waziri na kuwajulisha kuhusu kuanzishwa kwa TANUmjini Dar es Salaam na
aliwashauri waanzishe TANU pale Lindi. Jambo hilo lilipingwa moja kwa moja na
Mnonji, Waziri,
Said Nassoro, Abdallah Mhuji na wanachama wengine wa TAA.
Chama
cha Waafrika ambacho kilianzishwa siku nyingi mjini Lindi na kwa hakika ndicho
kilikuwa chama cha pekee kushughulikia maslahi ya Waafrika sehemu za kusini
kilikuwa African Welfrare Association ambacho mlezi wake alikuwa John Nevi,
Mjaluo kutoka Kenya na katibu wake alikuwa Casian Njunde, Mngoni wa Songea.
Makopa aliposhindwa kukishawishi kile kikundi cha wazee wa TAA aliwaendea
Yusufu Chembera na Rashid Salum Mpunga. Chembera alikuwa na umri wa miaka
thelathini na nne na Mpunga alikuwa kijana wa miaka ishirini na saba. Chambera
alikuwa amesoma hadi shule ya msingi na Mpunga alikuwa amemaliza madras.
Chembera alikuwa akifanya kazi katika kantini ya Lindi Welfare Centre, wakati
Mpunga alikuwa dereva wa lori aliyeajiriwa na mfanyabishara wa Kihindi. Makopa
aliwashauri Chembera na Mpunga juu ya uwezekano wa kuwahamasisha wananchi
wawaunge mkono ili tawi la TANU lifunguliwe pale mjini. Aliwaambia alitaka sana
kufanya hivyo yeye mwenyewe lakini asingeweza kwa sababu yeye alikuwa mtumishi
wa serikali na hakuwa akifahamika sana mjini. Uongozi kama wao ndiyo ungeweza
kuaminiwa na wananchi na usingetiliwa mashaka. Makopa, Chembera na Mpunga
walikubaliana kuwa kabla ya kuanza kufanya kampeni waziwazi kwa ajili ya TANU,
lazima wawaandikishe wanachama wachache kama waasisi wa chama. Mpunga na
Chembera walimwandikisha kijana mmoja akiitwa Abdallah Faraj na katika muda
mfupi waliweza kuwapata takriban wanachama 15 walioridhia
kujiandikisha kama wanachama waasisi wa TANU.
| Mwandishi Akiwasilisha Mada, ''Tanzania Nchi Isiyokuwa na Mashujaa,'' Nyuma Yake ni Picha Inayomuonyesha Dossa Aziz, Nyerere, Abdulwahid Sykes na Nangwanda Lawi Sijaona |

No comments:
Post a Comment