Wednesday, 12 February 2014

BAKWATA SEHEMU YA TANO

BAKWATA

Sehemu ya Tano
Mkutano wa Taifa wa Waislam, 1968

Hadi kufikia juma la kwanza la mwezi wa Desemba, mikoa mitatu kati ya kumi na saba ilikuwa tayari imeshajitenga kutoka EAMWS. Kile kikundi cha Adam Nasibu kikaunda kamati kwa ushirikiano na Kamati ya Maulidi ya Dar es Salaam, Adam Nasib akiwa katibu na Sheikh Abdallah Chaurembo mwenyekiti. Kamati hii ikaitisha mkutano Ukumbi wa Arnatouglo tarehe 3 Desemba, 1968 kujadilia ëmgogoroí. Aliyetumiwa kutoa tangazo lile alikuwa katibu wa Kamati ya Maulidi na Swala ya Iddi, Y. Osman. Kundi la Adam Nasib lilikuwa na mchanganyiko wa watu waliokuwa wanaungwa mkono na serikali Adam Nasib akiwa kiongozi, halikadhalika kulikuwa na Waislam waliokuwa na nafasi katika TANU kama Sheikh Abdallah Chaurembo na Juma Sued kiongozi wa TANU kutoka Bukoba. Ilikuwa wazi kuwa serikali ilikuwa inamtayarisha Sheikh Abdallah Chaurembo kuchukua nafasi ya mwalimu wake na mtu aliyemfikisha pale alipo, Sheikh Hassan bin Amir. Ikawa sasa lazima Sheikh Hassan bin Amir aondolewe na kupelekwa Zanzibar ili lile kundi la serikali chini ya Adam Nasibu liweze kuchukua uongozi wa Waislam bila ya kipingamizi chochote.

Wakati wa vurugu hizi Kamati Kuu ya TANU ilikuwa inafanya kikao chake Tanga. Sheikh Kassim Juma,  Adam Nasibu, Omari Muhaji, Sheikh Abdallah Chaurembo na Saleh Masasi  walipanda ndege hadi Tanga kwenda kushauriana na Kamati Kuu ya TANU jinsi ya kumaliza mgogoro wa Waislam.  Ujumbe huu ulikwenda Tanga kuonana na Nyerere huku ukiwa na orodha ya Waislam ambao kile kikundi cha Adam Nasibu walikuwa wanataka serikali wakamatwe na kutiwa kizuizini ili msuguano upate kumalizika. Dossa Aziz aliona Nyerere akipewa karatasi wakati kikao kikiendelea lakini hakufahamu ujumbe uliokuwamo ndani ya karatasi ile hadi hapo baadae. Alikuja kutambua habari za karatasi ile baada ya majuma mawili kupita wakati alipofatwa na jamaa yake mmoja na kumuomba aingilie kati ili rafiki yake (Ahmed Rashad Ali) aliyetiwa kizuizini na Nyerere aachiwe kutoka Jela ya Ukonga. Nyerere alipofahamishwa habari zile na Dossa, alisema kuwa yeye hakufahamu kuwa rafiki yake Dossa alikuwa katika orodha ile ambayo kwa umuhimu wa jambo lile ilibidi aletewe Tanga wakati wa mkutano wa Kamati Kuu. Kwa kejeli Nyerere akamwambia Dossa kuwa yeye huwa hachukuwi tabu ya kusoma majina ya watu anaowaweka kizuizini kwa kuwa anawaamini wale wanaofanya kazi ya kumletea majina yale.

Inspekta Jenerali wa Polisi, Hamza Aziz, mdogo wake Dossa alipopokea amri kutoka kwa rais kupitia Waziri wa Mambo ya Ndani kuwa amkamate Sheikh Hassan bin Amir, hakuweza kuamini masikio yake. Alitaka afahamishwe sababu za kutaka kukamatwa Mufti, kiongozi wa juu kabisa katika safu ya uongozi wa Waislam katika Tanzania. Alipoambiwa kuwa sababu ni kuwa anaihujumu serikali, Hamza Aziz alimwambia Waziri wa Mambo ya Ndani kuwa huenda kuna makosa katika amri ile. Alimfahamisha waziri kuwa yeye binafsi alikuwa anamfahamu mzee yule toka yeye Hamza alipokuwa mtoto mdogo. Akimfahamu Sheikh Hassan bin Amir kama mwalimu na mtu aliyeshiriki katika ukombozi wa Tanganyika.  Msimamo wake heshima na hadhi yake mbele ya Waislam ipo juu kabisa. Inspekta Jenerali wa Polisi alimwambia waziri kuwa haitawezekana kwake yeye kutii amri ile kwa sababu yeye haamini kuwa tuhuma zile dhidi ya Mufti Sheikh Hassan bin Amir ni za kweli. Nyerere alifahamishwa na Waziri wa Mambo ya Ndani kuwa Inspekta Generali wa Polisi, Hamza Aziz amekataa kutii amri yake ya kumkamata Mufti. Nyerere alitoa amri kwa Usalama wa Taifa kumkamata Sheikh Hassan bin Amir. Hii ilikuwa ni kinyume na utaratibu kwa kuwa Usalama wa Taifa hawana mamlaka ya kukamata watu.

Usiku wa manane siku hiyo hiyo Sheikh Hassan bin Amir alikamatwa na makachero wa Usalama wa Taifa akapelekwa uwanja wa ndege na kurudishwa Zanzibar.  Inaelekea kulikuwa na mpango uliokuwa umetayarishwa kabla ya serikali ya Mapinduzi Zanzibar kumpokea Sheikh Hassan bin Amir. Inasemekana mara kadhaa Karume alipata kumueleza Sheikh Hassan bin Amir kuwa Nyerere alikuwa hamtaki nchini kwake na akawa anamshauri arudi nyumbani Zanzibar. Sheikh Hassan alikataa ushauri ule hadi alipokamatwa na kurudishwa kwa nguvu. Karume alimpa Sheikh Hassan bin Amir hadhi zote alizostahili kama ulamaa na akamruhusu kuendesha madras. Lakini Zanzibar ilikuwa imebadilika. Mapinduzi ya mwaka 1964 yalikuwa yameingiza katika Zanzibar fikra potofu zilizokuwa zinapinga Uislam. Karume mwenyewe alikuwa ametoa amri ya kuchoma vitabu vyote vya dini. Nakala za Qurían Tukufu zilichomwa moto pamoja na taka za mji. Muslim Academy chuo kilichokuwa kikisomesha masomo ya dini kilifungwa. Mashine za kuchapa kwa lugha ya Kiarabu zikatupwa kutoka Government Press.  Maulama wengi na wanafunzi wa Sheikh Hassan bin Amir walikuwa wamekimbia Zanzibar kwenda kuishi uhamishoni. Zanzibar haikuwa tena kitovu cha elimu na maarifa ya Kiislam. Sheikh Hassan bin Amir akawa sasa mfungwa katika nchi yake mwenyewe kwa kuwa hakuwa na ruhusa ya kuondoka visiwani hapo na kurejea Tanzania Bara. Mara baada ya kukamatwa kwa Sheikh Hassan bin Amir, Adam Nasibu akatangaza kufanyika kwa mkutano ambao ulikuja kujulikana kama Mkutano wa Waislam wa Taifa. Mkutano ambao ilitangazwa utafanyika Iringa kuanzia tarehe 12-15 Desemba, 1968. Agenda kuu ya mkutano ule ilikuwa kujadili katiba kwa ajili ya jumuiya mpya ya Waislam.

Baada ya kukamatwa kwa Sheikh Hassan Bin Amir Tewa Said Tewa gazeti moja la Kiingereza lilimfuata ili afanye mazungumzo nalo. Tewa alimfahamisha mwandishi kuwa kulikuwa na hofu juu ya maendeleo yanayofanywa na Waislam na mikutano mikubwa ya Waislam iliyokuwa ikifanyika nchi nzima. Waislam waliokuwa na vyeo katika serikali walikataa kabisa  kuisaidia Tume ya Kikwima kwa njia yeyote wakidai kuwa kufanya hivyo ni sawasawa na kuchanganya dini na siasa. Waislam hawa walikaa pembeni kama watazamaji huku Nyerere kwa taratibu akivunja uongozi wa EAMWS na  kutayarisha watu wake kuwaongoza Waislam. Kundi la Adam Nasibu lilikataa kukutana na Tume ya Kwikima. Maulamaa wa Kiislam ambao walikuwa na hadhi na uwezo wa kuleta sulhu katika sakata ile hawakuweza kufanya hivyo kwa kuwa walikuwa wanajua fika kuwa aliyekuwa akivunja EAMWS hakuwa Adam Nasibu, yeye na wenzake walikuwa wakitumiwa tu. Kundi la Adam Nasibu lilikuwa halitaki chochote ila EAMWS ivunjwe na badala yake iundwe jumuiya itakayokuwa chini ya kivuli cha serikali.  Vilevile kukawa na uvumi kuwa Muislam yeyote ambae atakaejejihusisha na shughuli za EAMWS atawekwa kizuizini na serekali. Tume ya Kikwima haukuweza kupuuza vitisho hivyo kwa sababu serekali ilishawahi kuwaweka vizuizini masheikh.


Tume ya Kwikima ilikuwa inafahamu lile kundi la Adam Nasibu halikuwa na nguvu wala uwezo wa kuivunja EAMWS. Kufuatia kutangazwa kwa mkutano wa Iringa wa kundi la Adam Nasibu, Tume ya Kwikima ilitoa taarifa yake tarehe 11 Desemba ñ siku moja kabla ya mkutano wa Iringa kuanza.  Taarifa ambayo ilitolewa kwa Waislam wote, iliitisha mkutano mkuu wa EAMWS ambao ulikuwa ufanyike mwezi Februari mwaka unaofuata kujadili na kutoa uamuzi wa mwisho kuhusu mgogoro.  Tarehe ya mkutano ilibadilishwa  hapo baadae na kuwa Januari kutokana na umuhimu wa mgogoro uliokuwa ukikabili EAMWS. Gazeti la TANU baada ya kusoma taarifa ya Kwikima iliamua kutoa maoni yake kuhusu taarifa ile kwa kusema kuwa haikuwa sawa. Huu ulikuwa mpango uliosukwa mapema kuonyesha kuwa uongozi wa EAMWS ulikuwa na ubadhirifu. Juma lile lile Aga Khan ambae ndiye aliyekuwa akishambuliwa na kundi la Adam Nasibu, baada ya kutambua kuwa EAMWS isingeweza kamwe kuokolewa, akiwa Paris, Ufaransa alijiuzulu nafasi yake kama patron wa EAMWS.

No comments: