Friday, 21 February 2014

Dossa ‘’The Bank’’ Aziz: Tajiri Aliyefilisika Kwa Kupigania Uhuru wa Tanganyika: Sehemu ya Pili


Tarehe 27 Aprili, 1985 Julius Kambarage Nyerere, sasa akijulikana kama ''Baba wa Taifa,'' katika sherehe kubwa katika viwanja vya Ikulu, alitoa jumla ya medali 3979 kwa Watanzania waliochangia katika maendeleo ya taifa. Kati ya wale ambao walipewa medali hizo alikuwa Sheikh Abdallah Chaurembo. Wazalendo waliotajwa ndani ya kitabu hiki ambao walipigania uhuru wa Tanganyika, hakuna hata mmoja wao aliyekuwa katika orodha ile ya heshima. Baada ya siku chache kupita, Nyerere kama mtu aliyegutuka alimualika Dossa Aziz Ikulu. Dossa Aziz, wakati wa kudai uhuru wa Tanganyika alikuwa mtu maarufu, mwenye nafasi, na kujiweza sana. Sasa Dossa baada ya miaka kupita hakuwa akifahamika tena na ule umaarufu na utajiri wake ulikuwa umetoweka. Alikuwa akiishi maisha ya kawaida kijijini Mlandizi, maili chache nje ya Dar es Salaam. Katika sherehe ya faragha Nyerere alimtunukia medali Dossa Aziz, rafiki yake wa zamani. 

Fuatilia historia ya Dossa Aziz
Tunatengeneza...

Dossa ‘’The Bank’’ Aziz: Tajiri Aliyefilisika Kwa Kupigania Uhuru wa Tanganyika: Sehemu ya Pili

Urafiki kati ya Dossa na Nyerere ulishamiri kwa kipindi chote cha kudai uhuru na kuja kufifia mara tu uhuru ulipopatikana mwaka 1961. Sababu kubwa ya kukatika kwa urafiki wao ni kuwa kuanzia mwaka 1962 kwa mara ya kwanza nchi ilianza kukumbwa na migogoro ya dini kati ya serikali na Waislamu ambao walihisi kuwa Nyerere alikuwa akifanya njama za kuuhujumu Uislamu kinyume na maadili na ahadi ya TANU. Mwaka wa 1963 Halmashauri Kuu ya TANU ilivunja Baraza la Wazee wa TANU kwa kile kilichodaiwa kuchanganya dini na siasa. Nyerere taratibu aliwahama marafiki zake na wahimili wake wa siku za awali na akaanza kujenga nguvu mpya kutoka kwa wasio Waislamu kwa hofu ya kuwa akiwa karibu na waasisi wa TANU ambao wengi wao walikuwa Waislamu kungehatarisha nguvu zake na nguvu za Kanisa Katoliki. Kuanzia kipindi hiki Nyerere akawa mbali na Dossa na rafiki zake Dossa. 

Mwandishi wa makala hii alipomtembea Dossa Aziz nyumbani kwake Aprili, 1987 ilikuwa asubuhi kiasi cha saa nne na alimkuta Mzee Dossa amekaa barazani kwake akiwa amefungulia radio yake akisikiliza BBC. Mara alipotambulishwa kwake alimpokea kwa ukarimu mkubwa. Ukarimu ulikuwa ndani ya damu ya Dossa. 

Mbele ya baraza yake yalikuwepo mabaki ya Landrover ambayo Dossa alimfahamisha mwandishi kuwa gari ile aliitumia na Nyerere katika safari za kutembelea majimbo ya Tanganyika kwa niaba ya TANU wakati wa kudai uhuru. Mzee Dossa akionyesha kidole mabaki ya gari yake alisema, "Gari hii imetembea sehemu nyingi sana nikimpeleka Nyerere sehemu tofauti za Tanganyika na katika siku za mwanzo mimi mwenyewe ndiye nilikuwa nikiiendesha gari hii hadi pale tulipomwajiri Said Kamtawa kama dereva wa TANU." Hata kwa wakati ule Mzee Dossa alionyesha dalili zote za kupigwa na maisha. Katika picha ya pamoja ya waasisi wa TANU kuna watu wawili tu ambao wanaonekana wamevaa suti na tai, hao ni Abdulwahid Sykes na Dossa Aziz. Ishara tosha ya hadhi zao. Waliobaki wote wamejivalia mavazi yao ya kawaida. Nyerere akiwa amevaa kaptula na soksi ndefu zilizogota magotini, mavazi maarufu wakati ule kwa wasomi. Picha hii imebeba maneno elfu moja. Dossa aliyeonekana pale kibarazani Mlandizi si yule aliyekuwa kwenye picha ya waasisi wa TANU. Dossa mtanashati, mtoto wa Mwafrika tajiri, Aziz Ali, Waziri Dossa Aziz aliyetoa mali kuipa TANU ili Nyerere aitumie katika shughuli za kuikomboa nchi alikuwa amechoka akionyesha dalili zote za kusahauliwa na nchi aliyoipigania ijitawale. 

Tarehe 27 Aprili, 1985, Julius Kambarage Nyerere, sasa akijulikana kwa jina jipya la ''Baba wa Taifa,'' katika viwanja vya Ikulu alitoa jumla ya medali 3,979 kwa Watanzania walioiletea nchi hii maendeleo. Si Dossa wala yeyote aliyetajwa katika kumbukumbu hii ya marehemu Dossa Aziz alikuwa katika hao waliopata heshima hiyo. Lakini baadae kama mtu aliyegutushwa Baba wa Taifa alimkaribisha Dossa Ikulu na kumpa medali katika sherehe fupi.

Kwa muda mrefu sasa kumekuwa na hofu kubwa sana ya wale walioshika madaraka ya kuendesha serikali wakiogopa wananchi kuhusisha uasisi wa TANU na nguvu za siasa za Waislamu walioishi miaka ile. Matokeo yake ni kufutika kwa hisotoria ya wazalendo wengi waliojitolea maisha yao kuupigania uhuru wa Tanganyika. Dossa Aziz ni kati ya wazalendo ambao historia imedhulumu haki zao za kutambulika kama mashujaa wa uhuru wa Tanganyika. Kwa kipindi cha zaidi ya miaka thelathini si CCM wala si rafiki yake mpenzi Julius Nyerere alikuwa anafahamu Dossa anaishi vipi na ana hali gani. Rafiki zake wachache waliokuwa wakimtembelea nyumbani kwake pale Mlandizi walihuzunishwa na hali yake. Dossa mtu aliyekuwa na mali katika miaka ya 1950 alikuwa akiishi katika hali ya ufukara. Hali hii ya ufukara ilitaka kumkosesha kuhudhuria Mkutano Mkuu wa CCM mwaka1987 pale Kizota ambapo waasisi wote wa TANU walialikwa. Sababu kubwa ilikuwa ni ukosefu wa nguo na viatu vya kuvaa katika hadhara kama hiyo. Ilikuwa mmoja wa marafiki zake wa zamani Abbas Sykes ndiye aliyemnunulia nguo na viatu vya kumwezesha kwenda Dodoma. Rafiki zake walipomshauri aende kwa Nyerere ampatie msaada Dossa alijibu kuwa yeye hawezi kulifanya hilo kwa kuwa Nyerere anajua kuwa yeye alitumia fedha zake nyingi katika harakati za kudai uhuru na kama yeye Nyerere leo kamsahau yeye hana sababu ya kumfuata. Jibu la Dossa lilikuwa jibu la muungwana, mtu asiyekubali kujidhalilisha.

Kauli hii ya Dossa na msimamo wake huu thabiti ulithibitishwa na Mwalimu Nyerere mwenyewe siku ya Jumapili tarehe 19 Aprili 1998 katika khitma ya marehemu nyumbani kwa Dossa pale Mlandizi wakati Nyerere aliposimama kusema machache katika hadhara ile kuhusu uhusiano wake na Dossa na mchango mkubwa wa marehemu Dossa Aziz katika kuleta uhuru wa Tanganyika. Nyerere alisema kuwa hata siku moja Dossa hakupata kumuomba kazi au kuonyesha dalili za kutaka ukubwa. Mwalimu Nyerere aliposema maneno haya alibubujikwa na machozi na waliokuwepo nao walilia kwa huzuni.Subira aliyokuwanayo Dossa ndiyo sababu kubwa iliyomfanya astahamili dhiki kwa miaka yake ya mwisho ya uhai wake na afe masikini katika hospitali ya Tumbi, Kibaha badala ya St. Thomas Hospital, London, Dossa hakuwa wa kwanza kukutwa na haya. Haya yalimkuta Mzee Mshume Kiyate, Sheikh Mohamed Ramia na wengine wengi. Baada ya kuleta uhuru wazalendo hao wakageuzwa ganda la muwa. Hakuna unachoweza kufanya na ganda la muwa ulilolifyonza ila kulitema tu na kama utaweza kuelekeza mdomo wako kwenye jalala na kutembea humo hivyo ni bora zaidi kwani hata kulitema ganda hilo kwenye mkono wako wa kushoto kisha kulitupa jalalani ni kulipa hadhi ganda hilo. Habari za Dosa Aziz zinahitaji utafiti wa kina wa msomi makini. Hii ni changa moto kwa wana historia, wana historia wa Tanzania ya leo. Ni katika kuijua historia ya uhuru wa nchi hii ndipo wenye madaraka hivi sasa wanaweza kujua kwa nini hii leo wajukuu wa akina Dossa wameiona dhulma na wanapambana na polisi na askari wa kuzuia fujo kwa mawe kisha wanachoma moto ofisi za CCM ambacho asili yake ni mababu zao.

Dossa Aziz na Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam


Ilikuwa kawaida ya Dossa baada ya mikutano ya TANU pale Mnazi Mmoja kumchukua Nyerere na gari lake kumrudisha Pugu. Njia ya zamani kwenda Pugu ilikuwa inapita hapo kilipo Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam. Sasa ilikuwa kiza kimeingia na walitaka kutoka nje ya gari kuangalia mandhari ya Dar es Salaam maana kutokea pale mji ulikuwa unapendeza sana kwa taa zilizokuwa zikiwaka barabarani. Nyerere alimwambia Dossa, “Dossa tukipata uhuru wetu hapa lazima tujenge chuo kikuu.” Hili wazo lilifanyiwa kazi na wananchi wakahamasishwa kuchangia ujenzi wa Chuo hicho. Fedha zilichangwa na Chuo kikajengwa pale New Street kwenye kiwanja cha John Rupia alichokitoa kuwapa TANU.  Hapo ndipo kilipoanza Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam. (Chuo hiki sasa ni Chuo Cha Watu Wazima). Abdallah Salum alikuwa mmoja wa wachangiaji wa chuo hicho na mwanae Salum Matimbwa hadi leo amehifadhi stakabadhi ya malipo ya sh. 50.00 stakabadhi ambayo ina sahihi ya Bhoke Munanka. Wazee hawa walikuwa wazalendo wa kweli kabisa.  Baada ya uhuru kupatikana mwaka wa 1961 na zilipokuwa zikianzishwa harakati za ushirika Abdallah Salum Matimbwa alitoa lori lake Commer Fargo DSY 435 kama mtaji kuingiza katika Coast Region Transport Company (CORETCO). Pamojanae katika kuanzisha CORETCO walikuwa wazee wengine kama Sharia Bofu na nduguye Ibrahim Bofu, Salum Kambi, Juma Mzee na wengineo.

No comments: