Thursday, 20 February 2014

TANU Ilivyovunja Ngome ya Kanisa Katoliki Jimbo la Kusini, 1955 Sehemu ya Sita

TANU Ilivyovunja Ngome ya Kanisa Katoliki Jimbo la Kusini, 1955
Sehemu ya Sita

Siku iliyofuatia mkutano wa hadhara ulifanyika mjini Mikindani mahali palipojulikana kama Jangwani, karibu na ufuko wa Bahari ya Hindi. Mkutano huu uliohudhuriwa na watu wengi na uliendelea bila mushkeli wowote ukitoa kitendo kidogo kilichofanywa na mwalimu mmoja wa shule, Abdulrahman Muhibu aliyekuwa amelewa. Muhibu alikuwa ametoka kunywa pombe na alipita karibu na uwanja wa mkutano ambapo Nyerere alikuwa akihutubia. Katika hali yake ya ulevi alimpigia kelele Nyerere akamwita muongo. Huenda Muhibu alikuwa akifahamu vyema ujumbe wa Nyerere, na akiwa vile alivyokuwa, mtumishi wa serikali na mlevi, aliona wazo la mwalimu wa shule Mwafrika kama yeye kuwaongoza watu hadi uhuru upatikane ni jambo lisilowezekana. Kwa haraka Muhibu alikamatwa na watu na ilikuwa karibu wamtie adabu ndipo Nyerere alipoingilia na hivyo kumnusuru.

Jioni hiyo baada ya mkutano Nyerere na ujumbe wake waliondoka kwenda Newala, kwenye ngome ya Yustino Mponda. Mponda alikuwa mmoja wa wale wajumbe wa Baraza la Kutunga Sheria waliosafirishwa na Gavana hadi Umoja wa Mataifa, New York, kumpinga Nyerere. Sasa TANU ilikuwa ikichukua mkokoto wake wa kampeni hadi ndani ya ardhi ya Mponda ambayo yeye alikuwa liwali na mjumbe wa Baraza la Kutunga Sheria. Nyerere alipomaliza ziara yake ya Jimbo la Kusini, fikra za Wakristo zilibadilika. Wakristo hawakuamini tena kuwa TANU ilikuwa harakati za Waislam sawasawa na Vita Vya Maji Maji. Nyerere, Tambwe na Diwani walipokuwa wanashika njia kurudi Dar es Salaam, matawi ya TANU yalikuwa yamefunguliwa Masasi, Ndanda na Newala ambazo zilikuwa sehemu za Ukristo na ngome ya Ukatoliki katika Tanganyika.

Nyerere aliporudi Lindi mwaka 1959, TANU ilikuwa ina nguvu sana na ilikuwa imekumba kila mtu. Wale watumishi wa serikali wengi wao wakiwa Wakristo, walio kuwa wakiibeza  TANU mwaka 1955 kwa sababu ilikuwa ikiongozwa na Waislam ëwasiokuwa na elimu,í ukweli ulikuwa umewadhihirikia na sasa walikuwa wakionyesha heshima kwa chama. Hawakuwa na khiyari na ilibidi waonyeshe heshima kwa sababu bwana mwenyewe, yaani serikali ya kikoloni, ilikuwa na heshima kwa TANU. Serikali ilikuwa imetambua kuwa dhamiri ya watu ya kukataa kutawaliwa haiwezi tena kupuuzwa. Nyerere alikuwa amelihutubia Baraza la Udhamini la Umoja wa Mataifa mara mbili, mara ya pili ikiwa mwaka 1957. Ujumbe wa TANU ulikuwa wazi, watu wa Tanganyika walikuwa tayari kujitawala. Kila siku zilivyopita ndivyo TANU ilivyopata nguvu. Rashidi Salum Mpunga, dereva wa lori, aliweza kumshawishi na akafanikiwa kumuingiza TANU mmoja wa masheikh wenye kuheshimiwa sana mjini Lindi na mshairi maarufu, Sheikh Mohamed bin Yusuf Badi. Sheikh Badi alipoingia TANU kwa ajili ya heshima yake na kukubalika na watu, idadi kubwa ya Waislam walimfuata na kukata kadi za TANU. Nyerere alipokuja Lindi kujadili tatizo la kura tatu na uongozi wa Jimbo la Kusini, Sheikh Yusufu Badi alimpokea Nyerere na madras yake, wanafunzi wakimwimbia Nyerere kasda na kumpigia dufu. Kuanzia hapo sasa kila mtu alijiunga na TANU. Si Mponda wala Kanisa lilikuwa na uwezo wa kupambana na TANU kwa wakati ule. Polepole lakini na kwa kwa uhakika, TANU ilingia ndani ya maeneo ya Kikristo huko Songea, Masasi, Tunduru na Newala, nyumbani kwa Yustino Mponda.

Lakini matukio mawili ya kumbukumbu kubwa yalikuwa katika safari ya pili ya Nyerere alipozuru tena Jimbo la Kusini. Kumbukumbu ya kwanza ilikuwa tawaswil aliyosomewa Nyerere na Sheikh Yusuf Badi mwenyewe pamoja na Waislam aliowachagua yeye sheikh mwenyewe maalum kwa hafla hiyo, pamoja na waliochaguliwa na masheikh wengine. Kumbukumbu ya pili ni ile karamu  iliyoandaliwa kwa heshima ya Nyerere na Mussa Athumani Lukundu, kiongozi wa Dockworkersí Union. Hii ilikuwa heshima kubwa aliyoonyeshwa Nyerere, ilikuwa kilele cha upendo na heshima kwa Muislamu yoyote anaweza kumfanyia asiyekuwa Muislamu.

Siku ya ukumbusho mkubwa sana mjini Lindi ilikuwa siku ya uhuru, tarehe 9 Desemba, 1961. Sheikh Badi, bingwa wa mashairi, aliombwa na TANU kuandika hotuba ya uhuru itakayotolewa na Yusuf Chembera mbele ya DC akiwa kama mwakilishi wa utawala wa Kiingereza uliokuwa ukingíoka. Hotuba hiyo ya Sheikh Badi na iliandikwa kwa Kiarabu na Chembera. Akiwa mtoto mdogo Chembera alipelekwa kwa Sheikh Yusuf Badi na baba yake kwenda kusoma elimu ya dini na aliendelea kuwapo hapo chuoni kwa Sheikh Badi hadi alipohitimu. Sheikh Badi hakuona kama ipo hotuba yoyote iliyoandikwa na mwanadamu iliyostahiki hafla kama ile ya siku ya kujikomboa kutoka minyororo ya ukoloni. Sheikh Badi alimsomea mwanafunzi wake Chembera, dua ya kunut ambayo husomwa na Waislam katika kila sala ya alfajir. Usiku wa manane wa tarehe 9 Desemba, 1961 ulikuwa usiku adhim sana kwa wote wawili, mwalimu na mwanafunzi wake, pale watu walipokusanyika katika ule uwanja wa gofu na kumsikiliza Chembera akisoma kunut kupokea uhuru wa Tanganyika. Lakini mara tu baada ya uhuru Wakristo walianza kuuchimba ule waliouona kuwa uongozi wa Waislam katika TANU kwa kisingizio kuwa uongozi ule haukuwa na elimu. Suleiman Masudi Mnonji alikamatwa na kutiwa kizuizini kwa amri ya Nyerere chini ya Preventive Detention Act ya mwaka 1962 kwa kile kilichoitwa ''kuchanganya dini na siasa'' na Waislam wengine waanzilishi wa harakati za kudai uhuru walitupwa nje ya uongozi.


Mwisho

No comments: