Friday, 14 February 2014

TANU Ilivyovunja Ngome ya Kanisa Katoliki Jimbo la Kusini, 1955 Sehemu ya Pili


TANU Ilivyovunja Ngome ya Kanisa Katoliki Jimbo la Kusini, 1955
Sehemu ya Pili

Baada ya kuandikisha wanachama waasisi mkutano wa siri uliitishwa katika Welfare Centre ambako ndiko alikokuwa akifanya kazi Chembera. Chembera aliwaeleza kwa ufupi wale wanachama wa mwanzo kuhusu malengo na madhumuni ya chama hicho kipya cha siasa. Mkutano huo ulichagua kamati ya watu watatu yaani, Makopa, Chembera na Faraj ili kuwakabili Mnonji na Waziri kuwaleza kuwa TAA haipo tena nchini Tanganyika. Lengo lilikuwa kuwasadikishia kuwa ilikuwa kazi bure na kupoteza wakati kujaribu kuihuisha TAA mjini Lindi wakati ambapo Tanganyika nzima ilikuwa ikisonga mbele na TANU. Baada ya mjadala mrefu sana na mkali wa wale vijana watatu na ule uongozi wa TAA wa wazee, walikubaliana TANU lazima isajiliwe mjini Lindi.

Uchaguzi ulifanyika na Shaaban Msangi, kijana wa Kipare akifanya kazi kwa Smith Mc Kenzie, alichaguliwa rais na Ahmed Seif, katibu. Mpunga, Chembera, Mnonji na Idd Toto walichaguliwa wajumbe wa kamati. Ahmed Seif alikuwa kijana ambaye ndiyo kwanza amemaliza shule, yeye alikabidhiwa kuendesha ofisi kwa niaba ya uongozi.  TANU mjini Lindi ilimwajiri ili kukiandaa chama kiweza kufanya kazi zake kwa ufanisi. Hassan Mohamed Kinyozi aliajiriwa kama mhudumu wa ofisi. Hawa wawili walikuwa ndiyo wafanyakazi wa kwanza wa TANU waliokuwa wakilipwa mshahara katika Jimbo la Kusini na wakawa miongoni mwa wafanyakazi wachache sana walioajiriwa na TANU kwa wakati ule. Mnonji alitoa nyumba yake katika mtaa wa Makonde kuwa ofisi ya kwanza ya TANU Jimbo la Kusini. Baada tu ya kuanzishwa kwa TANU, Athumani Mussa Lukundu, kiongozi wa Lindi Dockworkersí Union, aliunganisha chama chake na TANU. Jambo hili, kwa TANU lilikuwa la kuitia moyo sana kwa sababu Dockworkersí Union ilikuwa na wananchama wengi na hatua ile iliongezea TANU nguvu.

Baada ya muda mfupi tu toka kufunguliwa kwa TANU Mkutano Mkuu wa Kwanza wa TANU wa mwaka 1955 ulifuatia. Tawi la Lindi lilikuwa tayari lina uhusiano na makao makuu ya TANU mjini Dar es Salaam, na lilikuwa likitarajia kuhudhuria mkutano huo na kukutana na Julius Nyerere na uongozi mzima wa TANU pale makao makuu Dar es Salaam. Mpunga, mwanachama muasisi wa TANU, na Ali Ibrahim Mnjale waliteuliwa kuhudhuria mkutano huo kama wajumbe kutoka Jimbo la Kusini. Halmashauri ya TANU ya Lindi iliwaelekeza wajumbe hawa wafikishe ombi rasmi kwa makao makuu ili Julius Nyerere aje kufanya ziara kusini kwanza, kukutana na wananchi na kufanya kampeni kwa ajili ya TANU na pili aje kupambana na propaganda dhidi ya TANU zilizokuwa zikitawanywa na Yustino Mponda.  Mponda akitumia uhusiano wake na serikali ya kikoloni na nafasi yake kama mjumbe wa Baraza la Kutunga Sheria kutoka Newala; na vilevile akitumia ushirikiano wake wa muda mrefu na kanisa ambao bila shaka yoyote lilikuwa serikali ndani ya serikali kule kusini, alikuwa ameanza kampeni yake ya kuipinga TANU. Hili lilikuwa likiathiri msukumo wa uanachama. Mponda alikuwa mmoja wa wajumbe waliotumwa na Gavana Twining kwenda Umoja wa Mataifa Februari, 1955 kwa niaba ya serikali ya kikoloni kwenda kuipinga. Uongozi wa TANU huko Lindi ulitaka Nyerere aende kupambana na Mponda akiwa katika uwanja wake mwenyewe, ndani kabisa ya ngome ya Ukristo wa Kikatoliki katika Tanganyika.

Mkutano mkuu wa mwaka wa TANU ulifanyika katika ukumbi wa Hindu Mandal mjini Dar es Salaam. Siku kabla ya mkutano TANU ilimwalika Gavana Edward Twining kwenye tafrija katika Ukumbi wa Arnatouglo lakini alikataa kistaarabu na akamtuma Chief Secretary, Bruce Hutt, kumwakilisha. Baada ya mkutano, wakati wajumbe wengine wanaondoka kurudi kwenye majimbo yao, Mpunga na Mnjawale walibakia nyuma kukutana na uongozi wa makao makuu wa Julius Nyerere, Sheikh Suleiman Takadir, John Rupia, Ali Mwinyi Tambwe, Said Chamwenyewe, Oscar Kambona na wengineo. Mpunga na Mnjawale waliwafahamisha viongozi wa makao makuu kuhusu hali mbaya ya siasa Jimbo la Kusini. Mbali na kampeni za kuipinga TANU za Mponda, katika ziara yake Lindi Gavana Twining aliwatahadharisha Waafriika wa Tanganyika wasijihusishe na ëwafaanya fujo wanaotaka kuzusha vuruguí. Twining alikuwa akitoa onyo hili akiikusudia TANU ambayo ilikuwa imeanzishwa mwaka uliopita. Hotuba hii ya Gavana iliwatisha wananchi kujiunga na TANU. Mpunga na Mnjawale walisisitiza kuwa kuja kwa Nyerere mjini Lindi kulitakiwa haraka sana kukabiliana na vyote viwili, kwanza ile hotuba ya gavana na pili zile kampeni za kupinga TANU zilizokuwa zikiendeshwa na Liwali Yustino Mponda.



Mkutano wa Kwanza wa TANU 1955
Wakati huo Abeid Amani Karume aliyehudhuria ule mkutano alimwalika Nyerere afanye ziara Zanzibar. Kitu cha kustaajabbisha ni kuwa, Nyerere alionekana kuiafiki zaidi ziara ya Zanzibar kuliko ile safari ya kwenda kusini kuiimarisha TANU. Mpunga alimsisitizia Nyerere umuhimu wa yeye kwenda Lindi ambako kunaweza kuwa ndiyo chanzo cha TANU kupata ufanisi Newala, Songea, Tunduru na Masasi ambako kulikuwa na upinzani mkubwa dhidi ya TANU. Kanisa lilikuwa likiwazuia Wakristo kujiunga na TANU. Sheikh Suleiman Takadir, Said Chamwenye, John Rupia, Ali Mwinyi Tambwe wote waliunga mkono ule ujumbe wa Lindi juu ya suala hili. Baada ya kufikia makubaliano, Mpunga na Mnjawale walipewa barua ya kuthibitisha safari ya Nyerere.  Ziara ya Nyerere ilikuwa ianze muda mfupi kutokea hapo kwa kuwa ilikuwa ndiyo siku za mwisho za kiangazi. Barabara sehemu ya kusini ya Tanganyika zilikuwa hazipitiki wakati wa masika, zikiitenga kabisa kusini toka sehemu zilizobaki za nchi. Ali Mwinyi Tambwe na Rajab Diwani walifuatana na Nyerere kwenda Jimbo la Kusini kuondoa wasiwasi na woga uliozushwa na Gavana Twining na kibaraka Yustino Mponda.

Ali Mwinyi Tambwe

No comments: