Katika hotuba hii ya Mwalimu Nyerere kuna jambo kakosea. Anasema safari ya kwanza kutangaza TANU alikwenda Mbeya. Hapana safari ya kwanza alikwenda Morogoro akiongozana na Zuberi Mtemvu 1954 na hii safari ya Mbeya aisemayo alozungumza na wanachama mkutano wa ndani ilikuwa mwaka 1955 alipokwenda Lindi akifuatana na Ali Mwinyi Tambwe na Rajab Diwani. Mbeya TANU ilikuja baadae sana. Ukisoma kitabu cha Abdul Sykes utayakuta haya na ithibati yake ni nyaraka nilizosoma katika majalada ya akina Sykes.
''Nyerere
na msafara wake ulipokelewa na uongozi wa TANU wa Lindi huko Mbanji, kijiji
kidogo nje ya mji. Msafara wa Nyerere ulipowasili Mbanji ilikuwa kiasi cha saa
moja jioni hivi na giza lilikuwa linaanza kutanda. Mbali na Mpunga na wale
wajumbe wawili waliokutana na Nyerere mjini Dar es Salaam mwezi uliopita, hakuna
hata mtu kati ya umma ule uliokuja kupokea ujumbe kutoka makao makuu ya TANU
aliyekuwa anajua Nyerere anafanana vipi. Mpunga, dereva wa lori, alijibagua
kutoka kwa lile kundi la watu akawa amesimama pembeni ili Nyerere apate
kumuona. Baada ya Nyerere kumtia Mpunga
machoni, Mpunga alimwendea kumsalimu Nyerere, Tambwe na Diwani; kisha
aliligeukia lile kundi la watu kumtambulisha Nyerere kwa wananchi akilitaja
jina lake kwa sauti kubwa. Baada ya hapo aliutambulisha ule ujumbe wa Nyerere.
Nyerere na ujumbe wake ulisindikizwa kwa shangwe na kundi la watu hadi ofisi ya
TANU kwenye nyumba ya Mnonji. Kupakana na ofisi ya TANU ilikuwepo nyumba ya
seremala mmoja, Issa bin Ali Naliwanda. Hii ndiyo nyumba iliyochaguliwa alale
Nyerere na ujumbe wake, si kwa sababu ilikuwa nzuri kupita zote. Ilichaguliwa
na kupewa heshima hii kwa sababu ilikuwa karibu sana na ofisi ya TANU na hivyo
basi ilirahisishia TANU kazi ya ulinzi wa Nyerere. Siku iliyofuata ilikuwa
Jumapili na Nyerere aliwaomba wenyeji wake apelekwe kanisani kwa ajili ya
ibada.
Kanisa
Katoliki mjini Lindi ni jengo la fahari lililoko ufukweni katika Bahari ya
Hindi. Lindi ulikuwa mji wa Waislam. Mbali na mlio wa kengele za kanisa hakuna
mtu pale mjini aliyekuwa akishughulishwa na kile kilichokuwa kikifanyika kwenye
viwanja vya kanisa. Watu wachache waliokuwa wakienda kusali kanisani walikuwa
Wakristo waliokuja Lindi kutoka sehemu nyingine za Tanganyika kufanya kazi
katika ofisi za serikali. Ghafla mahala hapa palipokuwa pweke, palipopuuzwa kwa
miaka na Waislam wa mjini, pakawa muhimu kwa sababu rais wa TANU ambae alikuwa
Mkatoliki alikuwa na haja ya kuhudhuria ibada pale kanisani. Hakuna mtu katika
uongozi wa TANU wa Lindi aliyejua ndani ya kanisa lile kulikuwa vipi wala
hapakuwa na yoyote kati yao aliyewahi kuingia ndani ya kanisa, si Lindi wala
mahali popote pale. Uongozi wa TANU wa Waislam mjini Lindi haukumwamini Mkristo
yoyote kumsindikiza Nyerere kanisani ili kumpa ulinzi. Baada ya kujadili suala
hilo kwa urefu hatimaye iliamuliwa kuwa
Mpunga na wanachama wachache Waislam wenye kuaminika lazima wamsindikize
Nyerere kanisani na wengine wabakie nje kulinda mlango.
Jumapili
hiyo Nyerere aliingia ndani ya kanisa Katoliki mjini Lindi akifuatwa nyuma na
walinzi wake Waislam wakiongozwa na Salum Mpunga, dereva wa lori shupavu. Misa
hii ‘’maalum’’ ilidumu katika fikra za
wale Wakristo waliokuwepo pale kanisani kwa miaka mingi kwa kuwa tukio hilo
liliwagusa sana Wakristo walioshuhudia mkasa ule ndani ya kanisa la Lindi. Hii
huenda ilikuwa mara ya kwanza na ya mwisho kwa Nyerere kumsalia Mungu wake huku
akiwa amesimamiwa na Waislam.
DC
mkoloni alikataa kutoa kibali kwa TANU kufanya mkutano wa hadhara. Akiwa
amekasirika sana, Shabaan Msangi aliitisha mkutano wa dharura wa tawi
uliohudhuriwa na Nyerere na Tambwe. Baada ya mkutano huo Tambwe alikwenda
kumwona DC. Ruhusa ilitolewa, na adhuhuri hiyo siku ya Jumapili, katika kiwanja
ambacho Wazungu walikuwa wakicheza gofu, ambako mwaka mmoja uliopita Gavana
Edward Francis Twining alitoa hotuba iliyowavunja moyo Waafrika, Nyerere alihutubia
mkutano wa hadhara. Kamwe haijapata kutokea kabla ya siku ile katika historia
nzima ya Jimbo la Kusini, watu wengi kiasi hicho kujumuika mahali pamoja.
Wazungu na Wahindi pamoja na askari, watu wakiwa wamekaa na wengine wamesimama
katika ya jua kali walikuja kumsikiliza
Nyerere akihutubia. Ili kuhakikisha amani na usalama pale mkutanoni serikali
iliweka askari waliouzunguka uwanja mzima wa mkutano. Nyerere aliwafikishia
watu ule ujumbe wa TANU wa kuwa, kutawaliwa ni fedheha, na Waafrika wa Tanganyika
lazima wadai uhuru wao. Uingereza ilikuwa ikiitawala Tanganyika chini ya
udhamini kwa niaba ya Umoja wa Mataifa, na wakati ukiwa muafaka inabidi
Uingereza ikabidhi nchi kwa wananchi wenyewe. TANU ilikuwa imewasili Jimbo la
Kusini.''
Huenda mkutano aliokusudia Mwalimu Nyerere kuufanya Mbeya ni huu aliofanya Mkindani nyumbani kwa Ahmed Adam baada ya kutoka Lindi:
Huenda mkutano aliokusudia Mwalimu Nyerere kuufanya Mbeya ni huu aliofanya Mkindani nyumbani kwa Ahmed Adam baada ya kutoka Lindi:
''Julius
Nyerere, Ali Mwinyi Tambwe na Rajabu Diwani waliwasili Mikindani kutoka Lindi
siku ya Jumamosi. Kabla ya kuwasili ujumbe huo, kazi kubwa kuliko zote
waliyokuwanayo uongozi wa TANU Mikindani ilikuwa kutafuta mahali pa kumlaza
Nyerere. Walimwendea Ahmed Adam, Mnubi mmoja tajiri na mtu wa makamo,
aliyemiliki nyumba moja ya fahari. Nyumba hii ilikuwa ya ghorofa moja na
ilijengwa kwa mawe na chokaa. Ahmed Adam aliombwa awe mwenyeji wa Nyerere na
ujumbe wake. Nyumba hii tayari lilikuwa na kisa chake. Ilijengwa na hayati kaka
yake Ahmed Adam baada ya Vita Kuu ya Kwanza. Kaka yake alikuwa askari wa Kinubi
aliyekuwa katika jeshi la Wajerumani. Huenda alichukuliwa Misri mwishoni
mwa mwa karne ya kumi na tisa na
Wajerumani kuja Tanganyika kama mamluki katika jeshi la Wajerumani wakati wa
vita vya Maji Maji. Baada ya vita alilipwa kiinua mgongo na serikali ya
Ujerumani na kwa kutumia fedha hizo alijenga nyumba hiyo. Katika Vita Kuu ya
Kwanza yeye alipigana katika jeshi la Wajerumani dhidi ya Waingereza. Baada ya
vita Wajerumani wakiwa wameshindwa vita,
Waingereza waliitikadi nyumba hiyo kama mali ya adui wa himaya ya
Kiingereza na kwa hiyo ilibidi itaifishwe. Hii ilikuwa ndiyo nyumba pekee
iliyokuwa nzuri yenye kumilikiwa na Mwafrika na kwa ajili hii haikuweza kukosa
kuhusudika.
Utawala
wa Waingereza ulikuwa katika taratibu ya kuitaifisha nyumba hiyo wakati
ilipofahamika kwamba serikali isingeweza kufanya hivyo kwa sababu ya kifungu
cha sheria ambacho kilisema kuwa mali ya Waafrika waliokuwa wakitumika katika
majeshi ya watawala wao haiwezi kutaifishwa.
Hii ilinusuru nyumba hiyo na hivyo ilibakia mikononi mwa mwenyewe mpaka
alipofariki na nyumba hiyo ikaja kuwa katika miliki ya mdogo wake, Ahmed Adam.
Ahmed Adam alikubali kumpokea Nyerere na ugeni wake nyumbani kwake. Nyumba hiyo
ilikuja kuwa tawi la kwanza la TANU Mikindani. Siku hiyo hiyo ya Jumamosi,
usiku Nyerere aliitisha mkutano na
wanachama kama thelathini hivi walihudhuria. Nyerere aliwaeleza kwa
ufupi juu ya ile safari yake ya Umoja wa Mataifa na hali ya siasa kwa ujumla
mjini Dar es Salaam. Nyerere aliwahakikishia waskilizaji wake kuwa kulikuwa na
uwezekano mkubwa sana kuwa Tanganyika itakuwa huru katika uhai wao.''
No comments:
Post a Comment