| Sheikh Ponda akizungumza na waandishi wa habari |
SHEIKH
Ponda Issa Ponda, Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania amesema,
serikali ina kisasi na yeye, anaandika Happiness Lidwino.
Amesema, ameshangazwa na hatua
ya Jamhuri kumkatia rufani katika kesi yake ambayo tayari imekwisha na yeye
kuonekana kutokuwa na hatia.
Juzi katika Mahakama ya Rufaa jijini Dar es Salaam, mbele ya
Jaji Jaji, Edson Mkasimongwa, Bernard Kongola ambaye ni Wakili Mkuu Mwandamizi
wa Serikali alisema kuwa, Jamhuri inapinga hukumu hiyo.
Mwaka 2013 Sheikh Ponda alishitakiwa kwa makosa matatu; la
kwanza alidaiwa kuwaambia waumini wa Dini ya Kiislam kwamba, wasikubaliane na
uundwaji wa kamati za ulinzi na usalama za misikiti zilizoanzishwa na Baraza
Kuu la Waislam Tanzania kwa madai ni vibaraka wa CCM na serikali.
Shitaka la pili lilihusu kuwa, Sheikh Ponda aliwaambia Waislamu
kwamba serikali ilipeleka jeshi Mtwara kushughulikia suala la vurugu
iliyotokana na gesi ili kuwaua, kuwabaka na kuwatesa wananchi, kwa sababu
asilimia 90 ya wakazi hao ni Waislamu.
Shitaka la tatu alidaiwa kulitendwa tarehe 10 Agosti mwaka 2013
kuwa, kauli yake katika shitaka la pili inadaiwa kuumiza imani za watu wengine
kinyume cha kifungu cha sheria namba 390 na kanuni ya adhabu namba 35 cha mwaka
2002.
Akizungumzia na Mwanahalisi Online kuhusu hatua ya kukatiwa
rufaa, Seikh Ponda ameeleza hatua hiyo kuwa ni ya kisasi naye.
Na kwamba, hatua hiyo haiheshimu uongozi wake (serikali) na pia
haitambui umuhimu wake katika jamii kwani ilimpotezea muda mwingi kifungoni pia
kushindwa kutoa huduma kwa jamii.
Lakini pia amesema, hatua hiyo inaweza kuakisi kwamba serikali
haiko makini kwa kuwa, sababu zilizotolewa hazina uzito.
“Sawa wanahaki ya kupinga ushindi wangu lakini kwa sababu
maalumu na zenye uzito. Kama kuwashitaki mimi ndiye nilipaswa kuishitaki
jamhuri kwa kunipotezea muda na kunifanyia baadhi ya mambo yasiyo ya kibinadamu
ikiwemo kukataa dhamana. Hii sio sifa ya utawala bora kwa serikali.
“Nina mpango wa kutoa taarifa hii katika miskiti yote na hata
kuitisha mkutano wa waandishi wa habari ili Tanzania yote ijue kinachoendelea
na wakipime kama ninastahili au hapana,” amesema Sheikh Ponda.
Rufaa hiyo ambayo inatarajiwa kuanza kusikilizwa Juni 30 mwaka
huu, itasomwa mbele ya Edson Mkasimongwa, Jaji wa Kanda ya Dar es Salaam.
Katika rufani hiyo upande wa Jamhuri umewasilisha sababu nne za
kupinga hukumu hiyo ikiwemo ya Mahakama ya Morogoro kwamba ilikosea kwa
kutozingatia uzito wa ushahidi wa kielektroniki, sababu ya pili Jamhuri inadai,
Mary Moyo, Hakimu Mkazi Mfawidhi alikosea kusema hati ya mshitaka ilikuwa
pungufu.
Sababu ya tatu upande wa Jamhuri inasema, Hakimu alikosea kusema
Sheikh Ponda hakuwa na nia ya kuwashawishi waumini wa morogoro kufanya kosa la
jinai siku ya tukio, na sababu ya nne ni, hakimu kukosea upande wa jamhuri
ulishindwa kuthibitisha kosa bila kuacha shaka dhidi ya Sheikh Ponda.
No comments:
Post a Comment