Tanbihi
ya Tanbihi: Kumbukumbu, Kusahau, na Zanzibar Mpya
Na
Harith Ghassany
Zanzibar 1950 |
Madhumuni
ya maandishi haya mafupi si kumjibu Mzanzibari mwenzangu na kaka yangu Ahmed
Rajab, mwandishi maarufu na mwenye kusifika barani Afrika. Nia yangu ni kuweka
sawa baadhi ya dhana zake kwa manufaa ya Zanzibar ndani ya wakati huu tulionao.
Mwandishi
maarufu wa riwaya, Milan Kundera, aliandika: “Mapambano ya binaadamu dhidi ya
nguvu [za dola] ni mapambano baina ya kumbukumbu na kusahau.” Suala kuu la kwa
kila Mzanzibari aliyeishi kabla au baada ya miaka 50 iliyopita ni, anakumbuka
au anakumbushwa nini, anasahau au anasahaulishwa kitu gani, na kwa nini? Suala
hilo ni la kwanza kabisa. Suala la chuki, kulipizana kisasi, au kusameheyana
bila ya kusahau, ni masuala ya mtitiriko wa suala kuu.
Kwa
hiyo, tunapolizungumzia suala la kumbukumbu na kusahau, la kwanza la kujiuliza
na kulizingatia ni, tunakumbuka au kusahau kitu gani? Na hicho kinachokumbukwa
ni kipi na jawabu yake inatokana na kundi au makundi yepi kati ya makundi
matatu aliyoyataja Rajab:
1.
La wahusika
2.
La walioshuhudiya
3.
La walioyasikiya
Rajab
kajiweka kwenye kundi la pili na kuzidi kujiaminisha na aaminike, ameandika
kuwa ana ushahidi wa maandishi wenye kuthibitisha yale anayoyakumbuka.
Nimefurahi sana kulijuwa hilo kwa sababu tuna mfano mzuri sana wa kufananisha
usahihi wa nguvu za historia ya maandishi ya wakati wa tukio na udhaifu wa
“historia simulizi” za baadae.
Napenda
kumuomba kaka yangu mpenzi atupatie japo kopi ya kumbukumbu za maandishi ya
mkutano wake na marehemu Abdalla Kassim Hanga pamoja na Wazanzibari wenzake
wawili, ili tupate kipimo cha kuyapima yale ambayo yeye ameyahifadhi kama ni
shahidi wa maandishi.
Lakini
turudi nyuma kidogo kwenye kumbukumbu na kusahau hata bila ya kujaribu
kuyakumbuka au kuyasahau yaliyotokeya katika mkutano wa miaka 47 iliyopita.
Kitabu
cha "Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru," (na si "Kwaheri Uhuru, Kwaheri Ukoloni," kama
alivyoandika Ahmed Rajab kwenye sehemu ya pili ya makala yake ya “Tanbihi”),
kina kurasa 496. Kati ya hizo ni kurasa tatu tu, ukurasa 267-270, zenye
kuuzungumziya mkutano wa London baina ya Wazanzibari watatu na Hanga. Lakini
hizo kurasa tatu ni muhimu katika muktadha wa maudhui ya kukumbuka na kusahau
kwa sababu, na Mungu awazidishie afya Ahmed Rajab na Bwana Salum Hamdan ambaye
anaishi Maskati, Oman, watu wawili hao wenye kuhusika moja kwa moja na suala la
changamoto za kuandika historia, Alhamdulillah, wote wawili wako hai na wana
akili zao.
Kwanza
napenda kumkumbusha msomaji kuwa Bwana Salum Hamdan ni wa kundi la pili, la
waliyoshuhudiya, kama anavyojinasibunalo Ahmed Rajab. Tafauti yao ni Ahmed
Rajab ameweka kumbukumbu ya maandishi ambayo narudiya tena, tutamshukuru sana
akitupatiya ili tujifunze namna ya kuzizidhibiti changamoto katika suala zima
la kuisajili historia na athari zake mbaya na nzuri za baadae.
Mzee
Salum Hamdan ni mzee wa hikma na busara. Nilipokwenda kuonana naye kwa mara
nyengine ili nizisajili kumbukumbu zake, aliniambia nisubiri mpaka
atakapozungumza na Ahmed Rajab kwa sababu kuna mambo ambayo huenda akawa
ameyasahau au hayakumbuki vizuri. Na hapo ndipo msomaji wa kurasa 267-270
katika kitabu cha “Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru,” atakutana na maneno
yafuatayo ya Salum Hamdan yenye kuonyesha kuwa alikuwa shahidi wa mkutano
ambaye aliamua kuzungumza na Ahmed Rajab kabla ya kuzungumza na mwandishi
(Harith):
“Sasa
tulivyokuwa London yeye [Ahmed Rajab] kataja watu watatu tu.” Ukursa 267.
“Nnavyokumbuka
mimi Oscar akatwambia sikilizeni bwana.” Ukurasa 268.
“Ndivo
navokumbuka mie na ndivo anavokumbuka Ahmed [Rajab].” Ukurasa 268.
“Mimi
skumbuki ile nilikwenda railway station. Kile mimi sijakumbuka. Kama ulivosema,
mimi nyumba nilikuwa naijuwa, sina haja ya Kasembe kunpeleka. Lakini inaweza
kuwa nimekwenda mimi na Kasembe kumpokea Ahmed Rajab. Yeye Ahmed kafikiri tu na
mie ni mgeni. Hajajuwa kuwa mimi na Kambona tunajuwana na jirani, na nyumba
yangu mie na yake si mbali.” Ukurasa 268. “Yeye Ahmed amekumbuka mambo
mimi sijayakumbuka.” Ukurasa 268.
Oscar Kambona |
Inasikitisha
kuwa mwandishi gwiji na mahiri kama Ahmed Rajab angalau kusema kuwa Salum
Hamdan alizungumza na yeye kama mwenzake kuyathibitisha yale walioyashuhudia
pamoja na Hanga kabla ya kumpa mkusanyaji (Harith) taarifa za mkutano wa
London. Ahmed Rajab kashindwa kuwa mkweli na muwazi na badala yake kaamua
kujaribu kunirushia ndoo ya tuhuma yenye uchafu wa “msimamo wa kisiasa,” “dhana
Fulani,” “kupotosha historia,” “kutoa maelezo kinyume na matukio halisi
yalivyotokea,” na kumumunya “wanaoendeleza chuki wakikataa kusamehe.” Hee!
Lumumba |
Kama
tayari nilikuwa nina dhana fulani, kwanini nilizitupilia mbali simulizi za kina
marehemu Ali “Lumumba” na wengineo, na kumfuata Mohamed Said Tanga na kuonana
na wazee wazito wa Dar es Salaam? Marehemu Mzee Hamza Aziz ambaye alikuwa
Kamishna wa Polisi aliniuliza suala dogo lakini zito. Aliniambia, “Sikiliza
kijana. Inataka kwanza ujiulize yale Mapinduzi ya Zanzibar yalipangwa huku
kwetu Tanganyika au kule kwenu Zanzibar?” Hapo ndipo nilipoipata ile Wazungu
wanayoiita “gestalt switch” au “paradigm shift.”
Aliyeshika Kiuno Katika Mavazi ya Polisi ni Inspector General of Police (IGP) Hamza Aziz Akiangalia Usalama Uwanja wa Mnazi Mmoja Mbele ya Kibarua Bar Nyerere Akihutubia Kumueleza Abdallah Kassim Hanga. Pembeni ya Hamza Aziz Kashika Kiuno ni Paschal Shija na Chini Yake Aliyekaa ni Kassim Hanga na Mbele ya Hanga Aliyekaa Mwenye Miwani Akitabasamu ni Mzee Omari Londo Mzee wa TANU |
Hassan Nasoro Moyo akisoma kitabu Kwaheri Ukoloni Kwaheri Uhuru |
Haikuwa dhana wala uhodari wangu. Na hiyo ilitokeya baada ya kupoteza kama miaka miwili Zanzibar kuyatafuta Mapinduzi mchana kwa vibatari na kandili ndani ya vichochoro vya Mji Mkongwe na N’gambo yake!
Dr. Harith Ghassany na Mohamed Said |
Hayo
yote bado sijayaona umuhimu wake kwa sababu kuna faida au somo gani katika
kukumbuka au kusahau kama Oscar Kambona ndiye au siye aliewaita Wazanzibari
kwake au kama alimtuma Kasembe? Muhimu Ahmed Rajab alifika kwa Oscar Kambona na
angelitaka angeliamua kutohudhuria mkutano baada ya kutambua kumbe Kasembe
hakuwaambia alikuwa amewachukuwa kwenda kwa kitimbakwiri na msaliti wa ukombozi
wa Afrika - Oscar Kambona. Haingii akilini hata kidogo kuwa Ahmed Rajab abebwe
tu na Kasembe kama pakacha la madoriani halafu ajikute anafunguliwa mlango na
Kambona!
Ali Mzee Mwenyekiti wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar akiwa na kitabu ''Kwaherri Ukoloni Kwaheri Uhuru,'' |
Rostam Aziz akiwa na kitabu Kwaheri Ukoloni Kwaheri Uhuru |
Na
ndio maana mazungumzo ya Hanga kwa mujibu wa Salum Hamdan niliyaweka katika
mlango wa “Hayeshi Majuto Yao.” Bwana Salum Hamdan ambaye yuhai amemnukuu
marehemu Hanga:
“…sisi
Mungu atusamehe, tumefanya mambo mengi ambayo mabaya, tumedhulumu, tumechukuwa
watoto na wake za watu, na Mwenye Enzi Mungu anisamehe na ninajuta kwa haya
nlioyafanya.” Ukurasa 269.
Kinyume
cha Salum Hamdan, Ahmed Rajab kayasahau maneno ya Hanga yaliyonukuliwa na Salum
Hamdan lakini ameyakumbuka maneno aliyojisafisha nayo Hanga kwa kumtusi
Kambona.
Salum
Hamdan ameeleza, “Lakini inasikitisa kuwa tangu wakati ule yeye [Hanga] yupo
pale London habari zishafika Cairo. Walioko Cairo maambassador wa pale
wameshapeleka habari Tanzania kwa Mzee Nyerere. Ikawa serikali inavosikia
wamekaa wakimgojea arejee tu. Yeye Hanga hajajuwa, wala sisi hatujajuwa.”
Ukurasa 270.
Anaandika
Rajab: “Kutoka Conakry, Hanga alirudi nyumbani, akipitia Cairo, ambako alikuwa
mgeni rasmi wa Ahmed Diria Hassan, Balozi wa Tanzania nchini Misri. Aliporudi
Dar es Salaam ndipo Hanga alipokamatwa kwa amri ya Rais Julius Nyerere na
akapelekwa Zanzibar ambako aliuliwa kikatili.” Ahmed Rajab hajui au hakumbuki
kuwa kumbe Hanga alikuwa ameshauliwa kutoka Cairo.
Kitabu
cha “Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru,” si kitabu kilichosimama juu ya midomo ya
simulizi peke yake. Kila mlango wa kitabu cha “Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru,”
una marejeo ambayo yanatokana na "primary" na "secondary" “sources.”
Kwenye utafiti wa kihistoria, "primary" “sources” ni marajeo ya watu
ambao walishiriki na waliyashuhudia yale ambayo wanayazungumzia.
"Secondary" “sources” zinaweza zikawa ni vitabu ambayo vinategemea
nini watu wengine wameandika na mwandishi mwenyewe si mwenye kuyashuhudia yale
yalioandikwa au kusemwa. Simulizi za wazee si zangu mimi bali ni za wazee
walioshiriki moja kwa moja au kwa karibu sana na tukio la Zanzibar la 1964. Na
ikumbukwe pia, historia ya maandishi inatokana na historia ya simulizi.
Yakumbuke ya Jibrili, Wahyi, na kukusanywa kwa Qur’an.
Kitabu
cha “Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru,” kina milango ishirini na moja.
Sasa
wacha twende mlango kwa mlango:
1.
Kwenye "Mapitiyo kwa Jumla" kuna endnotes (mapitio) 24.
2.
Mlango wa Kwanza una mapitio 25.
3.
Mlango wa Pili una mapitio 42.
4.
Mlango wa Tatu una mapitio 27.
5.
Mlango wa Nne una mapitio 6.
6.
Mlango wa Tano una mapitio 19.
7.
Mlango wa Sita una mapitio 11.
8.
Mlango wa Saba una mapitio 15.
9.
Mlango wa Nane una mapitio 20.
10.
Mlango wa Tisa una mapitio 14.
11.
Mlango wa Kumi una mapitio 2.
12.
Mlango wa Kumi na Moja una mapitio 16.
13.
Mlango wa Kumi na Mbili una mapitio 18.
14.
Mlango wa Kumi na Tatu una pitio 1.
15.
Mlango wa Kumi na Nne una mapitio 18.
16.
Mlango wa Kumi na Tano una mapitio 2.
17.
Mlango wa Kumi na Sita una mapitio 6.
18.
Mlango wa Kumi na Nane una mapitio 2.
19.
Mlango wa Kumi na Tisa una mapitio 84.
20.
Mlango wa Ishirini una mapitio 47.
21.
Mlango wa Ishiri na Moja una mapitio 3.
Na
ukiingia na ukazama ndani ya hayo mapitio ndipo utakapoweza kuunganisha na
kuona wapi penye udhaifu wa sahau na wapi ambapo sahau imepikuliwa na maandishi
ambayo hata mwenye sahau utamuona anajikuta hajui au hakumbuki kitu. Wakati
kweli nguvu za kukumbuka na kusahau zina uwezo wa kutupiga chenga, jee,
maandishi ambayo ni "primary sources" ambayo yako karibu sana ki
wakati na tukio lenyewe, hayana uzito wowote kwa gwiji wa fani ya habari na
uandishi mtamu kama ndugu yetu Ahmed Rajab? Au tuseme hakuwa na wakati na
alizisoma zaidi simulizi za wazee na ndio maana akaona udhaifu katika
"methodology" ya uandishi wa “Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru?” Au
alizilenga kurasa tatu tu kati ya kurasa 496?
Kuridhika
nako kuna miko yake. Mtu anaweza akakubali lakini asiridhike na jawabu wala
ushahidi. La msingi, kama nimekosea au nimedanganywa, kama ni muwongo au
nimezuwa; Alhamdulilllah, uhai na uwezo wa wengine kuja na maelezo mbadala na
yenye kusimama na hoja zenye ushahidi, bado upo. Suala: kwanini hawakosowi pale
wanapoona pametiwa chumvi au pamepotoshwa kwa kulitimiza lengo la mwandishi au
la watu fulani? Tumeweke wapi Salum Hamdan? Katika kundi la waliyoshuhudiya au
katika kundi walioyasikiya tu na kumkabidhi mwandishi wa makala hii?
Naanza
kuamini na kuridhika kuwa kuna tatizo kubwa zaidi hata kuliko kukukmbuka au
kusahau. Kitabu cha “Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru,” kimewashitusha,
kimewaporomosha na kuwashusha daraja baadhi ya watu katika majivuno na
majigambo waliyokuwa wakijivunia siku zote za Uwao. Kilichowashtuwa
zaidi kuwa kimepokewa na kukubalika na hata wale ambao hawakubaliani nacho
wameamuwa kukaa kimya.
Kimewashangaza
kuona kimefikia kua kigezo cha ushahidi wa kusadikika na kukubalika Bungeni,
hiyo ilikuwa fimbo. Walitamani angekuwa kiongozi au viongozi fulani kuipata
sifa hiyo. Ahmed Rajab anashaka juu ya nini hali anajuwa kuwa niliyoelezwa
yanatokana na mashahidi wa matukio hayo na washiriki wengine bado wahai na hadi
leo hakuna aliyeyapinga maelezo yao. Vipi yeye awe na shaka nayo! Yeye na walio
kama yeye hawaji na ushahidi au kitu kipya. Ni ushahidi wa kukosoa na kupanga
hoja kwa kutumia kipaji cha uandishi na mantiki za kupinduwa hoja.
Katika
mapambano baina ya kukumbuka na kusahau, kinachotakikana khasa ni ukombozi wa
kiroho kwanza, na wa kiakili baadae, wa kila Mzanzibari, anaeishi ndani au nje
ya Zanzibar na vizazi vyao. Ni ukombozi wenye kukubali, tena kwa hoja zenye
kusimama juu ya ushahidi juu ya yale ambayo yamekuwa yakiogopwa kuzungumzwa
hata kwa siri tena kwa zaidi ya nusu karne. Kinachotakikana ni uongozi mpya wa
kizazi kipya ambacho kiko tayari kuinusuru Zanzibar kutokana na maradhi ya
ukaidi na kujipambiya sifa ili kujitawadhisha na utawala.
Zanzibar
imezungukwa na bahari ya ushahidi wa kuvamiwa kutoka kila upande wa roho na
mwili wake lakini bado ina baadhi ya magenerali ambao wameamua kuingia kwenye
vita vya kuinusuru huku wakiwa hawana hakika baina ya kuuandama “umimi” au
kuyaweka juu kabisa maslahi ya Zanzibar na maslahi ya Wazanzibari ambao wengi
wao ni watu wema na wanyonge.
Kizazi
kipya hakikubali tena kudanganywa na kuingiliwa na mchwa wa miaka 51 iliopita.
Kizazi kipya ni aina ya mbao mpya ambayo mchwa hawezi kuila. Mchwa aliebakiya
Zanzibar na nje ya Zanzibar ni yule ambaye ameshaila fimbo ya Nabii Suleiman.
Na
hadithi ya Musa ndani ya nyumba ya Firauni haijamalizikia na tukio la
kihistoria liliomo ndani ya vitabu vitukufu vya Qur’an na Bibilia. Wakati hauko
tena mbali Firauni wa Zanzibar akatoa shahada huku anazama.
Hapo
ndipo suala la kukumbuka na kusahau litakapokuwa na maana mpya kwa Zanzibar
Mpya na vizazi vyake – Ameen.