Wednesday, 15 January 2014

Taazia: Shariff Hashim Saggaf 23 Februari 1943 - 13 Januari 2014


Shariff  Hashim Saggaf Alipokuwa Uingereza
Picha hii Imepigwa 1978

Hashim Sagaff Katika Uhai Wake Alikuwa Mtu Mwenye Kipaji Kikubwa Cha Kuzungumza kwea Fasaha
Kwa Lugha Nyingi -  Kiarabu, Kiswahili, Kiingereza, Kihindi na Kigogo



Taarifa ya kifo cha sahib wangu na kaka yangu Hashim Sagaff kilinikuta nikiwa ndani ya basi nikielekea Tanga.

Kwa kweli afya yake katika miaka hii michache haikuwa nzuri sana lakini si kwa kiasi cha kufikiria kuwa huenda akafariki.

Nimemjua Shariff Hashim kama mimi nilivyopenda kumwita, katika miaka ya mwishoni 1980 pale katika hoteli yao maarufu ya Salamander Mtaa wa Samora.

Haikuchukua muda mrefu tukawa marafiki wakubwa.
Aliyenijulisha kwake ni rafiki yangu na rafiki yake Tamim Faraj wote wakiwa wametokea Dodoma.

Kupitia Shariff Hashim nikawajua na ndugu zake, kaka yae mkubwa Dk. Mohamed Hashim, mdogo wao Ahmed Hashim na Hassan na jamaa zao wengi tu ambao tulikuwa tukikutana pale hotelini.

Shariff Hashim alikuwa msomi wa kuaminika na alikuwa na ujuzi mkubwa sana wa lugha ya Kiingereza. Nilikuwa nikipenda akizungumza Kiingereza.

Hakuna somo ambalo utakaloleta wewe kwake ikawa yeye awe hajui kitu.

Ukipenda unaweza kuanza na fasihi ya William Shakespeare hadi kitabu kilichotoka jana cha Mahathir Mohammed - ''A Doctor in the House.''

Ikawa kwa namna moja au nyingine tumeingiana katika mengi katika ulimwengu wa vitabu, siasa za Tanzania na nje na mengi ya kushughulisha akili.

Kuna kitu kimenijia hivi punde kwa kweli kiasi kimenistaajabisha na kuniachia simanzi na kumbukumbu ya rafiki yangu.

Kila mwezi wa Ramadhani baada ya sala ya tarwehe tulikuwa tunafanya darsa pale Mtaa wa Lumumba na Morogoro Road nje ya hoteli maarufu ijulikanayo kama ''Chef Pride.''

Masheikh tofauti huja pale na kutosomesha mambo mbalimbali katika Uislam. Katika miezi ya kula mchana hii huwa barza ya kawaida tu kama zilivyo mila za watu wa pwani kuwa jioni hukutana kwa mazungumzo na kunywa kahawa.

Lakini  ikiingia Mwezi Mtukufu wa Ramadhani barza hugeuka ikawa darsa.

Katika masheikh wakubwa wa kutajika katika ulimwengu wa Kiislam ni marehemu Sheikh Al Beit wa Mambrui, Mombasa. Yeye alikuwa kila akija Dar es Salaam wakati wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani alikuwa haachi kututembelea na kutoa waadhi pale barzani.

Lakini walimu wetu wa kila siku na kila mwaka ni Sheikh Mohamed Idd na Sheikh Burhani Bakari wote wawili ni wanafunzi wa marehemu Sheikh Mohamed Ayub wa Shamsiyya Tanga.

Shariff Hashim alikuwa mmoja wa wahudhuriaji wa darsa ile na katika wakarimu wake wakubwa.

Wakati darsa ikiendelea tulikuwa tunakunywa maji ya chupa, chai, uji wa ngano na vitafunio vya kutia hamu.

Siku nyingine huja jelebi lakini kaimati hii huwapo kuanzia Ramadhani Mosi hadi mwisho wa mfungo.

Nirejee katika lile nilisema kuwa kuna kitu kimenija kiasi kimenistaajabisha kwa hivi sasa baada ya kifo cha cha Shariff Hashim Sagaff.

Iko siku moja Ramadhani ya mwaka jana Shariff kaja darsani kama kawaida yake lakini baada ya kutohudhuria kwa muda mrefu kwa ajili ya maradhi.

Shariff alikuja ma vitabu vingi kavileta pale kugawa kwa mwenye kutaka.

Nathubutu kusema kuwa katika watu ambao aliwafikiria kuwapa hidaya ile mimi ni mmojawapo pamoja na rafiki yake mwingine Farouq Hussein.

Farouq yeye ni kama ''encyclopedia'' yake.

Ikiwa Shariff kakwama jambo na kwa haraka anatafuta jibu basi humuuliza Farouq iwe ni katika dini, tarikh (historia) au uchumi na Farouq palepale na kwa taratibu sana atamfahamisha na hapo itakuwa si Shariff peke yake atakaenufuika na ilm ile bali barza nzima.

Basi Shariff Hashim akaja na vitabu vingi katia kwenye gari yake akavileta pale darsani kila mtu achague anavyotaka.

Mimi nilichukua vitabu vingikwa kupapia tena katika ''hard cover.''

Katika vitabu hivyo kimoja ni ''Complete Works of William Shakespeare.'' Kitabu hiki kinapamba shubaka langu la vitabu nyumbani kwangu.

Nakumbuka siku moja usiku mwaka 1995 ghafla Shariff kanifuata nyumbani. Wakati ulikuwa umekwenda sana.

Nikashtuka kumuona kwangu mida ile. ''Kulikoni Shariff mboina saa hzi kwema huko?''
Mimi nikiishi Masaki na yeye akikaa Shariff Shamba ni mwendo kidogo.

''Kwema sana nimekufata kwa kuwa hili jambo siwezi kulalanalo lazima nikufikishie nikusikilize utaniambia nini.''

''Haya Bismillah...''
''Nimeamua kugombea ubunge Dodoma Mjini nipe fikra zako.''

''Wazo zuri sana...''
''Nitahitaji msaada wenu katika mbinu za kupata ushindi...''

Nini mimi naweza kufanya ili yeye apate ushindi sikuweza kujua.

Shariff Hashim ndivyo alivyokuwa.

Yeye ananijua mimi ni mpenzi wa CUF lakini aliweka udugu wetu mbele akijua kuwa nitamuunga mkono kwa ajili ya mapenzi yetu juu ya mapenzi yangu kwa CUF.

Shariff Hashim alishinda ubunge wa Dodoma na akaweka historia ya utendaji ndani na nje ya Bunge.

Akajenga urafiki na watu wengi ambao wengine akatupa ni sisi kuwa marafiki zetu akiwaleta barzani kwa mazungumzo.

Katika vipindi viwili alivyokaa Bungeni wengi watamkumbuka naamini kwa ule ujuzi wake wa kufanya majadiliano na fasaha ya lugha ya Kiingereza.

Katika yote Shariff Hashim alofanya moja lililogusa nyoyo za wengi ni pale alipofungua milango ya Jela ya Isanga kwa kuwapelekea wafungwa radio na magazeti wapate kusikiliza dunia ikoje huko nje na waburudike katika hali ile ya kuwa kifungoni.

Shariff alipata kunambia kuwa, ''Kweli ni wafungwa lakini bado wao ni binadamu kama binadamu wengine.''

Shariff Hashim kwa miaka mingi alikuwa katika uongozi wa Jamii wa Wayemini Tanzania na alisukuma mbele mipango mingi ya maendeleo. Mmoja  wapo ukiwa ujenzi wa shule iliyoko Chang' ombe na uendeshaji wa Radio Kheri katika radio hiyo akiwa mmoja wa wakurugenzi.

Shariff Hashim si kama wakati wote yeye alikuwa wa kugonga kichwa tu.

La hasha kuna wakati ukiwanae mtakwenda London wakati yeye mwanafunzi wakati wa ujana wake  katika miaka ya 1960/70.

Atakukumbusha habari za Woodstock, senema za Kihindi na nyimbo zake alizokuwa akizitazama Dodoma na rafiki yake toka udogo wao Dk Hajveyannis (sijui kama jina hili la Kigiriki nimeliandika sawa).

Shariff atakueleza habari za ''Rat Pack'' wacheza senema na waimbaji nguli wa Kimarekani - Frank Sinatra, Dean Martin, Sammy Davis...

Kuna watu wataumia sana kwa msiba huu labda hata zaidi yangu.

Watu kama Abdallah Jabir, Babu Isale, Sal Davis (Shariff Salim Abdallah), Farouq Hussein, Abdallah Miraj, Mahmoud Fundi,  Nizar Fazal...hawa walikuwa watu wake.

Hawa ni wana barza na wana darsa na wazungumzaji wake.

Mimi mailbox yangu itapata ukiwa.
Shariff alikuwa haishi kuniletea kila zuri alilopata katika mtandao na kwa hakika nikielimika sana.

Lakini siku nyigine akinichokoza akijua wazi katika hilo tutakuwa katika kambi pinzani.

Shariff ni mtu wa mijadala na wakati mwingine  huwa ana hamu ya ''ugomvi'' kutoka kwangu nami nikimjua Mwingereza wangu ''he is out looking for a good fight.''

Wamanyema hawajapigiwa wanacheza itakuwaje ngoma unapompelekea uwanjani kwake?
Lakini uzuri wa Shariff hutotoka ulingoni na tumbo tupu.

Siku zile ofisi yake iko pale kwenye hoteli yao ya Salamander, atanyanyua simu kupiga hotelini na atatoa ''order'' ya chai na vitafunio vyake.

Gumzo sasa litanoga na Shariff atawasha sigara.

Sisemi kuwa mimi nikimmudu Shariff la hasha wako watu wa uzito wake ndiyo wakiwezananae.

Mmoja wapo ni Nizar Fazal rafiki yake kipenzi na mwingine ni Tamim Faraj.

Wote wawili ni mabingwa wa kuhama kutoka katika misimamo yao na kuelekeza matanga yao kule wanapoona kuna upepo wa kuwafikisha bandarini.

Nizar ''akimsimanga'' Shariff akimwambia, ''Sikiliza Hashim usidhani kunipa mimi hii chai ya Salamander unapata khasara. Mimi nakuletea mambo makubwa hapa wewe umekaa tu kivulini.''

Siku moja tumekaa Shariff, Nizar na Tamim tunajadili mwendo wa serikali yetu.

Ghafla Nizar kakatiza, ''Nini mnapata tabu nenda Maktaba ya British Council kaazime kitabu kuhusu Tiny Rowland ''A Rebel Tycoon'' uone viongozi wetu wa Afrika wanavyochezewa na kuhongwa na Wazungu.''

Sote pale, Shariff Hashim, Tamim na mimi hatukuwa na habari ya kitabu hiki kuhusu Tiny Rowland wa Lonrho.

Sote kimya tunamsikiliza Nizar.

Kile kijembe sote tulijua kapigwa nani.
Shariff chama chake ndicho kinachoongoza nchi na magazeti yanakikomalia wakikituhumu kwa ufisadi.

Shariff hapo atazungumza Kihindi na Nizar kisha atakwenda kwenye Kiingereza na mwisho atarudi kwenye Kiswahili kwa haraka haraka kote huko apitapo.

Nyundo imepiga sawia kichwa cha msumari.

Nizar yeye ni Muhindi lakini anazungumza Kiswahili bila ''accent.''
Nizar akimuweza sana Shariff.

Msiba huu utakuwa umempiga sana Nizara Fazal.
Wapi rafiki yangu Nizar atapata ''punching bag'' inayoweza kuhimili ngumi zake?

Hizi ni kati ya siku zangu nzuri sana maishani mwangu na kipindi hiki ndicho kilichojenga katika moyo wangu heshima kubwa kwa Shariff Hashim Sagaff kama msomi makini na kuacha athar iliyodumu mpaka sasa.

Salamander haipo tena kama vile Shariff alivyokuwa katutoka.

Miezi michache iliyopita Shariff aliandika makala kuhusu katiba na hakutaka kuchukua mateka.

Magazeti maarufu ya Kiingerea na Kiswahili yalichapa makala ile.

Rafiki yake mmoja Khalifa Majid nikakutananae Msikiti wa Ibadh akanambia, ''Mohamed nenda kwa sahib yetu Sagaff mpe salamu zangu. Mwambie nilichostarehe katika ile makala yake ya Zanzibar ni kile Kiingereza chake basi.''

Khalifa Majid wazee wake ni kutoka Oman lakini yeye kazaliwa Singida na Shariff  Hashim Sagaff wazee wake ni kutoka Yemen lakini yeye kazaliwa Dodoma.

Khalifa Majid hakufurahia sana makala ile kwa kuwa Shariff Hashim kawasema ndugu zake.

Katika makala ile Shariff Hashim aliuita uchumi wa Zanzibar ''Uchumi wa kuuza mashokishoki,''
Alisema mengi.

Aliwaudhi wengi katika marafiki zake katika njia yake maarufu ya kukuchekesha katika ya kukushambulia.

''Uchumi wa mashokishoki'' sote tulikuwa tukicheka kila tukikumbuka maneno hayo.

Hii ilikuwa dhana mpya kabisa katika uchumi wa Zanzibar.
Shariff Hashim alikuwa bingwa wa kucheza na maneno.

Mimi sikushangaa na makala ile kwani nilikuwa namjua Shariff yeye ni mwana CCM ingawa siku nyingine hukitia chama chake chini ya chuma na juu akawa anapiga nyundo nzito kwa nguvu zake zote.

Shariff wakati mwingine alikuwa hana muhali.

Mimi nilimwandikia sahib wangu na kumshukuru kwa kunipa fikra zake kuhusu mchakato wa katiba na khasa jinsi anavyoona suala la serikali tatu na mengineyo kama ''uchumi wa mashokishoki.''

Hakika barza imeondokewa.
Shariff Hashim amekufa akiwa diwani wa kata ya Mchafukoge kwa tiketi ya CCM.

Ajabu wakati namaliza kuandika katika chombo changu anaingia Frank Sinatra anaimba, ''The World We Knew (Over And Over)''  huyu ni mwimbaji sote mimi na rafiki yangu tukimpenda.

Allah aiweke roho ya Shariff Hashim Sagaff mahali pema peponi.


Kushoto Kwenda Kulia: Sheikh Mohamed Idd, Mohamed Said na Khalifa Majid

Darsa la Mwezi Mtukufu wa Ramadhani 1434/2013
Abdallah Jabir Mmoja wa Waanzilishi wa Darsa la Ramadhani


Ukipenda Soma na Hii

TAAZIA: SHARIF HASHIM SAGAFF
 23 Februari 1943 – 13 Januari 2014



Taarifa ya kifo cha sahib wangu na kaka yangu Hashim Sagaff kilinikuta nikiwa ndani ya basi nikielekea Tanga. Kwa kweli afya yake katika miaka hii michache haikuwa nzuri sana lakini si kwa kiasi cha kufikiria kuwa huenda akatutoka. Nimemjua Shariff Hashim kama mimi nilivyopenda kumwita, katika miaka ya mwishoni 1980 pale katika hoteli yao maarufu ya Salamander Mtaa wa Samora. Haikuchukua muda mrefu tukawa marafiki wakubwa. Aliyenijulisha kwake ni rafiki yangu na rafiki yake Tamim Faraj wote wakiwa wametokea Dodoma. Kupitia Shariff Hashim nikawajua na ndugu zake, kaka yake mkubwa Dk. Mohamed Hashim, mdogo wao Ahmed Hashim na Hassan na jamaa zao wengi tu ambao tulikuwa tukikutana pale hotelini. Shariff Hashim alikuwa msomi wa kuaminika na alikuwa na ujuzi mkubwa sana wa lugha ya Kiingereza. Pamoja na Kiingereza Shariff Hasim akizungumza Kiarabu na Kihindi. Hiki Kihindi nadhani alikijua alipokuwa anasoma Aga Khan School, Dodoma. Nilikuwa nikipenda akizungumza Kiingereza. Kwa kuwa alikuwa na ulimi mzuri sana. Hakuna somo ambalo utakaloleta wewe kwake ikawa yeye awe hajui kitu.

Ukipenda unaweza kuanza na fasihi ya William Shakespeare hadi kitabu kilichotoka jana cha Mahathir Mohammed - ''A Doctor in the House.'' Katika hali kama hii ikawa kwa namna moja au nyingine tumeingiana katika mengi katika ulimwengu wa vitabu, muziki, siasa za Tanzania na nje na mengi ya kushughulisha akili. Kuna kitu kimenijia hivi punde kwa kweli kiasi kimenistaajabisha na kuniachia simanzi na kumbukumbu ya rafiki yangu.

Kila mwezi wa Ramadhani baada ya sala ya tarwehe tulikuwa tunafanya darsa pale Mtaa wa Lumumba na Morogoro Road nje ya hoteli maarufu ijulikanayo kama ''Chef Pride.'' Hoteli hii katika miaka ya nyuma ilikuwa ya rafiki yetu Salim Mahsen. Yeye akatupa nafasi katika hoteli yake iakwa kama ni ‘’club’’ yetu. Masheikh tofauti huja pale kutusomesha mambo mbalimbali katika Uislam. Katika miezi ya kula mchana hii huwa barza ya kawaida tu kama zilivyo mila za watu wa pwani kuwa jioni hukutana kwa mazungumzo na kunywa kahawa. Hapo wapo wapenzi wa CCM na wapo wapenzi wa upinzani wengi tu. Hawa ndiyo walikuwa wananogeshsa barza. Lakini  ikiingia Mwezi Mtukufu wa Ramadhani barza hugeuka ikawa darsa. Katika masheikh wakubwa wa kutajika katika ulimwengu wa Kiislam ni marehemu Sheikh Al Beit wa Mambrui, Mombasa. Yeye alikuwa kila akija Dar es Salaam wakati wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani alikuwa haachi kututembelea na kutoa waadhi pale barzani. Siku nyingine akitusomesha Sheikh Jabir Haidar Al Farsy na kaka yake Sheikh Ahmed Haidar kila wakija Dar es Salaam kutoka Zanzibar. Wote wawili ni wasomi vijana sana. Miongoni mwetu alikuwapo mjukuu wa Sheikh Ahmed bin Sumeit. Hakupenda kusomesha ila iwapo dharura atasema maneno machache.


Lakini walimu wetu wa kila siku na kila mwaka ni Sheikh Mohamed Idd na Sheikh Burhani Bakari wote wawili ni wanafunzi wa marehemu Sheikh Mohamed Ayub wa Shamsiyya Tanga. Shariff Hashim alikuwa mmoja wa wahudhuriaji wa darsa ile na katika wakarimu wake wakubwa. Wakati darsa ikiendelea tulikuwa tunakunywa maji ya chupa, chai, uji wa ngano na vitafunio vya kutia hamu na siku nyingine hupata matunda. Akipita muuzaji wa mchungwa au ndizi na mwana barza atumuita na kununua kwa ajili ya darsa. Siku nyingine huja jelebi lakini kaimati hii huwapo kuanzia Ramadhani Mosi hadi mwisho wa mfungo. Lakini la kufurahisha walikuwapo ‘’madaktari’’ kuwakataza wagonjwa wabishi wa kisukari kugusa vitu vitamu pale darsani.

Nirejee katika lile nilisema kuwa kuna kitu kimenija kiasi kimenistaajabisha kwa hivi sasa baada ya kifo cha cha Shariff Hashim Sagaff. Iko siku moja Ramadhani ya mwaka jana Shariff kaja darsani kama kawaida yake lakini baada ya kutohudhuria kwa muda mrefu kwa ajili ya maradhi. Shariff alikuja ma vitabu vingi kavileta pale kugawa kwa mwenye kutaka. Nathubutu kusema kuwa katika watu ambao aliwafikiria kuwapa hidaya ile mimi ni mmojawapo pamoja na rafiki yake mwingine Farouq Hussein. Farouq yeye ni kama ''encyclopedia'' yake. Ikiwa Shariff kakwama jambo na kwa haraka anatafuta jibu basi humuuliza Farouq iwe ni katika dini, tarikh (historia) au uchumi na Farouq palepale na kwa taratibu sana atamfahamisha na hapo itakuwa si Shariff peke yake atakaenufuika na ilm ile bali barza nzima. Basi Shariff Hashim akaja na vitabu vingi katia kwenye gari yake akavileta pale darsani kila mtu achague anavyotaka. Mimi nilichukua vitabu vingi kwa kupapia tena katika ''hard cover.'' Katika vitabu hivyo kimoja ni ''Complete Works of William Shakespeare.'' Kitabu hiki kinapamba shubaka langu la vitabu nyumbani kwangu. Labda Shariff Hashim alitaka kutuachai zawadi kabla hajaondoka. Sijui.

Nakumbuka siku moja usiku mwaka 1995 ghafla Shariff kanifuata nyumbani. Wakati ulikuwa umekwenda sana. Nikashtuka kumuona kwangu mida ile. ''Kulikoni Shariff mbona saa hizi kwema huko?'' Mimi nikiishi Masaki na yeye akikaa Shariff Shamba ni mwendo kidogo. ''Kwema sana nimekufata kwa kuwa hili jambo siwezi kulalanalo lazima nikufikishie nikusikilize utaniambia nini.''

''Haya Bismillah...''

''Nimeamua kugombea ubunge Dodoma Mjini nipe fikra zako.''

''Wazo zuri sana...''

 ''Nitahitaji msaada wenu katika mbinu za kupata ushindi...''

Nini mimi naweza kufanya ili yeye apate ushindi sikuweza kujua. Shariff Hashim ndivyo alivyokuwa. Yeye ananijua mimi ni mpenzi wa CUF lakini aliweka udugu wetu mbele akijua kuwa nitamuunga mkono kwa ajili ya mapenzi yetu juu ya ushabiki wangu kwa CUF.

Shariff Hashim alishinda ubunge wa Dodoma na akaweka historia ya utendaji ndani na nje ya Bunge. Akajenga urafiki na watu wengi ambao wengine akatupa ni sisi kuwa marafiki zetu akiwaleta barzani kwa mazungumzo. Katika vipindi viwili alivyokaa Bungeni wengi watamkumbuka naamini kwa ule ujuzi wake wa kufanya majadiliano na fasaha ya lugha ya Kiingereza. Katika yote Shariff Hashim alofanya moja lililogusa nyoyo za wengi ni pale alipofungua milango ya Jela ya Isanga kwa kuwapelekea wafungwa radio na magazeti wapate kusikiliza dunia ikoje huko nje na waburudike katika hali ile ya kuwa kifungoni. Shariff alipata kunambia kuwa, ''Kweli ni wafungwa lakini bado wao ni binadamu kama binadamu wengine.'' Shariff Hashim kwa miaka mingi alikuwa katika uongozi wa Jamii wa Wayemini Tanzania na alisukuma mbele mipango mingi ya maendeleo. Mmoja wapo ukiwa ujenzi wa shule iliyoko Chang' ombe na uendeshaji wa Radio Kheri na katika radio hiyo akiwa mmoja wa wakurugenzi. Shariff Hashim si kama wakati wote yeye alikuwa wa kugonga kichwa tu. La hasha.

Kuna wakati ukiwanae mtakwenda London wakati yeye mwanafunzi wakati wa ujana wake  katika miaka ya 1960/70. Atakutembeza Holborn na King’s Cross na Piccadilly Circus. Atakukumbusha habari za Woodstock, senema za Kihindi na nyimbo zake, senema alizokuwa akizitazama Dodoma na rafiki yake toka udogo wao Dk Hajveyannis (sijui kama jina hili la Kigiriki nimeliandika sawa). Shariff atakueleza habari za ''Rat Pack'' wacheza senema na waimbaji nguli wa Kimarekani - Frank Sinatra, Dean Martin, Sammy Davis Jr... au atakupa ujuzu wa kuigiza wa Marlon Brando.

Kuna watu wataumia sana kwa msiba huu labda hata zaidi yangu. Watu kama Abdallah Jabir, Babu Isale, Sal Davis (Shariff Salim Abdallah), Farouq Hussein, Abdallah Miraj, Mahmoud Fundi,  Nizar Fazal...hawa walikuwa watu wake. Hawa ni wana barza na wana darsa na wazungumzaji wake. Mimi mailbox yangu itapata ukiwa kwa hakika imefiliwa. Shariff alikuwa haishi kuniletea kila zuri alilopata katika mtandao na kwa kweli nikielimika sana. Lakini siku nyigine akinichokoza akijua wazi katika hilo tutakuwa katika kambi pinzani. Shariff ni mtu wa mijadala na wakati mwingine  huwa ana hamu ya ''ugomvi'' kutoka kwangu nami nikimjua Mwingereza wangu ''he is out looking for a good fight.'' Wamanyema hawajapigiwa wanacheza itakuwaje ngoma unapompelekea uwanjani kwake? Lakini uzuri wa Shariff hutotoka ulingoni na tumbo tupu. Siku zile ofisi yake iko pale kwenye hoteli yao ya Salamander, atanyanyua simu kupiga hotelini yeye mwenyewe akipenda kuiita ‘’restaurant’’ na atatoa ''order'' ya chai na vitafunio vyake. Gumzo sasa litanoga na Shariff atawasha sigara.

Sisemi kuwa mimi nikimmudu Shariff la hasha wako watu wa uzito wake ndiyo wakiwezananae. Mmoja wapo ni Nizar Fazal rafiki yake kipenzi na mwingine ni Tamim Faraj. Wote wawili ni mabingwa wa kuhama kutoka katika misimamo yao na kuelekeza matanga yao kule wanapoona kuna upepo wa kuwafikisha bandarini salama. Mdogo wake Ahmed wote walikuwa ofisi moja yeye alikuwa hampingi kaka yake na mwisho wa siku husimama na ndugu yake. Kama yao mkubwa Dk. Hashim akitokea kupita ofisini kwa wadogo wake na akalikuta lile zogo husikiza kwa muda kimya kasha akaaga. Yeye hakuwa anatia neno. Mimi nikiwatania mtu na ndugu yake nikisema, ‘’Vipi mimi nitashinda mjadala hapa wakati ndugu wawili wananichangia? Nizar ''akimsimanga'' Shariff akimwambia, ''Sikiliza Hashim usidhani kunipa mimi hii chai ya Salamander unapata khasara. Mimi nakuletea mambo makubwa hapa wewe umekaa tu kivulini.''

Siku moja tumekaa Shariff, Nizar na Tamim tunajadili mwendo wa serikali yetu.

Ghafla Nizar kakatiza, ''Nini mnapata tabu nenda Maktaba ya British Council kaazime kitabu kuhusu Tiny Rowland ''A Rebel Tycoon'' uone viongozi wetu wa Afrika wanavyochezewa na kuhongwa na Wazungu.'' Sote pale, Shariff Hashim, Tamim na mimi hatukuwa na habari ya kitabu hiki kuhusu Tiny Rowland wa Lonrho. Sote kimya tunamsikiliza Nizar. Kile kijembe sote tulijua kapigwa nani. Shariff chama chake ndicho kinachoongoza nchi na magazeti yanakikomalia wakikituhumu kwa ufisadi. Shariff hapo atazungumza Kihindi na Nizar kisha atakwenda kwenye Kiingereza na mwisho atarudi kwenye Kiswahili kwa haraka haraka kote huko apitapo. Nyundo imepiga sawia kichwa cha msumari. Nizar yeye ni Muhindi lakini anazungumza Kiswahili bila ''accent.''


Nizar akimuweza sana Shariff. Msiba huu utakuwa umempiga sana Nizara Fazal. Wapi rafiki yangu Nizar atapata ''punching bag'' inayoweza kuhimili ngumi zake? Hizi ni kati ya siku zangu nzuri sana maishani mwangu na kipindi hiki ndicho kilichojenga katika moyo wangu heshima kubwa kwa Shariff Hashim Sagaff kama msomi makini na kuacha athar iliyodumu mpaka sasa. Salamander haipo tena kama vile Shariff alivyokuwa katutoka.


Miezi michache iliyopita Shariff aliandika makala kuhusu katiba na hakutaka kuchukua mateka. Magazeti maarufu ya Kiingerea na Kiswahili yalichapa makala ile.

Rafiki yake mmoja Khalifa Majid nikakutananae Msikiti wa Ibadh akanambia, ''Mohamed nenda kwa sahib yetu Sagaff mpe salamu zangu. Mwambie nilichostarehe katika ile makala yake ya Zanzibar ni kile Kiingereza chake basi.'' Khalifa Majid wazee wake ni kutoka Oman lakini yeye kazaliwa Singida na Shariff  Hashim Sagaff wazee wake ni kutoka Yemen lakini yeye kazaliwa Dodoma. Khalifa Majid hakufurahia sana makala ile kwa kuwa Shariff Hashim kawasema ndugu zake Waunguja .Katika makala ile Shariff Hashim aliuita uchumi wa Zanzibar ''Uchumi wa kuuza mashokishoki,'' Alisema mengi. Aliwaudhi wengi katika marafiki zake katika njia yake maarufu ya kukuchekesha katikati ya kukushambulia kwa makombora. ''Uchumi wa mashokishoki'' sote tulikuwa tukicheka kila tukikumbuka maneno hayo. Hii ilikuwa dhana mpya kabisa katika uchumi wa Zanzibar. Shariff Hashim alikuwa bingwa wa kucheza na maneno. Mimi sikushangaa na makala ile kwani nilikuwa namjua Shariff yeye ni mwana CCM ingawa siku nyingine hukitia chama chake chini ya chuma na juu akawa anapiga nyundo nzito kwa nguvu zake zote. Shariff wakati mwingine alikuwa hana muhali na mtu. Atakusema hata kama utakasikrika lakini mwisho atakutaka radhi. Mimi nilimwandikia sahib wangu na kumshukuru kwa kunipa fikra zake kuhusu mchakato wa katiba na khasa jinsi anavyoona suala la serikali tatu na mengineyo kama ''uchumi wa mashokishoki.''


Hakika barza imeondokewa. Shariff Hashim amekufa akiwa diwani wa kata ya Mchafukoge kwa tiketi ya CCM. Ajabu wakati namaliza kuandika katika chombo changu anaingia Frank Sinatra anaimba, ''The World We Knew (Over And Over)'' huyu ni mwimbaji sote mimi na rafiki yangu tukimpenda.

Allah aiweke roho ya Shariff Hashim Sagaff mahali pema  peponi.
Amin.
Sheikh Jabir Haidar Al Farsy
Sheikh Ahmed Haidar Al Farsy

No comments: