UAMUZI
WA BUSARA WA TABORA
Kumbukumbu
ya Uchaguzi wa Kura Tatu 1958  
na Mohamed Said
na Mohamed Said
 KITABU KIPYA
KUHUSU HISTORIA YA KUDAI UHURU WA TANGANYIKA
Katika moja ya misiba ya Tanzania ni kutokuandikwa kwa ukweli historia ya wazalendo walopigania uhuru wa nchi hii. Vitabu vichache vilivyoandikwa vimejikita zaidi katika kujipendekeza kwa viongozi walio madarakani kuliko ukweli wenyewe ulivyokuwa. Hii imeifanya historia ya Tanzania kuwa sawasawa na mchuzi uliokosa viungo. Matokeo yake chakula kinakuwa doro hakina ladha. Sasa ni miaka hamsini toka siku ile kwa mara ya kwanza TANU katika mkutano uliofanyika Tabora ilipoamua kuingia katika uchaguzi mkuu wa kwanza licha ya masharti magumu yaliyowekwa na serikali ya kikoloni. Masharti ya kibaguzi na kudhalilisha ambayo TANU ilipania kuyakataa na kususa kushiriki katika uchaguzi ule kwa sababu mpiga kura alitakiwa ampigie kura Mzungu, Muasia na Mwafrika hna hapo ndipo lilipopatikana jina la kura tatu. Endapo hilo lingetendeka chama pinzani cha wazungu - United Tanganyika Party (UTP) ingepata mteremko na kuzoa viti vyote na hivyo kuingia katika Baraza la Kutunga Sheria. TANU ingebaki nje ya ulingo wa siasa na ikawa msemea pembeni.
Katika kitabu
hiki mwandishi anaeleza yale ambayo hayafahamiki kwa wengi ni kwa nini suala la
kura tatu lilitishia kuigawa TANU pande mbili. Moja likiwa na Mwalimu Nyerere
rais wa TANU na jingine likiongozwa na Zuberi Mtemvu, Sheikh Suleiman Takadir, Said
Chamwenyewe, Ramadhani Mashado Plantan na wazalendo wengineo. Katika kitabu hiki
mwandishi anamchukua msomaji na kumkutanisha na wazalendo ambao lau kama
wanahistoria wa leo wamewapuuza ukweli unabaki palepale kuwa bila ya kuwataja
hawa katika historia ya kupigania uhuru wa Tanganyika na hata historia ya
Mwalimu Nyerere mwenyewe basi historia hiyo si tu itakuwa haijakamilka bali
itakuwa historia ya uongo.
Mwandishi wa
kitabu hiki kwa hakika ni mpiga hadithi kwa jinsi anavyohadithia visa na mikasa
iliyowapata wazalendo pamoja na michango yao katika kurasa za kitabu. Mathalan
anawajulisha wasomaji wake mzalendo ambae wala hayumo katika vitabu vya
historia ya Tanganyika Mzee Mshume Kiyate, dalali wa samaki katika soko la
Kariakoo lile la zamani la miaka ya 1950. Katika soko lile mkuu wa soko alikuwa
Abdulwahid Sykes mmoja wa wazalendo 17 walioasisi TANU. Abdulwahid Sykes akiuza
kadi za TANU pale sokoni. Kwa ajili hii pale sokoni ndipo palipotoa wanachama
wa mwanzo wa TANU mmoja wapo akiwa Mzee Mshume Kiyate, mzee aliyeheshimika sana
mjini. Pale sokoni Kariakoo ndipo palipokuwa kituo chake cha mwanzo Mwalimu
Nyerere alipofikia kila alipotoka Pugu kuja Dar es Salaam akifika pale kumwona
Abdulwahid Sykes ofisini kwake na kisha kukutana na wazee wengine
wafanyabiashara pale sokoni kama Mzee Mshume Kiyate. Kitabu kinaeleza mchango
wa hali na mali wa Mzee Mshume Kiyate kwa Mwalimu Nyerere binafsi na katika
Baraza la Wazee wa TANU.  
Kitabu
kinamrejesha katika historia Said Chamwenyewe mzalendo aliyetoa kwa niaba ya
TANU taarifa ya hali ya siasa ya Tanganyika mbele ya Ujumbe wa Umoja wa Mataifa
unaoshugulikia makoloni ulipozuru Tanganyika mwaka 1955. Said Chamwenyewe ndiye
aliyeipatia TANU wanachama wake wa mwanzo kutoka Rufiji. Said Chamwenyewe
akipanda baiskeli kutoka Dar es Salaam hadi Rufiji huku akiuza kadi za TANU
katika vijiji vya njiani. Kitabu kimepambwa na picha hadimu sana ambazo
hazijapata kuonwa na yeyote kabla. Kuna picha ya Mshume Kiyate akiwa na Mwalimu
Nyerere, halikadhalika ya Sheikh Suleiman Takadir akiwa na Nyerere na John
Rupia na picha ya pamoja ya Mwalimu Nyerere na Dossa Aziz wakiwa na Wazee wa
Baraza la TANU ndani yake wakiwemo, Issa Nassir, Sheikh Haidar Mwinyimvua, Mwinjuma
Mwinyikambi, Jumbe Tambaza, Sheikh Suleiman Takadir, Mshume Kiyate, Said
Chamwenyewe na wengine wengi. Mwandishi kwa ufsaha na ustadi mkuu anaeleza historia
ya Yusuf Olotu mzalendo mwingine aliyesahaulika kutokea Moshi ambae peke yake alitembea
Kilimanjaro nzima kueneza TANU na ilipofika uchaguzi wa kura tatu ilibidi
afanye kazi ya ziada kuwarai Wachagga kujiandikisha kama wapiga kura wakatim
mwingine ikibidi ahutubie mikutano kwa Kichagga. Wachagga walikuwa na hofu kuwa
endapo watajiandikisha basi serikali ya kikoloni itawaendea kuwadai kodi kwa
mali walizonazo.
Mwandishi
anahadithia kwa ufasaha mkubwa kisa ambacho kwa muda mrefu ilikuwa siri. Vipi Mwalimu
Nyerere aliweza kuwapiku wapinzani wa kura tatu ambao walikuwa wengi katika
TANU si tu pale makao makuu Mtaa wa New Street Dar es Salaam bali hata
majimboni. Mwandishi anafichua  mkakati wa
siri uliopitika Tanga kati ya Mwalimu Nyerere na Amos Kisenge kwa upande mmoja
na viongozi wa TANU Tanga uliowakilishwa na 
Mwalimu Kihere, Hamisi Heri, Sheikh Rashid Sembe na wengineo. Kitabu
kinafichua ujanja wa Mwalimu Nyerere aliokuwanao kiasi cha kuweza kuwazidi
maarifa si maadui zake bali hata marafiki zake wa karibu na kupata kile
alichoamini yeye kuwa ndiyo mwelekeo unaofaa. 
Mwandishi
anaeleza jinsi TANU ilivyokuwa imetawaliwa na Uislam kiasi ambacho TANU haikufanya
jambo lolote kubwa bila ya kutanguliza dua. Hapa msomaji anaingizwa katika yale
ya ndani katika TANU ya wakati ule ya kufanya tawaswil na visomo Mwalimu
Nyerere lau kama alikuwa Mkristo akishiriki sawia. Msomaji atapata mengi kwa
kusoma kisa cha dua hii maalum kwa ajili ya kura tatu dua iliyosomwa katika
kijiji cha Mnyanjani nje kidogo ya mji wa Tanga. Kitabu kinafichua ni ujanja
gani aliotumia Nyerere kumwacha nyuma ofisini katibu wa TANU Mtemvu na
kumchukua Amos Kisenge badala yake kwendanae Tanga kupanga mbinu ya kupambana
na hila za Waingereza. Vipi Mtemvu ambae agenda ya kura tatu ilikuwa yake
alikubali apokonywe na kuamini kuwa Nyerere ataitetea kwa niaba ya Waafrika wa
Tanganyika ni swali linalotatanisha. Mtemvu aliposhtuka basi lilikuwa
limeshamwacha na Nyerere kaondoka. Matokeo yake alijuzulu TANU na kuanzisha
chama chake kipya Tanganyika African Congress akiwa na Said Chamwenyewe na
wazalendo wengine waliokuwa na msimamo mkali ndanin ya TANU.
Lakini juu ya
hayo yote msomaji atavutiwa sana na hotuba mbili za Mwalimu Nyerere alizotoa
wakati wa sakata la kura tatu. Hotuba ya kwanza ni ile aliyotoa ndani ya
mkutano kiasi ambacho aliweza kuzipiku hoja zote za wapinzani wa kura tatu na ya
pili ni ile hotuba ya machozi Mwalimu alipozungumza katika mkutano wa hadhara
Tabora sokoni na akalia na kuwaliza wasikizaji wake. Hata hivyo baadhi ya wana TANU
hawakuridhika na uamuzi wa TANU wa kuingia katika kura tatu. Walihisi kuwa
uamuzi ule haukuwa na maslahi na Waislam ambao ndiyo waliokuwa mstari wa mbele
katika kudai uhuru. Walijitoa na kuanzisha chama kipya All Muslim National
Union of Tanganyika (AMNUT). 
Juu ya hayo
yote sijui ni kwa utashi wake mwenyewe mwandishi au ni kwa sababu za uhariri
kitabu kimekuwa kimya kwa jambo muhimu sana katika historia ya kura tatu.
Mwandishi hakusema nani alipoteza katika kura tatu na nani alipata. Hofu kubwa
katika kura tatu ilikuwa itakuwaje Waislam walio mstari wa mbele katika
kupigania uhuru leo wanawekwa pembeni na Mwalimu Nyerere analeta watu kutoka
nje na wengi wao Wakristo kugombea viti vya TANU? Nukta hii ni katika mambo
muhimu sana ndani ya historia ya TANU. Ni katika jambo hili Sheikh Suleiman
Takadir alipotofautiana na Mwalimu Nyerere na likapelekea kwa Sheikh Takadir
kufukuzwa TANU kwa kosa la kuchanganya dini na siasa. Mwandishi hakugusa hata
kwa mbali kisa hiki muhimu. Kwa wale ambao wanaoijua kalamu ya mwandishi huyu
hili linaweza likawatatanisha sana. Lakini kitabu kina picha inayomwonyesha
Sheikh Takadir akiwa na Mwalimu Nyerere na nyuma yao wamesimama wahamasishaji
wa TANU waliokuwa wakijulikana kama Bantu Group iliyopigwa mwaka 1955. Picha
hii ya pamoja baina na Sheikh Takadir na Mwalimu Nyerere ni moja ya hazina
adhimu katika historia ya Tanganyika kwani inaaminika Sheikh Suleiman Takadir
alifutwa kabisa katika historia ya TANU na hakuna popote picha yake inaonekana.
Mwandishi anastahili pongezi kwa utafiti wake na kuandika kitabu hiki ambacho
kitasaidia kizazi kipya kuwajua wazalendo waliopigania uhuru wa Tanganyika
ambao leo hawatajwi. Hakika kitabu hiki kinatia nyama katika mifupa ya historia
ya TANU na historia ya Mwalimu Nyerere mwenyewe.
Wednesday, 04
March 2009
Kitabu kinapatikana:
- Dar es Salaam Bookshop
 - Duka la vitabu Chuo Kikuu
 - Ibn Hazim Bookshop Mkabala na Msikiti Manyema
 - Duka la vitabu mkabala na Msikiti Kipata
 - Khartan Bookshop Swahili na Narung’ombe
     karibu na Kariakoo Bureau De Change
 - Furaha Bookshop Msimbazi na Uhuru
 - Amnet Bookshop Msimbazi na Livingstone
 - Masomo Bookshop Zanzibar
 - Duka la Maalim Masudi Br ya 12 Tanga
 
Kwa wanunuzi wa jumla:
Abantu Publications Ltd Nyamwezi na Muhuro. Piga simu 0715 090 609 (Said
Mrisho) E mai
No comments:
Post a Comment