.jpg)
Twende mbele na turudi nyuma
na Ben Rijal
Msemo
wa Twende mbele na turudi nyuma ulikuwa ukitumiwa na wazee wetu katika siku za
kugombania Uhuru na hata wengine kuhoji nakusema iweje tushakwenda mbele kisha
turudi nyuma kipi tuanchokitafuta huko nyuma? Ukiziangalia hoja mbili hizo kila
moja ina mantiki iweje ushafika mbele unaangalia nyuma kuna nini
unachokitafuta? Kwa mazungumzo ya kawaida utasema hivyo ndivyo, lakini ndani ya
maendeleo nikusema kuwa lazima ushafika mbele urudi nyuma kujitathmini, ikiwa umefuzu
au umeharibikiwa ndipo utapofanikiwa.
Wengi
huwenda mbele tu mithili ya nguruwe mwitu asiojua kwenda mbele na kurudi nyuma.
Nilipokuwa nashiriki katika usasi wa nguruwe mwitu mahasidi wa mazao ya
wakulima ilikuwa tukifukuza nguruwe saa nyengine humuachia kisha tukafwatilia
njia yake ile aliopita nakuweza kumkamata kwa kirahisi kwa kuwa nguruwe mwitu
anajua kwenda mbele tu hajui kurudi nyuma. Siku zote kwenye usasi mukimkosa kumkamata nguruwe aliokuponyokeni kumua inabidi
muifwate ile njia muliomkuta kabla kisha kumsubiri siku nyengine mtamkuta
kapita hapo hapo bila ya kubadilisha upande ndio saa nyengine utawasikia weledi
wakisema umekuwa kama nguruwe mwitu njia yako hio kwa hio?
Najaribu
kujenga hoja ili nilitakalo kukieleza kieleweke, katika kwenda mbele na kurudi
nyuma, nitaanza na Mapinduzi, neno Mapinduzi kila mwenye lugha yake amelita kwa
namna yake mfano Kiafrikana hutamkwa Rewolusie, Ki-Albanian
Revolucion, Ki-Arabu Thawra ( ثورة), Ki-Indonesia Revolusi, Ki-Persia Inkilabu (انقلاب),
Ki-Vietnam Cuộc
cách mạng,
Ki-Welsh Chwyldro neno hilo lina maana mmoja na lengo moja nalo nikufanya na
kuleta mabadiliko lakini kila mmoja analitamka kivake.
John
Adams Rais wa pili wa Marekani aliyafafanua Mapinduzi kwa kusema
“mapinduzi huleta athari kabla
hayajatekelezwa, siku zote mapinduzi yapo katika fikra za watu, mapinduzi sio
chochote sio lolote lile ila ni mabadiliko yaliomuhimu yakiwa na misingi, hisia
na furaha kwa watu hayo ndio mapinduzi ya kweli ya Amerika” na mwanaharakati wa
mapinduzi aliojizatiti kutaka kuona haki na usawa katika ulimwengu uliogubikwa
na madhila na ubeberu raia wa Argentina aliojiunga na vugu vugu la mapinduzi ya
Cuba huyo sio mwengine ni Che Guevera anayachambua mapinduzi kwa kusema “mapinduzi
sio tunda la epuli (apple) huanguka wakati linapoiva, ukweli lazima ulifanye
lianguke,” na akaendela kusema “moja ya kazi nzito na ya mwanzo ya mapinduzi ni
kuelimishwa watu. (“The first duty of a revolutionary is to be educated.”
Mapinduzi yametekelezwa kwingi tu duniani kwa lengo kuu lakuleta mabadiliko ya
haraka na kuweza kuwaelimisha na kuwafunza wananchi kupata maendeleo na kuishi
katika maisha ya matumaini. Mapinduzi yamefanyika Marekani, Urusi, Ufaransa,
Nigeria, Ghana hata Zanzibar na kwengineko.
Zanzibar
ilijaribu kufwata mkondo ule ule wa kimapinduzi duniani na kujitahidi kuyafanya
maisha ya wananchi wake kulingana na kutoa matumaini, kati ya hayo ilikuwa elimu,
kilimo, afya, biashara na sekta mbalimbali ziliwekwa mikononi mwa Serikali na
kuweza kuiweka nchi ya Kimapinduzi kwa mwananchi wake kuwa na matumaini na
maisha yake ya baadae ya kujiweza kujikimu.
Moja
kati ya matunda hayo Serikali hio ya mapinduzi ilianzisha kitu kiitwacho
BIZANJE ambacho kiliwaweka wananchi kutohangaishwa na maisha yao ya kula na
kuvaa, maana ya BIZANJE ni Biashara za Nje na fikra hii iliasisiwa na muumini
wa Mapinduzi halisi katika visiwa hivi naye ni Dr. Ahmed Rashid aliokuwa
daktari mahiri wa wanyama, msomi huyu aliobobea fikra, yake ilikubalika na Rais
wa kwanza wa Zanzibar bada ya mapinduzi, Mheshimiwa Abeid A. Karume kumtaka
kuanzishwe kitu hicho nacho ni Biashara za Nje na kilichokuweko kikitekelezwa
ni ile dhana ya kijamaa wananchi wote mnatumia kitu cha aina moja au
vinavyolingana tena viliopo kwenye viwango, hapo ikawa Michele mizuri ikiliwa
na kila Mzanzibari, unga bul bul, sabuni za kila aina iwe Lux, Night Castle,
Life Buoy, Pears, Baby Soap zote zikipatikana, maziwa ya kibati yawe Tweco,
Ng’ombe wanne n.k. Samli za kila aina bila ya kuisahau Kismayou, kisha aina
mbalimbali za nafaka iwe Njugu mawe, Kunde, Maharagwe, sabuni za kufulia Omo,
Sunlight na nyenginezo, vitambaa vya suruali kina terelini. Mabuku ya kuandikia
na kalamu za kila aina na penseli zake zikiuzwa na kukaribia kusema ni bure.
BIZANJE
ilimuwezesha mnunuzi kuona sio ananunua anaona kama anatunukiwa kwani kila
mmoja alikuwa awe wa juu au yule hoe hahe wote wakimudu kuvinunua hivyo vitu na
kuvifurahia na kusema Shabasha sasa haya ndio maisha.
Bahati
mbaya fikra hizi huwa hazikubaliki na wale ambao unyang’anyi na ubepari umewazunguka
katika magenzi yao kwahio bahati mbaya ikatokea kwani wale waliokabidhiwa kuendesha
BIZANJE ndio waliokuwa wanafuja na hata yale maduka yaliokuwa yakiendeshwa na
Serikali yakawa kila siku zikenda zikiwakatisha tama watu kwa kuwa kunaanza
kukosekana yale mahitaji ambayo wananchi wakiyafaidi. Ureda ukapotea mambo
yakawa ni msege mnege.
Nilizungumza
na mmoja kati ya washika usukani katika uongozi nikamwambia wakati umefika
kurudisha BIZANJE alinistaajabu na kunambia “watu wanakwenda mbele wewe unarudi
nyuma, sasa ni biashara huria, biashara huru anayetaka anaingia kwenye
ushindani, siku za Serikali kufanya biashara ziko wapi?” Hakuwa tena anataka
kunisikiliza na fikra za kijamaa akaja na mazungumzo mengine kabisa na
nikajiona nimepwelewa.
Ukweli
sio mwenye kupinga juu ya biashara huru nitasema biashara huru ziwepo na
waendelee wananchi kuziendesha hizo biashara lakini bado Serikali ingeweza
kuleta vile vya mahitaji yalazima na kuviwekea katika maduka maalumu na kuona
hivyo vilivyoletwa vinauzwa katika bei hio iliopangwa itakayowezwa kila mmoja
wetu kuimudu, hapo kina Pangu pakavu mithili yangu tungesema Shabash tunarudi
tulikotoka kutokana na kujitathmini pale tulipo kwa kurudi nyuma.
Ukiangalia
katika pande zote mbili za Muungano fikra kama hizi zilipoasisiwa wengi
walishindwa kuzifahamu badala yake wakawa mstari wa mbele kuzivuruga, wengi
wanazitamani zirudi hawajui zitarudi kwa njia gani, lakini inawezekana tena
sana kama alivyopata kutushauri aliokuwa Naibu Waziri Mkuu wa Malaysia pale ujumbe
wa Visiwani ulipotembelea Malaysia mwandishi alikuwemo katika msafara huo, Anwar
Ibrahim alitwambia “sio kila kitu mubinafsishe vyengine viendelee kubakia
mikononi mwa Dola.” Malaysia waliweza kuwachukua wasomi katika fani mbalimbali
nakuwataka waendeshe biashara matokeo yake nikuwa kutokana na elimu na ujuzi waliokuwa nao walifanikiwa
wao kuboresha maisha yao na kuiongezea kipato taifa la Malaysia kwanini nasi
hatwendi huko?
No comments:
Post a Comment