Thursday 30 April 2015

KUTOKA JF PROF. IBRAHIM NOOR NA TARIKH YA ZANZIBAR AKIREJEA KITABU CHAKE "TANZANIA NA PROPAGANDA ZA UDINI"

Ndugu msomaji ingia hapo chini kwa somo kamili:

Bonyeza Kiungo Iki >> : #post12605365



MAKALA YA PROF. IBRAHIM NOOR

Siku zote, lengo kuu la propaganda ni kuzibaka akili za watu na kugandisha katika bongo zao yale wanayoyataka wana-propaganda; na wana propaganda hupendelea sana kuwapata watoto wakiwa wangali wadogo kuwajaza hizo propaganda zao ili hata wakiwa watu wazima uwe mgando huo umeshatapakaa kama kensa katioka bongo za walengwa ili zisiweze tena kuganduka. Hawakukosea wavyele wetu waliponena kuwa “udongo upatilize ungali umaji.”

Na vipi unaweza kumtambua mtu aliyelishwa propaganda kali, khasa za ubaguzi/ugozi na za udini? Kwanza utamwona ni mtu ambaye huwezi kumwambia lolote tafauti na zile sumu alizolishwa akalikubali, hata likiwa na ukweli na mantiki ya hali ya juu kabisa. Propaganda walizogandishwa bongoni mwao tokea utotoni huwafanya wajione wanajua kila kitu na wewe huelewi chochote! Wakati ni wao walioseelea na mtizamo finyu.

Mawazo ya mtu kama huyo hakika ni ya kusikitisha sana khasa kwa vile wengi wao, baada ya kuharibiwa akili zao shuleni, uwezo wao wa kufikiri kama bin Adam anavyotakiwa afikiri kwa kutumie akili yake ili kumtafautisha na mnyama, hupewa nafasi na wadhifa wa kuweza kuwaathiri watu wengi kwa fikra zao zilizojaa ubaguzi, kwani fikra zao hujikita katika ufinyu wa propaganda walizomiminiwa bongoni mwao tokea walipokuwa shuleni utotoni mwao na kuwafanya wakawa hawana haja ya kujua mengineyo ambayo huenda yakawatoa katika gereza la mawazo mgando waliyonayo; yaani, wametosheka na yale waliyosomeshwa shuleni hata yakiwa si ya kweli na yamejaa ubaguzi na udini na yana khatari kwa nchi. Kwa mfano, kiwango na mgando wa “ilimu” alionao Pasco umempelekea kuandika yafuatayo:

“Tangu Mlango wake wa Kwanza unaohusu “Taarikh ya Kuwasili Kwa Wabantu, Washirazi na Waarabu Pwani ya Afrikaya Mashariki.” ameanza na maurongo yaliyokubuhu!”

Anatuelezea haya hata kitabu hajakisoma! Lakini tusistaajabu, kwani, kama nilivyoeleza, hii ndio athari na lengo khasa la propaganda.  Waliotekwa na propaganda hawahitajii kusoma chochote kwanza, wao wameshafanywa, kwa njia za kipropaganda, waamini tokea utotoni mwao fikra fulani, basi wametosheka nayo. Bila ya kuzisoma hoja na ushahidi uliotolewa kitabuni na bila ya yeye kututolea ushahidi wowote wenye kuonesha kuwa yaliyoelezewa kitabuni ni ya “maurongo yaliyokubuhu!” anatutaka tuzikubali kauli zake kama yeye alivyokubali kumiminiwa propaganda za udini na ubaguzi alipokuwa shuleni hata ikamfanya yeye binafsi, kuwa na chuki kubwa sana dhidi ya wale alioambiwa awachukie na kuwabagua. Soma barua yake kwa makini na utamuona vipi alivyotopea katika chuki na vipi yeye (na wengine kama yeye) alivyokuwa hahitajii kusoma kwanza kabla hajaamua kumshambulia mwandishi wa kitabu pamoja na anayodhania ameyaandika! Ni muhimu kwake binafsi kuendelea na fikra mgando za chuki kuliko kuutafuta ukweli na kuwa mtu huru kimawazo.

La kusikitisha pia ni kumwona mtu huyohuyo anajinata kuwa kasoma sana na anaelewa vya kutosha hadi kufika kuwa na “sixth sense.” Mahabusi wa propaganda, khasa zikiwa za udini na ubaguzi, hawezi kabisa kutumia akili yake na akili hiyo kumwongoza hadi kufikia uamuzi unaokubali ushahidi wowote wala hoja yoyote inayopingana ufinyu wa propaganda za ubaguzi na za udini alizojazwa nazo. Nakariri, propaganda haimruhusu hata kuwa na “comon sense” wacha kuwa na “sixth sense” kwani mtu huyo huwa kama kasuku anayerejelea yaleyale ya chuki alizojazwa nazo tokea utotoni mwake. Jinginelo lolote, hata likitolewa ushahidi gani, hawawezi kulikubali kwani propaganda huwaondoshea hata “common sense."

Sifa ya pili waliyonayo ni kuwa daima kiumbe kama huyo anataka kulazimisha tukubali tu yale anayoyaamini yeye. Kwa mfano, lazima iwe ni Wabantu ndio wenyeji asilia wa pwani ya Afrika Mashariki. Wala hana hamu ya kutaka kujua nini wameandika mabigwa wa taarikh ya uhamiaji wa Wabantu na lini wamewasili katika upwa huo, ingawa siku hizi huna haja ya kuvitafuta na kuvisoma vitabu vya mabingwa wenye kuijua taarikh ya Afrika. Fungua hata mitandao na uangalie wajuzi wanatuelezea nini kukhusu uhamiaji wa Wabantu na khasa wapi walipotokea. Hakuna hata mmoja katika mabingwa hao anayedai kuwa Wabantu walitokea Afrika Mashariki na kuelekea Afrika Magharibi. Wote wanatuelezea kuwa ama wametoka Afrika Kati na kuelekea mashariki na Kusini, au wametokea Afrika Magharibi na kuelekea Mashariki na Kusini, na mabingwa wenye kusema haya ndio wengi zaidi. Fungua mtandao uandike “Bantu Migration” ujionee mwenyewe kwa maneno na kwa ramani kukhusu uhamiaji wao Wabantu. Lakini, kama nilivyosema kabla, waliolishwa vidonge vya sumu ya propaganda za udini na ubaguzi hawawezi kukubali lolote hata likiwa na ukweli wa aina gani ila propaganda ile ile waliosomeshwa tokea utototoni. Inasikitisha kushuhudia namna na kadiri ya vidonge vya sumu na chuki zilivyofanya kazi ya kuharibu akili za watoto wetu katika kuwasomesha historia.

Jambo linalomuuma zaidi ni kwanini Waarabu waweze kuwa wenyeji wa pwani ya Afrika Mashariki; hawezi kukubali Mwarabu awe raia wa Tanzania wa daraja ile ile moja sawa na Mbantu na Mtanzania yoyote yule. La! Hasha. Wao walivyokuwa wabaguzi kweli, wanataka pawe na matabaka ya uraia. Angalia mfano wa manenno yake mwenyewe:

“Yaani hapa huyu Mwarabu, anataka kuwafanyia Afrikanization hawa wavamizi wa Kiarabu ili kuwahalalisha eti na wao, ni wenyenyeji halali wa Afrika Mashariki…”
Angalia na mfano mwingine wa ugozi wake:

“Lengo ni kuzuia kinachoweza kuja kuwapata Waarabu wa Afrika Mashariki na sana sana Waarabu wa Zanzibar ambao wametoka kwao Omani juzi juzi tuu mwaka 1832 wakiongozwa na Sultan Sayyid Said aliye yahamisha makao yake makuu toka Oman hadi Zanzibar! Huyu sio tuu ni mvamizi bali pia ndiye mporaji mkuu, aliyejitwalia visiwa hivyo kama ameviokota as if hakumkuta mtu yoyote ili hali wenyeji walikuwepo! Siku ile ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar, siungi mkono mauaji yoyote ya Waarabu, bali wangeambiwa tuu kistaarabu, wafungashe kilicho chao, wao na wazalio wao, wajirudie kwao Omani walikotoka na kutuachia visiwa vyetu!”

Yaani huyu mbaguzi kutoka Bara ambaye Zanzibar si kwao hata chembe anafika kusema kwa ujeuri kabisa na kwa kinywa kipana kuwa mwenye asili ya Kiarabu hata akiwa ni wa kizazi cha ngapi hapo Zanzibar asiwe na haki yoyote ya uraia na uananchi, bali yeye Pasco mzalia na mkaazi wa Bara ana haki zaidi na kamili Zanzibar kuliko huyo Mzanzibari! Kama maneno haya ya Pasco na wenziwe kama Wahishimiwa akina Lukuvi na Sitta si onyo kubwa sana kwa Wazanzibari kukhusu nia zao na lengo lao hawa Wabara wenye chuki dhidi ya Wazanzibari, basi Wazanzibari endeleeni kulala mkione cha mtema kuni. Ishara zote za ubaguzi wao ziko wazi kabisa, na mwenye macho haambiwi “tazama.”

Waarabu wengi, na wengi walikuwa watu wa kawaida tu na wengine walikuwa mafakiri, waliuwawa kwa ghadhabu kubwa sana na wabara kama hawa, kwa bunduki, mapanga na mashoka kama nguruwe mwitu, ikisha anatuambia kuwa yalikuwa “Mapinduzi matukufu.” Yatakuwaje matukufu na ilihali roho za raia wengi sana ziliteketezwa na wavamizi kutoka Tanganyika ambao tumewashuhudia kwa macho yetu na kuwasikia kwa lafdhi zao za kibara wakipita mitaani mwetu na kunadi: “Arabu uwa, Muhindi uwa Muzungu siguse.” Utukufu ni sifa ya Mwenye-enzi Mungu. Mauwaji ya halaiki ya raia na uraruwaji wa wanawake, ufungwaji wa wengi bila ya sababu, unyanyasaji, unyang’anyi wa mali za raia, uadhibishwaji wa watu waliokuwa hawana kosa lolote ila kuwa hawakubaliani na siasa za Karume na Kambarage, zinakhusiana nini na “utukufu”? Nini kilichotukuka katika kutenda maovu haya yaliyokatazwa na Mwenye-enzi Mungu Mtukufu?
Pasco anendelea na haya yafuatayo:

“Prof. Ibrahim Noor Shariff, ni 'ill motive!' Tangu Mlango wake wa Kwanza unaohusu “Taarikh ya Kuwasili Kwa Wabantu, Washirazi na Waarabu Pwani ya Afrikaya Mashariki,” ameanza na maurongo yaliyokubuhu!, hapa anadanganya wazi mchana kweupe kwa maushahidi yake ya uongo kwamba eti Waarabu wamefika Pwani ya Afrika Mashariki maelfu ya miaka iliopita kabla ya Wabantu, tangu karne ya 16 B.K! The ill motive ya mlango huu ni kuonesha kwamba Waarabu si wageni bali ni wenyeji wenye haki hapa sawasasa kwenye Pwani ya Afrika Mashariki sawa na wenyeji wengineo.”

Kwanza anaanza kwa kunishambulia binafsi kwa dhana zake mwenyewe wala si kwa hoja nilizozitoa alipoandika kuwa mimi “ni 'ill motive!'” Tukiacha na Kiingereza chake chenye makosa, suala ni: amejuaje kama mimi nina sifa mbovu hiyo? Kitabu hajakisoma alau akadai kuwa amenisoma vizuri kabla hajautoa uamuzi wake huo, maajabu haya! Aliyekuwa "ill-motivated" ni nani hapa!

Anaonesha wazi kuwa taarikh ya Waarabu haijui zaidi ya hiyo aliyosomeshwa shuleni iliyojazwa chuki ndani yake. Hajui kabisa kuwa Waarabu ni watu walioanza kusafiria Bahari ya Hindi miaka elfu nyingi kabla, na walielewa taratibu za pepo za Musim na kufikia nchi zote ziliko pwanipwani ya Bahari ya Hindi. Haelewi kuwa taarikh ya Bara Arabu na nchi za Afrika kama Habash/Ethiopia zimefungamana kwa zaidi ya miaka elfu kumi. Taarikh kama hiyo haingii katika hisabu za akili yake! Kama sabini katika mia ya Waarabu wanaasili ya Afrika na wanaishi Afrika kama ni wenyeji makwao kutoka Sudan hadi Moroko.

Haelewi pia kuwa Waarabu wengi ni Wasemiti, na jamaa zao wako kutoka nchi za Ghuba hadi Nigeria. Kuwa Wahausa wa Afrika Magharibi ni katika jamaa zao Waarabu, na Waethiopia ni jamaa zao wa karibu sana, na hawa wote wako mbali kabisa kiujamaa na Wabantu. Afrika haina watu wa asili moja tu. Kuna makundi mengi mbalimbali ambayo Waingereza huita “race.” Nikupe mfano mmoja utakaokufanya ufikiri. Unadhani Wabaka (mbilikimo) na Watutsi wana asili moja kwa sababu rangi za ngozi zao zimekoza?

Barua yake yote Pasco ni mfano dhahiri kabisa wa mtu aliyefunzwa propaganda za udini na chuki zilizotopea khasa dhidi ya wenye asili ya Kiarabu. Soma na haya aliyoyaandika kwa kifua mbele: 

“Hili swali la Waarabu wamekujaje Pwani ya Afrika Mashariki, litakuja kurudi tuu mbele ya safari hivyo ushauri wangu, ni kujituliza tuu na kuishi kwa unyenyekevu wa hali ya juu sana kwa kujihesabu wanaishi hapo kwa hisani tuu, vinginevyo watatimuliwa warudi kwao Oman walikotoka, wao na vizalia vyao!.”
“Hizi historia za kutunga tunga kutaka kuwahalalisha madhalimu hawa waliowauza mababu zetu kama bidhaa! hazitasaidia kitu! no wonder kila siku wanashinda uchaguzi lakini kamwe hawatakabidhiwa nchi, na 2015 watashinda tena na moto ni ule ule! Mwarabu atoke kwao, aje akutawale, babu zako awauze, kisha mumpindue halafu leo mumrudishe eti kisa amechaguliwa! hii haitakaa itokee!.”

Huyu kiumbe kutoka Bara anawaambia Wazanzibari wenye asili ya Kishirazi, Kiarabu, Kihindi na nyinginezo, kuwa hawana haki yoyote ile kwao Zanzibar. Wenye haki ni wao Wabara! Kama huu si ujeuri mkubwa sana na ubeberu akhasi ya ukoloni, basi sijui tuuitaje! Ikisha anawaambia Wazanzibari hao kuwa hata wakishinda chaguzi vipi, wao wakoloni ndio watakaoamua, na wameamua kuwa Zanzibar itabakia kuwa koloni lao hata Wazanzibari wote wakitaka kutokana na ubeberu huo unaowakandamiza. Kwa hivyo akina Sefu na Jussa na Mansuri na Moyo na wafuasi wenu ndiyo mmeshapewa tahadhari na mabeberu wakoloni wepya kutoka bara wanaotaka kukutieni nyote vitanzi wakunyongeni, msiseme hamkutahadharishwa na waliyoyakusudia. Kivitendo wameshawauwa Wazanzibari 1961, 1964 na kuendelea. Wanadhani ukhabithi wao na mauwaji wanayoyafanya mara kwa mara ndiyo yatawawezesha kuitawala Zanzibar milele. Yaguju!
Huwezi kuzungumza na mtu ambaye kwake yeye taarikh ya Waarabu Zanzibar na pwani ya Afrika Mashariki imeanzia na Sayyid Said mnamo Karne ya Kumi na Tisa tu! Ni shida kubwa sana kumsomesha mtu taarikh asiyotaka kuisikia, na hakuna viziwi zaidi kuwashinda wale wasiotaka kusikia. Na uziwi unakufika upesi sana iwapo utotoni umepikwa na propaganda za chuki zinazokusudia kuufunga ubongo wako usiweze kufikiri kama mwana Adamu anavyotakiwa afikiri.


Ibrahim Noor

No comments: