Saturday, 19 September 2015

MAHOJIANO YA SIKU ZA MWANZO ZA MWL. NYERERE NA SAFARI YAKE UNO 1955





Mwl. Nyerere baada ya kujiuzulu ualimu aliishi nyumbani kwa Abdulwahid Sykes Mtaa wa Stanley na Sikukuu TANU ikamtafutia nyumba Magomeni Maduka Sita. Haya mabati yaamezungushwa kwenye kiwanja ilipokuwa nyumba hiyo ambayo kwa sasa haipo tena
Abdulwahid Sykes


Charles Kayoka Mtafiti wa Historia akimhoji Mwandishi

Abbas Sykes akimuhadithia mwandishi historia ya TANU katika mahojiano na TV Imaan ya Morogoro

Video ya mazungumzo na Kumbukizi ya Mwl. Nyerere In Sha Allah itawekwa...



Waliokuwa Katika Picha Hii na Ndilo lilikuwa Baraza la Wazee wa TANU
(Wengine: Hawapo)

  1. Abdallah Shomari (Tandamti No. 3) 
  2. Nassoro Kalumbanya (Simba) 
  3. Said Chamwenyewe (Aggrey/Congo) 
  4. Mtoro Ally (Muhonda) 
  5. John Rupia (Misheni Kota) 
  6. Julius Nyerere (Pugu Sekondari) 
  7. Said Chaurembo (Congo/Mkunguni) 
  8. Jumbe Tambaza (Upanga) 
  9. Sheikh Suleiman Takadir (Mafia/Swahili) 
  10. Dossa Aziz (Mbaruku/Somali Kipande) 
  11. Mshume Kiyate (Tandamti) 
  12. Juma Sultani (Kitchwele Karibu na Kanisa Dogo) 
  13. Maalim Shubeti (Masasi/Likoma) 
  14. Rajab Simba (Kiungani) 
  15. Waziri Mtonga (Kilosa 18, Ilala) 
  16. Mwinjuma Mwinyikambi (Mwananyamala) 
  17. Makisi Mbwana (Aggrey/Congo) 
  18. Usia Omari (Sungwi, Kisarawe) 
  19. Sheikh Issa Nasir (Bagamoyo).

Baraza la Wazee wa TANU lilichukua mafanikio ya safari ya Nyerere UNO kuwa  jukumu lao binafsi. Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa TANU alikuwa Sheikh Suleiman Takadir. Sehemu ya kwanza ya maandalizi ilitakiwa ifanyike kwa siri sana. Uongozi wa TANU ulimkabidhi Idd Faiz kazi ya kuandaa, kukusanya na kusimamia mfuko wa safari ya rais wa rais wa TANU Nyerere kwenda Umoja wa Mataifa, New York. Safari ilikuwa ifanyike mwezi wa Februari, 1955.


Kushoto: Sheikh Suleiman Takadir, John Rupia na Julius Nyerere, 1955

Mwenye miwani na kofia ni Abdul Faraj kama alivyo hivi sasa
 Mwaka wa 1953 Idd Faiz alikuwa na umri wa miaka arobaini na tatu, mwenye ari na nguvu tele. Alipokuwa katika Kamati kuu ya TANU mwaka wa 1959 aliteuliwa kuwa Mweka Hazina  wa Taifa wa TANU pamoja na kuwa mjumbe wa Kamati Kuu. Idd Faiz alikuwa mmoja wa viongozi wa chama walioanzisha TANU Press iliyokuwa katika njia panda ya Mtaa wa Mchikichi na Livingstone mjini Dar es Salaam. TANU Press ndiyo ilikuwa ikichapisha na kusambaza jarida  la TANU, Sauti ya TANU lililohaririwa na rais wa chama, Julius Nyerere, na baadaye kuchapisha Mwafrika  chini ya uhariri wa Rashid Heri Baghdelleh na Robert Makange. Kampuni hiyo ya kupiga chapa ilimilikiwa na Mwananchi Development Corporation TANU ilimteua Abdul Faraj kuiongoza kampuni hiyo.

Kushoto: Kanyama Chiume, Mwl. Julius Nyerere na Robert Makange miaka ya 1980

Kushoto: Idd Faiz, Sheikh Mohamed Ramia, Julius Nyerere, Saadan Abdul Kandoro
na Haruna Taratibu Dodoma 1956

TANU ilihitaji takriban shilingi elfu kumi na mbili kumwezesha Nyerere kusafiri kwenda Umoja wa Mataifa, New York. Kamati ya Abdu Kandoro, Japhet Kirilo na Abbas Sykes ilikuwa imekusanya kiasi cha fedha kutoka majimboni ambacho kilitumika katika ile safari ya Ally na Phombeah kwenda kwenye Pan African Congress mjini Lusaka. Kilichosalia hakikutosha kumpeleka Rais wa TANU, Nyerere Amerika. Ilibidi fedha za ziada zitafutwe kutoka kwa wananchi ili kumwezesha Nyerere kufanya safari hiyo. John Rupia alichangia zaidi ya theluthi moja ya fedha zilizotakikana. Wanachama wengine walichangia kwa uwezo wao wote lakini TANU katika siku zile ikiwa bado changa ilikuwa masikini, kiasi hicho kilikuwa bado kiko nje ya uwezo wake.  Ikitambua ule upungufu wa fedha za safari ya Nyerere, Idd Faiz aliombwa na uongozi wa Al Jamiatul Islamiyya fi Tanganyika (Umoja wa Waislam wa Tanganyika) kutoa fedha katika mfuko wa Al Jamiatul Islamiyya na kuzitia katika hazina ya TANU kukiwezesha chama kumpeleka Nyerere New York. Hata pamoja na fedha zile kutoka Al Jamiatul Islamiyya fedha hizo hazikuweza kukidhi haja.

Al Jamiatul Islamiyya haikuwa na jingine isipokuwa kumuomba Idd Faiz asafiri kwenda Tanga na kupata fedha zaidi kutoka huko. Mwalimu Kihere alikuwa tayari amekusanya fedha hizo na alikuwa anasubiri tu zije zichukuliwe na kupelekwa makao makuu.  TANU ilipata habari kwamba yeyote ambaye angeenda Tanga kuchukua fedha hizo kwa ajili ya safari ya Nyerere angekamatwa. Kabla ya kuondoka, Oscar Kambona, Katibu Mkuu wa TANU, na John Rupia, Makamo wa Rais wa TANU, walikwenda kuonana na Idd Faiz nyumbani kwake Ilala kumuaga, kumtakia safari njema na kumpa maelezo kwa ufupi. Safari ya kwenda Tanga haikuwa na tatizo lolote, lakini katika wakati wa kurudi basi ambalo Idd Faiz alikuwamo lilisimamishwa njiani Turiani na makachero wa Special Branch. Idd Faiz alikamatwa, akavuliwa nguo na kupekuliwa, lakini hakukutwa na fedha. Hili lilimshangaza na kumchanganya yule afisa aliyemkamata kwa sababu walikuwa na taarifa kwamba Idd Faiz alikuwa amechukua fedha kutoka kwa Mwalimu Kihere kule Tanga. Idd Faiz aliwekwa chini ya ulinzi na kupelekwa Dar es Salaam kwa usaili zaidi wakati wote akiwa analindwa na askari wenye silaha. Baadaye Idd Faiz aliachiliwa huru. Zile fedha za TANU zilifika makao makuu ya TANU Dar es Salaam, salama salimini. Zilizokuwa  zimepewa kubeba msichana mdogo aliyekuwa abiria ndani ya basi lile alimokuwa Idd Faiz.

Mwalimu Kihere
Mnamo tarehe 17 Februari, 1955 Nyerere aliondoka kwenda New York kuhutubia Baraza la Udhamini la Umoja wa Mataifa. Nyerere aliiweka wazi nia ya TANU kuwa alikuwa ametumwa na wananchi wa Tangayika kuwasilisha ujumbe ufuatao:

‘’Kuona kanuni ya uchaguzi ikianzishwa na Waafrika kujiwakilisha katika taasisi zote za umma... Hii tunaamini, ni kwa mujibu wa masharti ya Makubaliano ya Udhamini na Ibara ya 76 ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa.’’

Mbele ya Umoja wa Mataifa, TANU haikuwa ikidhihirisha tamko lolote jipya, yale yote yaliyowasilishwa pale yalikuwa ni maoni ya kamati ndogo ya siasa ya TAA yaliyowakilishwa kwa Constitutional Development Committee ya Gavana Edward Twining mwaka wa 1950. Gavana Twining aliyapuuza mapendekezo ya TAA na badala yake aliendelea na mipango yake ya kuwa na wawakilishi wa  rangi zote katika Baraza la Kutunga Sheria. Ili kuupa msukumo msimamo wake huo serikali ilituma ujumbe wake Umoja wa Mataifa kuipinga TANU uliowakilishwa na I. C. Chopra, Mwasia; Sir Charles Phillips, Mzungu na Liwali Yustino Mponda, mjumbe wa Baraza la Kutunga Sheria wa Newala.

Nyerere alirudi kutoka New York Jumamosi, tarehe 19 Machi, 1955 na alipokelewa uwanja wa ndege na halaiki ya watu. Dossa Aziz anakumbuka kuwa aliruhusiwa pale uwanja wa ndege kuingiza gari yake hadi ndani ya uwanja chini ya ndege ili kumrahisishia Nyerere kuingia ndani ya gari na kuepuka msongamano wa watu. Dossa Aziz anasema kama isingekuwa kwa msaada huo Nyerere angesongwa sana na watu. Watu walikuwa kila mahali wakisukumana na kusongamana wakijaribu angalau kumtia Nyerere machoni. Watu walikuwa wakiimba na kucheza ‘’mganda,’’ ngoma ya Kizaramo, wakiimba: ‘’Baba Kabwela Yuno,’’ yaani baba amerudi kutoka UNO. Jambo la kushangaza ni kwamba hakuna mtu aliyewahi kuusikia wimbo huu kabla ya siku ile na hakuna ajuaye lini ulitungwa. Ile gari ya Dossa Aziz aliyopanda Nyerere ilisukumwa kutoka uwanja wa ndege hadi nyumbani kwa Nyerere, Magomeni Majumba Sita, kiasi cha kama kilomita ishirini.


Dossa Aziz


Siku iliyofuata ilikuwa Jumapili. TANU ilifanya mkutano wa hadhara Mnazi Mmoja ambao ulihudhuriwa na umati ambao kamwe haukupata kuonekana Dar es Salaam. Inakisiwa zaidi ya watu 40,000 walikuja kutoka kila upande wa mji kumsikiliza Nyerere. Hakuna mtu aliyekuwa na raha ya kuandika kuhusu mkutano ule na safari ya kihistoria ya Nyerere kwenda Umoja wa Mataifa kuliko Mashado Plantan katika gazeti lake Zuhra. Mtambo wa gazeti wa Mashado uliokuwa Mtaa wa Ndanda, Mission Quarters ulichapisha nakala za ziada za gazeti hilo na toleo lote liliuzika.


Mkutano wa TANU Jangwani Miaka ya Mwanzoni 1950
Kushoto: Dossa Aziz, Julius Nyerere, Abdul Sykes na Lawi Sijaona Ukumbi wa Arnautoglo katika tafrija ya kumuaga Nyerere kwenda UNO safari ya mwaka 1957

Kushoto waliokaa wa kwanza ni Japhet Kirilo
Kushoto Abdulwahid Ally Sykes na Mwandishi Nyumbani kwa Japhet Kiriko Usa River 1989 nilikuwa nimekwenda kumfanyia mahojiano lakini nikamkuta amesafiri amekwenda Nairobi. Japhet Kirilo ndiyo Mtanganyika wa kwanza kuzungumza UNO mwaka wa 1952

No comments: