Ndugu
Salim,
Ni
juu ya wasomi, hasa wanahistoria wakisaidiwa na mashuhuda wa matukeo,
kuinusuru historia isipotoshwe au kupindwa kwa maslahi yoyote yale ya
kisiasa. Tuwe chonjo, angalau sisi mashuhuda tuliobaki bado hai. Mwenyezi Mungu
Atupe umri mrefu wenye afya.
Ndani
ya PAFMECA ( Pan-African Freedom Movement for East and Central
Africa), mshikamo wa Vuguvugu za vyama vyote vya kupigania huru katika nchi za
Afrika Mashariki na Kati, kulikuwemo pia ndani yake vyama vya ASP na Hizbu
( Nationalist) vya Zanzibar. Kwa hivyo mimi napata taabu kufahamu
kwamba PAFMECA hiyohiyo na tena wakati huohuo iwe ni taasisi ilioowanisha
mpango wa kufikiwa mapatano baina ya TANU na ASP ambayo moja katika ibara za
mapatano hayo ilitaja kwamba "Mwishowe, kupatikana uhuru wa
Tanganyika na Zanzibar kutapelekea nchi mbili hizo kuungana pamoja kuwa
Jamhuri ya Kiafrika." Napata taabu kukumbuka kwamba PAFMECA iliiunga
mkono ajenda ya aina hiyo, japokuwa viongozi wake waliungana na zile
hisia za kutaka Afrika nzima ilioungana katika miaka inayofuata.
Kweli
PAFMECA ilijaribu mara kadhaa kuwa mpatanishi ( kwa kuwatuma Dr. Hastings
Kamuzu Banda wa Malawi- wakati huo ikiwa katika Shirikisho la Rodesia/Kaskazini
na Kusini na Nyasaland- na pia Bibi Titi Mohammed wa TANU ) katika mvutano
uliokuweko Zanzibar wakati huo baina ya ASP na Hizbu. Vyama hivyo
vyote viwili vilitambuliwa sawasawa na PAFMECA kuwa ni vya kizalendo
vyenye kupinga ukoloni wa Kiingereza Visiwani. Japokuwa natambua kwamba baadae
ilikuja kujulikana kwamba kulikuweko baadhi ya viongozi wa PAFMECA walioelemea
zaidi, bila ya kuonesha hadharani,upande wa ASP, huenda kama unavyosema kupinga
tu uzalendo wa Kiarabu ulioambatanishwa pia na Rais Gamal Abdel Nasser wa
Misri.Hiyo hati ya TANU unayoitaja yawezekana yalikuwa tu maono ya baadhi ya
wana TANU wa wakati huo na ambayo wanachama wengi, hata viongozi, wa ASP
walikuwa hawana habari nayo.
Juni
1959 nilikuwa miezi minne kabla ya kufikia umri wa miaka 12. Licha ya utoto
wangu nilikuwa mfuatilizi wa karibu sana wa mikutano ya hadhara ya ASP na
Hizbu hapo Raha leo na karibu na Malindi huko Zanzibar. Licha ya hayo
nilifaidika kwa kuzaliwa katika "nyumba ya kisiasa" ambapo siasa
ilikuwa inazungumzwa kwa masaa 24 kila siku, kama chakula chetu, na ndani ya
nyumba hiyo wanafamilia wakiwa na mitizamo tafauti ya kisiasa miongoni
mwao. Ila Baba, Mungu Amrehemu, aliniambia "fuatiliza na soma siasa na
vitimbi vyake, lakini katu usithubutu kuwa mwanasiasa- huo ni mchezo
mchafu." Nimeifuata kauli yake hiyo, sijamsaliti na sijajuta.
Othman
(Othman writing to Salim)
No comments:
Post a Comment