Monday 12 September 2016

BARUA YA KUJIUZULU UALIMU YA JULIUS KAMBARAGE NYERERE 1955



Photo: Resignation Letter JKN


Nini kilitokea mwaka wa 1955 hadi kumfanya Father Walsh ampe chaguo Nyerere la kubaki mwalimu au aendelee na siasa? 

Julius Nyerere akiwa UNO 1955

Baada ya Nyerere kurejea kutoka UNO, TANU ilifanya mkutano mkubwa na hayo hapo chini ndiyo yaliyotokea baada ya mkutano ule:

''Hotuba hii aliyotoa Nyerere siku ile pale Mnazi Mmoja ambapo aliwaeleza watu  kuhusu safari yake kwenda Umoja wa Mataifa ilikuwa ndiyo mwanzo hasa wa historia mpya ya Tanganyika. Kabla ya hapo Waafrika wa Tanganyika hawakupata kuonyesha shauku na matumaini katika mustakbali wao. Katika viwanja vya Mnazi Mmoja Nyerere aliwaeleza halaiki ya watu wenye furaha na waliokuwa wakimsikiliza kwa makini kuwa miongoni mwa mataifa kumi na mbili yanayounda Baraza la Udhamini saba kati yao yalitoa idhini kuwa muda wa utawala wa ndani wa Tanganyika utakapowadia, Waafrika lazima wapewe nchi yao. Katika hotuba yake Nyerere alitilia mkazo sera ya TANU kuhusu mahusiano mema baina ya Waafrika na watu wa mataifa mengine na aliwaonya wanachama wa TANU ambao walikuwa wameanza kuwabagua watu wa rangi tofauti kuwaambia kuwa hivyo haikuwa sawa. Alisisitiza juu ya umoja miongoni mwa wananachi na hatimaye aliwadhihaki wasikilizaji kwa kuwauliza ikiwa wangesubiri kwa miaka ishirini na tano kuwa huru. Halaiki hiyo ya watu kwa pamoja ilipiga kelele, ëhapanaí. Wananachi kwa pamoja walijibu kwa sauti kubwa wakisema walitaka uhuru kesho au kesho kutwa.

Nyerere ambaye alikuwa akiogopa  kuchukua uongozi wa TANU tangu 1953 alikuwa amefarajika sana na mshikamano huu ulioonyeshwa na wananchi. Sasa ilikuwa dhahiri kwake kwamba rafiki yake Abdulwahid, Ally, Dossa Aziz, Rupia na uongozi mzima wa TANU pamoja na lile Baraza la Wazee lilikuwa limemsafishia njia kuongoza harakati kwa niaba yao. Lakini Padri Walsh na Wamishionari katika shule ya Mtakatifu Francis, Pugu, walitazama harakati hizi kwa mtazamo mwingine kabisa. Wamishionari hawakuweza tena kumvumilia Nyerere kuwa mmoja wa walimu katika shule yao. Hatima ile ile iliyowasibu wazalendo wengine kabla yake sasa ilimkabili Nyerere. Aliambiwa ama abakie mtumishi mtiifu wa kanisa au ajiuzulu; Kanisa halikuweza kukaa kimya na kumuangalia Nyerere akiwatumikia mabwana wawili.

Nyerere alilipeleka tatizo hili kwa Clement Mtamila, Mwenyekiti wa Kamati Kuu ya TANU. Mtamila aliitisha mkutano wa kamati kuu nyumbani kwake mtaa wa Kipata na TANU ilijadili tatizo hilo. Miongoni mwa wajumbe wa kamati ile mbali na Rupia na Kambona walikuwa Bibi Titi Mohamed na Bibi Tatu bint Mzee. Kamati Kuu ya TANU ilimshauri Nyerere ajiuzulu. Tafarani hii ilitokea wiki chache tu baada ya kurudi kutoka Umoja wa Mataifa katika wiki za mwisho za mwezi Machi. Tarehe 23 Machi, 1955 Nyerere alijiuzulu ualimu. Ilikuwa adhuhuri Nyerere alipokuja Dar es Salaam kutoka Pugu, akiwa si mwalimu wa shule tena. Inasemekana aliposhuka tu kwenye basi alikwenda moja kwa moja ofisini kwa Abdulwahid katika soko la Kariakoo kumpasha habari rafiki yake. Nyerere alikaa na Abdulwahid katika nyumba yake namba 78 Mtaa wa Stanley. Baadaye kidogo Nyerere alirudi kijijini kwake huko Musoma. John Hatch alipokuja Dar es Salaam kwa mwaliko wa TANU Nyerere alikuwa kwao kijijini. Tutaona hapo baadae kidogo jinsi mgeni huyu Mwingereza alivyomgutusha Schneider Abdillah Plantan kuhusu  TANU kuwashirikisha wanawake katika harakati za kudai uhuru.''


Kulia Bi. Tatu Biti Mzee, wa tatu Julius Nyerere na wa tano ni Bi. Titi Mohamed
Picha hii ilipigwa uwanja wa ndege wa Dar es Salaam siku ya kumsindikiza Nyerere
kwenda UNO
Hapa ndipo Nyerere alipoifikisha TANU katika uingozi wake wa miezi minane na hali ilianza moto Tanganyika nzima kiasi ya kuwa Nyerere hakuweza tena kuwatumikia mabwana wawili. Hii ndiyo iliyopelekea yeye kuandika barua hiyo hapo juu ya kujiuzulu kazi ya ualimu.


Mwandishi akifanya Kipindi Maalum: Miaka 60 ya Hotuba ya Mwalimu
Nyerere UNO katika Radio Kheri akiwa na Mtangazaji Hassan Abdulla
Sikiliza kipindi hapo chini:

Mwandishi akiwa na Happy Mtamila mtoto wa Clement Mtamila
alipomtembelea nyumbani kwake mwaka 2015 Happy anaishi Ulaya kwa miaka mingi




No comments: