Mufri Sheikh Abubakar Zubeir akiongoza Sala ya Jeneza |
Amenipigia simu mhariri wa gazeti moja
maarufu akiniomba niandike taazia ya Cisco kwa gazeti lake litokalo kila juma.
Nikamjibu kuwa hakika namfahamu Balozi Cisco Mtiro kwa miaka nenda miaka rudi
lakini sijui niseme nini kuhusu yeye. Nikamshauri amjaribu Balozi Mohamed
Maharage Juma maarufu kwa sisi tuliokuwa karibu na yeye kwa jina la ‘’Sancho.’’
Hakika kama kuna mtu anaweza kumweleza Cisco basi ni yeye Balozi Maharage.
Wakati tunanyanyukia mjini Dar es Salaam kila mtu alikuwa na jina lake la
kupanga, yaani, ‘’nickname,’’ na majina haya wakati mwingine yalimganda na
kumwenea mtu kiasi ya kuua jina lake halisi alilopewa na wazazi wake. Hili
ndilo lililomfika Abdulkarim Omar Mtiro. Ilikuwa ukimuuliza Cisco kwa jina la
Abdulkarim utahangaika sana lakini ukitaja jina la Cisco hata jiwe
litakuelekeza nyumbani kwake.
Cisco alizaliwa Mtaa wa Kipata baadae baba yake akahamia Temeke na huko ndiko alikokulia. Mimi binafsi kila Balozi Cisco anapokuja katika fikra zangu basi atafuatia na Balozi Mohamed Maharage Juma. Si kwa sababu ya wao kufanana kwa maumbo watu wa miraba minne au kwa kuwa wote waliingia katika kazi moja Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje la hasha, kinachonigusa mimi ni jinsi wawili hawa walivyoshabiana katika hulka zao ambazo hata kama utakutananao kwa mara moja tu basi wataacha alama katika kichwa chako kama si kuwa rafiki wa maisha. Mohamed Maharage alinipigia simu kuniuliza kama nilikuwa nina taarifa za msiba wa Cisco na akaniambia kuwa yeye tayari yuko nyumbani kwa Cisco pamoja na jamaa wengine na akaniomba nifanye hima niende mara moja. Alifanya hivi akijua ukaribu sote wawili tuliokuwanao na Cisco.
Cisco alizaliwa Mtaa wa Kipata baadae baba yake akahamia Temeke na huko ndiko alikokulia. Mimi binafsi kila Balozi Cisco anapokuja katika fikra zangu basi atafuatia na Balozi Mohamed Maharage Juma. Si kwa sababu ya wao kufanana kwa maumbo watu wa miraba minne au kwa kuwa wote waliingia katika kazi moja Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje la hasha, kinachonigusa mimi ni jinsi wawili hawa walivyoshabiana katika hulka zao ambazo hata kama utakutananao kwa mara moja tu basi wataacha alama katika kichwa chako kama si kuwa rafiki wa maisha. Mohamed Maharage alinipigia simu kuniuliza kama nilikuwa nina taarifa za msiba wa Cisco na akaniambia kuwa yeye tayari yuko nyumbani kwa Cisco pamoja na jamaa wengine na akaniomba nifanye hima niende mara moja. Alifanya hivi akijua ukaribu sote wawili tuliokuwanao na Cisco.
Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na Sheikh Alhadi Mussa na Paul Makonda wakitoka makaburini Kisutu baada ya maziko |
Kama jana vile namkumbuka Cisco akija
mjini katika, ‘’Boogie,’’ akiwa amepanda baiskeli yake nyeusi akitokea nyumbani
kwao Temeke. Boogie ilikuwa ni dansi za mchana maarufu kwa sisi, ‘’teenagers.’’
Hii ilikuwa miaka ya katikati ya 1960 na wastani wa umri wetu ulikuwa miaka 15.
Nawakumbuka vijana waliokuwa wakija mjini Arnautoglo Hall palipokuwa panachezwa
boogie kutokea Temeke pamoja na Cisco. Kulikuwa na Moses jina halisi Mussa,
Micky Jones, huyu jina lake ni Mikidadi, Allan Brown yeye ni Ali Ngotta akitoka
katika familia maarufu sana Temeke. Hawa walikuwa vijana watanashati sana. Turudi
katika baiskeli ya Cisco. Ukweli ni kuwa baiskeli ilikuwa haiendani na wakati
ule na hali ile ya ule ujana tuliokuwanao. Unaweza kupanda baiskeli kuja shule
lakini si kujanayo katika boogie. Huwezi kuja na baiskeli kwa kuwa utakuwa,
‘’umeuramba,’’ yaani umevaa vizuri sana sasa katika hali hiyo kuikwea baiskeli
na kupiga pedali kutoka Temeke hadi mjini kwa kweli kutavuruga nguo achilia
mbali hilo jasho litakalokutoka. Lakini Cisco toka utoto alikuwa mtu wa mikasa
na vituko akiyafanya haya kwa makusudi ya dhati yake.
Cisco alikuwa na uwezo mkubwa sana wa
kuzungumza suala lolote kwa umakini wa hali ya juu iwe ni siasa, muziki, mpira
nk. Lakini kubwa ambacho Allah alimjaalia Cisco ni kipaji chake cha kuchekesha
huku uso wake ukiwa unakupa wewe taswira ya kuwa lile analokueleza ni kweli
kabisa kwani uso wake haukutoa taswira kuwa anafanya maskhara. Nadhani kipaji
hiki alikitumia vyema katika kazi yake ya diplomasia. Miaka michache iliyopita
wakati Cisco amestaafu kazi nilimtembelea Balozi Maharage nyumbani kwake
Makongo. Balozi Maharage alikuwa likizo akitokea Abu Dhabi alikokuwa balozi wa
Tanzania akiwa pia akiwakilisha na Iran. Balozi Maharage akanambia kuwa Cisco
alipostaafu kampigia simu akiwa ofisini kwake Abu Dhabi kumpandisha midadi,
akimwambia kuwa yeye anapiga simu ile akiwa Butiama Hoteli na tayari ameshatoa
oda ya biriani anaisubiri iletwe mezani pake aishughulikie.
Hii Butiama Hoteli ina nafasi ya pekee
katika nyoyo zetu sisi vijana wa zamani. Hii ilikuwa moja ya hoteli maarufu
Magomeni Mapipa na ikiwa imemtokea mtu kuwa yuko mitaa ya Magomeni ilikuwa
hakosi kuingia hapo kupata biriani yake iliyokuwa inapikwa kwa umahiri mkubwa.
Hii kama utakuwa Magomeni wakati wa chakula cha mchana. Lakini ikitokea kuwa
uko mjini basi hoteli itakuwa Royal Restaurant, Zahir au Khalid migahawa hii
yote ilikuwa ikipika chakula kizuri sana na umaarufu wao mkubwa sana ilikuwa ni
upishi wa biriani. Miaka ikapita na sisi tukakua tukatoka katika utoto na ujana
tukawa watu wazima si kwa umri tu bali hata kwa nafasi kiasi ambacho ikawa
tumepita kuingia baadhi ya migahawa ambayo katika ujana wetu tulikuwa
hatupungui. Kama nilivyotangulia kusema, Cisco alikuwa mtu wa mikasa na kupenda
kukufanya ucheke na ufurahi. Usingetegemea balozi mzima leo aingie Butiama
Hoteli kwenda kula biriani kisha akabishana Simba na Yanga na wahudumu wake.
Balozi Cisco hakuwa limbukeni.
Wapi ambako mguu wake haukutua katika
dunia hii akifuatana na maraisi wote waliotawala Tanzania, achilia mbali
kusuguana mabega na wakubwa wa dunia kama Bill Clinton na Nelson Mandela,
kuwataja wachache. Hapa wala sitaki kugusa alipokuwa na Mwalimu Nyerere
akizungukanae kote duniani wakati wa South to South Commision ya Mwalimu
Nyerere. Mafanikio haya yote na ukubwa na ukuu wake wote huu haukumvuruga
kichwa chake. Barza zake na marafiki zake ni wale wale akina Mohamed Said, Ali
Ngota na Ali Mzuzuri waliokuwa pamoja toka utotoni. Mimi nilikuwa ni yule yule
‘’Sidney,’’ rafiki yake wa udogoni na alipokuwa akijisikia atanikumbuka katika,
‘’whatsapp,’’ kwa kuniwekea ‘’clip,’’ ya Earl Klugh mpiga gitaa wa jazz maarufu
ambae sote mimi na yeye tukimpenda kwa miaka au, ''clip,'' ya mpiga jazz yeyote
yule. Nami kwa kukataa kushindwa na kutaka kuoneshana mizungu nitamrushia,
''clip,'' ya Wes Montgomery, mpiga gitaa nguli lakini wa enzi kabla ya Earl
Klugh.
Balozi Cisco Mtiro na Nelson Mandela |
Kulia: Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi, Jaji Mkuu Mstaafu Mohamed Chande, Mkuu wa Usalama wa Taifa Mstaafu Rashid Othman na Benard Membe Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje Mstaafu |
Butiama bila shaka palimkumbusha mengi na
njia ndefu aliyopita hadi kufikia pale alipofika akiwa na ofisi ndani ya Ikulu
ya Jamburi ya Muungano wa Tanzania. Wafanyakazi wa Butiama wengi wao ni wale wale na wengi
wana Yanga wenzake na bila shaka alipata wasaa wa kukumbushana enzi zilizopita
na kucheka pamoja kisha kuwaachia, ‘’tip,’’ nono. Karibu na Butiama Hoteli
ilikuwapo hoteli ya marehemu Shomvi Yanga mwenzake na hoteli yake ‘’Michuzi
Mikali.’’ Shomvi akapichikwa jina Shomvi Michuzi Mikali. Shomvi yeye alijikita
katika kuku wa kukaanga aliotoa kwa ugali au wali. Shomvi alikuwa anatengeneza
pilipili ya ajabu chachandu nzuri kabisa iliyokwenda sawia na kuku wake wa
kukaanga.
Hivi vyote vilikuwa viwanja vyetu katika
miaka ile ya 1970 tukiwa vijana. Sehemu hizi si tu mtu alikuwa anapata chakula
kizuri bali alikuwa anapata pia maongezi mazuri ya ushabiki wa Simba na Yanga
na wakati mwingine wachezaji wa timu hizi hujumuika pale kwa chakula cha
mchana. Na wapenzi walikuwa hawabagui ikiwa watalipa chakula basi watawalipia
wote wachezaji wa Yanga na Simba bila matatizo na kwa utani kidogo kama
vile, ‘’Maulid kula nguvu yetu Simba uje utufunge tena,’’ na watu wote
watacheka na kufurahi pamoja. Huyu Maulid alikuwa marehemu Maulid Dilunga,
mshambuliaji mkali wa Yanga.
Pale alipokuwa ndani ya Butiama
Hotel,Cisco aliweza kuona Shibam Hotel vizuri kabisa kwani ukivuka Barabara ya
Morogoro ndipo ilipo Shibam hadi leo, ilipokuwa barza ya marehemu Mkanga
shabiki mkubwa wa Simba toka enzi za Sunderland. Miaka mingi ya kuwa Balozi
Cisco nje ya nchi haikumtenganisha Cisco na ndugu zake. Alikuwakumbuka na
kuwasaidia rafiki zake alioukuwanao African Temeke na Good Hope za Temeke. Timu
hizi za mchangani huko Temeke kwao Balozi Cisco ndizo zikitoa wachezaji hodari
vijana kuja Yanga na Simba katika miaka ile kama akina Lenard Chitete na Shaibu
Ngotta kuja Simba na Yanga.
Balozi Cisco kiti chake kilikuwapo Leaders
Club lakini halikadhalika hakusahau kijiwe chake cha mtaani kilichomkuza. Meza
yake ilikuwapo katika mahoteli makubwa ya sifa duniani lakini haikumpa shida
kuja kula Butiama na kuwasalimia nduguze.
Turudi hoteli ya Butiama na biriani.
Cisco alijua hii ya Butiama atakuwa
amemkomesha rafiki yake Balozi Maharage. Ndipo aliponyanyua simu yake ya bei
kali akampigia kumfahamisha kuwa yeye yuko hapo Butiama anakula biriani. Balozi
Cisco akamaliza mazungumzo yake kwa kumtahadharisha balozi mwenzake kuwa
achukue tahadhari ya kuacha ofisi mapema apate mafao yake maana shilingi
inaweza kuporomoka na yeye akatoka kapungukiwa pakubwa. Balozi Maharage
alipomaliza kunihadithia salamu na indhari aliyopewa na Cisco akaanza kucheka
na mimi sikuweza kustahamili tukawa sote tunacheka na kupiga gonga. Hakika
Cisco hawezekani tulikubaliana sote.
Siku moja niko darasani Chuo Kikuu Cha Dar
es Salaam mwalimu Mzungu kutoka Uholanzi akitusomesha kozi, ‘’Politics of
Industrial States,’’ bila shaka alikuwa kahisi jambo kwetu sisi wanafunzi wake
akasema kutuambia kuwa Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje inashangazwa na kiwango
cha chini cha miaka ya karibuni ya vijana kutoka Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam
waliokuwa wanajiunga na wizara hiyo. Mwalimu akaendelea kusema kuwa kulikuwa na
wakati hakika chuo kilikuwa kikitoa wahitimu hodari katika nyanja zote kuanzia
lugha, Kiingereza na Kifaransa hadi ujuzi wa siasa za dunia. Akamaliza kwa
kusema kuwa wizara inashangaa kimepitika nini kuwa vijana kama hawa ghafla
wamepotea.
Cisco alikuwa ameingia Wizara ya Mambo ya
Nchi za Nje akiwa mmoja wa kundi hili la vijana, ‘’smart,’’ wa ‘’Foreign,’’
ambao walikuwa wa kupigiwa mfano na baadhi nikiwafahamu kama Eliud Aickim
‘’Brown,’’ Mwandembwa, Ami Mpungwe, Kassim Mwawado, marehemu Gasper Yusuf
Hakili kwa kuwataja wachache. Vijana hawa walikuwa na, ''sophistication,'' ya
aina yake kuanzia, ''etiquettes,'' hadi mavazi. Naukumbuka sana utanashati wa
Cisco akiniacha mie kwa mbali sana.
Iko siku mimi na Mohamed Maharage tuko
London Underground tunasubiri treni. Pembeni yetu walikuwa wamekaa viajana wa
Kifaransa na walikuwa wanazungumza Kifaransa. Katika kusubiri kule hawa vijana
ambao walikuwa watalii, maana walikuwa wakipiga picha nyingi mimi na Mohamed
tukawa tunaingia katika picha zao. Mmoja kati yao, kijana wa kiume akawa
anazangumza na binti aliyekuwanae kisha wanacheka kwa sauti kubwa. Mara nikaona
Mohamed kawageukia na anaanza kuzungumza nao Kifaransa kwa kama dakika mbili
tatu. Kutokana na jinsi niliyomuona yule kijana wa kiume anazungumza na Mohamed
nikahisi pale pamepitika jambo.
Kweli kwa hakika palikuwa pamepitika
jambo. Yule kijana alituita mimi na Mohamed ‘’maua meusi,’’ akimwambia
mmoja wa wale akina dada kuwa picha zao zitapendeza sana kwa kurembwa na ‘’maua
meusi,’’ ya London. Alisema maneno haya kwa Kifaransa. Hapo ndipo Mohamed
akawageukia na kuwaambia kwa lugha hiyo hiyo yao kuwa, ‘’Basi ingawa
mmeyapenda, ‘’maua meusi,’’ ingependeza kama mngeyaomba ruhusa kabla
hamjayapiga picha. Vijana wenzetu Wafaransa wakatutaka radhi. Hawa ndiyo akina
Cisco, vijana, ‘’smart’’ wa Foreign Affairs,’’ wa enzi zile. Mambo haya
yametokea sasa zaidi ya miaka 30 imepita.
Balozi Mohamed Maharage Juma |
Nimempa pole Balozi Mohamed Maharage kwa
kuwa najua yeye msiba wa Cisco ni mkubwa sana juu yake umemuelemea kwa kuwa
ameishi na Cisco kwa miaka mingi toka udogo wao hadi kufika kufanyakazi pamoja
Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje kisha kustaafu na kuwa pamoja. Halikadhalika
nimempa pole Ali Mzuzuru rafiki kipenzi wa Cisco toka utoto wao na ambao wazee
wao walikuwa kati ya wazee wa Temeke waliojenga Msikiti wa Tumbi, Temeke
wakisaidiwa na Aga Khan wakati wa enzi za East African Muslim Welfare Society
(EAMWS).
Kushoto: Salum Matimbwa, Shaibu Ngotta Nyuma Kulia: Ali Ngotta, Magombe Makongoro na Hamisi Chenja Nyuma wa pili kulia Ilyas Abdulwahid Sykes |
Nimempa pole Micky Jones ambae kanineletea
picha akiwa na Cisco VIP Longe Copenhagen pamoja na Rais Kikwete alipokwenda
huko. Nimempa mkono wa pole Ali Ngotta na mdogo wake Shaibu Ngotta. Nikiwapa
pole na hawa wote hawa wote wakawa wananirejeshea mimi pole wakinambia na mimi
pia nipoe.
Iko siku wakiwa safarini Cisco
alimchekesha Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere hadi machozi yakammwagika.
Lakini kisa hiki In Shaa Allah nakitafutia
siku yake.
There was never a dull moment with Cisco.
Hakika Cisco amevuka milima na mabonde
kutoka Kipata na Temeke hadi kufika duniani. Tunamuomba Allah amweke ndugu yetu
Abdulkarim Omar Mtiro mahali pema peponi.
Amin
Cisco na Mwandishi katika Khitma ya Saigon 2010 |
No comments:
Post a Comment