Monday 5 June 2017

TAAZIA: SALUM ABDALLAH MATIMBWA NA KUMBUKUMBU YA ABDULKARIM OMAR MTIRO (CISCO)


Abdulkarim Omar Mtiro (Cisco)

Maskini kaka yangu "Cisco" umetangulia mbele ya haki.

Huyu kwangu mimi ni baba maana marehemu mzee wangu Abdallah Salim Matimbwa alikuwa ni mmoja wanaosoma katika darsa ya marehemu Sheikh Omar Mtiro hapa Mtaa wa Kipata nyumba no. 1 ambae ni baba yake Abdulkarim Mtiro maarufu kwa jina la, ''Cisco.''

Hii nyumba no. 1 Mtaa wa Kipata na Msimbazi na Congo ndimo alimozaliwa Cisco. 

Nyumba yetu ni no. 2 kwa hiyo nyumba zetu zikitazamana miaka nenda miaka rudi na wazee wakifahamiana vyema kabisa.

Mwezi kama huu wa Ramadhani enzi hizo chano kiko barazani kwa Sheikh Omar Mtiro,  uji unapikwa kwetu na mama yangu na futari zote zinapelekwa kwa Bibi bint Seif (mama yake mzazi Cisco).

Dar es Salaam hii ya miaka ile ya 1950 wakati sisi tunazaliwa leo haipo tena.

Kwa daraja hiyo niliyoizungumza hapo juu, ya baba yangu Mzee Abdallah bin Salim Matimbwa kuwa mwanafunzi wa Sheikh Omari bin Mtiro, kwa nidhamu ya Kiislamu Sheikh Mtiro anakuwa babu yangu na Abdulkarim Mtiro, mwanae anakuwa baba yangu kwa maana yeye anamwita baba yangu kaka yake ki daraja.

Kwa umri aliokuwanao baba yangu anamzaa Abdulkarim pasi na shaka yoyote lakini ada ni ada Abdulkarim alibaki kuwa mdogo wake na kwangu baba.

Dada yangu wa kwanza Bi. Hidaya bint Abdallah Salim watoto wake kina marehemu Shaaban Juma Semlangwa Assistant Commissioner of Police (ACP) na dada yake Bi Mwanahawa Juma ndiyo walikuwa mchezo mmoja na Balozi Cisco katika utoto wao.

Hivyo nimeondokewa na baba yangu, kaka yangu, mzaliwa mwenzangu mtaani Kipata (sasa Mtaa wa Kleist Sykes) na kiongozi wangu katika nyanja mbalimbali.

Mwenyezi Mungu amuondolee adhabu ya kaburi na amsamehe makosa yake.
Aiweke roho yake mahala pema peponi.


Amin.

No comments: