Sunday 26 November 2017

TAAZIA: BURIANI NDUGU NA RAFIKI YANGU MPENZI MUUNGWANA KLEIST…(1950 - 2017)


TAAZIA: BURIANI NDUGU NA RAFIKI YANGU MPENZI
MUUNGWANA KLEIST…
(27 June, 1950 – 24 November, 2017)

Kleist Abdulwahid Sykes

Usiku wa Jumanne tarehe 23 nimeona katika ukurasa wa FB wa kaka kaka yangu Prof. Charles Mgone kuwa yuko Glasgow, Scotland akaandika kuwa anafurahi kurudi tena katika mji huo. Nami nikaandika kumwambia kuwa amenikumbusha Dumbarton Road mtaa ambao yeye akiishi na mimi nikienda kumtembelea katika miaka ya mwanzoni ya 1990 kwanza nikitokea Dar es Salaam na baadae nikitokea Cardiff, Wales. Asubuhi yake nikapokea ujumbe mfupi kutoka kwake ukisema, ‘’Nasikitika kuwa sintokuwapo kumsindikiza ndugu na rafiki yangu katika safari yake ya mwisho.’’ Jina la aliyefariki hakuliandika bila shaka akiamini kuwa taarifa tayari ninazo. Nikashtuka kwani ujumbe huu ulikuwa ukinitaarifu msiba na haraka nikarejesha ujumbe kumuuliza nani kafariki? Mimi ndiyo kwanza nilikuwa nimeamka na kuwasha simu yangu. Jua lilikuwa limeshapanda pakubwa. Hata sekunde tatu hazikupita taarifa nyingi zikawa zinaingia kwa kufukuzana katika simu zikitoa taarifa ya kifo cha Kleist na taarifa ya kwanza ilikuwa kutoka Saigon Club.

Imesadifu kifo cha Kleist ikutane na kumbukumbu zangu za Glasgow ambako takriban miaka 30 iliyopita kila nilipokuwa hapo Dumbarton Road kwa labda ule upweke wa Ulaya tulikuwa tukikumbushana habari za utoto wetu Dar es Salaam Mtaa wa Kipata tulipozaliwa na Charles mara kwa mara atanihadithia habari zake za udogoni na Kleist. Hawa walikuwa marafiki toka utoto na mama zao walikuwa mashoga. Charles alimtangulia Kleist kwa mwaka mmoja. Charles kazaliwa 1949 na Kleist 1950. Charles alikuwa akinihadithia mchezo aliokuwa akicheza na Kleist kwenye bomba la maji lililokuwa Mtaa wa Kipata na Swahili pembeni ya nyumba ya Mama Kilindi. Miaka ile ya 1950 si kila nyumba ilikuwa na maji ndani na haya mabomba yalikuwa kila mtaa kwa ajili ya watu kuteka maji.

Taarifa ya kifo cha Kleist haraka ilinirudisha nyuma katika historia hii ya Dar es Salaam ya Tanganyika ya miaka 1950 wakati sisi tunazaliwa wazee wetu ndiyo walikuwa wanaanza harakati za wazi za kupambana na Waingereza kuidai Tanganyika. Baba yake Kleist, Abdulwahid Sykes katika mwaka wa 1950 ndiye alikuwa Katibu na Kaimu rais wa Tanganyika African Association (TAA). Siku hizo wakiishi Mtaa wa Stanley na Sikukuu katika nyumba ya kupendeza katika hali za wakati ule, nyumba iliyoezekwa bati ina maji na umeme na nyumba ambayo si ya mtindo wa vyumba sita bali numba yenye veranda na vyumba vya kulala na ua mkubwa na vyoo vyenye mabomba ya mvua ya kuogea. Nyumba nyingi wakati ule zilikuwa za makuti na zilizoezekwa kwa madebe na kujengwa kwa udongo, fito na kutomelewa kwa chokaa na sementi. Hii ndiyo Dar es Salaam ambayo Kleist alikuwa kazaliwa pamoja na wengi ambao niliwaona pale mazikoni walipokuja kumsindikiza ndugu yao katika safari yake ya mwisho.

Bomba la maji la Kipata lilikuwa pembeni ya nyumba ya Mama Kilindi mumewe Mzee Hassan bin Khamis kabila Mnubi ambae kivazi chake siku zote kilikuwa ni kanzu koti na tarbush. Mzee Hassan alikuwa akifanya biashara Soko la Kariakoo ambako baba yake Kleist alikuwa ndiyo Market Master yaani Mkuu wa Soko. Watu mfano wa Mzee Hassan diyo walikuja kununua kadi za kwanza za TANU pale sokoni wakiuziwa na Abdul Sykes na ndiyo watu wa mwanzo kumtia machoni Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere mwaka wa 1952 akiwa na Abdul Sykes katika mitaa ya Gerezani au pale Sokoni Kariakoo. Makaburi ya Kisutu wakati tunamzika Kleist, nilimuona kasimama Amani, mjukuu wa Mama Kilindi na Mzee Hassan bin Khamis. Amani hakumuwahi Kleist katika mitaa ya Gerezani akicheza jirani ya kwao kwenye bomba la maji kwani yeye ni uzawa wa miaka ya 1970, lakini siku hii Gerezani na Dar es Salaam yote kwa ujumla ilitoka kuja kumzika mwana wa mji kindakindaki kuanzia babu, bibi na baba. Makaburini niliwaona pia wajukuu wa Hassan Machakaomo. Huyu Machakaomo ni katika kizazi cha kwanza cha Wazulu. Mzee wa Kizulu Machakaomo aliingia Tanganyika akiwa askari mamluki kama alivyoingia babu yake mkuu Kleist, Sykes Mbuwane miaka ya mwishoni 1800 wakiwa wamebeba mikuki na ngao mikononi. Ukoo wa Machakaomo hadi leo hawa bado wanaishi Kipata.

Kleist wazee wengi waliokuwa wanamfahamu baba yake wanasema alishabihina sana na baba yake kwa tabia na hulka hususan katika uungwana na ukarimu. Nilipatapo kumsikia Mzee Kitwana Kondo akisema, ‘’Abdul alikuwa mtu muugwana sana.’’ Sifa hii ya ungwana aliitoa pia Mhariri wa Africa Events (London) Mohamed Mlamali Adam katika utangulizi wa makala niliyoandika mwaka wa 1988 ambamo nilimtaja Abdul Sykes. Katika utangulizi wake Mlamali alimwita Abdul Sykes, ‘’…the sweet Abdul Sykes…’’ kwa tafsiri nyepesi ni sawa na kusema, ‘’Muungwana Abdul Sykes.’’ Hivi ndivyo ilivyokuwa tabu sana Kleist kukikwepa kivuli cha baba yake lau kama katika uhai wake Kleist aliweza kujijengea haiba na historia yake mwenyewe nje ya haiba na historia ya baba na babu yake ambao wote walitoa mchango mkubwa katika kukita misingi ya Tanganyika kujikomboa kutoka minyororo ya ukoloni wa Waingereza. Juu ya juhudi zake za kusimama na miguu yake mwenyewe miwili siku zote kivuli cha historia ya baba na babu yake ilimwandama Kleist na kumuelemea sana.

Ingekuwa labda si kwa udugu waliokuwanao wazee wetu na pengine pamoja na mapenzi yangu ya kupenda kusoma kuandika na kuvutiwa na stori yoyote ya kusisimua nisingepata hamu ya kuandika maisha ya Abdulwahid Sykes. Historia ya ukoo wa Sykes dhidi ya ukoloni na juhudi yao kaika kuwaunganisha Waafrika ni kisa cha kuvutia. Hii ilikuwa historia ya kupigania uhuru wa Tanganyika na Kleist akijua mengi katika historia hii na vipi asijue ilhali Baba wa Taifa alipokelewa Dar es Salaam na kutiwa katika uongozi wa TAA na TANU kwa juhudi za baba yake? Historia hii ya kusisimua ilinisogeza karibu zaidi na Kleist kiasi cha sasa kufunika ule urafiki na udugu wetu wa asili ulioanza na babu zetu hadi sasa kutufikia sisi wajukuu, historia ambayo sasa imetimiza karne moja.

Kleist alikuwa na kisa cha kueleza cha historia hii ambayo kwa sababu zisizoweza kufahamika ilikuwa inatoweka taratibu, lakini alikuwa hana msikilizaji wala mtu anaetaka kuijua. Nilipotokea mimi kama muulizaji maswali na msikilizaji kifua cha Kleist na moyo wake vyote vilifunguka na kuanza kueleza mambo ambayo kwangu yalikuwa kama vile nimekaa kwenye kiti cha Empire Cinema naangaalia filamu nzuri mfano wa ‘’Hercules in the Land of Cyclopes,’’ filamu iliyotusisimua watoto wote wa wakati ule. Siku moja mdogo wake Kleist marehemu Omari alinambia, ‘’Mohamed dada Daisy ameandika kitabu kuhusu babu kitafute ukisome.’’ Ikasadifu kuwa nilikuwa nakwenda Arusha na nilipokuwa nimemaliza shughuli zangu nikaingia Maktaba ya Taifa, Arusha na hapo nikakikuta kitabu kilichohaririwa na John Iliffe, ‘’Modern Tanzanians,’’ na ndani nikamkuta Daisy kamwandika babu yake ‘’The Townsman: Kleist Sykes,’’ yaani, ‘’Mwanamji: Kleist Sykes. Kuanza kusoma utangulizi tu nikawa nimeshatoka katika karne ya 20 hii, dada yangu Daisy amenipeleka karne ya 19 niko Mozambique, Mhambane katika kijiji cha Kwa Likunyi nipo na Mjerumani Herman von Wissman anawapakia askari mamluki wa Kizulu katika manowari bandari ya Laurenco Marquis (leo Maputo) anawaleta Pangani kuja kupigana na Abushiri bin Salim na Chief Mkwawa. Katika askari hawa mamluki wa Kizulu waliokuwa wanakuja Tanganyika alikuwapo babu yake mkuu Kleist, Sykes Mbuwane na nduguye kipofu Ally Katini.


Bushiri bin Salim Al Harith
Nilibakia na maswali mengi sana nayatafutia majibu. Nilifahamu fika kuwa huyu aliyeandika maisha ya Kleist katika mji wa Dar es Salaam ya 1900 hakuwa Daisy Sykes. Hii ni kalamu ya mtu mwingine kabisa. Siku hizo Kleist yuko Geneva anafanya kazi United High Commission for Refugees (UNHCR). Maswali yangu yakawa yanamsubiri Kleist. Nyumba ya Kleist ilikuwa inaangalia shule yake aliyosoma, Aga Khan School. Kiasi Kleist asome shule hiyo maana baba yake alikuwa kwa miaka mingi wakati wa uhai wake mjumbe katika Aga Khan Education Committee. Kleist alikuwa naamini akifurahi sana kuzungumza na mimi kuhusu historia ya ukoo wao. ‘’Sheikh Mohamed ngoja nikuletee kinywaji chako.’’ Kleist alikuwa akijua kuwa mimi ni mpenzi wa muziki wa jazz kama yeye basi hapo ataniwekea santuri baada ya santuri ya muziki wa wapigaji maarufu kutoka maktaba yake, muziki ukija kwa sauti ya chini sana.

Tulikuwa kama vile tuna ratiba yetu maalum tunayoifuata. Ilikuwa kwanza lazima tubadilishane ‘’notes,’’ kuhusu baba zetu na maisha yao walipokuwa vijana mitaa ya Gerezani. Hapo tukicheka sana na kuwarehemu wazee wetu. Baba yangu katika umri mdogo sana alikuwa na wake wawili na baba yake Kleist pia alikuwa na wake wawili. Basi tutatia yetu huku tunacheka na kushangaa maisha ya wazee wetu na hawa wakijiona kuwa wao walikuwa watu wa kisasa kwa wakati wao. Wazee wetu wote walikuwa ‘’sharp dressers’’ na wapenzi wakubwa wa muziki. Baadhi ya mambo naona na sisi watoto waliturithisha na yameathiri sana mtindo w maisha yetu.

Tukimaliza hapa ndipo tutaingia katika mazungumzo mazito. Nitakuwa na maswali ya kumuuliza Kleist kuhusu historia ya baba yake na ukombozi wa Tanganyika kupitia TAA na kisha TANU. Ghafla ile hali ya vicheko itatoweka na Kleist anabadilika anazungumza kwa kuchunga sana ulimi wake akichagua maneno na hali ya simanzi nyepesi itatanda.  Kleist alinifahamisha kuwa katika vitu ambayo yeye vimemstaajabisha sana ni kuwa Iliffe akimtegemea sana Daisy katika kupata taarifa za African Association kuasisiwa kwake na mambo mengine na Daisy akimuuliza baba yake lakini kitu cha kustaajabisha ni kuwa Iliffe hakutaka kukutana na Abdul Sykes kupata historia ile moja kwa moja. Wakati ule Daisy alikuwa mwanafunzi Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam akiwa mmoja wa wasichana wachache wa Kariakoo kupata elimu ya juu.  Namna hii ikawa nakusanya ‘’notes,’’katika mazungumzo yangu na Kleist na nilihisi kama vile Kleist alikuwa kama mtu aliyekuwa anahitaji, ‘’therapy,’’ ya aina fulani kupunguza joto katika nafsi yake. Alikuwa ni mtu ambae alitaka sana mchango wa baba yake utambuliwe katika kuunda TANU na kupigania uhuru wa Tanganyika. Kwa miaka mingi haya ndiyo yakawa maisha yetu mimi na Kleist. Mimi nikijichukua kama mwanafunzi na Kleist ndiyo mwalimu wangu.

Mimi na Kleist tukawa sasa tuna maisha yetu tumejizingirisha sisi wawili tu tuko nje ya lile duru letu la kawaida la marafiki zetu wengine kama marehemu Yusuf Zialor, Wendo Mwapachu, Abdallah Tambaza, Abdul Mtemvu kwa kuwataja wachache na ikawa kama chama cha wachawi. Huingii hadi nawe uwe mwanga. Hii ikawa ‘’Exclusive Club,’’ yaani chama makhsusi cha watu wawili tu. Miaka ilivyokuwa ikipita nami ndivyo nilivyokuwa nafaidika na kuzidi kuchota elimu ile kutola kwa Kleist. Akienda Geneva na akija Dar es Salaam tunakutana kama ada yetu na mazungumzo yanaendelea. Lakini Kleist hakuwa mtu wa kusukumwa aharakishe. Kila kitu kilikuwa kikienda kwa kasi aliyokuwa akiitaka yeye. Alipatapo kuniambia mwanzo kabisa nilipomwambia kuwa nataka kuandika kitabu cha baba yake, ‘’Mohamed haya mambo yanataka subira na wewe ujue lipi la kusema na lipi la kuacha kusemwa.’’ Maneno haya aliyoniambia Kleist yalikuwa sawasawa na maneno ambayo Daisy aliambiwa na mwalimu wake wa historia, John Iliffe mwaka wa 1968 alipotaka kuandika historia ya baba yake. Sababu ya haya ni kuwa tayari palishazuka sintofahamu chinichini katika historia ya TANU.


Kulia waliosimama ni Mohamed Said, Yusuf Zialor, Kleist Sykes, Bubby, Abdallah Tambaza,
waliochutama Abdul Mtemvu, Wendo Mwapachu na Kaisi 1968

Siku moja nikamwambia Kleist maneno aliyonieleza Dossa Aziz nyumbani kwake Mlandizi Nilimwambia Kleist, ‘’Mzee Dossa kaniambia kuwa TANU ilitaka kuandika historia ya TANU miaka ya mwanzoni ya uhuru.’’ Kleist akanijibu kuwa hiyo ni kweli na yeye alikuwa akienda pale Ofisi ya TANU akitoka shule kwenda nyumbani wakati baba yake na Dr. Wilbert Klerruu wakiandika historia ile. Kwa huzuni Kleist akanieleza kuwa kazi ule haikuweza kukamilika licha ya kuwa baba yake alikuja na nyaraka zote za TAA na TANU. Kleist hakunambia kwa nini ile kazi iliishia njiani. Miaka mingi ya mazungumzo na Kleist nilijua wapi nisimame. Akitumia lugha ya kiungwana Kleist alikuwa akinambia kuwa TANU ilikuwa inaikataa historia ya baba yake katika uhuru wa Tanganyika. Jambo hili lilichoma sana moyo wa Kleist. Nilijua hapa ni mahali pa kusimama nirejee wakati mwingine kwa mazungumzo. Mambo haya yalinifikirisha sana.


Kushoto mbele Kleist Sykes na mwanae Abbas Sykes
Waliosimama kulia ni Abdul Sykes katika sare ya King's African Rifles (KAR) na Ally Sykes, 1942
Mwaka wa 1988 katika kukumbuka ya miaka 20 baada ya kifo cha Abdul Sykes, Ally Sykes alinunua nafasi katika Daily News na Uhuru ili kuchapa kumbukumbu ya kifo cha kaka yake.  Usiku Kleist akapokea simu kutoka kwa Reginald Mhango wa Daily News akimwomba radhi kuwa ingawa wamelipia tangazo la kumbukumbu ya baba yake lakini yeye hawezi kuidhinisha ichapwe hadi atakapopata ruhusa kutoka Makao Makuu ya CCM Dodoma kwa sababu maisha ya baba yake yamegusa historia ya TANU na uhuru wa Tanganyika. Kleist alisoma na Mhango Aga Khan School kwa hiyo wakijuana vizuri. Kleist alimwambia Reginald kuwa hayo ndiyo yalikuwa maisha ya baba yake na hana namna ya kuweza kubadili historia hiyo. Kleist akamshauri Mhango aende kwenye gazeti la Sunday News la tarehe 20 October 1968 atakuta taazia ya baba yake iliyoandikwa na Mhariri wa Tanganyika Standard Brendon Grimshaw  inayoeleza hayo yaliyopelekwa Daily News.  Kumbukumbu zile zilichapwa na Daily News na Uhuru lakini uhariri uliopitishwa uliondoa utamu wote wa kumbukumbu ile. Lile ambalo lililokusudiwa halikupatikana.


Earle Seaton na Julius Nyerere
Inawezekana huu mtiririko wa dharau kwa baba yake ndiyo uliomfanya Kleist anipe moja ya labda siri kubwa katika historia ya uhuru wa Tanganyika. Ilikuwa mkakati aloweka baba yake na Hamza Mwapachu katika kuunda TANU toka mwaka wa 1950. Hiyo ndiyo siku aliponitajia jina la Earle Seaton. Mimi nilikuwa nikimjua Seaton kijuujuu tu. ‘’Earle Seaton alikuwa rafiki ya baba yangu,’’ Kleist alianza. ‘’Seaton alikuwa anatoka Bermuda. Seaton alikuwa mwanasheria Moshi. Seaton akimsukuma baba aondoke Tanganyika aende kusoma Amerika baada ya kujua kuwa baba alikosa kwenda Makerere College 1942 kwa kuwa Waingereza walimtia katika jeshi lao, King’s African Rifles (KAR) kwenda Burma katika Vita Kuu ya Pili.’’ Mkakati huu wa Abdul Sykes na Hamza Mwapachu pamoja na Stephen Mhando na Dr, Vedasto Kyaruzi na Dossa Aziz ndiyo uliomwingiza Seaton katika siasa za Tanganyika kupitia TAA Political Subcommittee. Seaton akawa mshauri mkuu wa TAA na akaisaidia TAA katika kutayarisha mapendekezo ya katiba yaliyoitishwa na Gavana Edward Twining mwaka wa 1949. Kleist akanambia kuwa hotuba ya Nyerere UNO ilitoka katika mapendekezo haya ambayo pia yalijadiliwa katika mkutano wa kuasisi TANU 1954.  Sasa nikawa namwangalia Kleist kwa jicho jingine. Huyu anaezungumza na mimi hakuwa Kleist kwani ilinidhihirikia kuwa haya hayakuwa maneno yake Kleist, huyu ni baba yake anazungumza na mimi kutoka kaburini.  Kleist alikuwa mtu wa subira kubwa sana. Yote haya akiyajua na akikaa kimya wakati baadhi ya watu ndani ya TANU baada ya uhuru kupatikana 1961 wakawa akiifanyia dhihaka TAA na kukipa chama kile kila aina ya majina ya kebehi kuwa hapakuwa na siasa katika TAA bali starehe nk. nk. Kleist sasa akawa moja ya funguo katika uandishi wa maisha ya baba yake na historia ya TANU na uhuru wa Tanganyika.

Ndiyo siku moja Kleist akaniangushia bomu nusura likatishe maisha yangu. Akanionyesha shajara (diary) za baba yake akaniambia, ‘’Hizi shajara siwezi kuzitoa humu ndani nikakupa kwani zina na mengi sana kuhusu historia ya TANU na uhuru wa Tanganyika na sijaweza kuzisoma zote kwa kuwa baadhi zimeandikwa katika hati mkato.’’ Kleist akanambia kuwa amesoma nini baba yake aliandika siku alipozaliwa tarehe 27 June, 1950. Kleist akacheka akanambia, ‘’Baba aliniita, ‘’Prince.’’ Hakika baba yake hakukosea kumvika taji mwanae kwani Kleist alikuwa na sudi ya kupendeka. Alipokuwa UNHCR Lusaka, Zambia naambiwa Thabo Mbeki alikuwa akitembea na ufunguo mmoja wa nyumba ya Kleist ili aweze kuingia wakati hata kama yeye hayupo. Huu ndiyo ulikuwa wakati ule wa mapambano ya ANC na makaburu wa Afrika Kusini yamepamba moto.

Halikadhalika mmoja wa mawaziri wakuu wa Mozambique alipata kumuomba Kleist arejee ‘’nyumbani,’’ Msumbiji ampe kazi. Ilikuwa wakati yupo na UNHCR, Lusaka basi siku moja katika mazungumzo na Waziri Mkuu huyu mjini Maputo, Kleist akamueleza kuwa yeye asili yake ni Msumbiji, Kleist akanambia Waziri Mkuu akashtuka sana Kleist alipompa historia ya ukoo wake. Waziri Mkuu akamwambia, ‘’Kleist tuko huru sasa rudi nyumbani nikupe kazi.’’ Kleist anasema huyu bwana alidhamiria khasa kuwa arudi ‘’nyumbani,’’ ampe kazi waijenge pamoja Msumbiji. Kleist alikuwa na mengi na si rahisi kuyaeleza yote.

Siku chache kabla hajafariki Kleist alikuwa alinipigia simu akaniahidi kunipa nyaraka mbili.  Moja ilikuwa ''Admission Letter,'' ya 1953 ya baba yake kutoka Princeton University na nyingine barua pia ya 1953 kutoka kwa Earle Seaton. Ndani ya barua ile Seaton alimwambia Abdul Sykes kuwa asiache kufika UNO kufuatilia mijadala ya Mandate Territories atakapokuwa Princeton, New Jersey. Akaniambia pia alikuwa anataka niende kwake akanionyeshe picha za ufunguzi wa Petrol Station ya baba yake iliyokuwa Ilala mkabala na Ilala Boma. Petrol Station hii ilikuwa chanzo cha fedha nyingi ambazo baba yake alizitoa kwa TANU wakati wa kupigania uhuru wa Tanganyika.

Namuomba Allah amsamehe ndugu yetu Kleist Abdulwahid Sykes madhambi yake na ampe kitabu chake kwa mkono wa kulia.
Amin.

No comments: