Showing posts sorted by relevance for query Abdalla kassim hanga. Sort by date Show all posts
Showing posts sorted by relevance for query Abdalla kassim hanga. Sort by date Show all posts

Thursday 26 December 2013






Mohamed Omari Mkwawa (Tindo) mwanamapinduzi aliyesahauliwa,  mwamasishaji, mpelelezi, mtekelezaji mipango ya upigaji kura Zanzibar 1963, mwanamapinduzi Zanzibar 1964,  askari wa msituni wa Afro Shirazi Party, mvushaji askari mamluki wa Kimakonde na makabila mengineo kwenda Zanzibar kupiga kura na kushiriki katika mapinduzi akiwa amekishika kitabu Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru!




Mmoja wa washirika wa Mohamed Omari Mkwawa alikuwa Victor Mkello.


Photo

Kassim Hanga ni huyo aliyekaa chini ya jukwaa kavaa miwani. Aliyevaa sare ya polisi ni Hamza Aziz kushotoni kwake ni Andrew Shija aliyevaa pama. Aliyekaa mbele ya Kassim Hanga ni Omari Londo. Nyerere ndiye huyo katika ulingo akihutubia.  Hapo ni Mnazi Moja. Baada ya mkutano huu Hanga alirejeshwa Zanzibar na huko akauawa mwaka 1967 au 1968

Utangulizi
Kwa kipindi kirefu historia ya mapinduzi ya Zanzibar ilikuwa ni ile historia rasmi ambayo imeathiri historia nyingi Afrika. Viongozi wa Afrika wanapenda ile historia itakayowakweza na kuwaonyesha wao katika mwanga wa kupendeza. Vinginevyo historia hiyo haitakiwi. Wazalendo wenyewe hawakuwa na hamu ya kuandika historia hii na watu wa nje walioandika historia ya mapinduzi ya Zanzibar hawakupata kuifanyia haki historia ya Zanzibar labda kwa ugeni wao na kwa kuyaamini maelezo yaliyokuwa “wazi” kwa wakati ule, mfano mkubwa ukiwa ni kule kuamini kuwa mapinduzi ya Zanzibar yalipangwa na makomredi wa Umma Party.

Hapajakuwapo udanganyifu mkubwa katika uandishi na utafiti kama huu. Dkt Ghassany amekiweka chano uwanjani bila kawa. Akizungumza na Abdushakur Aboud wa Sauti ya Amerika Dkt Ghassany amesema kuwa historia ya Zanzibar ni historia ya kujijuwa maisha yake akiwa mjukuu wa babu wa mababu Muomani na mabibi wa Kimanyema na Kimwera– mchanganyiko wa damu ya Kiarabu na Kiafrika. Hii kwa hakika ndiyo historia ya wananchi wa Zanzibar. Ni tabu sana kumpata huyo Muarabu Zanzibar kila umuonae Muarabu basi ana mjomba na shangazi Mwafrika. Maadui wa Zanzibar wakiweka mkazo katika ubaguzi wa rangi na kuwafitinisha Wazanzibari. Ukweli huu ndiyo chanzo cha matatizo yote yaliyoikumba Zanzibar toka vyama vya siasa vilipoanza katika miaka 1950 na matatizo yaliyosababisha mauaji ya mwisho yakiwa mwaka 2001.

Mohamed Omari Mkwawa
Mwaka 1995 wakati wa uchaguzi wa kwanza wa vyama vyingi Tanzania nilibahatika kufuatana na mgombea urais wa CUF Prof. Ibrahim Haruna Lipumba katika kampeni za uchaguzi katika mikoa ya Kilimanjaro na Tanga. Prof. Lipumba alifanya mkutano mkubwa sana Tangamano kiasi cha kuishtua CCM. Baada ya mkutano ule Prof. Lipumba na ujumbe wake walialikwa nyumbani kwa mama mmoja akijulikana kama Mama Ummie (sasa ni marehemu) ambako walifanyiwa dhifa kubwa. Kote tukipita mitaa ya Tanga msafara wetu ulikuwa ukishangiliwa kwa nguvu sana. CUF ilikuwa imeingia Tanga kwa kishindo kikubwa.

Mimi kazi yangu ilikuwa kuangalia niliyokuwanayaona na kupiga picha. Kwa hakika nilikuwa nikishuhudia historia ikijiandika. Historia ambayo ilikuwa imeshahibiana sana na ile ya wakati wa kudai uhuru wa Tanganyikakatika miaka 1950. Lakini ninalotaka kusema si hili bali ni picha ambayo niliipiga ndani ya nyumba ya Mama Ummie. Picha hii ilikuwa inamuonyesha mzee mmoja wa makamo aliyevaa fulana ya CUF mbele ikiwa na picha ya Prof. Lipumba. Mzee huyu alikuwa amekaa nyuma ya Prof. Lipumba. Kwa wakati ule picha hii haikuwa na maana yoyote kwangu na hata nilipokuwa naitazama mara kwa mara sura yake si iliyokuwa inanivutia bali ile fulana ya CUF aliyovaa ambayo ilikuwa na picha ya rafiki yangu Prof. Lipumba.

Mungu ana mipango yake. Mihangaiko ya kutafuta riziki yakanihamishia Tanga na nikawa karibu sana na baadhi ya viongozi wa  CUF na wanachama wake. Sasa hapa ndipo nilipokujakuonana uso kwa uso na mzee yule kwenye picha yangu niliyoipiga hata kwa wakati ule ilikuwa miaka mingi iliyopita. Jina la huyu mzee wangu ni Mohamed Omar Mkwawa.  Ilikuwa katika barza yetu ya kawaida  ya kunywa kahawa na kula pweza huku tukijadili historia ya Tanzaniaambako siku moja Mzee Mkwawa alinambia, “Mohamed nataka nikuambie kitu. Unajua mimi nimehusika sana katika mapinduzi ya Zanzibar?”

Nilimuangalia Mzee Mkwawa kwa makini. Fikra yangu ya utafiti na uandishi ishashtuka haipo tena usingizini. Mzee Mkwawa aliendelea, “Mimi ndiye niliyekuwa nikiwavusha Wamakonde kutoka Kipumbwi kwenda Zanzibarkuipigia kura ASP na wakati wa mapinduzi mie ndiye niliyewavusha Wamakonde kwenda kuipindua serikali ya Jamshid.” Sasa moyo wangu ukaanza kudunda kwa nguvu. Naisemesha nafsi yangu, “Huyu mzee anajua uzito wa maneno haya?” Tuishie hapa. Kuanzia siku ile nikawa sasa namtazama Mzee Mkwawa kwa jicho jingine na heshima yangu kwake ikawa imepanda maradufu. Nilikuwa nimeshatambua kuwa Mzee Mohamed Omari Mkwawa alikuwa mmoja wa wanamapinduzi waliosahaulika katika historia ya Tanganyika na Zanzibar. Juu ya hayo nilishangazwa na kitu kimoja. Iweje leo huyu mwanamapinduzi wa ASP ambae Abeid Amani Karume alimpa jina la “Tindo” kwa ujasiri wake amekuwa mstari wa mbele CUF chama ambacho kinanasibishwa na Hizbu hasimu mkubwa wa ASP?


Dr Harith Ghassany
Nilikutana na Dr Harith Ghassany mwaka 1999 nyumbani kwake Maskati, Oman. Naikumbuka siku ile kama jana vile. Kanipeleka kwake mwenyeji wangu Farouk Abdulla lakini kabla ya kunipeleka nilikuwa nimeshalisikia jina lake mara nyingi sana pale Maskati kila nikikutana na jamaa wenye asili ya Tanzania jina lake litaibuka. Katika fikra yangu ikanijia kuwa Dkt Ghassany atakuwa ni mtu mzima. Sielewe kwa nini nilipata picha hii. Tulipopiga hodi na akatokea Dkt Ghassany kuja kutufungulia mlango nikapata mshangao mkubwa.

Aliyekuwa mbele yangu alikuwa ni kijana mdogo sana tofauti na nilivyodhani. Kwa njia ya utani hata kabla sijatoa salamu. Nikamgeukia Farouk nikasema, ”Ah! Dkt Ghassany, Dkt Ghassany, Dkt mwenyewe ndiye huyu?” Mila na tamaduni za watu wa pwani wakikutana hazipishani. Maskhara ni dalili ya mapenzi. Dkt Ghassany pale pale alipokea yale maskhara na akajibu, ”Bwana  wangu we wanakutisha bure kwani we ulidhani litakuwa jitu kubwa?” Urafiki na udugu wetu umedumu hadi leo na ndipo katika mazungumzo aliponifahamisha kuwa anataka kuandika historia ya kweli ya mapinduzi ya Zanzibar. Hapo ndipo nilipomjuvya kuhusu Mzee Mkwawa na nikamuomba aje Tanga amuhoji.

Kitu kimoja mashuhuri kwa mashujaa wa harakati za siasa katika Tanzania ni kuwa takriban wote wana hali ngumu sana za maisha. Sikujua vyema hali ya Mzee Mkwawa hadi nilipofika nyumbani kwake na Dkt Ghassany. Utu uzima na udhaifu wa maisha ulikuwa umempiga barabara. Nilimjulisha Dkt Ghassany kwa Mzee Mkwawa na kuwaacha waendelee na maongezi yao. Niliporudi mchana kumchukua Dkt Ghassany rafiki yangu alinambia nimuache nije jioni kumfuata. Niliporudi jioni nilimkuta Dkt Ghassany amechoka na uso umesawijika. Tukiwa ndani ya  gari yangu tunaondoka nikamuuliza kulikoni. Dkt Ghassany akanambia maneno ambayo hadi leo yamebaki kichwani mwangu, ”Mohamed ufunguo wa kitabu changu anao Mzee Mkwawa na kama nisingeonana nae utafiti wangu wote wa kabla ungelikuwa hauna maana yoyote.”

Dkt Ghassany alikuwa amechukuliwa na Mzee Mkwawa katika safari ya zaidi ya nusu karne. Mzee Mkwawa akimshika mkono kwanza kumpeleka Pemba ambako akiwa kijana wa kiasi cha miaka 25 akifanya kazi ya uashi. Huo ndio ulikuwa wakati wa siasa za ASP na Hizbu zimepamba moto. Mzee Mkwawa alikuwa mmoja wa wachezaji wa ngoma ile hata kama alikuwa anatoka Tanganyika. Dkt Harith akavushwa na kuletwa pwani ya Kipumbwi na Sakura ambako Mzee  Mkwawa alikuwa akisimamia kambi ya mafunzo iliyokuwa msituni ya wakata mkonge wengi wao wakiwa Wamakonde, kambi ambayo ilitoa askari waliotumika kuipindua serikali ya Mohamed Shamte 12 Aprili 1964.

Dkt Ghassany hakuwa amejitayarisha kwa haya. Alishangwazwa na uwezo wa kumbukumbu wa Mzee Mkwawa, akitaja majina na mahali na akirudia mazungumzo neno kwa neno kati yake na maofisa wa serikali ya Tanganyika kutoka vyombo vya usalama waliomtia katika operesheni maalum ya kuipindua Zanzibar kutoka Tanganyika. Majina ya Abdulla Kassim Hanga, Jumanne Abdallah, Ali Mwinyi Tambwe, Victor Mkello, Oscar Kambona na wengine yakawa yanadondoka moja baada ya lingine. Taarifa hizi ndizo zilizommaliza Dkt Ghassany na kumsawajisha uso.

Mimi binafsi nilipigwa na butwaa. Nilibaini kama alivyobaini Dkt Ghassany kuwa Mzee Mkwawa alikuwa hazina na tulikuwa tumevumbua mgodi wa dhahabu. Kazi yetu sasa ilikuwa kuchimba tu. Kumekuwa na uvumi kwa miaka mingi katika duru za wanasiasa wapya na wa zamani na katika wanafunzi wa historia ya Tanzania na Mapinduzi ya Zanzibar kuwa Ali Mwinyi Tambwe alihusika sana katika kupinduliwa kwa serikali ya Zanzibar lakini hakuna aliyejuwa ni kwa kiwango gani na alihusika vipi. Lakini zito ni kuwa yeye mwenyewe akiudhika sana mtu akimuuliza habari zile. Kwa nini ilikuwa hivyo? Kitabu cha Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru cha Dkt Ghassany kilikuja kutoa majibu. Hakuna binadamu apendae historia yake ihusishwe na mauaji na dhulma na kufutwa kwa nchi yake.

Kwa kipindi cha takriban miaka saba Dkt Ghassany alikuwa akija Tanga kwa mahojiano na Mzee Mkwawa na katika kipindi hicho Mzee Mkwawa alitupeleka Kipumbwi na Sakura na kutuonyesha sehemu zile ambazo walikuwa na kambi na wakifanya mazoezi ya kivita na matumizi ya silaha. Mkahawa ambao wale wakata mkonge walikuwa wakila chakula cha usiku kabla ya kuvushwa kwa vyombo vya bahari kwenda Unguja bado upo hadi leo ingawa kwa sasa kijumba kile hakitumiki tena kama mkawaha. Endapo itakuja siku serikali ya Zanzibar itataka kuhifadhi historia ya Mapinduzi ya Zanzibar bila shaka moja ya vitu vitakavyokuwa katika makumbusho ni picha ya hicho kibanda.

Victor Mkello
Kipumbwi haijabadilika iko kama vilevile iliyokuwa miaka ya 1960. Kipumbwi imebaki vilevile kama kijiji cha uvuvi. Mzee Mkwawa alitupeleka hadi sehemu ambapo bahari imeingia katika kijiji lakini sehemu hiyo imefunikwa na mikoko mingi na vichaka. Tuliingia ndani na kuangalia mandhari ya pale mahali. Hakika pale palikuwa sehemu nzuri ya kujificha. Leo imekuwa sehemu hii ni maarufu kwa watu wa magendo.  Mzee Mkwawa alitueleza kuwa hapo ndipo walipojificha na ndipo walipopandia vyombo vyao kwa usiri mkubwa wakati wote wakiwa wamevaa nguo matambara na kofia za makuti kama wavuvi. Tanga ilikuwa kituo muhimu cha kufanikisha mapinduzi ya Zanzibar. Haikuwa bure kuwa Ali Mwinyi Tambwe, Jumanne Abdallah na Victor Mkello walikuwa hapo na wala haistaajabishi kwa Dkt Ghassany kutueleza kuwa vinara wa mapinduzi kwa upande wa bara, Mkello na wenzake, walisubiri taarifa za mapinduzi katika mkesha ndani ya ofisi ya TANU Tanga.

Napenda kukiri kuwa sikupata kushiriki kama msikilizaji wa mahojiano wakati wa utafiti wa Kwaheri Ukoloni Kwaheri Uhuru. Kazi yangu kubwa sana ilikuwa kufungua milango na kumwendesha daktari. Kwa ufupi kazi yangu ilikuwa kumwekea mwandishi mazingira mazuri ili kazi yake iwe nyepesi. Kwa hakika ilikuwa kazi ambayo na mimi vilevile nilisoma, kujifunza mengi na kupata faida kubwa. Katika haya nakumbuka sakata la kumtafuta Victor Mkello. Leo si wengi wanaomjua Victor Mkello au hata kupata kusikia jina lake likitajwa. Lakini kwa sisi tuliokuwa wadogo tukiwa shule katika miaka ya 1960 Mkello alikuwa hapungia katika magazeti ya Ngurumo na Mwafrika. Mzee Mkwawa ndiye aliyetusaidia kumtafuta alipo. Victor Mkello ndiyo aliyekuwa ”Amiri Jeshi Mkuu” wa lile jeshi la Wamakonde lililokuwa na makao yake makuu katika mashamba ya mkonge ya Sakura na Kipumbwi. Bila ya kupata kauli ya Mkello kitabu kisingeweza kuandikika.

Ilichukua muda kuweza kumpata. Kwanza tulikwenda Muheza ambako ndiko kwao. Huko tukaambiwa kuwa hakuwapo hapo bali kwa muda mrefu alikuwa Tanga. Mwishowe tulimkuta nyumbani kwake Nguvumali. Mkello alikuwa katika kitanda cha mauti. Kisukari kilikuwa kikimla kiwiliwili chake. Hakuwa anaweza kunyanyuka kitandani wala kukaa. Kwa hakika alikuwa anasikitisha. Huyu hakuwa Victor Mkello niliyekuwa namsoma katika magazeti wala yule ambae Mzee Mkwawa alikuwa akituelezea. Mtu mjanja aliepambana na Magiriki wamiliki wa mashamba ya mkonge akitetea haki za Waafrika katika miaka ya 1960. Huyu kwa kweli hakuwa yule Victor Mkello aliyekuwa akisaidiana na TANU na Mwalimu Julius Nyerere kupigania uhuru wa Tanganyika. Hiki mbele yetu kilikuwa kivuli chake. Hapakuwa na wasiwasi wowote Victor Mkello alikuwa akisubiri malaika wa mauti amtembelee na yeye hilo alikuwa akilijua fika.

Victor Mkello na Mzee Mkwawa wanamapinduzi waliofutwa katika historia walitazamana na wakasalimiana kama vile hakuwapata kujuana. Jicho la Mkello lilikwenda kwa Dkt Ghassany kisha likaangukia kwangu kisha likarudi kwa mwanamapinduzi mwenzake Mzee Mkwawa. Baada ya utambulisho uliofanywa na Mzee Mkwawa nilihisi woga na wasiwasi kwenye sura ya Victor Mkello. Hakuwa anaamini kuwa Dkt Ghassany katoka Maskati kwa ajili ya utafiti wa historia na hili lilijidhihirisha alipofunua kinywa kuzungumza. Victor Mkello alikuwa na hisia kuwa alifuatwa kukamatwa kwa vifo vya Waarabu vilivyotokea Zanzibar wakati wa mapinduzi ili apelekwe Mahakama ya Kimataifa. Baadae Dkt Ghassany alinifahamisha kuwa jinsi Waingereza walivyomueleza katika taarifa zao za siri ambazo yeye alizisoma London zimeafikiana kabisa na jinsi alivyomuona pale. Waingereza walimsifia Mkello kwa kusema kuwa alikuwa bingwa wa kuteleza kama samaki ndani ya maji.

Kufupisha maelezo. Ilichukua karibu miaka mitatu kwa Victor Mkello kukubali kuzungumza kuhusu mapinduzi ya Zanzibar. Dkt Ghassany akienda Maskati na kurudi Tanga na kila akienda kwa Victor Mkello, Mkello hakuwa tayari kueleza kile alichokijua kuhusu mapinduzi ya Zanzibar. Kila nilipokwenda na Dkt Ghassany kumuona Mkello hali yake ilikuwa inazidi kudidimia. Sasa alikuwa kakatwa mguu mmoja kwa ajili ya kisukari. Ilikuwa katika hali ile katika siku zake za mwisho ndipo siku moja alipomwambia Dkt Ghassany aje siku ya pili na yeye atazungumza na angependa azungumze mbele ya mkewe ili amkumbushe pale atakapokuwa kasahau kitu.

Hapa ndipo ilipo moja ya sehemu tamu kabisa ya kitabu hiki Kwaheri Ukoloni Kwaheri Uhuru. Victor Mkello Amiri Jeshi Mkuu wa Mamluki wa Kimakonde alizungumza. Mimi sikushiriki katika mazungumzo yale nilijiweka pembeni ili Mkello azungumze na Dkt Ghassany kwa utulivu. Nilikuwa nimeegesha gari yangu karibu ya msikiti jirani ya nyumba ya Mkello nikimsubiri daktari akamilishe upasuaje mgonjwa apate nafuu. Mwendo wa Dkt Ghassany wa kudunda alipokuwa ananijia pale nilipoegesha gari ulidhihirisha furaha yake.

Haukupita muda mrefu baada ya mazungumzo yale na Dkt Ghassany, Victor Mkello akaaga dunia kimya kimya. Hakuna mtu aliyejua kifo chake kama ilivyokuwa vifo vingi vya mashujaa waliopigania uhuru wa Tanganyika. Hakuna hata gazeti moja lililotoa taazia yake wala hotuba hazikusomwa kaburini kwake. Mkello aliondoka katika historia ya Tanzania kimya kama jinsi mamluki wake walivyokuwa wakiingia Zanzibar kimya kimya usiku mkuu  na kwa siri, mapanga yao makali ya kukata mkonge yakiwa chini ya nguo zao za ndani yakisubiri kuivamia Zanzibar na kuua watu wasio na hatia. Kazi hii kwao haikuhitaji mafunzo kwani  mafunzo walikuwanayo muda mrefu katika kazi yao ya kukata mkonge katika mashamba ya mkonge ya Tanga. Pigo moja lilitosha kuangusha chini jani zito la mkonge seuze kiungo cha binadamu.

Kwaheri Ukoloni Kwaheri Uhuruni kitabu kilichoandikwa kwa staili ya pekee wahusika wenyewe wa matokeo katika mapinduzi kujitolea kueleza kile kilichotokea katika mapinduzi, kabla na baada yake. Kuanzia mipango ya kuangusha serikali ya Zanzibar hadi katika kuwaua wale waliokujakushukiwa kuwa ni maadui wa mapinduzi hadi kufikia hata kuweka wazi jinsi walivyoshiriki katika mengi ya kusikitisha kupelekea hata msomaji kujiuliza kwa nini hawa watu baada ya miaka yote hiyo kupita wameamua kueleza yote hayo. Vipi Abdallah Kassim Hanga, Othman Shariff, Mdungi Ussi, Jaha Ubwa, Abdulaziz Twala na wengineo walivyouliwa, nani alitoa amri ya mauaji, nani aliwauwa na katika mazingira gani. Kifo cha Karume mwenyewe kwa mtutu wa bunduki hakikuwekewa pazia na chanzo cha kuamuliwa kuwa auawe ni tofauti ya kilichozoeleka kuelezwa. Karume hakuuawa na ”wapinga mapinduzi” kama ilivyozoeleka kuelezwa katika historia rasmi.

Kwa kumaliza tusubiri mapitio ya kitabu hiki na ni wazi kuwa wasomaji watapata mengi ya kuelimisha na kuhuisha. Tunategemea wasomi wa somo la historia watakaopitia kitabu hiki watatufanyia hisani kubwa kwa kuwaleta katika picha wahusika wakuu wa mapinduzi – Mwalimu Julius Nyerere – fundi mkuu mwenye kishindo kikubwa lakini hakisikiki, mkono wake wa chuma hauonekani, uso wake nyuma ya pazia, Abdallah Kassim Hanga – kiongozi hasa na mpangaji wa mapinduzi, Victor Mkello – mtumishi wa Hanga na Nyerere  bila ya yeye mwenyewe kujua kati ya hao wawili nani aliyekuwa bingwa kumshinda mwenzake katika mchezo mchafu wa siasa ya kuiuwa Zanzibar na Wazanzibari na wengineo.

Lakini juu ya hayo yote mipango hii ilikuwa ni ya akina Nyerere, Hanga na Mkello pekee? Dkt Ghassany anaeleza nini kuhusu mkono wa Waingereza, Algeria, Misri, Wachina, Warusi, Marekani na Mayahudi? Nini kilichowasukuma hao wote katika mapinduzi ya Zanzibar? Nini kilimsukuma Nyerere, kuwapindua Waislam walioupigania Uhuru wa Tanganyika na baadae kuwapinduwa Waislam walioupigania Uhuru wa Zanzibar na kuendelea kuwadhibiti hata baada ya kuipindua Zanzibar? Nini kilichowasukuma Waingereza na Wamerekani kuachia mapinduzi yafanyike? Lakini kubwa zaidi kipi kilichowasukuma Wayahudi kuingia na kusaidia mapinduzi, ni ile chuki yaoya asili dhidi ya Waarabu au kulikuwa na jengine ambalo liliwatia khofu? Na kwanini kitabu kiitwe Kwaheri Ukoloni Kwaheri Uhuru: Zanzibarna Mapinduzi ya Afrabia? Kitabu kina majibu ya haya maswali mengine ambayo bado hayajaulizwa na chemchemu mpya za utafiti.

Dkt Ghassany anastahili pongezi kubwa sanakwa kuinusuru historia ya mapinduzi ya Zanzibarna kuwaamsha Wazanzibari na Watanganyika toka lepe zito la usingizi ili wajitambue na wamjue adui yao. Anastahiki pongezi kubwa zaidi si kwa kukiandika kitabu cha Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru bali kwa kutumia mrengo usiokuwa na mrengo. Huna pa kumuweka Dkt Ghassany na baada ya kumaliza kukisoma kitabu ukaridhika napo. Kamautafikiria kuwa kitabu ni cha CUF basi baada ya kusoma mpaka mwisho utavunjika moyo. Kama utamtumbukiza ndani ya CCM basi ataelea. La kama unataka upae nje ya masunduku na mapakacha basi utamuona katulia ndani ya uhuisho wa umoja wa Zanzibarna Tanganyika Mpya – Tanzania Mpya.

Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru ni ngoma nzito ambayo watu wameanza kuicheza hata mdundo haujaanza kupigwa! Tayari imeshaingia katika rikodi za Hansard za Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tayari imeshasikika katika Sauti ya Marekani. Tayari daktari anafuatilia kwa karibu ukweli wa Maridhiano na kuwa kwa mara nyengine tena ukweli wake umeshaanza kupotoshwa na waroho na tayari historia mpya na kubwa zaidi hata kuliko ile ya Mapinduzi ya Zanzibar ya 1964 imeshaanza kuvurugwa.

Watengenezaji wa filamu Hollywoodwana mtindo wa kumaliza senema zao za matokeo ya kweli kwa kueleza katika maandishi yale yaliyowafika wahusika wa kisa kilichotengenezwa hiyo senema. Huonyesha majina na mwisho wa hao wahusika, kama wahai, wako wapi, wamekufa na kama wamekufa ni kwa kuuliwa au kwa amri ya Mungu nk. Katika Kwaheri Ukoloni Kwaheri Uhuru majina ya wahusika machache ambayo yametajwa katika makala haya yako kamahivi:

1.     Mohamed Omar Mkwawa:           Yu hai na anaishi Makorola Tanga
2.     Abeid Amani Karume:                            Ameuawa 1972
3.      Abdallah Kassim Hanga:             Ameuawa 1967/68
4.     Mustafa Songambele                      Yuhai anaishi Songea.
5.     Victor Mkello                                  Amekufa kifo cha kawaida
6.     Ali Mwinyi Tambwe                      Baada ya mapinduzi alikuja kuhusika katika mchakato wa kuunda muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Amekufa kifo cha kawaida.
7.     Jumanne Abdallah                         Alitumikia serikali kwa muda mrefu hadi alipofariki kifo cha kawaida
8.     Oscar Kambona                              Aligombana na Nyerere na akakimbia nchi mwaka 1967 na kwenda kuishi uhamishoni Uingereza
9.     Kuna vigogo kadhaa ambavyo viko hai na kwa sasa wameomba majina yaoyahifadhiwe.

17 Ramadhani 1431

28 August 2010

Photo

Ali Mwinyi Tambwe na Abeid Amani Karume



Abdalla Kassim Hanga

Kuwa Hanga ndiye aliyekuwa kinara wa Mapinduzi ya Zanzibar hili si jambo lenye utata tena. Ikiwa hivyo ndivyo Hanga hatoweza kuutua mzigo wa roho zilizopotea katika mapinduzi hayo. Ikiwa Hanga atalaumiwa kwa vifo vya maelfu ya Wazanzibari nani alaumiwe kwa umauti uliomfika Hanga tena kwa kuuliwa kishenzi kwani hapana neno zaidi ya hilo linaloweza kutosheleza kuelezea jinsi Hanga alivyouliwa. Kichekesho kikubwa ni kuwa wale waliopoteza roho kwa hiyo kutangulia mbele ya haki, yao yalikuwa yamekwisha. Lakini kwa wale wajane na mayatima waliobakia nyuma wakihangaika, kifo cha Hanga na wenzake katika wale waliofanikisha mapinduzi kuuliwa kwao kulikuwa muujuza wa aina yake, uchawi usioelezeka nani fundi wake. Ilikuwa vigumu kueleza. Ingeeleweka vyema endapo kisasi cha kuitoa roho ya Hanga kingetimizwa kutoka katika mikono ya maadui zake waliopinduliwa. Haikuwa hivyo.

Wale wajane na mayatima walililipiziwa kisasi na watu waliokuwa maadui wakubwa wa waume na baba zao waliopinduliwa. Vipi Hanga kiongozi mkuu wa mapinduzi aje kuwa adui wa mapinduzi yenyewe kiasi cha kuwa hukumu ya kumtosheleza haikuwa kifo tu bali kifo cha kishenzi. Fikra ya Hanga ilikuwaje alipokuwa peke yake ndani ya selo Ukonga Prison…usiku ukimpita bila ya hata lepe la usingizi akiwaza yanayomkabili. Nini kilikuwa kikipitika katika ubongo wake wakati wauaji wake walipomtoa katika selo yake na yeye akawakabili ilhali aikijua kuwa walikuwa wamekuja kuitoa roho yake. Fikra yake ilikwenda wapi? Ilikwenda kwa Sultan Jamshid bin Abdullah aliyempindua na kwa Masultani wengi waliopita ambao wameiaga dunia mikono yao ikiwa haina damu au kwa Abeid Amani Karume aliyeingia madarakani kwa mapanga ya Wamakonde kutoka Tanganyika, wakata mkonge kutoka Tanganyika wakifanya kazi mashamba ya Sakura na Kipumbwi? Fikra ya Hanga ilielekea wapi? Kwa Nyerere aliyemsaliti?

Hakika ni wazi hakutegemea mapinduzi aliyoyasisi yangemgeukia na kuwa sababu ya yeye kutolewa roho kwa kuuliwa kishenzi. Jambo la kusikitisha ni kuwa hadi pale alipokamatwa na kuwekwa jela Ukonga na kufikishwa mbele ya mkutano wa hadhara na kuadhiriwa na Julius Nyerere tayari alikuwa keshapoteza kila kitu achilia mbali dira ya mapinduzi aliyokusudia ingeongoza Zanzibar. Hanga hakuwa kamwe na uwezo wa kumfanya Karume lolote kwani Karume tayari alikuwa chini ya mbawa za Nyerere ngome ambayo Hanga asingeweza kuitikisa achalia mbali kuibomoa. Muungano baina ya Tanganyika na Zanzibar ilikuwa hirizi tosha ya kumkinga Karume.

Katika mkasa wa kuuliwa kwa Hanga ndipo msemaji mmoja akasema, “Maiti toka makaburini mwao walionyesha ujuzi wa kufanya miujiza na uchawi wao kwani laiti kifo cha Hanga kingesababishwa na wale waliopinduliwa kisasi chake kingekuwa cha kutisha. Ilibidi Hanga kwa miujiza ya maiti zile auliwe na wale wale aliowaweka madarakani watu ambao hapakuwepo na sababu ya wao kumuona adui. Halikudondoka chozi kwa kifo cha Hanga. Kila aliyepata mnong’ono wa kuuliwa kwake alikuwa kimya kama vile ile taarifa ile ya kifo haimuhusu.


10 February 2010
Kutoka Kushoto: Farouk Abdullah, Mwandishi, Sheikh Ali Muhsin na Sheikh Abdallah Muhsin
Muscat, Oman 1999
Mzee Mkwawa Akionyesha Kitabu cha Historia ya Mapinduzi ya Zanzibar 

Mwandishi akifanya mahojiano ya televisheni  (TV Imaan) na aliyekuwa katibu wa kwanza wa
 Baraza la Mapinduzi  Zanzibar  Salim Rashid 
Aliyevaa shada la maua ni Mohamed Abdulrahman Babu, pembeni yake Ali Muhsin Barwan na mwisho
ni Mohamed Shamte 
Waliokaa kushoto ni Abdallah Kassim Hanga akifuatiwa na Abeid Amani Karume

Friday 5 June 2015



Tanbihi ya Tanbihi: Kumbukumbu, Kusahau, na Zanzibar Mpya

Na Harith Ghassany

Zanzibar 1950
  
Madhumuni ya maandishi haya mafupi si kumjibu Mzanzibari mwenzangu na kaka yangu Ahmed Rajab, mwandishi maarufu na mwenye kusifika barani Afrika. Nia yangu ni kuweka sawa baadhi ya dhana zake kwa manufaa ya Zanzibar ndani ya wakati huu tulionao.

Mwandishi maarufu wa riwaya, Milan Kundera, aliandika: “Mapambano ya binaadamu dhidi ya nguvu [za dola] ni mapambano baina ya kumbukumbu na kusahau.” Suala kuu la kwa kila Mzanzibari aliyeishi kabla au baada ya miaka 50 iliyopita ni, anakumbuka au anakumbushwa nini, anasahau au anasahaulishwa kitu gani, na kwa nini? Suala hilo ni la kwanza kabisa. Suala la chuki, kulipizana kisasi, au kusameheyana bila ya kusahau, ni masuala ya mtitiriko wa suala kuu.

Kwa hiyo, tunapolizungumzia suala la kumbukumbu na kusahau, la kwanza la kujiuliza na kulizingatia ni, tunakumbuka au kusahau kitu gani? Na hicho kinachokumbukwa ni kipi na jawabu yake inatokana na kundi au makundi yepi kati ya makundi matatu  aliyoyataja Rajab:
1.        La wahusika
2.         La walioshuhudiya
3.         La walioyasikiya

Rajab kajiweka kwenye kundi la pili na kuzidi kujiaminisha na aaminike, ameandika kuwa ana ushahidi wa maandishi wenye kuthibitisha yale anayoyakumbuka. Nimefurahi sana kulijuwa hilo kwa sababu tuna mfano mzuri sana wa kufananisha usahihi wa nguvu za historia ya maandishi ya wakati wa tukio na udhaifu wa “historia simulizi” za baadae.

Napenda kumuomba kaka yangu mpenzi atupatie japo kopi ya kumbukumbu za maandishi ya mkutano wake na marehemu Abdalla Kassim Hanga pamoja na Wazanzibari wenzake wawili, ili tupate kipimo cha kuyapima yale ambayo yeye ameyahifadhi kama ni shahidi wa maandishi.

Lakini turudi nyuma kidogo kwenye kumbukumbu na kusahau hata bila ya kujaribu kuyakumbuka au kuyasahau yaliyotokeya katika mkutano wa miaka 47 iliyopita.

Kitabu cha "Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru," (na si "Kwaheri Uhuru, Kwaheri Ukoloni," kama alivyoandika Ahmed Rajab kwenye sehemu ya pili ya makala yake ya “Tanbihi”), kina kurasa 496.  Kati ya hizo ni kurasa tatu tu, ukurasa 267-270, zenye kuuzungumziya mkutano wa London baina ya Wazanzibari watatu na Hanga. Lakini hizo kurasa tatu ni muhimu katika muktadha wa maudhui ya kukumbuka na kusahau kwa sababu, na Mungu awazidishie afya Ahmed Rajab na Bwana Salum Hamdan ambaye anaishi Maskati, Oman, watu wawili hao wenye kuhusika moja kwa moja na suala la changamoto za kuandika historia, Alhamdulillah, wote wawili wako hai na wana akili zao.  

Kwanza napenda kumkumbusha msomaji kuwa Bwana Salum Hamdan ni wa kundi la pili, la waliyoshuhudiya, kama anavyojinasibunalo Ahmed Rajab. Tafauti yao ni Ahmed Rajab ameweka kumbukumbu ya maandishi ambayo narudiya tena, tutamshukuru sana akitupatiya ili tujifunze namna ya kuzizidhibiti changamoto katika suala zima la kuisajili historia na athari zake mbaya na nzuri za baadae.

Mzee Salum Hamdan ni mzee wa hikma na busara. Nilipokwenda kuonana naye kwa mara nyengine ili nizisajili kumbukumbu zake, aliniambia nisubiri mpaka atakapozungumza na Ahmed Rajab kwa sababu kuna mambo ambayo huenda akawa ameyasahau au hayakumbuki vizuri. Na hapo ndipo msomaji wa kurasa 267-270 katika kitabu cha “Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru,” atakutana na maneno yafuatayo ya Salum Hamdan yenye kuonyesha kuwa alikuwa shahidi wa mkutano ambaye aliamua kuzungumza na Ahmed Rajab kabla ya kuzungumza na mwandishi (Harith):

 “Sasa tulivyokuwa London yeye [Ahmed Rajab] kataja watu watatu tu.” Ukursa 267.
“Nnavyokumbuka mimi Oscar akatwambia sikilizeni bwana.” Ukurasa 268.
 “Ndivo navokumbuka mie na ndivo anavokumbuka Ahmed [Rajab].” Ukurasa 268.

“Mimi skumbuki ile nilikwenda railway station. Kile mimi sijakumbuka. Kama ulivosema, mimi nyumba nilikuwa naijuwa, sina haja ya Kasembe kunpeleka. Lakini inaweza kuwa nimekwenda mimi na Kasembe kumpokea Ahmed Rajab. Yeye Ahmed kafikiri tu na mie ni mgeni. Hajajuwa kuwa mimi na Kambona tunajuwana na jirani, na nyumba yangu mie na yake si mbali.” Ukurasa 268. “Yeye Ahmed amekumbuka  mambo mimi sijayakumbuka.” Ukurasa 268.


Oscar Kambona
Inasikitisha kuwa mwandishi gwiji na mahiri kama Ahmed Rajab angalau kusema kuwa Salum Hamdan alizungumza na yeye kama mwenzake kuyathibitisha yale walioyashuhudia pamoja na Hanga kabla ya kumpa mkusanyaji (Harith) taarifa za mkutano wa London. Ahmed Rajab kashindwa kuwa mkweli na muwazi na badala yake kaamua kujaribu kunirushia ndoo ya tuhuma yenye uchafu wa “msimamo wa kisiasa,” “dhana Fulani,” “kupotosha historia,” “kutoa maelezo kinyume na matukio halisi yalivyotokea,” na kumumunya “wanaoendeleza chuki wakikataa kusamehe.” Hee!

Lumumba

Kama tayari nilikuwa nina dhana fulani, kwanini nilizitupilia mbali simulizi za kina marehemu Ali “Lumumba” na wengineo, na kumfuata Mohamed Said Tanga na kuonana na wazee wazito wa Dar es Salaam? Marehemu Mzee Hamza Aziz ambaye alikuwa Kamishna wa Polisi aliniuliza suala dogo lakini zito. Aliniambia, “Sikiliza kijana. Inataka kwanza ujiulize yale Mapinduzi ya Zanzibar yalipangwa huku kwetu Tanganyika au kule kwenu Zanzibar?” Hapo ndipo nilipoipata ile Wazungu wanayoiita “gestalt switch” au “paradigm shift.” 

Aliyeshika Kiuno Katika Mavazi ya Polisi ni Inspector General of Police (IGP) Hamza Aziz Akiangalia Usalama Uwanja
wa Mnazi Mmoja Mbele ya Kibarua Bar Nyerere Akihutubia Kumueleza Abdallah Kassim Hanga. Pembeni
ya Hamza Aziz Kashika Kiuno ni Paschal Shija na Chini Yake Aliyekaa ni Kassim Hanga na Mbele ya Hanga
Aliyekaa Mwenye Miwani Akitabasamu ni Mzee Omari Londo Mzee wa TANU
Hassan Nasoro Moyo akisoma kitabu Kwaheri Ukoloni Kwaheri Uhuru

Haikuwa dhana wala uhodari wangu. Na hiyo ilitokeya baada ya kupoteza kama miaka miwili Zanzibar kuyatafuta Mapinduzi mchana kwa vibatari na kandili ndani ya vichochoro vya Mji Mkongwe na N’gambo yake!

Dr. Harith Ghassany na Mohamed Said

Hayo yote bado sijayaona umuhimu wake kwa sababu kuna faida au somo gani katika kukumbuka au kusahau kama Oscar Kambona ndiye au siye aliewaita Wazanzibari kwake au kama alimtuma Kasembe? Muhimu Ahmed Rajab alifika kwa Oscar Kambona na angelitaka angeliamua kutohudhuria mkutano baada ya kutambua kumbe Kasembe hakuwaambia alikuwa amewachukuwa kwenda kwa kitimbakwiri na msaliti wa ukombozi wa Afrika - Oscar Kambona. Haingii akilini hata kidogo kuwa Ahmed Rajab abebwe tu na Kasembe kama pakacha la madoriani halafu ajikute anafunguliwa mlango na Kambona!

Ali Mzee Mwenyekiti wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar akiwa na kitabu ''Kwaherri Ukoloni Kwaheri Uhuru,''

Rostam Aziz akiwa na kitabu Kwaheri Ukoloni Kwaheri Uhuru
Narudia tena. Yote hayo si muhimu kwa sababu suala muhimu kwa kila Mzanzibari ni kukumbuka au kusahau namna Zanzibar ilivyotoweka na kupotea au kupotezwa kama ni nchi yenye mamlaka kamili kupitia tukio la tarehe 12 Januari, 1964, na yaliofuatiliya.  Suala si nani alikuwa akitawala, uhalali au uharamu wake. Suala ni kupotezwa nchi kwa kuvamiwa na baada ya muda mfupi kumezwa ndani ya muungano. Ni kama vile kumbaka mwanamke halafu ukaamua kufunga pingu za maisha naye kwa kufanya harusi!

Na ndio maana mazungumzo ya Hanga kwa mujibu wa Salum Hamdan niliyaweka katika mlango wa “Hayeshi Majuto Yao.” Bwana Salum Hamdan ambaye yuhai amemnukuu marehemu Hanga:

“…sisi Mungu atusamehe, tumefanya mambo mengi ambayo mabaya, tumedhulumu, tumechukuwa watoto na wake za watu, na Mwenye Enzi Mungu anisamehe na ninajuta kwa haya nlioyafanya.” Ukurasa 269.

Kinyume cha Salum Hamdan, Ahmed Rajab kayasahau maneno ya Hanga yaliyonukuliwa na Salum Hamdan lakini ameyakumbuka maneno aliyojisafisha nayo Hanga kwa kumtusi Kambona.

Salum Hamdan ameeleza, “Lakini inasikitisa kuwa tangu wakati ule yeye [Hanga] yupo pale London habari zishafika Cairo. Walioko Cairo maambassador wa pale wameshapeleka habari Tanzania kwa Mzee Nyerere. Ikawa serikali inavosikia wamekaa wakimgojea arejee tu. Yeye Hanga hajajuwa, wala sisi hatujajuwa.” Ukurasa 270.

Anaandika Rajab: “Kutoka Conakry, Hanga alirudi nyumbani, akipitia Cairo, ambako alikuwa mgeni rasmi wa Ahmed Diria Hassan, Balozi wa Tanzania nchini Misri. Aliporudi Dar es Salaam ndipo Hanga alipokamatwa kwa amri ya Rais Julius Nyerere na akapelekwa Zanzibar ambako aliuliwa kikatili.” Ahmed Rajab hajui au hakumbuki kuwa kumbe Hanga alikuwa ameshauliwa kutoka Cairo.

 Kitabu cha “Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru,” si kitabu kilichosimama juu ya midomo ya simulizi peke yake. Kila mlango wa kitabu cha “Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru,” una marejeo ambayo yanatokana na "primary" na "secondary" “sources.” Kwenye utafiti wa kihistoria, "primary" “sources” ni marajeo ya watu ambao walishiriki na waliyashuhudia yale ambayo wanayazungumzia. "Secondary" “sources” zinaweza zikawa ni vitabu ambayo vinategemea nini watu wengine wameandika na mwandishi mwenyewe si mwenye kuyashuhudia yale yalioandikwa au kusemwa. Simulizi za wazee si zangu mimi bali ni za wazee walioshiriki moja kwa moja au kwa karibu sana na tukio la Zanzibar la 1964. Na ikumbukwe pia, historia ya maandishi inatokana na historia ya simulizi. Yakumbuke ya Jibrili, Wahyi, na kukusanywa kwa Qur’an.

Kitabu cha “Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru,” kina milango ishirini na moja.

Sasa wacha twende mlango kwa mlango:
1. Kwenye "Mapitiyo kwa Jumla" kuna endnotes (mapitio) 24.
2. Mlango wa Kwanza una mapitio 25.
3. Mlango wa Pili una mapitio 42.
4. Mlango wa Tatu una mapitio 27.
5. Mlango wa Nne una mapitio 6.
6. Mlango wa Tano una mapitio 19.
7. Mlango wa Sita una mapitio 11.
8. Mlango wa Saba una mapitio 15.
9. Mlango wa Nane una mapitio 20.
10. Mlango wa Tisa una mapitio 14.
11. Mlango wa Kumi una mapitio 2.
12. Mlango wa Kumi na Moja una mapitio 16.
13. Mlango wa Kumi na Mbili una mapitio 18.
14. Mlango wa Kumi na Tatu una pitio 1.
15. Mlango wa Kumi na Nne una mapitio 18.
16. Mlango wa Kumi na Tano una mapitio 2.
17. Mlango wa Kumi na Sita una mapitio 6.
18. Mlango wa Kumi na Nane una mapitio 2.
19. Mlango wa Kumi na Tisa una mapitio 84.
20. Mlango wa Ishirini una mapitio 47.
21. Mlango wa Ishiri na Moja una mapitio 3.

Na ukiingia na ukazama ndani ya hayo mapitio ndipo utakapoweza kuunganisha na kuona wapi penye udhaifu wa sahau na wapi ambapo sahau imepikuliwa na maandishi ambayo hata mwenye sahau utamuona anajikuta hajui au hakumbuki kitu. Wakati kweli nguvu za kukumbuka na kusahau zina uwezo wa kutupiga chenga, jee, maandishi ambayo ni "primary sources" ambayo yako karibu sana ki wakati na tukio lenyewe, hayana uzito wowote kwa gwiji wa fani ya habari na uandishi mtamu kama ndugu yetu Ahmed Rajab? Au tuseme hakuwa na wakati na alizisoma zaidi simulizi za wazee na ndio maana akaona udhaifu katika "methodology" ya uandishi wa “Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru?” Au alizilenga kurasa tatu tu kati ya kurasa 496?

Kuridhika nako kuna miko yake. Mtu anaweza akakubali lakini asiridhike na jawabu wala ushahidi. La msingi, kama nimekosea au nimedanganywa, kama ni muwongo au nimezuwa; Alhamdulilllah, uhai na uwezo wa wengine kuja na maelezo mbadala na yenye kusimama na hoja zenye ushahidi, bado upo. Suala: kwanini hawakosowi pale wanapoona pametiwa chumvi au pamepotoshwa kwa kulitimiza lengo la mwandishi au la watu fulani? Tumeweke wapi Salum Hamdan? Katika kundi la waliyoshuhudiya au katika kundi walioyasikiya tu na kumkabidhi mwandishi wa makala hii?

Naanza kuamini na kuridhika kuwa kuna tatizo kubwa zaidi hata kuliko kukukmbuka au kusahau. Kitabu cha “Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru,”  kimewashitusha, kimewaporomosha na kuwashusha daraja baadhi ya watu katika majivuno na majigambo waliyokuwa wakijivunia siku zote za Uwao. Kilichowashtuwa zaidi kuwa kimepokewa na kukubalika na hata wale ambao hawakubaliani nacho wameamuwa kukaa kimya.

Kimewashangaza kuona kimefikia kua kigezo cha ushahidi wa kusadikika na kukubalika Bungeni, hiyo ilikuwa fimbo. Walitamani angekuwa kiongozi au viongozi fulani kuipata sifa hiyo. Ahmed Rajab anashaka juu ya nini hali anajuwa kuwa niliyoelezwa yanatokana na mashahidi wa matukio hayo na washiriki wengine bado wahai na hadi leo hakuna aliyeyapinga maelezo yao. Vipi yeye awe na shaka nayo! Yeye na walio kama yeye hawaji na ushahidi au kitu kipya. Ni ushahidi wa kukosoa na kupanga hoja kwa kutumia kipaji cha uandishi na mantiki za kupinduwa hoja.

Katika mapambano baina ya kukumbuka na kusahau, kinachotakikana khasa ni ukombozi wa kiroho kwanza, na wa kiakili baadae, wa kila Mzanzibari, anaeishi ndani au nje ya Zanzibar na vizazi vyao. Ni ukombozi wenye kukubali, tena kwa hoja zenye kusimama juu ya ushahidi juu ya yale ambayo yamekuwa yakiogopwa kuzungumzwa hata kwa siri tena kwa zaidi ya nusu karne. Kinachotakikana ni uongozi mpya wa kizazi kipya ambacho kiko tayari kuinusuru Zanzibar kutokana na maradhi ya ukaidi na kujipambiya sifa ili kujitawadhisha na utawala.

Zanzibar imezungukwa na bahari ya ushahidi wa kuvamiwa kutoka kila upande wa roho na mwili wake lakini bado ina baadhi ya magenerali ambao wameamua kuingia kwenye vita vya kuinusuru huku wakiwa hawana hakika baina ya kuuandama “umimi” au kuyaweka juu kabisa maslahi ya Zanzibar na maslahi ya Wazanzibari ambao wengi wao ni watu wema na wanyonge.

Kizazi kipya hakikubali tena kudanganywa na kuingiliwa na mchwa wa miaka 51 iliopita. Kizazi kipya ni aina ya mbao mpya ambayo mchwa hawezi kuila. Mchwa aliebakiya Zanzibar na nje ya Zanzibar ni yule ambaye ameshaila fimbo ya Nabii Suleiman.

Na hadithi ya Musa ndani ya nyumba ya Firauni haijamalizikia na tukio la kihistoria liliomo ndani ya vitabu vitukufu vya Qur’an na Bibilia. Wakati hauko tena mbali Firauni wa Zanzibar akatoa shahada huku anazama.

Hapo ndipo suala la kukumbuka na kusahau litakapokuwa na maana mpya kwa Zanzibar Mpya na vizazi vyake – Ameen.  

Thursday 7 January 2016

Mwandishi na Dr. Harith Ghassany, Muscat Oman
 Utangulizi
Dr. Harith Ghassany ana ''sense of homour,'' kama wasemavyo Waingereza mbali ya kuwa msomi makini. Hata pale unapozungumzanae jambo zito kama la Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka wa 1964 na roho zilizoteketea atakutafutia jambo akuchekeshe. Ngoja nikupe mfano mmoja.

Tuko Kipumbwi Tanga katika fukwe ya Bahari ya Hindi tumetoka kuangalia zile sehemu ambazo mamluki wa Kimakonde kutoka mashamba ya mkonge ya Sakura walipokuwa wakivushwa kwa majahazi kwenda Unguja tayari kushiriki katika kuiangusha serikali ya Waziri Mkuu Mohamed Shamte.

Siku ile daktari alikuwa na furaha kubwa sana kwa kuwa kitendawili kikubwa katika historia ya mapinduzi kilikuwa kimeteguliwa. Hakuna mtafiti yeyote katika historia ya mapinduzi aliyewahi kufika pale. Tulikuwa tushamaliza kupiga picha na zingine za video. Ile video camera kanikabidhi mimi tulipokuwa pangoni huko ambako mamluki walikuwa wakijificha na kupanda majahazi kiza kiingia wakivushwa na Mohamed Omari Mkwawa au kwa jina lingine ''Tindo,'' (jina alilopewa na Mzee Karume), kwenda Unguja wamejivika mavazi kama wavuvi wa Kidigo. Basi mimi napiga picha huku nafanya, ''narration.'' Yeye ananitia moto kwa kunisifia ati nahadithia vizuri. Nami bichwa linavimba kwa kusifiwa na msomi wa Harvard.

Sasa tuko juu pwani na upepo wa bahari unatupiga. Dakari ananiuliza, ''Guy sasa katika kazi hii nikuandike wewe nini kazi yako katika utafiti huu?'' Mimi najua daktari ananitania kwa kuwa kazi yangu yeye anaijua sana. Mimi shughuli yangu kuu ilikuwa ni dereva, nikimuendesha. Nami kwa maskhara  na bila kufikiri nikamjibu, ''Mimi kazi yangu Guy ni ''Research Assistant.'' Kwa anaejua kazi hii katika utafiti atajua uzito wake.

Nimesahau ya Kipumbwi na yeye kesharudi Marekani nami nimebaki Tanga. Baada ya miaka kama miwili hivi 2010 kitabu kimechapwa. Ndani ya kitabu nakuta picha yangu na cheo changu, ''Mtafiti Msaidizi.'' Kila nikileta hii ''subject,'' kwake yeye anashikilia kuwa hiyo ndiyo ilikuwa kazi yangu na wala sikupatapo kuwa dereva wake. Mimi na yeye humaliza ubishi huu kwa vicheko na kwa kweli ''the joke is on me.'' 

Zanzibar 1950s

Huyu ndiye Dr. Harith Ghassany.
Sasa hebu msome hapo chini akilihadithia baibui la Abdulrahman Babu
na kinachonichekesha mie ni kule kufikiri zile sharubu za Babu ndani ya baibui
la ukaya:

Assalam Alaykum,

Inna Lillah wa Inna Ilayhi Raajiun - Mzee Ahmed Badawi Qullatein ametutangulia kunako haki.

Mara yangu ya kwanza kuonana na marehemu Mzee Badawi ilikuwa pale alipokuja Zanzibar kwa matembezi kutoka Dar es Salaam. Nilikwenda kuonana nae nyumbani kwake Malindi na ilikuwa tarehe 26 Julai 2005.

Ilibidi nimsubiri kidogo kwa sababu alikuwa anasoma Qur'an nyakati za asubuhi. Tulizungumza kiasi na alinikaribisha nikipata wasaa nende nikaonane nae kwake Dar es Salaam lakini sikujaaliwa.

Nilionana nae tena mara pili alipokuja Uroa na Bwana Ali Mohamed Yahya ambaye alikuwa ana tabia ya kumtembelea marehemu baba yangu. Nakumbuka vizuri marehemu Mzee Badawi kuniambia kuwa suluhisho la matatizo ya Waislam ni kuanzishwa kwa Dola ya Kiislam, na si jengine.

Tumebahatika wakati wa maombolezi ya kifo cha almarhum Mzee Badawi kupata maelezo ya mchango wake wa kisiasa kama ni kipande cha sehemu ya mwanzo wa maisha yake ya ujanani. Sheikh Salim Msoma ametueleza kuwa marehemu alifariki Makka wakati alipokwenda kufanya Hijja.

Ingelipendeza zaidi kama Salim Msoma angetueleza pia mabadiliko ya nafsi na ya kimtazamo ya marehemu Sayyid Ahmed Badawi alietokana na ukoo wa Masharifu, akawa mmoja wa waasisi wa "Marxist Umma Party of Zanzibar", na akafika kuipata bahati ya kufariki Makka wakati akiweko huko kwa ajili ya kufanya Hijja.

Salim Msoma ana uhuru wake lakini hakumtendea haki marehemu Mzee Badawi ambaye pia inasemekana aliomba "Tawbat Nasuha" kabla ya kufariki kwake dunia ambayo ndio kilele cha kujuta na kuomba maghfira kutoka kwa Muumba. Hilo ni jambo binafsi baina ya muumbwa na Muumba wake lakini linatuambia kitu sisi waja wake kuhusu hali ya marehemu Mzee Badawi kabla ya kurudi kwa Mola wetu sote. Wa Allahu Yaalam!

Sasa nakuja pale Salum Msoma alioitumia nafasi ya maombolezi ya kifo cha marehemu Mzee Badawi kutoa dukuduku lake juu ya kitabu cha Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru! Bado jini mkali wa historia anaendelea kuwasumbua baadhi ya Makomred na ndio maana hata marehemu Mzee Badawi aliefariki Makka akiwa na umri wa miaka 80 wanaona bora wamrudishe nyuma alipokuwa kijana mbichi kwenye umri wa miaka 30.
Hakuna kitu kilichowaudhi baadhi ya Makomred kama pale marehemu Mzee Aboud “Mmasai” aliposema na alivonukuliwa akisema “Tukaingia ndani, Migombani huku, buibui la Sauda akavaa Babu, sasa tunamwambia “wewe tukitoka uringeringe kidogo.” Dereva wa gari alikuwa Ali Saidi, taxi-driver, tulimchukuwa, kwa sababu yeye huyu alikuwa ni memba wa mapinduzi. Alikuwa ni mwenzetu. Tukampita asikari, akaingia ndani ya gari ile, tukatoka tukenda Kizingo. Kizingo Babake Fuko, mzazi, alikuwa na ngarawa na mwanawe mdogo Huseni, ndo akapakiwa Babu kupelekwa…kateremkia Mlingotini. Akateremshwa pale, sie tukarudi huku.”
Kabla ya Salim Msoma,  yuko Komred mwengine (jina nalihifadhi) ambaye tuliwasiliana mwaka jana na alinipa uoni wake juu ya kitabu cha Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru! kwa kusema “Ninachotaka kusisitiza hapa, bila ya kuigeuza barua hii pepe na kuwa insha, ni kwamba zipo hizo tofauti kati ya wenye kukumbuka” na akatoa mfano:
“Tofauti nyingine ya makumbusho niliyoiona ni katika maelezo ya jinsi Babu alivyokimbizwa kutoka Unguja.  Nijuavyo mimi hakuvalishwa buibui wala mke wa Marhemu Saleh Saadallah hajakuwako kwa Babu wakati wa yeye Babu kukimbizwa kama alivyohadithia Aboud Mmasai.  Waliokuwapo hapo walikuwa Saadallah, Twala, Ashura aliyekuwa mkewe Babu...”
Mwaka jana nilibahatika kupokea mualiko jijini Washington DC ambao wageni rasmi walikuwa ni Bibi Ashura na mumewe. Nikajiambia kuwa hii itakuwa fursa ya kuusikiliza upande wa pili wa shilingi na kujua kama maelezo ya kutoroshwa marehemu Abdulrahman Babu ya marehemu Mzee Aboud “Mmasai” yalikuwa sahihi au yanahitajia marekebisho. Bi Ashura hakutaka kuingia katika mazungumzo haya na mie nikayawacha.
Maelezo ya Salim Msoma yanapingana na yale ya marehemu Mzee Aboud “Mmasai” juu ya mahala alipotoroshwa Babu kupelekwa Dar es Salaam kwa msaada wa kina marehemu Saleh Saadalla na Abdulaziz Twala. Mzee Aboud anasema ilikuwa ni Kizingo, Salum Msoma anasema ilikuwa Fumba.
Sijui kwanini Salum Msoma akangojea mpaka Mzee Badawi akafariki dunia ndio hii leo akaamua kutuletea kumbukumbu muhimu kama hii. Jambo la kutia tamaa ni Msoma anasema kuwa mtu alioiendesha gari iliomchukua Babu na Badawi Fumba yuhai na anaishi Dar es Salaam.


Kulia: Abdulrahman Mohamed Babu na Abdallah Kassim Hanga
Sasa lilobaki ni kumuomba Bwana Msoma atuletee, hadharani au hata kwa pembeni, jina na maelezo ya dereva aliyempeleka marehemu Babu Fumba ili tuyahakiki maneno yake na yale ya marehemu mzee Aboud “Mmasai” tuweze kuiweka rekodi sawa katika toleo lijalo la kitabu cha Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru!
Muhimu katika maneno ya Bwana Msoma ni kukiri kwake kuwa marehemu Mzee Badawi alipewa taarifa ya mapinduzi na waandalizi wa mapinduzi ambao walikuwa kina marehemu Abdalla Kassim Hanga, Saleh Saadalla, na Abdulaziz Twala. Ameongeza kuwa Umma Party waliarifiwa kwanza hata kabla kuarifiwa marehemu Mzee Karume na viongozi wengine wa chama cha Afro-Shirazi.
Mungu amlaze mahala pema marehemu Mzee Ahmed Badawi Qullatein – Amin.


Dr. Harith Ghassany na Mzee Mohamed Omari Mkwawa wakati wa utafiti wa kitabu picha ilipigwa 2009 Tanga
Mwandishi picha kapiga Dr. Harith Ghassany na nyuma ni kijiji cha Kipumbwi Tanga