Thursday 7 January 2016

TUJIKUMBUSHE NYEPESI NYEPESI KATIKA MAPINDUZI YA ZANZIBAR KUTOKA KALAMU YA DR. HARITH GHASSANY

Mwandishi na Dr. Harith Ghassany, Muscat Oman
 Utangulizi
Dr. Harith Ghassany ana ''sense of homour,'' kama wasemavyo Waingereza mbali ya kuwa msomi makini. Hata pale unapozungumzanae jambo zito kama la Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka wa 1964 na roho zilizoteketea atakutafutia jambo akuchekeshe. Ngoja nikupe mfano mmoja.

Tuko Kipumbwi Tanga katika fukwe ya Bahari ya Hindi tumetoka kuangalia zile sehemu ambazo mamluki wa Kimakonde kutoka mashamba ya mkonge ya Sakura walipokuwa wakivushwa kwa majahazi kwenda Unguja tayari kushiriki katika kuiangusha serikali ya Waziri Mkuu Mohamed Shamte.

Siku ile daktari alikuwa na furaha kubwa sana kwa kuwa kitendawili kikubwa katika historia ya mapinduzi kilikuwa kimeteguliwa. Hakuna mtafiti yeyote katika historia ya mapinduzi aliyewahi kufika pale. Tulikuwa tushamaliza kupiga picha na zingine za video. Ile video camera kanikabidhi mimi tulipokuwa pangoni huko ambako mamluki walikuwa wakijificha na kupanda majahazi kiza kiingia wakivushwa na Mohamed Omari Mkwawa au kwa jina lingine ''Tindo,'' (jina alilopewa na Mzee Karume), kwenda Unguja wamejivika mavazi kama wavuvi wa Kidigo. Basi mimi napiga picha huku nafanya, ''narration.'' Yeye ananitia moto kwa kunisifia ati nahadithia vizuri. Nami bichwa linavimba kwa kusifiwa na msomi wa Harvard.

Sasa tuko juu pwani na upepo wa bahari unatupiga. Dakari ananiuliza, ''Guy sasa katika kazi hii nikuandike wewe nini kazi yako katika utafiti huu?'' Mimi najua daktari ananitania kwa kuwa kazi yangu yeye anaijua sana. Mimi shughuli yangu kuu ilikuwa ni dereva, nikimuendesha. Nami kwa maskhara  na bila kufikiri nikamjibu, ''Mimi kazi yangu Guy ni ''Research Assistant.'' Kwa anaejua kazi hii katika utafiti atajua uzito wake.

Nimesahau ya Kipumbwi na yeye kesharudi Marekani nami nimebaki Tanga. Baada ya miaka kama miwili hivi 2010 kitabu kimechapwa. Ndani ya kitabu nakuta picha yangu na cheo changu, ''Mtafiti Msaidizi.'' Kila nikileta hii ''subject,'' kwake yeye anashikilia kuwa hiyo ndiyo ilikuwa kazi yangu na wala sikupatapo kuwa dereva wake. Mimi na yeye humaliza ubishi huu kwa vicheko na kwa kweli ''the joke is on me.'' 

Zanzibar 1950s

Huyu ndiye Dr. Harith Ghassany.
Sasa hebu msome hapo chini akilihadithia baibui la Abdulrahman Babu
na kinachonichekesha mie ni kule kufikiri zile sharubu za Babu ndani ya baibui
la ukaya:

Assalam Alaykum,

Inna Lillah wa Inna Ilayhi Raajiun - Mzee Ahmed Badawi Qullatein ametutangulia kunako haki.

Mara yangu ya kwanza kuonana na marehemu Mzee Badawi ilikuwa pale alipokuja Zanzibar kwa matembezi kutoka Dar es Salaam. Nilikwenda kuonana nae nyumbani kwake Malindi na ilikuwa tarehe 26 Julai 2005.

Ilibidi nimsubiri kidogo kwa sababu alikuwa anasoma Qur'an nyakati za asubuhi. Tulizungumza kiasi na alinikaribisha nikipata wasaa nende nikaonane nae kwake Dar es Salaam lakini sikujaaliwa.

Nilionana nae tena mara pili alipokuja Uroa na Bwana Ali Mohamed Yahya ambaye alikuwa ana tabia ya kumtembelea marehemu baba yangu. Nakumbuka vizuri marehemu Mzee Badawi kuniambia kuwa suluhisho la matatizo ya Waislam ni kuanzishwa kwa Dola ya Kiislam, na si jengine.

Tumebahatika wakati wa maombolezi ya kifo cha almarhum Mzee Badawi kupata maelezo ya mchango wake wa kisiasa kama ni kipande cha sehemu ya mwanzo wa maisha yake ya ujanani. Sheikh Salim Msoma ametueleza kuwa marehemu alifariki Makka wakati alipokwenda kufanya Hijja.

Ingelipendeza zaidi kama Salim Msoma angetueleza pia mabadiliko ya nafsi na ya kimtazamo ya marehemu Sayyid Ahmed Badawi alietokana na ukoo wa Masharifu, akawa mmoja wa waasisi wa "Marxist Umma Party of Zanzibar", na akafika kuipata bahati ya kufariki Makka wakati akiweko huko kwa ajili ya kufanya Hijja.

Salim Msoma ana uhuru wake lakini hakumtendea haki marehemu Mzee Badawi ambaye pia inasemekana aliomba "Tawbat Nasuha" kabla ya kufariki kwake dunia ambayo ndio kilele cha kujuta na kuomba maghfira kutoka kwa Muumba. Hilo ni jambo binafsi baina ya muumbwa na Muumba wake lakini linatuambia kitu sisi waja wake kuhusu hali ya marehemu Mzee Badawi kabla ya kurudi kwa Mola wetu sote. Wa Allahu Yaalam!

Sasa nakuja pale Salum Msoma alioitumia nafasi ya maombolezi ya kifo cha marehemu Mzee Badawi kutoa dukuduku lake juu ya kitabu cha Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru! Bado jini mkali wa historia anaendelea kuwasumbua baadhi ya Makomred na ndio maana hata marehemu Mzee Badawi aliefariki Makka akiwa na umri wa miaka 80 wanaona bora wamrudishe nyuma alipokuwa kijana mbichi kwenye umri wa miaka 30.
Hakuna kitu kilichowaudhi baadhi ya Makomred kama pale marehemu Mzee Aboud “Mmasai” aliposema na alivonukuliwa akisema “Tukaingia ndani, Migombani huku, buibui la Sauda akavaa Babu, sasa tunamwambia “wewe tukitoka uringeringe kidogo.” Dereva wa gari alikuwa Ali Saidi, taxi-driver, tulimchukuwa, kwa sababu yeye huyu alikuwa ni memba wa mapinduzi. Alikuwa ni mwenzetu. Tukampita asikari, akaingia ndani ya gari ile, tukatoka tukenda Kizingo. Kizingo Babake Fuko, mzazi, alikuwa na ngarawa na mwanawe mdogo Huseni, ndo akapakiwa Babu kupelekwa…kateremkia Mlingotini. Akateremshwa pale, sie tukarudi huku.”
Kabla ya Salim Msoma,  yuko Komred mwengine (jina nalihifadhi) ambaye tuliwasiliana mwaka jana na alinipa uoni wake juu ya kitabu cha Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru! kwa kusema “Ninachotaka kusisitiza hapa, bila ya kuigeuza barua hii pepe na kuwa insha, ni kwamba zipo hizo tofauti kati ya wenye kukumbuka” na akatoa mfano:
“Tofauti nyingine ya makumbusho niliyoiona ni katika maelezo ya jinsi Babu alivyokimbizwa kutoka Unguja.  Nijuavyo mimi hakuvalishwa buibui wala mke wa Marhemu Saleh Saadallah hajakuwako kwa Babu wakati wa yeye Babu kukimbizwa kama alivyohadithia Aboud Mmasai.  Waliokuwapo hapo walikuwa Saadallah, Twala, Ashura aliyekuwa mkewe Babu...”
Mwaka jana nilibahatika kupokea mualiko jijini Washington DC ambao wageni rasmi walikuwa ni Bibi Ashura na mumewe. Nikajiambia kuwa hii itakuwa fursa ya kuusikiliza upande wa pili wa shilingi na kujua kama maelezo ya kutoroshwa marehemu Abdulrahman Babu ya marehemu Mzee Aboud “Mmasai” yalikuwa sahihi au yanahitajia marekebisho. Bi Ashura hakutaka kuingia katika mazungumzo haya na mie nikayawacha.
Maelezo ya Salim Msoma yanapingana na yale ya marehemu Mzee Aboud “Mmasai” juu ya mahala alipotoroshwa Babu kupelekwa Dar es Salaam kwa msaada wa kina marehemu Saleh Saadalla na Abdulaziz Twala. Mzee Aboud anasema ilikuwa ni Kizingo, Salum Msoma anasema ilikuwa Fumba.
Sijui kwanini Salum Msoma akangojea mpaka Mzee Badawi akafariki dunia ndio hii leo akaamua kutuletea kumbukumbu muhimu kama hii. Jambo la kutia tamaa ni Msoma anasema kuwa mtu alioiendesha gari iliomchukua Babu na Badawi Fumba yuhai na anaishi Dar es Salaam.


Kulia: Abdulrahman Mohamed Babu na Abdallah Kassim Hanga
Sasa lilobaki ni kumuomba Bwana Msoma atuletee, hadharani au hata kwa pembeni, jina na maelezo ya dereva aliyempeleka marehemu Babu Fumba ili tuyahakiki maneno yake na yale ya marehemu mzee Aboud “Mmasai” tuweze kuiweka rekodi sawa katika toleo lijalo la kitabu cha Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru!
Muhimu katika maneno ya Bwana Msoma ni kukiri kwake kuwa marehemu Mzee Badawi alipewa taarifa ya mapinduzi na waandalizi wa mapinduzi ambao walikuwa kina marehemu Abdalla Kassim Hanga, Saleh Saadalla, na Abdulaziz Twala. Ameongeza kuwa Umma Party waliarifiwa kwanza hata kabla kuarifiwa marehemu Mzee Karume na viongozi wengine wa chama cha Afro-Shirazi.
Mungu amlaze mahala pema marehemu Mzee Ahmed Badawi Qullatein – Amin.


Dr. Harith Ghassany na Mzee Mohamed Omari Mkwawa wakati wa utafiti wa kitabu picha ilipigwa 2009 Tanga
Mwandishi picha kapiga Dr. Harith Ghassany na nyuma ni kijiji cha Kipumbwi Tanga

No comments: