UDHALILISHWAJI
WA WAISLAM NA VYOMBO VYA DOLA VYA TANZANIA
Mkasa
Wangu wa Kukamatwa Uwanja wa Ndege wa Mwl.
Nyerere, Dar es Salaam Mwaka 2006
Mohamed Said
![]() |
| Mwandishi akiwa katika studio za Radio Tehran Iran kulia kwake ni Ahmed Rashid na kushoto Abdufatah Mussa |
![]() |
| Wapenzi wa CUF wakienda mkutanoni wakati wa Uchaguzi Mkuu |
| Mwandishi na Watangazaji wa Radio Tehran |
| Mwandishi akiwa mkutanoni Tehran |
![]() |
| Mwandishi akifanya mahojiano na Mtangazaji Abdufatah Mussa Radio Tehran Iran |
Mambo yalianza wakati sasa narudi Dar es Salaam na
ndege ya Emirates iliyokuwa inatua usiku. Inaelekea maofisa wa pasi pale
uwanjani walikuwa na taarifa zangu mapema na walikuwa wakinisubiri kwa hamu
kubwa kwani nilipotoa pasi yangu kwa afisa wa pasi hapo ndipo shughuli za
kunishughulikia zilipoaanza. Mimi sikuwa na hili wala lile. Nikawa namuona yule
dada aliyekuwa kwenye kile kizimba akikukurika na pasi yangu akiitia katika
mashine na kuitoa mara kadhaa. Fikra iliyonijia kwa haraka ilikuwa mashine ni
mbovu na harakati zile zilikuwa ni kurekebisha mitambo. Kumbe sivyo wahusika
nadhani walikuwa wanahakikisha kuwa mimi ndiyo huyo waliokuwa wakimwinda na
kumsubiri na sasa kapatikana, kaingia mwenyewe kwenye mtego na kanasa. Yule
afisa wa pasi akanambia nikae pembeni natakiwa kwa mahojiano na watu wa
usalama. Hofu haikuwa imeniingia kwa kuwa nilikuwa natambua kuwa harakati dhidi
ya ugaidi zilikuwa zimepamba moto na labda nilitakiwa kwa mahojiano mafupi
kutaka kujua nyendo zangu. Sikujua wala kutarajia kuwa mshtuko mkubwa ulikuwa
unanisubiri.
Nilichukuliwa hadi kwenye chumba kimoja na hapo
niliwakuta maofisa wa usalama watatu wakanikaribisha kwa taadhima kisha
wakanambia kuwa niko chini ya ulinzi kwa kuwa zimewafikia taarifa zangu kuwa
mimi nasafirisha mihadarati. Mpaka hapa sikuwa na hofu bado ilinijia picha kuwa
yawezekana wamefananisha majina. Niliwaambia huenda Mohamed Said muuza madawa
ya kulevya siyo mimi niliye mbele yao. Wakaniambia kwa kujiamini kabisa kuwa
taarifa zao ni madhubuti muuza unga ni mimi na wamekuwa wakinifuatilia siku
nyingi. Hapo ndipo walipotoa pasi yangu
na kuniomba niitambue kama hiyo pasi ni yangu au la. Niliwajibu kuwa hakika
hiyo ndiyo pasi yangu khasa. Wakaniamuru sasa tutoke twende nikachukue mizigo
yangu ili wafanye upekuzi wa mihadarati katika mizigo niliyotokanayo Tehran.
Hapo ndipo nilipojuwa kuwa niko katika lindi kubwa la matatizo na ubongo wangu
ukaanza kufanya kazi kwa haraka huku nikisoma dua kumuomba Allah ulinzi wake
kwani kwa hakika nilijua kama ni njama zimekamilika na leo imefika siku yangu.
Nikajiuliza itakuwaje watakapotoa madawa kwenye mizigo yangu. Nikaanza kufikiri
vichwa vya habari vya magazeti yatakavyopambwa na habari zangu. Ikanijia yakini
kuwa watu wa usalama wameniwekea madawa ya kulevya katika mizigo yangu ili
waniangamize na maadui zangu wapumzike na shari yangu.
Nilimgeukia yule ofisa mkuu aliyekuwa ananihoji
nikamwambia kuwa sitokubali kugusa mizigo yangu bila kuwapo mashahidi isijekuwa
mizigo yangu ishawekewa hayo madawa ya kulevya kwani nilikotoka Tehran mizigo
ilikuwa imekaguliwa na ilikuwa salama. Hoja yangu kubwa kwao ilikuwa kupata
uhakika kutoka kwao kuwa wananijua vizuri kiasi cha kuthibitisha kuwa kweli mie
ni msafirishaji wa madawa ya kulevya. Jibu nililopewa ni kuwa wao wanafanya
kazi kutokana na taarifa zilizowafikia. Wakasema, “Sisi tunazo taarifa zako
kamili kuwa wewe ni msafirisha madawa ya kulevya.” Nikawauiza,“Baada ya
kupata taarifa hizo zangu nyie mmechunguza kutafuta ukweli?” Wakasema, “Ndiyo
maana leo tumekukamata.” Nikawaambia, “Si kweli kama kwa sababu mie nafahamika
Dar es Salaam takriban kwingi maana ndio nilikozaliwa na kukulia. Hapo Kariakoo
ukiwaambia watu kuwa Mohamed ni “Mzungu wa Unga” kila mtu atacheka maana huo
kwao ndugu zangu ni mzaha mbaya.” Walitaka kujua nilkwenda kufanya nini Iran.
Niliwaambia nilialikwa na serikali ya huko kuhudhuria mkutano. Wakataka kujua
vipi nilipata mwaliko. Nikawajibu kuwa hilo swali sina jibu labda waiulize
serikali ya Iran. Nikawaeleza kuwa mbona siku zote napita hapo uwanjani nikenda
sehemu tofauti duniani kwa mialiko na kutoa mada sijakamatwa kimezidi nini
katika hii safari ya Iran? Niliwaeleza kuwa miezi michache iliyopita nilikuwa Chuo Kikuu Cha Ibadan kwa
mwaliko tena mkutano umefadhiliwa na serikali ya Marekani na
wamenipa na tiketi toka Dar es
Salaam hadi Lagos na kuniweka hoteli na kunilipa fedha. “Mbona
hamkunikamata wakati ule?” Nikafungua mlango mwingine nikawaambia, “Nakuapieni
nyie msingethubutu kumkamata Mkristo anaetoka Vatican mkutanoni. Lakini kwa kuwa mie ni
Muislam sina wa kunitetea. Nchi hii nani atakuuliza kwa
kumnyanyasa Muislam?” Walishtuka na wakawa wanyonge sana wakasema si kweli
kuwa naponzwa na dini yangu.
Baada ya kukurukakara nyingi na mabishano makubwa
kuhusu mie kukubali kufanyiwa upekuzi wa mizigo yangu alikuja binti mmoja
katika wao na yeye akanihakikishia kuwa wao ni serikali na sio wahuni.
Hawathubutu kuniwekea dawa katika mizigo yangu hivyo akanisihi sana kwa upole
nikubali ili wajitoe wasiwasi na wataniachia endapo hakuna kitu. Niliomba
apatikane shahidi wa kushuhudia mizigo yangu kabla ya kufanyiwa upekuzi lakini
hakuna mtu aliyekubali kuchukua dhima ile katika maofisa waliokuwa kazini pale
uwanja wa ndege usiku ule. Upekuzi ukafanyika hadi mwilini. Hakuna kitu.
Wakanipela katika choo maalum cha kutolea madawa kwa njia ya haja kubwa.
Nikakataa kujisaidia pale. Ilikuwa ndio mara yangu ya kwanza kuona choo kama
kile. Choo chenyewe ni cha aluminium. Tofauti na vyoo vya pale ambavyo siku
zote ni vichafu, hiki kilikuwa kisafi sana kiasi mtu unaweza hata kutengewa
chakula na akala bila ya kuhisi kinyaa.
Nilitegemea wataweka ahadi yao kuwa ikiwa
hawatakuta madawa ya kulevya katika mizigo yangu watanirejeshea uhuru wangu
wataniachia niende nyumbani. Haikuwa hivyo. Wakanirudisha ofisini kwao. Sasa
wakaacha madawa ya kulevya wakahamia katika vitabu na “audio cassette”
nilizokuwa nimepewa kama zawadi kule Tehran wakaniluliza kwa nini naingiza vitu
vile khasa kanda za Khomeni na vitabu vyake nchini. Nikawauliza, “Kwani kanda
na vitabu vya Khomeni haviruhusiwi kuingizwa Tanzania? Maana mimi hata nyumbani
kwangu hii leo mkifika nina vitabu vya Khomeni na wanafalsafa wengine kama Karl
Marx ambao nimesomeshwa pale Chuo Kikuu Cha Dar
es Salaam. Sasa hapo ikaja kejeli. “Ala wewe mtu wa Kariakoo lakini
umefika hadi Chuo Kikuu!” Sikujibu kitu. Awali waliponitia mbarani
waliniuliza kwetu na nikawaeleza kuwa
nimezaliwa Kariakoo.
Hawakunipa jibu kuhusu kuingiza vitabu na cassette
za Khomeni. Ikawa sasa kama vile wameishiwa maswali. Nikaona kuwa sasa ni zamu
yangu nami kuwapiga maswali.
Yule aliekuwa akinihoji
nikamwambia, “Mimi wewe nakufahamu vizuri sana kwa sababu ukicheza mpira Simba
Sports Club na mie ni mpenzi wa club hiyo toka utoto wangu wakati huo
ikiitwa Sunderland na mmoja wa baba zangu alikuwa mchezaji marufu wa club hiyo
katika miaka ya 1950 akafiikia hadi kucheza Kombe la Gossage.” Nilihisi amepata
mfadhaiko kidogo akanambia,“Unanifananisha yule aliekuwa akicheza Simba ni
ndugu yangu.” Alikuwa anasema uongo lakini mie nikamkubalia. Hapo nikajua kuwa
nishampata sasa hana nguvu tena ya kuuliza maswali. Kusema uongo ni dalili ya
kujihami. Nikamrushia kombora lingine, “Sasa tuhuma za madawa ya kulevya
zimekwisha tuko katika kwa nini naingiza vitabu vya Khomeni nchini?”
Akanijibu kinyonge, “Tumeridhika huna madawa.”
Kufika hapa tukawa tumemaliza
mahojiano.
Wakati huo sasa ni usiku wa manane na nishapeleka
SMS kwa sahib yangu mmoja bingwa wa mambo ya mtandao wa kompyuta kumjulisha
kuwa nimekamatwa uwanja wa ndege kwa tuhuma za uongo za kuvusha mihadarati na
yeye ile kuipata tu ule ujumbe wangu akaifahamisha dunia kuwa nimekamatwa
uwanja wa ndege nikitokea mkutanoni Iran na nimebambikiziwa tuhuma za kuingiza
nchini mihadarati. Waliponitia mbaroni tu walinionya kuhusu kutumia simu yangu
ya mkononi lakini bahati nzuri hawakuninya’ganya. Aliyenipa onyo hili alikuwa
mkuu wa kituo cha polisi cha uwanja wa ndege. Huyu rafiki yangu akawa
kanisaidia sana maana hadi kumekucha wapenzi wangu wote ndani na nje ya nchi
pamoja na vyombo vya habari vinavyonifahamu walikuwa na taarifa za kukamatwa kwangu.
(Kwa kipindi takriban miaka ishirini nyuma kwa nyakati fofauti nimekuwa nifanya
mahojiano na radio zote muhimu kama, BBC, VOA, Sauti ya Ujerumani, Sauti ya
Iran nk.).
Nikawaomba
wale watu wa Usalama waniachie basi nende zangu kulala nyumbani nirudi hapo
kesho asubuhi kwa kuwa sikuwa nimebeba madawa ya kulevya. Wakaniambia, “Itabidi
tukulaze hapa hadi asubuhi wakubwa wetu watupe amri ya kukuachia. Maana amri ya kukukamata wewe imetoka juu.”
| Mwandishi Akiwa KAtika Studio za Radio Iran Tehran Idhaa ya Kiswahili |




No comments:
Post a Comment