MAONI
YA WAISLAM KUHUSU MUSWADA WA WRITTEN LAWS
(MISCELLANEOUS
AMENDMENT)(NO. 2) ACT, 2014
…………………………………………………………
UTANGULIZI:
Kama taasisi ya Kiislam
tumepitia muswada wa Written Laws (Miscellaneous Amendment)(No. 2) Act wa
2014 na malengo ya kuletwa kwake. Hapana shaka kwamba kwa
kuwa sisi ni sehemu ya watanzania, na yote yaliyomo katika muswada huo
yanatuhusu. Hata hivyo, kama asasi ya kidini, hususan ya Kiislam, tunaona kuwa
tunahusika zaidi na Sehemu ya V ya muswada huo ambayo inahusu mapendekezo ya
marekebisho ya Sheria ya Islamic Law (Restatement Act), Sura ya 375 ya
Mapitio ya 2002. Hivyo basi, tutatolea
maoni eneo hilo la muswada huu.
SEHEMU YA KWANZA - MAELEZO YA JUMLA:
La kwanza tunapata
faraja kuona kuwa hatimaye imefika wakati Serikali imetambua ukweli kuwa
upo ulazima wa kupitishwa kwa sheria ya Mahakama za Kadhi hapa nchini. Hii
ni hatua ndogo lakini muhimu katika safari ya kuelekea kujibu kiu ya Waislamu
ya muda mrefu kutaka kuhukumiwa kwa mujibu wa Sheria inayoafikiana na
mtazamo na imani yao katika masuala yanayohusu familia na hadhi binafsi kwa
mujibu wa imani, mila na desturi zetu kama Waislamu.
Haja na kiu hii inatokana
na mambo matatu makubwa: -
- Mosi, kuwa Uislam una
mfumo wake kamili wa utoaji haki wenye sheria, misingi na taratibu zake. Kuchukua sheria peke yake na kuacha misingi na taratibu zake
kumepelekea sheria za Kiislamu kutumika visivyo na hivyo kupelekea kupotosha
haki,
- Pili, Mfumo wa sasa
unatoa nafasi kwa maafisa wa mahakama kama majaji na mahakimu kuhukumu
masuala ya sheria ya Kiislamu ambapo mara nyingi maafisa hao
hawana sifa, ujuzi na uzoefu wa kushika nafasi ya kuhukumu chini ya
utaratibu wa Kiislamu. Moja ya kigezo muhimu ni majaji na mahakimu
kuruhusiwa kuhukumu masuala ya sheria ya Kiislamu bila kuwa mejifunza
sheria ya Kiislamu na nidhamu ya uhakimu, na
- Tatu, licha ya maafisa
wa mahakama zetu kuwa hawajafunzwa sheria, misingi na taratibu za
sheria za Kiislamu, lakini pia, wengi wao wamethibitika
kutoridhika na kufuata ipasavyo Sheria za Kiislamu katika kusikiliza na kuamua
mashauri ya Sheria ya Kislamu mpaka wengine hata kufikia kupotosha kwa
makusudi kanuni na misingi ya sheria za Kiislamu. Ipo mifano mingi
inayothibitisha hili.
- Kutokana na hali hiyo Waislamu wamekuwa wakidai kurudishwa kwa mfumo wa utoaji haki wa
Kiislamu katika masuala ya familia na hadhi binafsi kama vile ndoa,
talaka, matunzo ya mke, matunzo ya watoto, uzazi wa watoto, ulezi na
usimamizi wa watoto, wosia, mirathi na wakfu. Serikali imekuwa ikikwepa suala
hili kwa sababu mbalimbali zisizo waridhisha Waislamu.
Kwa hiyo ni faraja kuwa
leo Serikali walau imefikia kutoa muswada huu unaohusu makahama za kadhi hapa
nchini. Hata hivyo, ingawa
tunafarijika kuona kuwa hatimaye Serikali inakiri umuhimu wa kuwepo kwa Mahakama ya
kadhi inayotambuliwa na sheria za nchi, muswada huu una makosa, kasoro na
udhaifu mwingi kiasi cha kutia shaka juu ya uthabiti wa nia ya Serikali wa kutaka
kuleta sheria itakayowezesha mfumo wa utoaji haki wa Kiislamu kufanya kazi
hapa nchini. Mfumo huu hautaweza kufanya kazi kwa ufanisi. Pia uhalali wa
maamuzi yake utakuwa na shaka kubwa. Vilevile, utaleta migogoro, migongano na
matatizo mengi baina ya makundi na asasi za Kiislamu.
Tutataja hapa chini
makosa, kasoro na upungufu huo katika Sehemu ya Pili hapa chini. Badala yake,
tunapendekeza kuwa marekebisho muhimu yafanywe katika muswada ili kuwezesha kupatikana kwa sheria ya mfumo wa utoaji haki wa Kiislamu unaoafikiana na
mtizamo wa Waislamu na unaokidhi mahitajio ya kimuundo, kitaratibu na
kiutendaji.
SEHEMU YA PILI: MAKOSA,
KASORO NA UPUNGUFU WA MUSWADA:
1. MUSWADA HAUNA KIFUNGU
CHA UANZISHAJI WA MAHAKAMA YA
KADHI:
1.1 HOJA:
Sheria yoyote inayotaka
kuweka utaratibu wa kufanya kazi kwa mahakama Fulani, ni lazima iwe na kifungu
kinachotamka kuwepo kwa mahakama hiyo. Vinginevyo, kama kusudio ni kutambua
mahakama iliyopo, basi hakuna budi kiwepo kifungu kinachotoa tamko la
kutambua kuwepo huko kwa mahakama hiyo. Muswada unaopendekezwa
hauna tamko la kuanzisha au kuweka Mahakama ya kadhi wala tamko la
kutambua kuwepo kwa Mahakama ya Kadhi. Lakini, haitokuwa sawa
kutoa tamko la kutambua kuwepo kwa Mahakama ya Kadhi hapa nchini ilhali
hakuna mahakama hiyo ambayo tayari imeanzishwa kwa utaratibu unaotambuliwa
na sheria.
Ingewezekana tu kutambua
kuwepo kwa mahakama ya kadhi kama Waislamu wa Tanzania kupitia jumuiya
na taasisi zao zote za kitaifa wangekubaliana na kuanzisha mahakama hiyo.
Makubaliano hayo hayapo. Ikiwa Serikali itambua
kuwepo kwa mahakama ya kadhi iliyoanzishwa na BAKWATA kwa sasa,
itakuwa ni sawa na kuitambua BAKWATA kuwa ndicho chombo halali cha
kuwawekea Waislamu mahakama ya kadhi jambo ambalo linapingwa na sehemu
kubwa ya Waislamu na taasisi nyingi za Waislamu. Kuipa BAKWATA nafasi ya
kuwawekea Waislamu Mahakama ya Kadhi kutahesabiwa na waislamu
kuwa ni hila ya Serikali kutaka kulazimisha mamlaka ya BAKWATA juu ya
Waislamu hata wale wasioikubali taasisi hiyo. Jambo ambalo litakuwa
limekiuka haki ya msingi ya kila Mtanzania kujumuika kwa uhuru bila kutenzwa
nguvu au kushinikizwa.Uhalali wa BAKWATA kuwa ndicho chombo kikuu cha uongozi
wa waislamu nchini umehojiwa na Waislamu mara nyingi. Na hata BAKWATA
yenyewe imetoa matamko mara kadhaa kuwa si chombo cha Waislamu
wote. Ni ukweli uliowazi kuwa
makadhi waliotangazwa na BAKWATA si makadhi halali kwa kuwa:-
- Wametangazwa kinyume
na matakwa ya Waislamu walio wengi, - BAKWATA imetangaza
makadhi wake kwa kukiuka utaratibu uliokuwa umekubaliwa na makundi
mengi ya Waislamu wa majadiliano baina ya Serikali na Waislamu kwa
kujitangazia makadhi peke yake na kusababisha kuvunjika
kwa mchakato huo, - Serikali imearifiwa na
wajumbe wa Jopo la Masheikh lililokuwa likijadiliana na
Serikali wasiokuwa wajumbe kutoka BAKWATA kuwa BAKWATA imekiuka
utaratibu na hivyo kutaka mchakato wa majadiliano uendelee
lakini Serikali imepuuza.
Kwa maana hiyo basi,
njia pekee ya kuweka chombo muhimu kama Mahakama ya Kadhi itakuwa ni kwa
kupata ridhaa ya taasisi zote kubwa za Kiislamu nchini kwa maafikiano yao ya pamoja
kama itakavyopendekezwa hapa chini. Hivyo basi, muswada huu
una upungufu mkubwa kwa kukosa tamko la kuweka au kuanzisha au kutambua
kuwepo kwa mahakama ya kadhi kwanza kabla ya kuanza kuipangia taratibu za
utendaji. Kosa hili litapelekea
mwenendo, maamuzi, hukumu na amri za mahakama hiyo kuwa batili kwa kuwa
kimsingi yatakuwa yamefanywa na chombo kisichotambulika
kisheria.
Iwapo atajitokeza mtu
yeyote kupeleka malalamiko katika Mahakama Kuu ya Tanzania kutaka mapitio
ya mwenendo, maamuzi, hukumu na amri za Mahakama ya Kadhi, Mahakama Kuu
itabatilisha mwenendo, maamuzi, hukumu na amri hizo kwa kutolewa na chombo
kisichotambuliwa na sheria.
Kutokana na hayo,
muswada huu haukidhi haja na matakwa ya kisheria na kitaratibu ya kuwepo kwa
mahakama ya kadhi kama chombo cha kimahakama hapa nchini.
1.2 MAPENDEKEZO YETU:
i) Tunapendekeza kuwa
kwa kuwa mahakama ya kadhi haipo kisheria, sheria iwe na tamko la kuanzishwa
kwa mahakama ya kadhi hapa nchini.
2. MUSWADA HAUWEKI
MUUNDO WA MAHAKAMA INAYOKUSUDIWA:
2.1 HOJA:
Mahakama ni lazima iwe
na muundo. Ijulikane mahakama hiyo ina ngazi zipi, ngazi yake ya chini ni
ipi, kama kuna ngazi ya kati, na ngazi yake ya mwisho juu.
Inapasa pia ijulikane
mashauri gani yanaanzia katika ngazi ya mwanzo chini na yapi mengine katika
ngazi nyingine za juu. Pia muundo wake wa kijiografia unapasa ujulikane. Haya ni masuala muhimu
sana kwa kuwepo kwa mahakama madhubuti inayoweza kukidhi haja za mfumo
thabiti wa utoaji wa haki. Kinyume cha hivyo, mahakama hiyo itakuwa ni dhihaka
katika utoaji haki na itapelekea migogogoro na migongano katika utendaji wake.
2.2 MAPENDEKEZO YETU:
Sheria iweke muundo wa
mahakama inayokusudiwa. Kwa kuwa muundo wa mahakama ni jambo nyeti
linaloamua pia masuala ya mamlaka (jurisdiction), ni lazima uwekwe na sheria
mama, sio na kanuni zitakazowekwa chini ya sheria hiyo. Tuna pendekeza sheria
iweke mfumo wa mahakama ya Kdhi yenye ngazi tatu kama ifuatavyo:
- Mahakama ya Kadhi ya
Eneo (local Kadhi’s Court) itakayokuwa katika kila Kata
- Mahakama ya Kadhi ya
Wilaya (District Kadhi’s Court) itakayokuwa katika kila Wilaya
- Na Mahakama ya Kadhi
Mkuu(Chief Kadhi’s Court) itakayokuwa ndiyo
mahakama ya juu kabisa.
Hii itakuwa na Kadhi Mkuu (Chief Kadhi) na
makadhi waandamizi
(Principal Kadhis) wane.
3. MUSWADA KUTOELEZA
SIFA ZA KADHI:
3.1 HOJA:
Muswada huu umeacha
mwanya kwa wasio kuwa na sifa kuteuliwa kuhudumu katika Mahakama za
Kadhi. Haiyumkini watu muhimu wenye mamlaka ya kutoa haki wakateuliwa bila ya
sheria kutaja sifa stahiki za wanaofaa kuchukua jukumu hilo na utaratibu wa
kuwapata watu hao. Hili lazima lielezwe na sheria yenyewe inayounda Mahakama ya
Kadhi au kanuni zitakazoundwa chini ya sheria hiyo na chombo chenye kuaminika
na wananchi wote watakao tumia huduma ya Mahakama hiyo.
3.2 MAPENDEKEZO YETU:
Muswada utaje sifa za
makadhi wa daraja mbalimbali na vigezo vya kuhudumu katika mahakama za kadhi
za ngazi mbalimbali.
4. MASUALA YA UTEUZI WA
MAKADHI:
4.1 HOJA:
Muswada unaeleza kuwa
makadhi watateuliwa na “Mufti”. Hili lina kasoro nyingi zitakazoleta matatizo
mengi. Baadhi ya kasoro ni hizi:
4.1.1 Mufti
i) Kwanza muswada
unataja afisa aitwaye Mufti lakini hauelezi huyo Mufti ni nani na anapatikana vipi. Ni
vyema Serikali ikatahadharishwa kuwa zipo taasisi nyingi za Kiislamu
zilizoandikishwa na mamlaka mbalimbali za uandikishaji wa asasi huru na vyama vya
kijamii (NGOs) zenye maafisa wenye cheo cha Mufti.
Baadhi ya asasi hizo ni
–
(a) Baraza Kuu la
Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania (BARAZA KUU),
(b)Umoja wa Wanazuoni wa
Kiislamu Tanzania (Hay-at), na
(c) Barza Kuu la Waislam
wa Tanzania (BAKWATA).
Kwa hivyo kama sheria
haikuweka wazi Mufti ni afisa gani na anapatikana vipi kunaweza kutokea
mgongano na mgogoro mkubwa kwa kila asasi kutaka kutumia Mufti wake kuteua
makadhi.
ii) Pili, si busara
kuweka suala zito kama la uteuzi wa maafisa wa mahakama watakaokuwa na wajibu na
dhima ya kutoa haki mikononi mwa mtu mmoja ambaye hata namna
anavyopatikana haijulikani. Pia, huyu hachaguliwi na ummah wa Waislamu wote kama
vile anavyochaguliwa Rais wa Jamhuri na wananchi wote wa Tanzania. Licha
ya kuchaguliwa kwake na wananchi wote, bado
mapendekezo mengi
yametolewa kuwa Rais apunguziwe madaraka ya uteuzi ukiwemo uteuzi wa
majaji. Kwa hivyo hili ni jambo
lisilokubalika. Utaona kuwa katika maoni
na mapendekezo yote yaliyotolewa na taasisi mbalimbali za Kiislamu
juu ya mfumo wa uteuzi wa makadhi, zote zimependekeza kuwepo na baraza, jopo,
bodi au chombo cha namna moja au nyingine kitakachokuwa ndiyo
mamlaka ya kuteua makadhi. Hakuna hata taasisi moja iliyopendekeza kuwa
uteuzi ufanywe na mtu mmoja, kwa cheo, hadhi au daraja yoyote aliyonayo. Kwa hiyo suala la uteuzi
kuweka mikononi mwa mtu mmoja halikubaliki kwa sababu linatoa mwanya wa
nafasi hiyo kutumika vibaya.
iii) Tatu, kuweka
mamlaka ya uteuzi wa makadhi kwa afisa aitwaye Mufti hakukubaliani na
utaratibu wa mfumo wa uongozi wa Kiislam. Kilugha, istilahi
“mufti” maana yake ni alim mwenye upeo mkubwa wa elimu ya dini na sheria. Ni mtu
aliyebobea katika taaluma za dini na sheria. Si afisa wa serikali wala hana dhima
ya utawala au uongozi. Alim hutambuliwa kuwa Mufti na maulamaa wenzake wa eneo
husika kwa kutambua upeo wake mkubwa katika fani za elimu ya dini na
sheria. Alim akitambuliwa na kupewa hadhi ya mufti huchukuliwa kuwa ni
marejeo kwa ajili ya kutolea ufafanuzi masuala ya elimu ya dini na sheria. Kwa hiyo mufti jukumu
lake ni kufutu mas’ala ya dini na sheria. Si kuwa mtawala au mpangaji wa masuala
ya utawala. Kwa upande wa pili,
Kadhi ni cheo cha kimahakama na kiserikali. Ni afisa wa serikali au umma mwenye
mamlaka. Katika taratibu za
kiutawala za Kiislamu, kadhi ni cheo na hadhi kubwa kuliko mufti. Kwa maana hiyo si
jambo linalokubalika, kwa mujibu wa mfumo wa utawala na uongozi wa
Kiislam kupindua mizani na kuweka mufti juu ya kadhi. Kwa hivyo, Kiislamu,
haifai makadhi kuteuliwa na Mufti.
4.2 MAPENDEKEZO YETU:
Sheria iunde Baraza la
Sheria za Kiislam litakalokuwa na mamlaka ya kuteua makadhi na kusimamia
nidhamu na maadili yao. Iwapo itaonekana kuwa ni
lazima sheria iweke mamlaka ya kuteua makadhi juu ya afisa mmoja mkuu
atakayetajwa na sheria, basi sheria ifanye kuwa ni lazima afanye hivyo kutokana na
orodha itakayopendekezwa kwake na baraza au mamlaka itakayoundwa
rasmi kwa ajili hii.
5. MUSWADA HAUELEZI
KUHUSU AJIRA NA USALAMA WA AJIRA YA
MAKADHI:
5.1 HOJA:
Muswada hautaji popote
iwapo kama hao makadhi watakuwa ni maafisa wa kuajiriwa au wa
kujitolea. Na iwapo wanaajiriwa, basi wanaajiriwa na chombo gani. Ni jambo la lazima
makadhi wawe wa kuajiriwa. Kufanya makadhi wawe wa kujitolea kutasababisha
mfumo mzima kuingia dosari zinazotokana na shida na haja za kibinadamu za
watu watakaokuwa wakihudumu kama makadhi. Muswada pia hauelezi ni
nani mwenye mamlaka ya kumuondoa kadhi na utaratibu na vigezo au sababu za
kumuondoa kadhi. Hili liaacha mwanya kwa makadhi kuingiliwa katika
utendaji wao.
5.2 MAPENDEKEZO YETU:
Sheria iweke Bodi ya
Ajira ya Makadhi ambyo ndiyo itakuwa mwajiri wa makadhi na ndiyo itakayowapa
mafao yao ya ajira. Sheria pia ieleze wazi
mamlaka ya nidhamu na udhibiti wa mwenendo na maadili ya makadhi kama
inavyopendekezwa katika ibara ya 8 hapa chini.
6. MUSWADA UNAWEKA
MAMLAKA YA KUWEKA KANUNI ZA MAHAKAMA KWA MUFTI:
6.1 Kasoro za kutegemeza
mamlaka yahusuyo masuala ya Mahakama ya Kadhi kwa Mufti tumeshazitaja
katika ibara ya 4 hapo juu. Kwanza kuwa Mufti mwenyewe hatajwi na
sheria yoyote. Pili kuwa mamlaka muhimu kama hayo isingekuwa vyema
kuyaweka mikononi mwa mtu mmoja. Hivyo basi, ni kasoro na
kosa kubwa kuweka mamlaka ya kuweka kanuni za mahakama mikononi mwa
Mufti.
6.2 MAPENDEKEZO YETU:
Sheria iunde Baraza la
Sheria za Kiislam litakalokuwa na mamlaka ya kanuni za mahakama. Inapendekezwa
kuwa Baraza la Sheria za Kiislam lililopendekezwa katika ibara ya 4.2 hapo
juu ndilo liwe Baraza la Sheria za Kiislam ya kuweka kanuni za mahakama za
Mahakama ya Kadhi. Iwapo itaonekana kuwa ni
lazima sheria iweke mamlaka ya kutunga kanuni juu ya afisa mmoja mkuu
atakayetajwa na sheria, basi sheria ifanye kuwa ni lazima afanye hivyo kutokana na
orodha itakayopendekezwa kwake na baraza au mamlaka itakayoundwa
rasmi kwa ajili hii. Tunapendekeza kuwa
Baraza la Sheria za Kiislam la uteuzi ndilo liwe pia Baraza la Sheria za Kiislam la
utungaji wa kanuni kama itakavyopendekezwa hapa chini.
7. MUSWADA UNAWEKA
MAMLAKA YA KUWEKA KANUNI ZA KUKAZIA HUKUMU KWA
WAZIRI:
7.1 HOJA:
Muswada unaweka mamlaka
ya kuweka kanuni za kukazia amri, maamuzi na hukumu za makadhi kwa
Waziri wa Sheria. Kasoro iliyopo ni kuwa muswada haumlazimishi waziri
kushauriana na chombo au mamlaka yoyote ya Waislamu kabla ya kuweka kanuni
hizo.Hili linaweza
likapelekea migogoro na migongano kati ya Waislamu na Serikali. Kwanza kwa kuwa hili
litahusu utekelezaji wa amri, maamuzi na hukumu za makadhi, litahusu pia
kanuni na taratibu za Kiislam. Kwa hiyo kuna umuhimu mkubwa kuwahusisha
wataalam na viongozi wa ummah wa Kiislam katika maandalizi ya kanuni za
mahakama.
7.2 MAPENDEKEZO YETU:
Tunapendekeza kuwa
sheria ieleze kuwa Waziri atashauriana na mamalaka au baraza linalotajwa
katika ibara ya 4 hapa juu katika kuandaa kanuni za mahakama.
8. UDHIBITI WA NIDHAMU,
MWENENDO NA MAADILI YA MAKADHI:
8.1 HOJA:
Muswada hauweki maelezo
yanayohusu udhibiti wa mwenendo, nidhamu na maadili ya makadhi.
Ukisoma muswada, utaona
kuwa waziri amepewa mamlaka ya kuweka kanuni za ukaziaji wa hukumu,
maamuzi na amri za mahakama ya kadhi. Utaona pia kuwa Mufti amepewa mamlaka ya
kuweka kanuni za mahakama (rules of court). Hakuna maelezo yanahusu
kanuni za nidhamu, mwenendo na maadili ya makadhi. Hii ni kasoro kubwa sana
inayoweza kusababisha madhara makubwa sana katika utendaji wa mahakama
hiyo.
8.2 MAPENDEKEZO YETU:
Tunapendekeza kuwa
mamalaka au baraza linalopendekezwa katika ibara ya 4 hapo juu liwe ndicho
chombo cha udhibiti wa nidhamu, mwenendo na maadili ya makadhi. Baraza la Sheria za
Kiislam hilo pia liwe na mamlaka ya kuweka kanuni za nidhamu, mwenendo na
maadili ya makadhi.
9. WIGO WA MAMLAKA WA
MAHAKAMA YA KADHI:
9.1 HOJA:
Wigo wa mamlaka ya
mahakama ya kadhi ni finyu sana. Kwa mujibu wa kifungu cha 3 cha Sheria mama
kama kitakavyorekebishwa, mamlaka ya mahakama ya kadhi yataishia katika
kusikiiza mashauri yanayohusu sheria ya Kiislamu katika maeneo yale tu yaliyomo
katika matamko ya Waziri ya Sheria ya Kiislamu yanayoweza kutolewa
chini ya kifungu cha 2 cha sheria hiyo.
“4.-(1) The statements
of Islamic law published in the Gazette in terms of sections 2 and
3 shall be applied and given effect to by Kadhis‟
Courts at any place within the geographical jurisdiction of such courts in any cases
and matters to be determined relating to personal status,
marriage divorce or inheritance”.
Hili liko wazi hata
katika kauli ya madhumuni ya muswada: “In addition, it is
proposed to amend section 4 so as to allow statements issued under
sections 2 and 3 to be applicable and given effect by Khadhi Courts
within geographical jurisdiction of the court on matters relating to
personal status, inheritance, marriage, divorce and probate”. Hii ni kasoro na
upungufu mkubwa sana. Hasa ikizingatiwa kuwa waziri halazimishwi kutoa
matamko katika maeneo yote ya sheria ya Kiislamu yanayohusu masuala ya
familia na hadhi binafsi.
Utaona kuwa toka
ilipopitishwa sheria ya Islamic Law (Re-Statement) Act mwaka 1964 kuna tangazo moja
la matamko ya waziri ya Sheria ya Kiislamu nalo ni Tangazo la Serikali Na.
222 la 1967 linalohusu sheria ya ndoa ya Kiislamu. Na tangazo hilo nalo mpaka
leo halijaanza kutumika kwa sababu Waziri wa Sheria hajatoa tangazo katika
gazeti la Serikali la tarehe ya kuanza kutumika kwake. Hii inaonyesha kutokuwepo
kwa nia thabiti upande wa Serikali wa kuwezesha mfumo wa Sheria za Kislam
kufanya kazi ipasavyo hapa nchini.Hivyo, mahakama ya kadhi ikipitishwa leo,
makadhi hawatakuwa na kazi ya kufanya mpaka Waziri wa Sheria atakapoamua kwa
hiyari yake kutoa matamko ya sheria ya Kiislamu na kuyaanzisha kutumika. kwa hali hii, mahakama
zilizopo sasa zina wigo mpana zaidi wa mamlaka kuliko mahakama ya kadhi kwa
sababu mahakama za kawaida hazifungwi na matamko ya Waziri pekee. Na kwa
sasa, mahakama ya kadhi haitakuwa na mamlaka kabisa.
9.2 MAPENDEKEZO YETU:
Mmlaka ya kawaida:
Wigo wa mamlaka ya
mahakama ya kadhi upanuliwe. Mahakama ya kadhi iwe na mamlaka ya kusikiliza na
kuamua mashauri yanayohusu sheria ya Kiislamu katika maeneo yote ambayo
mahakama za kawaida zina mamlaka bila kutegemea kuwepo kwa matamko ya waziri wa
Sheria.
Mamlaka ya ziada:
Pia mahakama ya kadhi
iwe na mamlaka ya kusikiliza na kuamua, kwa mamlaka ya hiyari, mashauri
yoyote ya madai ikiwa ni pamoja na mashauri yanayohusu mikataba ya Kiislamu na
masuala ya fedha ya Kiislamu pale pande zote husika zinapo hiyari kwa
maandishi kuwa mashauri yao yasikilizwe na kuamuliwa na mahakama ya kadhi.
Sheria iyape maamuzi ya Kadhi katika masuala ya hiayari kama inavyopendekzwa
hapa uzito sawa na hukumu, maamuzi na amri zake
nyingine.
10. MAMLAKA YA PEKEE:
10.1 HOJA:
Muswada unatoa hiyari
kwa mdaawa Muislamu kufungua shauri lake la sheria ya Kislamu katika mahakama
ya kadhi au mahakama nyingine. Hili lina hatari ya kuleta matatizo mengi.
Likiachwa hivyo kunaweza kukatokea mgongano baina ya mahakama ya kadhi na
mahakama za kawaida ikiwa kila upande katika mgogoro utaamua kufungua shauri
katika mahakama tofauti.
10.2 MAPENDEKEZO YETU:
Sheria inapasa kuipa Mahakama
ya Kadhi mamlaka ya kipekee (exclusive jurisdiction)
kushughulikia migogoro inayohusu sheria za Kiislamu. Mahakama ya kadhi iwe na mamlaka ya
kipekee pale sheria ya Kiislamu inapotumika.
11. UGHARIMIAJI WA
MAHAKAMA YA KADHI:
11.1 HOJA:
Hoja ya kwanza ni kuwa
mahakama haiwezi kujiendesha yenyewe. MUSWADA huu unaitaka
mahakama ya kadhi ijiendeshe yenyewe badala ya kuendeshwa na serikali,
jambo ambalo hatuna kumbukumbu ya kutokea kwake sehemu yeyote duniani
kuwa chombo kama mahakama kujiendesha chenyewe. Mahakama si mradi wa
kibiashara. Haiwezi kujiendesha yenyewe kwa sababu ima itabidi ifanye ada zake
ziwe juu sana ili iweze kupata pesa ya kutosha kujigharimia, au itabidi
iwe na miradi ya biashara, au iwe na taratibu za kutafuta pesa (fund raising).
Haya yote hayatawezekana kwa sababu zifuatazo:-
- Chombo cha kutoa haki
hakitakiwi kufanya huduma zake kuwa ghali kiasi cha kuwafanya
wadaawa wanaotafuta haki washindwe kukiendea kwa sababu ya kutomudu
gharama. Kufanya hivyo kutafunga mlango wa jumba la haki kwa
wahitaji waliowengi. Hiyo itakuwa ni "denial of access to justice." Haki ya
kupata haki ni haki ya msingi sana na ndiyo inayofanya dhana ya
kuwepo na haki iwe na maana.
- Mahakama jukumu lake
la msingi ni kutoa haki, sio kutafuta fedha kwa ajili ya kujiendesha.
Mahakama ina wataalam wa sheria, sio wataalam wa miradi ya uchumi wala
wataalam wa fund rasing. Kwa hiyo dhana ya
mahakama kujiendesha yenyewe ni potofu. Hoja ya pili ni kuwa
hakuna sababu kwa kwa mahakama ya kadhi kutogharimiwa na Serikali. Zipo sababu
kadhaa za kupendekeza hivi:-
i) Katika mamlaka yake
ya kawaida mahakama ya kadhi itasikiliza na kuamua mashauri yaleyale ya
sheria ya Kiislam ambayo sasa yanasikilizwa na kuamuliwa na mahakama za kawaida
za Serikali kwa gharama za Serikali. Tatizo kubwa ni kuwa mahakama hizo
hazina sifa wala nia ya dhati ya kushughulikia migogoro ihusuyo Sheria ya
Kiislam. Kwa hiyo kinachotakiwa
sasa ni kushughulikia migogoro hiyohiyo kwa kupitia mahakama yenye sifa
stahiki na utayari wa kufanya hivyo. Hakuna gharama mpya katika kuendesha
mashauri haya kwani ni mzigo uleule utatolewa katika
mahakama za kawaida na
kuwekwa katika mahakama za kadhi.
ii) Maeneo ya migogoro
yanayopendekezwa kushughulikiwa na mahakama ya kadhi ni pamoja na ndoa,
talaka, uzazi wa watoto, mirathi, ulezi na matunzo ya watoto, wakfu, na
kadhalika. Wale wasiotumia sheria ya Kiislam nao pia wanayo migogoro katika maeneo
haya na wanahudumiwa na mahakama za kawaida. Baada ya Mahakama ya kadhi
kuanzishwa, wasiotumia sheria ya Kiislam wataendelea kuhudumiwa na mahakama
za kawaida kwa gharama za Serikali. Lakini watumiaji wa Sheria ya Kiislam
wawapo na migogogoro iliyosawa na hiyo ya wenzao, wao wanatakiwa wagharimie
wenyewe. Hili linakinzana na
dhana ya usawa mbele ya sheria. Wakati mashauri ya wengine yanagharimiwa na
Serikali kwa kodi za wote, Waislam wanaambiwa wayagharimie ya kwao wao
wenyewe.
iii) Suala la Serikali
kugharimia vitu vya watu wa dini moja si geni wala si jipya. Wakristo kupitia
Memorandum of Understanding wanajipatia mabilioni ya shilingi kutoka katika bajeti ya
Serikali kugharimia mahospitali yao na mashule na vyuo vyao. Kitendo cha kuyapa
makanisa mapesa hayo yoyote kwa mkataba wa kipekee na wa siri baina yao na
Serikali ambao hautoi fursa na wasiokuwa wakristo nao kupatiwa fedha kama hizo ni
kitendo cha kibaguzi. Hapa hakuna usawa. Si sawa na suala la mahakama kwa kuwa watu
wote wanapata fursa ya kutatuliwa migogoro yao kwa gharama za Serikali. Lakini
makanisa yanapewa fedha ambazo wengine hawapewi sio kwa sheria bali kwa
mkataba hususia. Huu ndio upendeleo halisi na ubaguzi. Kwa kutoa fedha kwa
makanisa Serikali inaajingiza katika mambo ya kidini kwani hayo makanisa yanaita
utoaji wa huduma hizo kuwa ni utume. Ukisoma machapisho mbalimbali
ya makanisa husika utaona kuwa wanatumia huduma hizo kufikisha ujumbe wao wa
kiroho. Kwa Serikali kujiingiza kuyapa fedha makanisa kwa ajili ya kuyasaidia
katika kutoa huduma hizo inayasaidia kufanya kazi ya kidini.
iv) Mahakama ya Kadhi
ipo na inafanya kazi Zanzibar katika Jamhuri hii hii. Zanzibar mahakama ya
kadhi ni chombo cha kiserikali na inagharimiwa na serikali. Ikiwa ni
halali Zanzibar, chini ya Katiba hii hii ya Jamhuri ya Muungano, itakosa vipi uhalali
Tanzania Bara? Vipi mahakama iwe halali upande mmoja wa Muungano na ivunje
katiba upande wa pili misingi ya kikatiba ni ileile.
v) Zipo mahakama za
makundi ya watu maalumu ambazo zinaendeshwa kwa pesa za serikali ambazo ni
kodi za watanzania wote. Mfano ni kama vile mahakama ya kazi, Ardhi, Biashara
n.k ni kwanini mahakama itakayotafsiri sheria za Kiislamu iwe tofauti?
11.2 MAPENDEKEZO YETU:
Sheria iweke wazi kuwa
mahakama ya kadhi itagharimiwa na Serikali sawa na zinavyogharimiwa
mahakama nyingine.
12. MAMLAKA YA WAZIRI
KUTOA MATAMKO YA SHERIA YA KIISLAMU:
12.1 HOJA:
Sheria kama ilivyo sasa
na hata baada ya marekebisho yaliyomo katika muswada inampa Waziri wa Sheria
mamlaka ya kutoa matamko ya sheria ya Kiislamu. Sheria haimlazimishi
waziri kufanya hivyo kwa kufuata muongozo wa maulamaa wa Kiislamu au baada ya
kushauriana na chombo chochote cha Kiislamu. Hili si jambo zuri kwa
sababu Waziri si mtaalamu wa sheria ya Kiislamu. Ni vyema Waziri katika
kutekeleza hili akapata ushauri na mwongozo wa maulamaa wa Kiislamu kwa kuwa wao
ni wataalamu katika fani hiyo. Sheria hii, The Islamic
Law (Re-Statement) Act, sura ya Sura ya 375 inampa Waziri mamlaka ya kutoa
matamko ya sheria ya Kiislamu. Lakini hakuna mamlaka ya kufanyia matamko hayo
marekebisho pale itakapo bainika kuwa kuna makosa, kasoro au upungufu
katika matamko hayo.
12.2 MAPENDEKEZO YETU:
Tunapendekeza kuwa
Baraza la Sheria za Kiislam liliotajwa katika ibara ya 4 hapo juu ndiyo litaandaa
matamko hayo, Waziri wa Sheria mamlaka yake yawe ni kuyapitisha matamko
yaliyoandaliwa na Baraza la Sheria za Kiislam hilo kuwa kanuni. Pale Baraza la Sheria za
Kiislam tajwa litakapobaini kuwa kuna kosa, kasoro au upungufu katika tamko
lolote lile la Waziri, basi litaandaa marekebisho na kuyapendekeza kwa waziri
ili ayapitishe.
13. ULAZIMA WA MAHAKAMA
YA KADHI KUTAJWA NDANI YA
KATIBA:
13.1 HOJA:
Kutokutajwa ndani ya
Katiba inayopendekzwa kunaweza kukaifanya mahakama ya kadhi kutokutambuliwa
kama mahakama halali kikatiba. Hii inaweza kupelekea mgogoro mkubwa kwa
mahakama nyingine kuweza kuhoji uhalali wa kikatiba wa mahakama ya kadhi.
Mahakama nyingine, huhusan Mahakama Kuu ya Tanzania na Mahakama ya Katiba
zinaweza kubatilisha maamuzi yake na hata kutoa maamuzi ya kuifuta
kabisa.
13.2 MAPENDEKEZO YETU:
Kuna ulazima wa kuiwekea
mahakama ya kadhi msingi wa Kikatiba ili uhalali wa kuwepo kwake na utendaji
wake usihojiwe na mahakama nyingine ili kuepusha migongano na migororo
huko mbeleni.
SEHEMU YA TATU: PENDEKEZO LA MUSWADA ULIOREKEBISHWA:
Pamoja na maoni yetu
haya tunawasilisha katika Kiambatanisho na. 1 pendekezo la muswada
uliorekebishwa ili kukidhi matakwa tuliyoyaelezwa katika Sehemu ya Pili ya maoni haya.
Tunaomba kuwasilisha:
Jina Kamili /Taasisi /Wadhifa/ Sahihi
- Sheikh Suleiman A. Kilemile
- Hay Atul- Ulamaa Mwenyekiti
- Sheikh Abdallah A. Bawazir Hay Atul -Ulamaa Makamu Mwenyekiti
- Sheikh Abdallah R. Ndauga Hay Atul - Ulamaa Mdhamini
- Sheikh Hassan Abbas Semkuya Shura ya Maimamu Makamu Amir
- Sheikh Hamad Iddi Almas Shura Ya Maimamu Imamu
- Dr. Said A Sima DUMT Makamu Mwenyekiti
- Musa M. Hans DUMT Katibu
- Eng. Sherally H. Sherally BASUTA Mdhamini
- Sheikh Mohammed Issa BASUTA Naibu Katibu
- Sheikh Shams Elmi BASUTA Mjumbe
- Sheikh Shaaban Mussa BASUTA Katibu
- Eng. Alliy S. Kilima An-Nahl Trust Amir
- Dr. Hamdun Sulayman An-Nahl Trust Katibu
- Sheikh Mussa Yusuf Kundecha Baraza Kuu Amir Mkuu
- Maulana Ramadhan Sanze Baraza Kuu Katibu Mkuu
- Mwl. Fadhil Ally Chambo Jumuiya na Taasisi Mwenyekiti
- Ust. Jaffar Said Mneke Jumuiya na Taasisi Katibu
- Sheikh Khalfan Athuman Khalfan JASUTA Katibu Mkuu
- Sheikh Awadhi Mussa Mfinanga JASUTA Mdhamini
- Dr Pazi TAMPRO Katibu Mkuu Sheikh Karmal Msuya TAMPRO Kaimu Mwenyekiti
- Advocate Othman Kalulu IPC Katibu
No comments:
Post a Comment