Sheikh Ali Mzee Comorian Akizungumza Katika Khitma Saigon Club 2012 |
Taa Iliyozimika Ghafla


Na
Alhaj Abdallah Tambaza
WENGI wa wenyeji wa jiji la Dar
es Salaam, hususan waumini wa dini ya Kiislamu, Jumapili ya Desemba 28, 2014
itakuwa siku ya kukumbukwa baada ya kuondokewa na mmoja wa masheikh mashuhuri
wa jiji hili, Ali Mzee Komorian.
Kwa hakika jiji lilizizima
baada ya habari za msiba ule mzito kusambaa miongoni mwa ndugu, marafiki na
waumini wa dini ya Kiislamu— hasa wa maeneo ya Kariakoo— kwamba Sheikh wa
‘Darisalamu’(kama alivyopenda kujiita), hatunaye tena.
Nilikuwa ofisini kwenye Chumba
cha Habari cha gazeti la Raia Mwema, Kinondoni, Dar es Salaam wakati simu yangu
ya kiganjani ilipoashiria ujumbe mfupi:
“…msiba
mzito wa mpenzi wa Mtume Sheikh Ali bin Mzee Komorian amefariki leo saa 5
asubuhi na mazishi bado kupangwa… Inna lillah…”
Alikuwa Alhaj Mussa Shaggow,
aliyenitumia ujumbe ule kunipasha habari zile nzito ambapo baada ya hapo, simu
nyingine nyingi zilifululiza kuleta habari zile za huzuni kubwa. Haikuwa siku nzuri kwangu hata kidogo.
Maziko ya Sheikh Ali
yalifanyika siku ya Jumatatu asubuhi na mwandishi huyu alikuwa miongoni mwa
maelfu ya waombolezaji waliofurika kwenye Msikiti wa Makonde kupata fursa ya
kuswalia jeneza lake.
Watu walikuwa wengi sana kiasi
cha kusababisha wengine kuswalia nje barabarani na wengine kukosa fursa hiyo
kabisa. Swala ya jeneza iliongozwa na rais mstaafu Sheikh Ali Hassan Mwinyi,
aliyekuwa na uhusiano naye wa karibu mno.
Kama vile kuashiria namna
fulani ya muujiza, jeneza lilobeba mwili wa marehemu lilipoanza kuwekwa
mabegani tu, yakaanza kuanguka manyunyu mepesi mepesi ya mvua, kitu ambacho
kilitafsiriwa na wengi kwamba ilikuwa ni bishara njema.
Mvua ile iliongezeka na kuwa
kubwa iliyoambatana na mingurumo na radi zenye kutisha. Giza nene likatanda
maeneo yote ya Kariakoo kuelekea makaburi ya Ngazija.
Allah (S.W.T), pengine alikuwa
akituonyesha kwamba mja wake yule tunayekwenda kumzika hakuwa mtu wa kawaida.
Vyovyote vile iwavyo, mvua ile
ilisababisha mimi na ‘sahib’ yangu Alhaj Mohamed Said, kushindwa kufika
makaburini.
Gari letu lilikwama kwenye
foleni maeneo ya Faya kwa zaidi ya saa nzima huku barabara zote za kuelekea
Kisutu zikiwa zimejaa maji yasiyo kifani.
![]() |
Mvua Kubwa Iliyonyesha Siku ya Maziko |
Safari yetu iliishia hapo;
tukamwombea dua ya ‘ghaib’ tukaelekea nyumbani kupumzika.
Said ‘Kilomoni’ Marjebi, yeye
alikuwapo pale makaburini Ngazija wakati wa maziko. Nilikutana naye jioni— huku
machozi bado yakimlengalenga – alinisimulia yaliyojiri: “… eh, bwana wee! Mungu
katuonyesha utukufu wa Sheikh Ali kupitia mvua…“mwili wa marehemu ulipokuwa
unashushwa kaburini, radi za vishindo ziliongezeka …paa
…puu puu… mithili ya mizinga ile wapigiwayo watukufu wa kidunia
wazikwapo,” alimaliza.
Nilimfahamu Ali Mzee Komorian, (60),
miaka miaka mingi iliyopita (1960s), sote tukiwa vijana wadogo, ingawa mimi ni
mkubwa kwake kiumri.
Yeye alikuwa akisoma na wadogo
zangu binamu, Ibrahim Mussa Pazi na Said Marjebi maarufu Said Kilomoni pale
Shule ya Msingi Olympio, Upanga, jijini Dsm.
Kijana Ali, alikuwa akija kwetu
mara kwa mara akiwa na rafiki zake hao, wakiwa ama wanakwenda au wanarudi
kutoka shule wakati wa mchana wakicheka na kufurahi pamoja.
Lakini nikiangalia nyuma
sawasawa (in retrospect), kumbukumbu zinanielekeza kwamba nilimfahamu mamake kwanza
kabla ya kumjua Sheikh Ali mwenyewe.
Mwalimu Bahia, ndiye mama mzazi
wa Sheikh Ali Komorian. Mama huyu, kwenye miaka ya 50 wakati nchi yetu ikiwa
bado inatawaliwa na wakoloni, alikuwa akitembelea shule za msingi za Dar es
Salaam kufundisha dini ya Kiislamu.
Kuanzia mwaka 1958 mpaka mwaka
1961 nilipokuwa mwanafunzi pale Shule ya Mnazi Mmoja, alikuwa ni Mwalimu Bahia
aliyekuwa akija kutufundisha somo la dini wanafunzi wote wa Kiislamu kwenye ‘holi’
la shule kila Ijumaa.
Kamwe siwezi kuisahau kazi hiyo
ya mamake Sheikh Ali, kwani katika umri ule wa utoto, nilikuwa ‘nainjoi’ sana
kashata nzuri za nazi ambazo mwalimu Bahia alikuwa akituuzia na sisi kuzila
wakati darasa likiendelea.
Mwalimu Bahia, pia ndiye
mwanamke anayeongoza shughuli nyingi za kidini jijini Dar es Salaam kwa upande
wa wanawake wa Kiislamu.
Huwa mbele katika mazishi;
huratibu na kuongoza shughuli za maulid kwa upande wa kina mama; na pia huwepo
kwenye harusi upande wa kina mama iwe majumbani au kwenye maholi akiwa pamoja
na watoto wake wa madrassa.
Katika miaka yangu ile ya
ukuaji katika jiji la Dar es Salaam, nilimfahamu pia babake marehemu Sheikh Ali.
Alikuwa msomi bobezi wa dini ya Kiislamu na mtunzi mahiri wa vitabu mbalimbali
vya dini vikiwamo vya utenzi na mashairi ambayo sasa ni nadra au haiwezekani
kabisa kumpata mtunzi wa kiwango cha bwana mkubwa yule.
Sheikh Mzee bin Ali (baba) pia
ameacha kumbukumbu itakayodumu miaka mingi, kwani aliweza kutafsiri na kuyafanya
Maulid ya Barzanji kuweza kusomwa Kiswahili kwa maghani yake yaleyale ya asili.
Marehemu Sheikh Ali bin Mzee
bin Ali Komorian, alizaliwa mnamo mwaka 1954 mtaa wa Kibambawe, Kariakoo, Dar
es Salaam akiwa mtoto mkubwa na pekee wa kiume kati ya watoto saba familiani.
Habari zinasema, elimu yake ya
madrassa (elimu ya dini) ya mwanzoni, aliipata nyumbani kwao kwa babake na
mamake kabla ya kwenda kwa masheikh wengine akiwamo aliyewahi kuwa Mufti na
Mudir wa Zanzibar Muslim Academy, Sayyid Omar Abdallah (Mwinyibaraka), Sheikh
Ramadhan Abbas na masheikh wengi wengine jijini Dar es Salaam.
Alijiunga na Shule ya Msingi
Olympio ya Upanga, Dar es Salaam kwa masomo ya elimu ya kizungu na baadaye
kumalizia elimu ya Sekondari, Kinondoni Muslim kwenye miaka ya 1970s.
Ukiachilia mbali mambo ya
elimu, Ali Mzee, kama walivyo vijana wengi wa umri wake, alijiunga na vilabu
mbalimbali vya watoto kucheza mpira.
Mwandishi huyu alimshuhudia
akiwa golikipa machachari kwenye timu maarufu ya watoto ya West England
iliyokuwa maeneo ya nyumbani kwao.
Timu hiyo ilikuwa ikiongozwa na
kina Abdallah Katungunya, Ndege na Kocha Muharam Shakuku.
Baadaye, Ali Komorian, alikuja
kuwa mwanachama wa klabu ya Saigon ya Dsm, ambako alijijengea jina kwa kuwa
kioo cha klabu hiyo kila zinapofanyika hafla mahala hapo.
Klabu ya Saigon, leo hii bado
imeendelea kuwa kivutio na mfano wa kuigwa (exemplary) kwa kudumisha silka,
silsila na tamaduni za watu wa ‘Kidarisalama’.
Saigon, kwa miaka mingi sasa
imedumu katika kufanya kumbukumbu ya kuwaenzi na kuwaombea dua wazee, masheikh,
pamoja na wanachama wenzao waliokwishatangulia mbele ya haki.
Kila mwaka, almarhum Ali Komorian amekuwa mshereheshaji mkubwa kwenye hafla hizo— piga ua atakuwa mzungumzaji au mtoaji dua wa mwisho.
Bila shaka, katika hafla
itakayofanyika mwaka huu jina lake litakuwa miongoni mwa warehemewa wa mwanzo
kabisa.
Daima ilikuwa ni hapo Saigon
ambapo mara nyingi amekuwa akihubiri upendo, subira na kukemea maovu miongoni
mwa jamii. Hakupenda hasama na mifarakano baina ya watu.
Hili lilidhihirika katika
maudhui ya tungo zake za mashairi na Qassida
alizozitunga zikiwa na maneno mazito yenye mafunzo hayo.
Msomaji zingatia beti hizi hapa
chini:
“Ugomvi wa nini; patana…patana…
Tutagombana mpaka lini…
Patana…patana…patana
Ni khasara leo na kesho
kiyama…”
KHITMA YA SAIGON CLUB
Sheikh Ali bin Sheikh Mzee Comorian Akizungumza Katika Khitma ya Saigon Club Tarehe 24 Juni 2012 |
Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi Akiwasili Katika Khitma Saigon Club |
Wa Pili Kushoto Kwenda Kulia - Stephen Rupia (Mpuya) Alhaj Abdallah Tambaza na Alhaj Ali Momba |
Mbele ni Alhadi Mussa Sheikh wa BAKWATA Mkoa wa Dar es Salaam na Kulia ni Boi Juma Risasi. Nyuma ni Mufti wa BAKWATA Sheikh Shaaban Simba Akisindikizwa na Muharram Mkamba |
Hao Watatu Wenye Kanzu ni Wahudumu Katika Khitma Kushoto Kwenda Kulia: Abdulbari, Juma Abeid na Alhaj Musa Shagow Pembeni Yao Kushoto ni Stone na Kulia ni Simba |
Aliyevaa Kashda Kushoto ni Shariff Hussein Badawiy na Kulia kwake ni Iddi Simba na Kushoto Kwake ni Hamza Kassongo |
Balozi Abbas Sykes Akizungumza na Mwinyi Mangara |
Kutoka Kushoto: Dk. Tamim Bushiri, Mohamed Said, Abdallah Miraj na Mbwana |
Maneno ya mashairi hayo hapo juu yameweza kusaidia kupatanisha watu wengi sana waliokuwa wamegombana na kushindwa kupatana kirahisi.
Miongoni mwa tungo zake nyingi nyengine
ambazo zitadumu kupendwa na kuenziwa na jamii ni; ‘Usisikitike Allah
alilokadiri…’ na ‘Haya Tumpendeni…’ wenye kumsifu na kumtukuza Mtume Muhammad
(S.A.W).
Ali Komorian, alikuwa mpenzi
mkubwa wa Mtume Muhammad (SAW), kiasi cha kufikia kujiita (self proclaimed)
Ahbabi Rassul (mpenzi wa Mtume).
Alikuwa kweli mpenzi wa Mtume
na wala alikuwa hafanyi mzaha; kwani katika uhai wake hakuchoka kuhudhuria
hafla za Maulid kila zilipofanyika na yeye kupata habari zake.
Almarhum Sheikh Ali, alikuwa si
mtu wa kupenda kujikweza na kupenda ukubwa na utukufu. Fahari na majivuno pia
vilimpitia mbali.
Akikazia
nukta hiyo ya udhalili (simplicity) wa Ali Komorian, Imam Mkuu wa Msikiti wa
Mtoro, Sheikh Zubeir Yahya aliyepewa fursa ya kutoa wasifu wa rafiki yake
kwenye khitima anasimulia kisa hiki:
“…kuna
tajiri mmoja anaitwa Zakaria alimwita marehemu na kumpa gari la kifahari liwe
mali yake limsaidie katika maisha yake marehemu alilikataa gari lile na kumjibu
Zakaria kwamba yeye hufurahi zaidi
anapokanyaga kwenye ardhi ya Allah…
Marehemu
alichelea huenda gari lile likamfanya ajione bora na kuwa mtu wa majivuno kitu
ambacho hakukipenda,’’ alisimulia Sheikh Zubeir na kuuliza;“Je, ni
nani kati yetu hapa msikitini, nikiwamo mimi na wewe, anaweza kupewa gari kama
hilo na alirudishe namna hiyo?”
Mvua
kubwa iliyonyesha asubuhi ile ya maziko ilimzuia Rais Jakaya Kikwete kufika
makaburini kuzika. Kufuatia hali hiyo, rais alielekea nyumbani kwa marehemu
kwenda kutoa mkono wa tahania kama vyombo vya habari vilivyomwonyesha akiwa
pale na ndugu wa marehemu.
Tunamwomba
Mungu awape subira na uvumilivu wafiwa wote na marehemu ampumzishe kwenye pepo
yake ya Firdaus:
Yailahi
Yasatari Tustiri Yalatwifu,
Utupe
riziki za kheri viumbe vyako dhaifu;
Kila
jema liwe ndilo tusamehe Mola wetu;
Mikono
tumeinua kukuomba Yakarimu;
Utakalo
Mola huwa pasi dakika kutimu.
Simu:
0715 808 864 /0784 808 864
No comments:
Post a Comment