CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM) YAVUNJA NYUMBA ILIPOANZISHWA TANGANYIKA AFRICAN ASSOCIATION NA KUASISIWA (TANU) 1954
Mohamed Said
Iliyokuwa Makao Makuu ya African Association 1929 – 1954 na TANU 1954 – 1977
| Mtaa wa Kariakoo na Mbele ni Mtaa wa Lumumba Mabati Yamezungushwa Ilipokuwa Ofisi ya African Association, TANU na CCM |
Historia ya Chama Cha
Mapinduzi (CCM) haianzi tarehe 5 February, 1977. Historia ya CCM inaanza mwaka
1929 katika nyumba ya Cecil Matola (sasa mali ya marehemu Mzee John Rupia). Mtaa wa Masasi Misheni Kota. Katika nyumba
ile mwaka 1929 ndipo walipokutanika hawa wafuatao kuunda African Association: Kleist
Sykes, Ibrahim Hamis, Zibe Kidasi, Ali Said Mpima, Suleiman Majisu, Raikes
Kusi, Mzee bin Sudi, Rawson Watts na Cecil Matola. Wazalendo hawa ndiyo baadae
wakaja kujenga Makao Makuu ya African Asociation Mtaa wa New Street na Kariakoo
kwa kujitolea. Abdul Sykes katika kumbukumbu zake anasema alikuwa akifuatana na
baba yake, Kleist Sykes kila siku ya Jumapili kwenda pale New Street kwa
shughuli ya ujenzi. Nyumba ikakamilika mwaka 1933 na ikaja kufunguliwa na
Gavana Donald Cameroon.
Katika nyumba hii ndipo
palipofanyika mkutano wa TAA wa mwaka 1954 ambako TANU ilizaliwa tarehe 7 Julai.
Nyumba hii kwa miaka mingi sana ikijulikana kama ofisi ya TANU ilibeba
kumbukumbu nyingi katika mioyo ya Watanganyika. Waafrika ndani ya ukoloni wa
Waingereza waliiona nyumba ile kama alama ya matumaini yao ya kuwa, iko siku
watakuwa watu huru. Maandamano ya kwenda kwenye mikutano ya TANU Mnazi Mmoja na
baadae Jangwani yalikuwa yakianzia pale wananchi wakitembea kwa miguu mbele
umetangulia mganda (ngoma ya Wazaramo), njiani ukikumba kila mtu. Kwa yule
ambae katoka bara na alikuwa akimsikia Nyerere kwa jina tu na sasa ana hamu ya
kumtia Nyerere machoni ilikuwa yeye afike tu pale ofisi ya TANU azubaezubae nje
haitapita muda atamuona Nyerere akiwa hayuko majimboni, akishuka kutoka katika
gari akiendeshwa na dereva wake Said Kamtawa. Said Kamtawa alikuja kupewa jina
akaitwa, “Said TANU,” jina lililomkaa hadi anaingia kaburini. Hawa waliokuwa
wanakuja pale New Street kwa nia ya kumuona Nyerere kisha warudi makwao
wakahadithie walikuwa wengi.
| Waasisi wa TANU Mwaka 1974 Katika Kusheherekea Miaka 20 Toka Kuasisiwa TANU |
| Waasisi wa TANU 1954 Wamesimama Mbele ya Makao Makuu ya TAA |
Pale ofisi ya TANU ndipo
ilipokuwa majlis ya Baraza la Wazee wa TANU wakikutana hapo na halikadhalika
ndipo yalipokuwa makao ya Bantu Group chini ya uongozi wa Yusuf Bakis.Hawa
ndiyo walikuwa walinzi wa Nyerere. Katika miaka katikati 1970 nikipita nje ya
ofisi ya TANU nilikuwa nikimuona Juma Selemani maarufu kama Juma Mlevi, sasa
mtu mzima akiwa mlangoni kukaribisha wageni. Huyu Juma Mlevi kwa watoto wa
Kariakoo ya 1950 na 1960 alikuwa mtu muhimu sana kwetu kwa kuwa siku za Idd
pale Mnazi Mmoja alikuwa akichezesha karagosi na kutuimbisha nyimbo iliyoitwa,
“Karagosi Kalewa Tembo.” (Juma Selemani au Juma Mlevi kama alivyojulikana na
wengi) alikuwa mmoja wa wajumbe wa mkutano wa Kura Tatu Tabora mwaka 1958. Sasa ikiwa historia ya CCM itakuwa inaanza kwa
kuitanguliza TANU bila ya kuitaja African Association kama inavyostahili
kukumbukwa historia ya Tanganyika historia ya CCM yenyewe itakuwa imepunjika. Wengi
wa wazalendo hawa hawapo tena wameshatangulia mbele ya haki. Angalau basi na
tuwakumbuke kwa kuhifadhi historia yao.
Nyerere alianza maisha
yake ya siasa katika ofisi ya TANU pale New Street. Lakini ikiwa mtu ataliweka
jicho lake pale tu Makao Makuu ya TANU wakati ule bila kuangalia viwanja
vingine vya mapambano hakika atakuwa kajihini sana kwani wanaharakati wa wakati
ule ukiondoa pale New Street walikuwa na sehemu nyingine walizokuwa wakikutana
kupanga mikakati yao. Ajabu katika historia ya TANU ni kule kupuuzwa kwa
historia yake ambayo kwa hakika inasisimua. Ningependa msomaji wangu nikupe
historia ya nyumba moja iliyokuwa Mtaa wa Aggrey kona na Sikukuu. Nyumba hii ndiyo alikuwa akiishi Abdulwahid
Sykes rais wa TAA 1951- 1953. Mikutano ya siri ya kuunda TANU ikifanyika hapa
pamoja na mazungumzo mengine ya kubadilishana mawazo kati ya wanaharakati wa
wakati ule.
Hapa ndipo kwa mara ya
kwanza Julius Nyerere alikutana na Abdul Sykes, Nyerere akiongozana na mwenyeji
wake Joseph Kasella Bantu. Hata Nyerere alipojiuzulu ualimu mwaka wa 1955
nyumba hii ndipo alipoishi kabla TANU haijamtafutia nyumba Magomeni Majumba Sita.
Lakini nyumba hii haina historia ya Nyerere peke yake. Nyumba hii ina hitoria
nyingine kubwa ya kusisimua ambayo si wengi wanaifahamu. Historia ya Chief
David Kidaha Makwaia wa Wasukuma. Baada ya kuchukua uongozi wa TAA mwaka wa
1950 hamu kubwa ya Abdul Sykes ilikuwa kuunda TANU kikiwa chama chenye nguvu na
kujumuisha wananchi wote. Ilikuwa fikra yake kuwa kiongozi ambae angefaa
kuchukua uongozi wa TAA kisha wakaunda TANU alikuwa Chief Kidaha. Chief Kidaha wakati
ule alikuwa katika Baraza la Kutunga Sheria la kikoloni, Legislative Council
(Legico). Abdul Sykes ilimjia fikra kuwa Chief Kidaha angeliweza kuwa kiongozi
atakaewaunganisha Watanganyika chini ya TANU kudai uhuru wao. Katika nyumba hii
Abdul Sykes alifanya mijadala kadhaa na Chief Kidaha kuhusu hili lakini Chief
Kidaha hakutaka kubeba jukumu lile.
Inawezekana moja ya
sababu zilizomzuia Chief Kidaha kujiweka pembeni na harakati zile za TAA labda
ni namna Abdul Sykes, Hamza Mwapachu na Dk. Vedasto Kyaruzi walivyochukua
uongozi. Inawezekana pia zilikuwapo sababu nyingine lakini hiki ni kisa kirefu In
Sha Allah tutakitafutia siku yake tukieleze. Itoshe tu kusema kuwa uongozi mpya
wa TAA uliokuwa wa vijana waliwapindua wazee - Mwalimu Thomas Sauti Plantan
aliyekuwa rais na Clement Mohamed Mtamila katibu. Vijana walichukua TAA kwa
nguvu kabla Waingereza kuingilia na kusema ufanyike uchaguzi. “Vurugu” hii
ndiyo iliyowatia katika uongozi Dk. Vedasto Kyaruzi na Abdul Sykes. Dk. Kyaruzi
akiwa Rais na Abdul Sykes katibu. Uongozi huu toka mwanzo haukupendeka kwa
Waingereza. Kisa cha uongozi huu mpya kuchukiwa na Waingereza ni kuandika
katiba waliyoiwasilisha serikalini na katika waraka ule waliwaeleza Waingereza
umuhimu wa kura ya mtu mmoja kura moja kuchagua watu wa kuingia Legco.Hawakuishia hapo wakamaliza kwa kuwaeleza
Waingereza kutoa uhuru kwa Tanganyika baada ya miaka 13.
Inawezekana Chief Kidaha
aliona wenzake wanaiepeleka nchi kwa kasi kubwa. Chief Kidaha alikuwa kipenzi cha Waingereza na
heshima yake ilikuwa juu sana kwa wanasiasa wa wakati ule. Kwa ufupi Chief
Kidaha aliiachia nafasi ile ikampita. Hivi ndivyo jukumu lile Abdul Sykes akaja
kumtwisha Julius Nyerere walipokujajuana mwaka 1952 na mwaka wa 1953 mwezi Juni
Nyerere akachaguliwa kuwa rais wa TAA, Abdul Sykes akiwa makamu wa rais. Nyumba
hii vilevile ilikuwa kituo kisicho rasmi cha Tanganyika African Government
Servant Association (TAGSA)
chama cha Waafrika wafanyakazi serikalini. Viongozi wa TAGSA walikuwa - Ally
Sykes, Thomas Marealle, Rashid Kawawa, Stephen Mhando, Othman Chande na Leonard
Bakuname. Mikutano yao mingi walikuwa
wakifanya katika nyumba hii. Nyumba hii iliyo na historia
kubwa ya kupigania uhuru wa Tanganyika leo haipo. Ally Sykes ameivunja na
kujenga ghorofa. Nilipomuuliza kwa nini kavunja nyumba ile yenye kumbukumbu
kubwa jibu lake lilikuwa, “Hakuna aneitaka historia hii.” Kwa utani nikamwambia,“Baba
tunakupeleka mahakamani kwa kuvunja “national monument,” yeye akawa
anacheka.
Ingekuwa nchi yetu
inathamini kumbukumbu zake nyumba hii muhimu
katika historia yetu ingekuwa chini ya uangalizi wa mambo ya kale na ndani yake
vimehifadhiwa vyote vilivyokuwa mle wakati wa kupigania uhuru wa Tanganyika.
Ndani ya nyumba ile zingebakishwa samani zake, vitabu vilivyokuwa katika
mashubaka, picha zilizokuwa ukutani nk nk. Kizazi kijacho kingeona chumba
alicholala Mwalimu Nyerere kiti alichokalia Chief Kidaha Makwaia, Julius Nyerere
na wapigania uhuru wengine wakati wa kupambana na ukoloni. Wakati ule Abbas
Sykes alikuwa kijana mdogo na yeye ndiye aliyehamishwa chumba kumpa nafasi
Mwalimu Nyerere. Chumba hiki kingehifadhiwa kama kilivyokuwa wakati ule. Hivi ndivyo
wanavyofanya wenzetu katika kuenzi historia zao. Turudi kwenye nyumba ya
TANU iliyovunjwa.
Tarehe 10 Oktoba 1953 katika nyujmba hii kamati ya ndani na ya
siri ya TAA akiwamo Abdul Sykes na mdogo wake Ally, Dossa Aziz, John Rupia na
Julius Nyerere walikutana Makao Makuu ya TAA kujadili vipi wajitokeze wazi sasa
kuibadili TAA kiwe chama cha siasa kamili. Wakati ule nyumba ile ilikuwa haina hata
umeme. Chumba walichokutania kilikuwa hakina viti vya kutosha. Baadhi ya wazalendo hawa walikuwa wamekaa
kwenye viti na wengine kwenye masanduku ya bia yaliyopinduliwa. TAA wakati ule
ilikuwa taabani na kuna chumba walikuwa wamempangisha dobi wa Kihindi wapate
fedha ya kuendesha ofisi. Mkutano huu muhimu ulifanyika miezi sita baada ya
Nyerere kumwangusha Abdul Sykes katika uchaguzi uliofanyika Ukumbi wa
Arnautoglo tarehe 17 April. Uchaguzi huu una mengi ya kueleza lakini hapa si
mahali pake.
Unapozungumzia ile ofisi
ya TANU pale New Street ni lazima uunganishe na “matawi” yake mengine nje ya
pale na kote huku kunahitajika kuwekewa kumbukumbu. Shariff Abdallah Attas
anamkumbuka Nyerere pale Soko la Kariakoo ambako Abdul Sykes alikuwa
akifanyakazi kama Market Master na yeye akiwa Dalali Mkuu wa soko. Shariff
Attas anasema Nyerere alikuwa akija pale sokoni ofisini kwa Abdul Sykes na hapo
ndipo Nyerere akafahamiana na mmoja wa wazee maarufu wa Dar es Salaam na
aliyekuwa mmoja wa wafadhili wakubwa wa
TANU na harakati zote za kudai uhuru, Mzee Mshume Kiyate.
![]() |
| Mzee Mshume Kiyate Akimvisha Nyerere Kitambi Kama Ishara ya Kuungwa Mkono na Wazee Baada ya Kurudi Madarakani Kufuatia Maasi ya Tanganyika Rifles Tarehe 20 Januari 1964 |
Ofisi ya Abdul Sykes
ilikuwa Mtaa wa Swahili pembeni kidogo ya soko. Mtaa wa nyuma yake uliokatiza
ulikuwa Tandamti na Mbele yake Mtaa wa Mkunguni. Mtaa wa Tandamti ndipo alipokuwa akiishi Mzee Mshume (Mtaa huu ulikuja kupewa jina la
Mshume Kiyate kama kumuenzi mpigania uhuru huyu lakini hadi leo wahusika wamekataa
kubadili jina). Abdul Sykes aliuza kadi za mwanzo za TANU hapa na nusra
afukuzwe kazi na wakoloni. Mimi naikumbuka ofisi ile kama vile naiona. Ilikuwa
imezungukwa na mikungu na jirani yake ilikuwa sehemu ya wauza kuku na njiwa.
Mmoja wa babu zangu Shariff Mohamed alikuwa na matundu yake ya njiwa pale. Hii
ndiyo ilikuwa biashara yake. Huenda vijana wa leo wakashangaa kusikia njiwa wanauzwa.
Naam njiwa walikuwa wakiuzwa na walikuwa wakihitajika sana na waganga katika
kufanya uganga wao katika kupunga na mengineyo. Tumetoka mbali. In Sha Allah
tutafuta siku tuzungumze habari hizi maana siku ya Jumapili ndiyo ilikuwa siku
ya kupunga wagonjwa na mashetani kulishwa chano. Haya yalikuwa mambo ya kawaida
katika Dar es salaam ya miaka hiyo na kulikuwa na mabingwa wa sifa katika
shughuli hizi mmoja ninaemkumbuka alikuwa Mwalimu Bakari na akapewa jina la
utani “Seti Khabar,” kwa ubingwa wake.
| Mwalimu Nyerere Akifungua Soko Jipya la Kariakoo 1975 |
Tawi jingine la harakati dhidi ya Waingereza
lilikuwa ofisini kwa Hamza Mwapachu Ilala Welfare Centre na tawi jingine
nyumbani kwa Dossa Aziz Mtaa wa Mbaruku ambako kila Jumapili vijana hawa wanasiasa
walikutana kuzungumza hali ya baadae ya Tanganyika. Nyumba ilipozaliwa TANU
haipo tena kama zilivyotoweka sehemu nyingi ambazo zilibeba kumbukumbu nyingi
za kupigania uhuru wa Tanganyika. Jambo la kusikitisha ni kuwa hata kabla ya
kuvunjwa jengo lile ukiingia ndani ya nyumba ile ilipokuwa ofisi ya CCM, kulikuwa
hakuna kumbukumbu yoyote ya wazalendo walioweka misingi ya kuwaunganisha
wananchi kupigania uhuru wa Tanganyika. Hapakuwa na picha za waasisi wa TAA
wala wa TANU. Hata pale Arnautoglo ambako Nyerere ndipo alipochaguliwa kuongoza
TANU pale ukumbini hakuna kumbukumbu yoyote ya uchaguzi ule muhimu si tu katika
maisha ya Nyerere bali pia kwa historia ya taifa letu. Ilikuwa katika ukumbi
ule ndipo Nyerere alipopiga hatua yake ya kwanza kuingia katika siasa na
mapambano ya wazi dhidi ya ukoloni. Lakini ikiwa tutasimama hapa kwa Nyerere peke yake tutajipunja sana. Ukumbi ule wa Arnautoglo una historia nyingine. Naomba niilete hapa.
Baada ya yale mapinduzi ya Abdul Sykes na Hamza Mwapachu walipoteka ofisi ya TAA na kuchukua madaraka kwa nguvu, Waingereza waliitisha mkutano wa pande zote mbili hapo Arnautoglo na wenyewe wakawepo. Sasa ikawa tabu kwa wanachama kuzungumza kwa uhuru na uwazi kwa kuwahofu wale maofisa Wazungu kutoka serikalini. Hapo ndipo aliposimama Schneider Abdillah Plantan, Mzulu, aliyepigana Vita Vikuu vya Kwanza akiwa katika jeshi la Wajerumani pamoja na Kleist dhidi ya Waingereza na katika Vita Vikuu vya Pili Waingereza wakamkamata na kumfunga kisiwani Ziwa Victoria kama adui. Schneider hakuwa na mengi aliwaambia Waingereza bila hofu kuwa kinachotakikana hapo na Waafrika ni uchaguzi tu. Hivi ndivyo Dk. Vedasto Kyaruzi na Abdul Sykes walivyoingia katika uongozi. Huu ndiyo ukawa mwelekeo mpya kuelekea kuunda TANU mwaka 1954. Uamuzi huu ulifanyika kwenye Ukumbi wa Arnautoglo. Hakika ukumbi ule una historia ya kipekee katika kupigania uhuru wa Tanganyika.
Naomba nimalize kwa hili.
Ukumbi ule ulijengwa na George Arnautoglo tajiri wa Kigiriki na akautoa kwa Waafrika wa Tanganyika. TANU ilipoanza Arnautoglo alitoa fedha kwa siri zisaidie chama na hizi fedha akamkabidhi Ali Mwinyi Tambwe.
Baada ya yale mapinduzi ya Abdul Sykes na Hamza Mwapachu walipoteka ofisi ya TAA na kuchukua madaraka kwa nguvu, Waingereza waliitisha mkutano wa pande zote mbili hapo Arnautoglo na wenyewe wakawepo. Sasa ikawa tabu kwa wanachama kuzungumza kwa uhuru na uwazi kwa kuwahofu wale maofisa Wazungu kutoka serikalini. Hapo ndipo aliposimama Schneider Abdillah Plantan, Mzulu, aliyepigana Vita Vikuu vya Kwanza akiwa katika jeshi la Wajerumani pamoja na Kleist dhidi ya Waingereza na katika Vita Vikuu vya Pili Waingereza wakamkamata na kumfunga kisiwani Ziwa Victoria kama adui. Schneider hakuwa na mengi aliwaambia Waingereza bila hofu kuwa kinachotakikana hapo na Waafrika ni uchaguzi tu. Hivi ndivyo Dk. Vedasto Kyaruzi na Abdul Sykes walivyoingia katika uongozi. Huu ndiyo ukawa mwelekeo mpya kuelekea kuunda TANU mwaka 1954. Uamuzi huu ulifanyika kwenye Ukumbi wa Arnautoglo. Hakika ukumbi ule una historia ya kipekee katika kupigania uhuru wa Tanganyika.
Naomba nimalize kwa hili.
Ukumbi ule ulijengwa na George Arnautoglo tajiri wa Kigiriki na akautoa kwa Waafrika wa Tanganyika. TANU ilipoanza Arnautoglo alitoa fedha kwa siri zisaidie chama na hizi fedha akamkabidhi Ali Mwinyi Tambwe.
Kushoto Dossa Aziz, Julius Nyerere, Abdulwahid Sykes na Lawi Sijaona Ukumbi
wa Arnautoglo Katika Sherehe ya Kumuaga Nyerere Kwenda UNO Safari ya Pili 1957
Hata hivyo
hatujachelewa kuinusuru historia ya Tanganyika. Nyumba ya Mzee Rupia ambayo wakati ikiwa ya Cecil Matola ndipo
ulipofanyika mkutano wa kuasisi African Association mwaka wa 1929 ipo. Fikra hii ya kuanzisha African Association Kleist aliipata kutoka kwa Dr. Aggrey alipokuja Tanganyika mwaka wa 1924 kama mgeni wa serikali kuja kusaidia tatizo la elimu kwa Waafrika wa Tanganyika. Si kazi
kubwa kwenda pale na kupachika kibao cha shaba kinachoeleza kuwa hapa ndipo
palipoasisiwa African Association na majina ya wazalendo wale yakaonyeshwa. Arnatouglo
bado ipo. Inawezekama kabisa kama nia ipo pakawekwa kibao cha kueleza kisa cha
ule uchaguzi maarufu kati ya Abdul Sykes na Nyerere. Uchaguzi wenyewe ulikuwa
wa kunyanyua mkono. “Aneamtaka Abdul Sykes anyanyue mkono.” Wajumbe wananyanyua
mkono wanahesabiwa. “Anaemtaka Julius Nyerere…” Nyumba aliyokuwa akiishi Abdul
Sykes sasa haipo badala yake kuna jigorofa kubwa. Sidhani
kama itakuwa shida sana napo kuweka kibao cha shaba na maelezo ya yote
yaliyokuwa yakitendeka pale kuanzia Chief David Kidaha Makwaia hadi Julius
Nyerere yakaandikwa na kueleza kuwa hapa ndipo alipoishi Baba wa Taifa baada ya
kujiuzulu ualimu ili aongoze TANU kudai uhuru. Soko la Karikakoo lipo ingawa si
lile la zamani. Halikadhalika hapa pia panaweza kuwekwa kumbukumbu yake. Ilala
Welfare Centre nayo ipo. Hatujachelewa ikiwa azma na utashi wa kuiokoa historia
ya nchi yetu ipo.
| Dr. Kwegyr Aggrey |
| Mwandishi Mbele ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Dodoma |
| Mwandishi Akihojiana na Balozi Abbas Kleist Sykes Kuhusu Historia ya Ukombozi wa Tanganyika |
| Ofisi Ndogo ya CCM Shrehe ya Miaka 50 ya Uhuru Pembeni ni Iliyokuwa Ofisi ya TANU |
| Ofisi ndogo ya CCM kama ilivyo baada ya kujengwa upya |

No comments:
Post a Comment