![]() |
| Ebby Sykes |
| Ebby Kwenye Msiba wa Baba Yake Mdogo Ally Sykes 20 May 2013 |
| Dully Sykes |
| Kushoto:Kleist Abdulwahid Sykes, Ebby Abdulwahid Sykes, Sauti Thomas Plantan na Abdulwahid Ally Sykes |
| Khitma Nyumbani kwa Kaka Yake Kleist Sykes |
| Jaji Joseph Sinde Warioba, Paul John Rupia na Mzee Shomari Nyuma Aliyevaa Suti Nyeusi ni Mohamed Maharage Juma "Contemporary" wa Ebby wote walikuwa Wanamuziki Katika Ujana Wao Mohamed Maharage ni Mkuu wa Itifaki, Ikulu |
![]() |
| Kushoto wa Kwanza Mohamed Maharage Juma Katika Miaka ya 1970 |
| Sheikh Mahdi Akisoma Talakini Kwenye Kaburi la Ebby |
| Mwinyi Mangara na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Said Mecky Sadiki (Katikati) Kulia kwa Mangara ni Ahmed mwinge na Kushoto ni Kube, Chande na Hussein |
| Kushoto: Abbas Sykes, Mshike, Abdul Faraj, Mwinyi Mangara na Said Mecky Sadiki |
| Baada ya Maziko |
Katika maisha yangu sijapata kuandika taazia ya mtu aliyekuwa
karibu nami. Hii itakuwa ya kwanza In Sha Allah. Hata hivyo sijui kama itakuwa
na maneno mengi kwa kuwa mengi niliyonayo ni binafsi zaidi kwa hiyo nahisi kama
hakuna ambae atataka kusoma kitu kama hicho.
Ngoja nijaribu.
Ebby alinitangulia kuja duniani kwa siku moja. Yeye kazaliwa
tarehe 24 Februari, 1952 mimi nikazaliwa siku ya pili yake tarehe 25 Februari
na mama yangu Bi. Baya biti Mohamed akalala kunizaa mimi kitanda kile kile
alicholala jana yake mama yake Ebby Bi. Regina. Nilikuja kumuona mama yetu
miaka mingi sana baadae mimi nishakuwa kijana mkubwa nyumbani kwa rafiki yangu
Yassin Idd (marehemu) Mtaa wa Bonde ambae alikuwa amemuoa dada yake Ebby,
Miski. Miski alikuwa kajifungua mtoto na mama alikuja pale kutoka Morogoro kuja
kumkalia binti yake.
Mimi na Ebby tumekuwa pamoja toka utoto wetu tukawa pamoja katika
ujana na tukawa watu wazima pamoja ingawa baada ya kutoka katika ujana kila mtu
akawa ameshughulika na maisha yake. Babu zetu hata kabla hatujazaliwa sisi wao
walikuwa marafiki na bibi zetu wakiwa mashoga. Hiyo ilikuwa katika miaka ya
1930. Ebby alikuwa Kipata karibu na New Street (sasa Lumumba) na sisi tulikuwa
Kipata ya Mtaa wa Nyamwezi. Sina mengi ya kusema kuhusu babu zetu ila kuwa
walikuwa majirani wakiishi Mtaa wa Kipata (sasa Kleist Sykes) na wote wakifanya
kazi Tanganyika Railways lakini nina kumbukumbu nyingi za bibi yake Ebby Bi.
Mruguru biti Mussa ambae shoga yake alikuwa bibi yangu Zena biti Farjalla.
Tulipokuwa watoto tukipenda sana kula kaukau. Hii ni "snack" inayotengenezwa
na unga wa ngano. Kaukau ilikuwa inauzwa katika hoteli ya Mzee Saidi. Huyu
alikuwa Mzee wa Kiyemeni na hoteli yake ilikuwa Mtaa wa Narung’ombe na
Sikukukuu.
![]() |
| Mtaa wa Kipata Kama Ulivyokuwa Katika Miaka ya 1970 Nyumba zote Hizo Sasa ni Magorofa Mimi nimezaliwa Hiyo Nyumba Baada ya Nyumba Yenya Rangi Nyeupe Nyumba ya Pili Na. 32 |
Hapo ndipo baba yake Ebby marehemu Abdulwahid Sykes, Dossa Aziz na
wanasiasa wengine walikutana kupoteza wakati. Palikuwa hakuna viti wakikaa
kwenye kigogo cha mnazi. Ebby atakwenda kwa bibi yake Bi. Mluguru kuomba hela
ya kaukau. Bi. Mluguru pale barazani kwake alikuwa na biashara yake akiuza
togwa. Siku ikiwa shetani wa kaukau katuondokea tunakwenda kumwamkia Bi. Mluguru
na yeye hatatutoa kapa. Atatupa chupa moja moja ya togwa tujiburudishe. Turejee
kwa Ebby. Punde Ebby atarudi na hela na safari itaanza kuelekea hoteli kwa Mzee
Said kununua kaukau. Ebby alikuwa kiongozi wetu na iko siku ataamua leo
tusicheze mpira twendeni sokoni Kariakoo tukaokote mabua tutengeneze miti ya
kurukia “high jump.” Ebby ndiye aliyenifundisha mimi “high jump.” Mchezo huu
tulikuwa tukifanyia kwetu Mtaa wa Gogo kwa mama yangu mdogo Bi. Mtoro biti
Mohamed, kwa kuwa kulikuwa na tifutifu. Haya yote tukifanya wakati wa likizo.
Miaka ikenda sasa tukawa vijana. Michezo ya kitoto tukaiacha. Hiki
ndicho kipindi mimi nilishakamana sana na Ebby. Huu sasa ulikuwa ule wakati Waingereza
waliuita, "The Roaring 60s." Ebby alizaliwa katika nyumba ya muziki.
Baba zake wakati wa ujana wao walikuwa na bendi iliyoitwa, "The
Skylarks." Hii ilikuwa katika miaka ya 1950 wakati sisi tunazaliwa. Ebby
katika miaka ile ya 1960 katikati yeye tayari akiwa kijana mdogo wa miaka kama
14 hivi tayari alikuwa amekwisha kuwa mpiga gitaa mzuri. Alikuwa Ebby ndiye
alinifunza mimi "chords" za gitaa. Ebby alikuwa na gitaa lililokuwa
kwao. Nalikumbuka hili gitaa aina yake ilikuwa “Gibson.” Gibson lilikuwa gitaa
mashuhuri Marekani na Marekani ya Kusini kwa ajili ya sauti yake ya kuvuma
tofauti na magita yaliyokuwa yakitumika Ulaya ambayo yalikuwa yanaitwa, “solid”
yakitoa sauti kavu, maarufu katika haya lilikuwa, “Hofner.”
Siku moja nazugumza na Balozi Mohamed Maharage nyumbani kwake
Makongo, akanambia, "Unajua Sidney (hii ilikuwa nickname yangu) wewe ndiye
ulionifunza mimi "chords.” Ebby alikuwa mwimbaji mzuri pia. Akiwaiga
waimbaji wa wakati ule - Percy Sledge, Wilson Picket, Ottis Redding na wengineo.
Mimi nilichelewa kuhama nilikokuwa wakati "Soul" ishaingia Dar es
Salaam. Mimi bado nilikuwa kwa Elvis Presley na Cliff Richard. Nakumbuka wakati
ule nikifanya mazoezi na rafiki yangu Abdul Yusuf kuupiga mwimbo wa Cliff
Richard, "You and I," wakati Ebby rafiki yangu akishika gitaa
anapiga, “Hold On,” ya Sam and Dave. Abdul Yusuf tulisoma darasa moja St,
Joseph's Convent na wakati ule umri wetu ulikuwa miaka 15. Abdul Yusuf alikuja
kuwa Aeronautical Engineer. Ebby akizisikiza "soul" kwenye
"record player," nyumbani kwao kisha akizikopi na kuzipiga kwa
"key" ile ile waliopigia wenyewe. Wakati huo baba yake, Bwana Abdul
Sykes alikuwa kajenga nyumba Magomeni Mikumi na wamehamia hapo.
| Kushoto: Kamili Mussa, Yusuf Zialor (marehemu), Abdallah Mgambo, Othmani Chande Aliyekaa Kleist Sykes, Ebby Sykes, Miriam Max, Janeth Zebedayo, Erica Kissa, Elizabeth Frisch (1960s) (Picha kwa Hisani ya Abdallah Mgambo) |
Mitaa hiyo kwa wakati ule wazee wetu wengi walijenga hapo, Chifu
Fundikira alikuwa na nyumba Mikumi, Mzee Mzena, Chihota, Mzee Amri, Mzee Mgone,
Mzee Muhuto, Ally Sykes, Abbas Max, Mzee Mwakinyo ili muradi mitaa hiyo ilikuwa
na uchangamfu wa aina yake kwa ajili ya watoto wa wazee hawa, wa kike na wa
kiume. Sisi tuliokuwa tukiishi, Upanga, Karikoo, Temeke na kwengineko mchezo
wetu ulikuwa Mikumu na tukapaita, "Soulville." Hii ni kwa sababu
wakati ule muziki uliokuwa ukitamba dunia ulikuwa "soul" na bingwa wa
"soul music," alikuwa James Brown. Ikawa sasa tukijifunza kupiga
muziki kwa staili ya Motown. Hii ndiyo ilikuwa “record label,’ mashuhuri ya
muziki wa “soul,” kutoka Detroit. Miaka mingi sana baadae naingia Marekani na
“entry point” yangu ilikuwa Detroit. Nilipokuwa nimesimama kwenye foleni
kusubiri kugonga pasi yangu, fikra zangu zilinirudisha nyuma sana.
| Kushoto: Adam Kingui, Vuli, Ebby Sykes, kwenye drums Khalid, Kulia Bob Dean, Nasser (Mick Jagger), Choge Sly |
Siku ya Jumatano shule mwisho saa sita. Hiyo ndiyo ilikuwa siku
tunakutana Magomeni Mikumi nyumbani kwa akina Mohamed “Captain Mike” kufanya
mazoezi ya nyimbo zetu. Ebby siku zote alikuwa "centre stage." Huu
ndiyo wakati Adam Kingui, katika vijana waliokuwa na kipaji kikubwa cha muziki
akiwa na kundi la The Rifters pamoja na Simon Ngocho (Simon alikuja akawa Civil Engineer) sasa ni
marehemu, Mohamed Ali Abbas (marehemu), Vuli kijana kutoka Afrika Kusini, Nassoro maarufu kwa jina la Mick Jagger, na vijana wengine siwakumbuki. Leo nikiangalia nyuma naona wakati ule ulikuwa
mgumu sana kwetu lakini sioni sababu ya sisi kujilaumu tulikuwa tunaitika
mazingira ya wakati uliokuwapo. Miaka ya 1970 tunamaliza sekondari. Sasa
tunaanza kuwa na akili zilizotulia. Ebby akaenda Mombasa kujaribu bahati yake
katika muziki. Hakukaa sana Mombasa akenda Piraeus Greece. Huo ulikuwa wakati
vijana wengi wanatafuta kazi ya ubaharia. Ebby hakukaa sana Ugiriki akarudi Dar
es Salaam. Miaka ikapita...
| Kushoto: Dimitri, Vyas, Kleist Sykes, Abdallah Mgambo na Adam Kingui 1965 |
Ebby alikuwa mpole lakini alikuwa na uwezo mkubwa wa kumdhibiti
mbabe yoyote. Siku zile za madansi ya mchana tukiita "Boogie," tukimaliza dansi wakati wa kurudi
nyumbani tunachokozana. Kulikuwa na “gang,” za vijana wa Temeke, Magomeni na
kwengineko. Ukiwa umefuatana na Ebby jua uko salama. Wababe wakimjua hivyo
wakimfanyia staha. Ebby Mungu alimjaalia mshipa wa kula. Alikuwa anaweza kula
sana kiasi ilikuwa zamani tukienda kula chips haikuwa ajabu Ebby kupiga sahani
mbili za chips kwa samaki au kuku peke yake kisha akashushia na soda. Nakumbuka
siku moja naingia kwenye kimgahawa kimoja kilikuwa Maggot hii ilikuwa hoteli
maarufu katikati ya mji. Ebby alikua ameshaniona toka nakuja akawa kapiga oda
yangu. Nafika tu tunasalimiana muhudumu namuona ananiwekea kilima cha kababu.
Mimi nimeshangaa. “Ebby akanambia, “Sidney yako hiyo nimekuodea.” Sasa nikaanza
kulalamika kuwa siwezi kumaliza na nini. Ebby hakusema kitu. Alinyanyua ile
sahani yangu akajipunguzia kababu kwenye sahani yake ambayo tayari ilikuwa ni
kilima akaendelea kula.
Buriani ndugu yangu, rafiki yangu Ebby. Si haba Allah katukadiria
umri wa kutosha na tushukuru kwa hilo. Miaka 63 si haba ingawa mwenzangu ulibakisha siku tisa tu kukamilisha hiyo miaka 63.
Allah akuweke mahali pema peponi.
Amin
| Ebby na Mimi 2010 |


.jpg)
No comments:
Post a Comment