Tuesday, 17 February 2015

Imekuwa Hamkani Sio Shwari Tena Kituo Kikuu cha Daladala Kuhamia Kiswandui Na Ben Rijal


Imekuwa Hamkani Sio Shwari Tena
Kituo Kikuu cha Daladala Kuhamia Kiswandui
Na Ben Rijal
Hamkani sio shwari tena, kumekuwa hakukai sawa na kila kukicha yanakuwa hayo kwa hayo maji ya futi na nyayo. Kusema kweli tunaambiwa kuwa ili tuweze kuendelea na kujua hapa tulipo kama kuna mustakbala mwema huko mbele ni muhimu kuzingatia kufanya utafiti katika nyanja mbalimbali kuanzia kilimo, afya, kijamii, mazingira, elimu, mawasiliano, n.k.

Tafiti nyingi za nchi za Ki-Africa zinakosa kupatiwa fedha za kutosha na matokeo yake huwa kinyume na matarajio ya matokeo ya hizo tafiti, inaelezwa kuwa kila kukicha katika nchi za Africa badala ya kuongezewa bajeti za tafiti matokeo yake huwa fedha za tafiti hupunguzwa. Kwa mfano nchini Africa Kusini nchi ambayo ina uchumi imara kati ya nchi za Ki-Africa mwaka wa 2014 iliripotiwa kuwa fedha za kufanyiwa tafiti zimeporomoshwa na serikali kuu kwa asilimia 0.71 kutokana na pato la kila mtu (GDP),  unaposikia haya unapata kiwewe na kujiuliza Africa inaelekea wapi?

Najaribu kuzungumzia tafiti kijuu juu kwasababu mengi yanayotupeleka kombo nikutokana kuwa hatufanyi tafiti, tunaulizana kwanini siku hizi Polisi wamekuwa wakimkamata mtu huanza kumtwanga vya kutosha hata akifika kituoni huwa yupo hoi au kama huku tusemavyo chicha kabisa. Kuna sababu ya haya kutendeka na ili tuweze kupata jawabu kunatakiwa kufana utafiti, suala la magari ya daladala kupiga nyimbo kwa sauti kubwa na madereva wake kuuweka uhuni mbele koliko ustaarabu, kwanini yanakuwa hayo?

Kuna sababu ulufu ndani yake, wakati mmoja nchini Kenya waliwahi kufanya utafiti juuya  makondakta na maderva kujua kwanini wanafanya mambo yalio sio ya kikawaida, tafiti ilikuja kufichua kua zaidi ya asilimia 80 kati ya madereva na utingo wa matatu  huwa wanavuta bhangi. Nchini India walikuja kupata soko la kuuza vyura nchini Sweden na vyura vyote vilikuja kutokomea katika mashamba ya mpunga, wakulima walipata tija ya muda mfupi, bada ya mwaka tu, uliingia ugonjwa wa mpunga kukunyaa na kushindwa kuvunwa, utafiti ulipofanyika ilikua kujulikana sababu ya maradhi hayo kua vyura walikuwa wakila bakteria ambao bakteria hao ndio waliokuja kuleta madhara,  kwa kukosekana kukuweko kwa vyura bacteria wakaja juu na kuogezeka na kushambulia mpunga. Tafiti ni muhimu sana sana na kukosekana kufanyika tafiti matokeo yake ni kuendelea kuwa na kilema kisichoponyeka ikiwa kilema hicho kinaponyeka.

Nimejaribu kujenga hizi hoja kutokana na azma ya makala haya juu ya kituo cha Daladala kilichohamishwa kutoka hapo Darajani na kuhamishiwa Kiswandui na eneo hilo lilokuwa kituo cha daladala hivi sasa ni sehemu ya kuegesha magari ambao watu hutozwa ada. Nitanena kama wanenavuo wengine  kunena kuwa kuondolewa kwa kituo cha Darajani kulifanyika pasina kufanywa utafiti ila tu jazba na utashi wa wahusika ndio walikurukupa na matokeo yake kwa sasa kuwa kuna kila aina ya adha, baa na belwa mtaa wa Kiswandui.

Kama wakuu wa Baraza la Mji wangefanya utafiti ingebidi kubakia na kituo kile cha Darajani na huku wanatafuta njia nyengine ya kudumu, lazima mwenye kuhusika na watu ajuwe idadi yao ni wangapi na wangapi wenye vipando vyao hawategemei vipando vya Umma na wangapi wanatumia magari ya serikali n.k.

Aidha mtafiti anaangalia kukua na kuongezeka kwa watu nini kinahitajika kufanyika, kwa mfano kisiwa cha Zanzibar katika mwaka wa 1964 idadi ya watu wake ilikuwa ni watu laki tatu (300,000) lakimbili ikiwa imestakimu Unguja na laki moja ipo Pemba na kutokana na Sensa iliopita ya mwaka wa 2012 inatueleza kuwa idadi ya watu wa Zanzibar kwasasa ni Milioni moja na laki tatu (1,300,000) ongezeko hili la watu linaingia katika masafa yaleyale ya kisiwa ambacho watu wameongezeka lakini masafa ya kisiwa ndio yale yale au unaweza kusema hata yanapungua kwani tunafahamishwa kuwa kuna maeneo yasiopungua 125 yamevamiwa na maji ya chumvi baadhi ya maeneo hayo yalikuwa ni ya kilimo, mengine ni makazi ya watu.

Katika miaka ya sitini kituo hicho cha magari kiliopo Darajani kilikuwa kinapokea  magari kwa siku nzima magari yasiozidi 15 yakiwa ya Makunduchi mawili, Fuoni moja, Jumbi mawili, Nungwi moja, Mkokotoni moja, Kizimkazi moja, Chwaka moja, Ndijani moja, Bumbwini, Mangapwani moja, Bwejuu moja, Matemwe moja n.k hio ni miaka ya sitini. Kwa mfano gari kutoka Makunduchi likiingia mjini linabakia hapo hadi mchana ndio linarudi huwa na safari moja tu kwa siku, leo gari hizo zinafanya hata safari tatu kwa siku kutokana na mahitaji ya watu. Magari yameongezeka kutokana na idadi ya watu kuongezeka ambao wanahitajia usafiri mathubuti, kwa siku ingia toka ya magari hapo Darajani yanafikia idadi ya magari mia na khamsini au nazaidi.

Kituo cha Darajani kilikuwa kinachukua abiria wa Bububu, Saateni, Mwanakwerekwe, Kiembe Samaki, Chukwani, Mombasa, Amani, Daraja bovu n.k. Kwamatafiti atapotaka kukiondosha kituo kama kile cha Darajani kwanza atatafakari kujua anahamisha kukipeleka wapi? Atataka kujua kwa wastani wa magari mangapi kwa siku yanaingia hapo kituoni, ataangalia katika saa magari mangapi yanaingia na ni wakati gani kunakuwa na abiria wengi wanaovutana kutaka usafiri.

Baada ya kujiuliza hayo anakuchukua takwimu na kuzichambua na jawabu atakayoipat atachokifanya ni kujaribu kukihamisha gari la eneo moja tuseme Mwanakwerekwe atakihamishia kwa muda sehemu moja kisha atapima adha na urahisi wa abiria na atapata sura halisi bada ya majaribio hayo kusema kupunguza msongamano wa Darajani itakuwa vyema kuhamisha magari yaendao Kiembesamaki, Mwanakwerekwe na Chukwani kuwahamishia sehemu ya iliopata kuwa Baraza la wakilishi au tuite jina lilozoeleka Peoples Club.

Mtafiti huyo hatosita hapo bali atatoa na Dodoso au tuite Hojaji (Questionnaire) kuwauliza abiria wanaokusanyika hapo nini mapendekezo yao juu ya kuhamishwa kituo. Zaidi ya hapo wahusika ambao ni wa Baraza la Mji watatakiwa wakae na watu wa Mipango Miji na Vijiji kuangalia njia iliokuwa mbadala, isitoshe watatakiwa wafanya vipindi vya Radio na TV kuwaelimisha wananchi kuweza kufahamu sababu ya kuhamishwa kwa kituo hicho na wao watasema nini kuhusu uamuzi huo? Watafiti hao hapo tena ndipo watapokuja na suluhisho ambalo litakuwa la kisayansi kabisa lisioleta adha.

Waswahili wana msemo wao ambao mie nitausema kwa njia ya tarwia nayo ni unaruka kukimbia kukanyaga haja ndogo huku unakanyanga kinyesi. Ikiwa ilikuwa kupunguza kelele na adha kwa skuli za Darajani na Vikokotoni basi kituo hicho kimehamishiwa kwenye skuli ya Kiswandui ambayo hapo ndipo panapotakiwa kuwepo utulivu wa hali ya juu kwani wale watoto taahira (Mongoose) ndipo wanaposoma aidha Makao Makuu ya Chama cha CCM ndipo yalipo. Lakujiuliza ndio kipi kilichofanyika? Jengine ambalo linawapa watu mashaka nikuona kituo kilekile cha Darajani kilichofikiriwa kunampango mwengine unataka kuratibiwa sasa kinaegeshwa magari ya watu binafsi na kutozwa shilling alfu moja kwa saa, aah, hii ni Hamkani Sio Shwari Tena.
Abiria wa daladala wapo tafshanini hawajui la lufanya hawajui la kutenda inagwa wamegubikwa na maudhi ambayo hawajui jawabu yake litatokana na nini wapo wanaona ni Hamkani isiokuwa na ushwari.

Narudia tena utafiti ni jambo la muhimu, ikiwa watu wataongezeka kila kitu cha mahaitaji juu ya watu hao nacho kitaongezeka, sasa watu wameongezeka na magari yameongezeka, afana alek unaingia mjini hujui wapi uegeshe gari lako utapata upenyu uliweke utakuja kukuta umeshatiliwa chuma na hao hao watu wa Baraza la Mji ulipe alfu kumi ndio ufunguliwe gari yako upate kuondoka na wiki iliopita magari yakibebwa juu kwa juu sijui yakipelekwa wapi? Unajiuliza hawa wahusika wamefanya tafiti? Wametembea nchi za visiwa kama Mauritius na Seychelles wakaona taratibu za wenzetu wazifanyazo? Nimeshuhudia kule Mauritius hata hizo sehemu za pembeni ambazo huku kwetu ni dhambi kuegesha gari huko wao huegesha na zimeekewa michoro wa ukomo wa gari za kuegeshwa, wenzetu hao wa visiwa walikuja na fikra hizo kwa kujua wao ni watu wa visiwa na vipi ardhi ilivyokuwa inapungua, wakajiuliza  vipi wataweza kuondoa adha na kuwa na matumizi bora ya sehemu ndogo ya ardhi walionayo.

Hapa Unguja imekuwa mashaka na adha baina ya wenye vipando na watu wa Baraza la Mji. Jengine ambalo halijafanyiwa utafiti ni kuona kuwa baada ya kuchwa jua bado watu hao wa Baraza la Mji katika eneo la Forodhani wanaendelea kukusanya fedha za maegesho pamoja na siku za mapumziko jambo hilo halipo popote pale duniani, ndio nikasema Hamkani Sio Shwari Tena mambo yapo mchafu koge, msege mnege.

Tatizo la kuegesha magari katika maeneo ya mjini na Darajani ni adha tupu, bado nawanasihi wakuu wa Baraza la Mji kufanya utafiti wa juu ya suala hili, watafiti Alhamdulillahi wamejaa kama pishi ya mchele iwe SUZA, Chuo cha Fedha ChChwaka, Chuo cha Elimu Chukwani, Zanzibar University hata  watafiti mmoja mmoja wanaweza kusaidia pakubwa, jambo hili linahitajia kuangaliwa kwa makini kwani linawakosesha utulivu wakazi wanaotegemea vipando vya daladala.

Wakazi wa Kiswandui hawana raha kuanzia asubuhi ya saa moja hadi nne ya usiku kwa makelele na moshi wa magari wanajiuliza hayo yataendelea mpaka lini? Watoto wao wamo kujifundisha matusi yanayoporomoshwa na madereva na utingo, wanapambana na uchafuzi wa mazingira ya moshi na maeneo hayo kwa kuwa hayana vyoo vya kwendea haja ndogo watu hujikojolea ovyo, wakazi wa Kiswandui hujiuliza “tumekosa nini?” Mie nitawambia hamjakosa kitu wala hamtiwi adabu bali tafiti zimeonekana sio lolote wala sio chochote kile amua, amua twende mbele ndio hayo yanayowatesa wakazi hao.

Tabu ya watu wetu nayo nikuwa wanashindwa kuhoji kila kitu utasikia kimeandikwa sijui kimeandikwa na nani na hio kamwe sio Tawhidi. 

Aaah Hamkani Sio Shwari Tena.


No comments: