Sheikh Ali bin Hemed Al-Buhry
JAMII YA TANZANIA NA
MAHAKAMA YA KADHI:
TANZANIA INAANZA
KUVUNA MATUNDA YA KUIKATAA HISTORIA YA KWELI
Mohamed
Said
Mtu yoyote hii leo ikiwa
ataingia katika mitandao ya kijamii na kusoma mjadala unaofanyika kuhusu
Mahakama ya Kadhi ni lazima atapata mshtuko mkubwa kutokana na lugha kali na
wakati mwingine matusi kati ya hao wanaojadiliana. Kila upande ukitupa shutuma
na maneno makali dhidi ya upande mwingine. Ukipitia majadiliano yote kitu
kimoja kinachojitokeza wazi na dhahiri kabisa ni kuwa kuna mpasuko mkubwa kati
ya Waislam na Wakristo kuhusu Mahakama ya Kadhi. Chuki na uadui sasa upo wazi
bila kificho. Hili linawezekana vipi wakati viongozi wetu wanatuambia kuwa Baba
wa Taifa alituachia misingi imara ya umoja? Wahenga wamesema dalili ya mvua ni
mawingu. Suali la kujiuliza ni hili, wapi sisi kama taifa tumejikwaa? Wengi
katika hao wanaojadili hiyo Mahakama ya Kadhi ukweli ni kuwa hawaijui vyema
historia ya Tanzania au ukipenda Tanganyika. Wengi katika hawa waliojizinga
katika malumbano haya baadhi ni watu wazima walio na umri zaidi ya miaka 50 na
vijana ambao wamezaliwa baada ya Tanganyika kupata uhuru wake mwaka 1961.
Mjadala unafanyika katika mazingira ya ujinga wa kutojua historia. Sasa hapa linakuja swali imekuwaje kuwa watu
hawa ambao kwa sasa ndiyo wengi katika jamii yetu hii leo hawaijua historia ya
nchi yao? Vipi tumekuwa na Chuo Kikuu kwa karibu ya nusu karne na sasa vimeongezeka
vingine vingi lakini hadi sasa ikawa historia yetu ni ya kubabaisha haijakaa
sawa hadi leo? Mimi sitatoa jibu kwa sasa ingawa jibu ninalo. Huko vyuoni ni
historia gani inasomeshwa ambayo inawafanya watu wasijijue?
Baadhi ya wachangiaji
katika hiyo mitandao ya kijamii na inaelekea hao ni Wakristo wanasema iweje
Mahakama ya Kadhi igharimiwe na serikali ilhali serikali hii haina dini?
Waislam wanaleta jibu wakisema mbona serikali inatoa mabilioni kila mwaka kwa
makanisa kuhudumia taasisi zao kupitia “Memorandum of Understanding (MoU)?” Kwa
wale ambao labda hawaujui huu mkataba ni kuwa mwaka wa 1993 Serikali ya
Tanzania ilitiliana sahihi mkataba na makanisa, mkataba uliokuja kujulikana
kama Memorandum of Understanding. Makubaliano ambayo serikali iliridhia na kuidhinisha
elimu, huduma za jamii na afya ziendeshwe na Christian Council of Tanzania
(CCT) na Tanzania Episcopal Conference (TEC) kwa kushirikiana na serikali.
Mkataba huu ulitayarishwa na Dr. Costa Mahalu, wa Kitivo cha Sheria Chuo Kikuu
Cha Dar es Salaam na ukatiwa sahihi na Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri
Mkuu, Edward Lowassa. Kikubwa katika mkataba huu kwanza ni ule usiri uliogubika
mpango mzima na pili ni kuwa ulitiwa sahihi bila ya kuwashirikisha au
kuwafahamisha Waislam. Ili makubaliano haya yaweze kutekelezeka, serikali
ilibidi ifanye marekebisho kifungu 30 cha Education Act No. 25, 1978. Katika
mabadiliko haya kuletwa Bungeni ndipo Waislam wakajua kuhusu hii MoU kati ya
Serikali na Makanisa.
Suali lingine la kujiuliza
ni inakuwaje jambo zito kama hili lilipitishwa na Bunge letu bila kipingamizi? Suala
hili limepita kwa kuwa Waislam Bungeni waliamini kuwa uamuzi huo una maslahi na
taifa letu? Au limepita kwa kuwa Waislam katika Bunge ni wachache wameelemewa na
ndugu zao Wakristo kupelekea kuwa sasa hawana sauti kwa uchache wao? Ikiwa huu
ndiyo ukweli wenyewe, tumefikaje hapa na nini athari ya jambo hili kwa mustakbali
wa taifa letu? Kwa uchache unaweza mtu ukajiuliza kwa nini basi serikali hiyo
hiyo haikuja na mpango wowote hata kama si sawa na ule wa Makanisa wakatoa
fedha kwa taasisi za Kiislam na wao wajiletee maendeleo kama hayo ya Makanisa? Mimi
sitatoa jibu ingawa majibu ninayo. Kwa kuhitimisha hebu tujiulize kwani
Mahakama ya Kadhi ni kitu kipya katika nchi hii kiasi cha kusababisha mtafaruku
huu ambao hivi sasa tunaushuhudia?
Ukweli ni kuwa ukoloni
umeingia Tanganyika umekuta Waislam wakijihukumu kwa kitabu chao. Mmishionari Johan
Krapf kaja Tanganyika na alipokelewa na Chifu Kimweri wa Usambaa mwaka 1848.
Krapf alipokelewa kwa ukarimu wa hali ya juu na alimkuta Chifu Kimweri Muislam,
anajua kusoma na kuandika kwa herufi za Kiarabu akihukumu katika barza yake
iliyokuwa Vuga. Ni wazi kuwa Chifu Kimweri hakuwa anahukumu kutoka, “Order in
Council,” kutoka India kwani Waingereza walikuwa bado hawajafika. Chifu Kimweri
alikuwa anahukumu kwa sheria kama walivyohukumiana Waislam katika ukanda wa
pwani ya Afrika Mashariki kwa miaka mingi. Mimi nimekuwa na kupata fahamu
katika Tanganyika ya 1950/60 na nina kumbukumbu za hizi mahakama za kadhi na
baadhi ya hawa mahakimu nimewaona kwa macho yangu aidha wakiwa katika mahakama
wakihukumu na wengine nimewaona mitaani na wengine nimewaona wakisuhubiana na
wazee wangu. Namkumbuka Sheikh Abdallah Simba kutoka Songea. Nikifumba macho ni
kama vile namuona Sheikh Abdallah Simba. Alikuwa kija Dar es Salaam na Land
Rover yake mwenyewe na siku zote akivaa kanzu, koti na tarbush. Sheikh Abdallah
Simba alikuwa na watoto wawili Bi.
Habiba na Mwajuma. Bi Habiba alikuwa na umri sawa na mama yangu na alikuwa ‘’nurse’’
Princes Princess Margret Hospital (sasa Muhimbili Hospital) lakini Mwajuma yeye
alikuwa makamu ya dada yangu mkubwa. Mwajuma akisoma St. Joseph’s Convent
School (sasa Forodhani). Sheikh Abdallah Simba alikuwa akihukumu katika
mahakama huko Songea kwa sheria za Kiislam na akifahamiana na babu yangu Salum
Abdallah toka ujana wao katika Dar es Salaam ya 1920. Sheikh Abdallah Simba
akiishi Songea lakini alikuwa na nyumba mbili moja Mtaa wa Kipata (sasa Mtaa wa
Kleist Sykes) nyingine Mtaa wa Somali (Sasa Mtaa wa Omari Londo). Majina ya
mitaa hii ilibadilishwa kuwaenzi wazee hawa Kleist Sykes na Omari Londo
walioacha alama katika historia ya uhuru wa Tanganyika.
Kulikuwa na Sheikh Said
Chaurembo akihukumu katika Mahakama ya Kariakoo. Sheikh Said Chaurembo alikuwa
katika Kamati Ndogo ya Siasa ya TAA (TAA Political Subcommittee) mwaka 1950.
Kamati hii chini ya Mufti Sheikh Hassan bin Amir ilifanya makubwa katika
kujenga mazingira ya kuunda TANU mwaka 1954 na kumweka Mwalimu Nyerere katika
uongozi wa kudai uhuru lakini hapa si mahali pake kuyaeleza hayo. Huyu Sheikh
Said Chaurembo alikuwa na nduguye akiitwa Iddi Chaurembo huyu ndiye baba yake Sheikh Abdallah Chaurembo na wakati ule
Sheikh Abdallah Chaurembo alikuwa mwanafunzi katika chuo cha Mufti Sheikh
Hassan bin Amir. Sheikh Said Chaurembo ndiyo aliyekuwa na lile ghorofa maarufu
Mtaa wa Msimbazi na Congo linalojulikana hadi leo kama Ghorofa la
Chaurembo. Kwa kumalizia kuhusu hizi
mahakama hapa Dar es Salaam napenda kueleza kuwa katika miaka ya 1960 baada ya
uhuru Sheikh Kassim Juma alikuwa akihukumu katika Mahakama ya Kadhi Mkwajuni
hadi mahakama hizo zilipovunjwa na serikali mwaka 1963. Sheikh Kassim Juma na
yeye ana historia kubwa katika siasa za Waislam, BAKWATA na serikali baada ya
uhuru.
Sheikh Abdallah
Chaurembo akiwa msomi wa dini ya Kiislam alihusika sana katika harakati za
kudai uhuru wa Tanganyika. Sheikh Abdallah Chaurembo alikuwapo katika mkutano
wa TANU uliofanyika Mtaa wa Pemba usiku mmoja mwaka 1955 agenda kuu ikiwa vipi
TANU itapunguza joto kali la Uislam ndani ya chama ili kupunguza ile taswira
kuwa TANU ni chama cha Waislam. Jambo hili lilikuwa muhimu ili kumwezesha Mwalimu
Nyerere kuongoza harakati za kudai uhuru kwa utulivu. Pamoja na Sheikh Abdallah
Chaurembo katika mkutano ule alikuwapo Sheikh Nurdin Hussein na Rajab Diwani
lakini mzungumzaji mkuu na aliyesukuma agenda hii ikakubaliwa na TANU na kutoa
azimio alikuwa Mufti Sheikh Hassan bin Amir. Azimio lenyewe lilikuwa yeyote
atakaeleta udini katika TANU “atatoswa.” Ningependa sana kueleza historia hii
lakini nachelea itakuwa nje ya maudhui. Lakini mtu unaweza ukajiuliza vipi
katika historia ya uhuru wa Tanganyika majina haya hayasikiki kutajwa? Haiyumkiniki hata kidogo kuwa wazalendo hawa
walipigania uhuru wa Tanganyika ili waiweke kwenye madaraka serikali ambayo
itakuja kuvunja misingi ya dini yao.
Tanga kulikuwa na
Mahakama ya Kadhi na mahakama hii ilikuwa katika jengo la TAA Barabara ya 7 ambako Kadhi, Sheikh Ali bin
Hemed Al-Buhry alihukumu jamii ya Waislam kwa kutumia sharia. Huyu Sheikh Ali
bin Hemed Al Buhry ndiye baba yake Sheikh Mohamed Ali Al-Buhry na yeye ndiye
alikuwa hakimu wa mwisho kwenye mahakama hiyo. Sheikh Mohamed Ali Al-Buhry alikuja
baadae katika miaka ya 1968 kuhusika sana katika BAKWATA na kuna kisa cha
kusisimua sana kati yake na serikali katika siasa za Waislam na BAKWATA lakini
hapa si mahali pake kueleza makasa huu. Hapo Tanga kulikuwa na Liwali Abdallah
Rished na mtaa aliokuwa akikaa ulipewa jina la Liwali Street kwa heshima yake.
Baada ya uhuru ukaitwa Makoko Street kwa heshima ya mpigania uhuru na
mwanachama shupavu wa TANU Rashid Makoko. Kulikuwa na Sheikh Seif Nassor
Alhinawy ambae alikuwa Akida pale Tanga na akihukumu kwa sheria. (Akida Seif
ndiye baba ya wachezaji mpira mashuhuri katika miaka ya 1960 hadi 1970, Hemed
Seif, Marshed Seif na Rashid Seif ambao ukimtoa Marshed wote ndugu zake waliva
jezi ya taifa). Kwa kuthamini taasisi
hizi za Kiislam kuna mtaa Waingereza waliupa jina Akida Road (sasa Mkwakwani
Road) kwa heshima ya Akida Seif Nassor. Katika
Tanganyika Tanga ndiyo moja ya miji iliyokuwa na historia nzuri sana ya Mahakama
ya Kadhi. Mwanzo wa miaka ya 1900 kulikuwa na Kadhi Omar Stambuli kisha akaja
Kadhi Ali bin Hemed Al-Buhry, Liwali Abdulrahman bin Ali Diwani, Liwali Rished
Abdallah, Omar Stambuli, Juma Mwindadi , Said bin Ali Al-Buhry (OBE), Mohamed
bin Ali Al-Buhry. Masheikh hawa baadhi yao walifanya kazi ya ukadhi Tanga na
wengine walikuwa Moshi, Arusha, Mwanza na kwengineko Tanganyika.
Tabora Sheikh Bilali Ali Mshoro alikuwa akihukumu kwa sheria mahakamani. Huyu Sheikh Bilali Mshorwa
akifahamiana vizuri sana na babu yangu, Salum Abdallah pale Tabora kwani wao
ndiyo walikuwa wanamji na wazee wa mjini wakati wao. Hapo hapo Tabora alikuwapo Ramadhani Nasibu na yeye vilevile alikuwa liwali. Moshi kwa Wachagga
alikuwapo Liwali Mussa Minjanga akihukumu Bomani. Liwali Mussa alikuwa
akifahamiana na baba yangu na mtaa aliokuwa akiishi Liwali Mussa Minjanga toka
enzi hizo za ukoloni ulikuwa ukijulikana kama Liwali Street na jina hili
limebaki hivyo hadi hii leo. Hali ilikuwa hivi Tanganyika nzima na Mahakama ya
Kadhi haikupata kuwa katika agenda ya kufutwa uhuru utakapopatikana. Nini
kilifanya serikali mwaka 1963 ivunje mahakama hizi? Jibu ninalo lakini
sitalitoa kwa sasa.
Kuna watu wanasema ati
kuwa na Mahakama ya Kadhi itavunja umoja wa taifa letu. Hapa linakuja swali
kwani Tanzania huo umoja unaozungumziwa tunao hivi sasa? Mbona kumekuwa na
malalamiko mengi tu kutoka kwa Waislam kuwa serikali ina udini na inawabagua?
Hii ilianza kama manung’uniko ya chinichini kwa miaka mingi na mwisho ikaibuka
kwa sauti kubwa kuwa nchi yetu inatawaliwa na “Mfumokristo” yaani nchi inaendeshwa kwa maslahi ya Kanisa. Mwaka wa 2012 Waislam
walifanya mikutano nchi nzima wakitahadharisha kuhusu hili. Video za mikutano
hii imezagaa nchi nzima na kwenye mtandao. Bahati mbaya hadi leo serikali
imekuwa kimya. Labda mtu unaweza kujiuliza kwa nini serikali imekuwa kimya kwa
shutuma nzito na za hatari kama hizi? Imekaa kimya kwa kuwa yanayosemwa na
Waislam hayana ukweli na ithibati yoyote au iko kimya kwa kuwa inaogopa kulifingua
Sanduku la Pandora? Jibu la swali hili vilevile ninalo. Nadhani msomaji wangu
angalau kwa mbali umeweza kusoma angalau kwa muhtasari historia ya nchi yetu
ilivyokuwa. Vipi tumejikuta katika huu uhasama tunaoushuhudia hivi sasa hii ni
mada ya kujitegemea na In Sha Allah tutaizungumza.
Sheikh Nurdin Hussein na Julius Nyerere baada ya miaka mingi baada ya uhuru kupatikana mwaka 1961 |
Tuesday 3 February 2015
MAHAKAMA YA KADHI KUTOKA UKOLONI HADI TANGANYIKA HURU
About Mohamed Said Historia, Siasa na Maendeleo Tanzania
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment