TAMKO LA TAASISI
11 ZA KIISLAMU KWENYE MAENEO AMBAYO YAMEPOTOSHWA NA MATAMKO YA BAADHI YA
TAASISI ZA KIDINI NA MAGAZETI IKIWEMO MAASKOFU, BAKWATA NA GAZETI LA MIZANI
KWENYE MCHAKATO WA KUTOA MAONI JUU YA MUSWADA
UNAOHUSU MAHAKAMA YA KADHI
Utangulizi
Sisi
waislam, kupitia Jumuiya na Taasisi zetu za Kiislamu chini, tumepitia matamko
kadhaa yaliyotolewa na taasisi mbalimbali, watu binafsi, viongozi wa serikali
na magezeti, hususan, maaskofu, jukwaa la Wakristo Tanzania, gazeti la Mizani,
Sheikh Jongo na Sheikh Mohammed Idd kutia kipindi cha Ar-risala kinachorushwa
na Kituo cha TV cha Channel 10.
Matamko
hayo yana malengo ya kupotosha baadhi ya maeneo ya maoni yaliyotolewa na Waislamu,
kupitia Jumuiya na Taasisi zao kuhusu muswada wa marekebisho ya sheria yanayohusu
mahakama ya kadhi kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge
ya Katiba, Sheria na Utawala tarehe 19/01/2015.
Muhtasari wa Maoni ya Taasisi
Kumi na Moja
Kwa muhtasari maoni ya Waislamu ambayo matamko tuliyoyataja hapo juu yanalenga kuyapotosha
yalibainisha makosa, kasoro na udhaifu mwingi ulioko kwenye
muswada unaohusu Mahakama ya Kadhi kiasi cha kutia shaka juu ya uthabiti wa nia
ya Serikali wa kutaka kuleta sheria itakayowezesha mfumo wa utoaji haki wa sheria
za Kiislamu kufanya kazi hapa nchini kwa ufanisi zaidi kulio mfumo wa sasa
unatoa nafasi kwa maafisa wa mahakama kama majaji na mahakimu kuhukumu masuala
ya sheria za Kiislamu ambapo mara nyingi maafisa hao hawana sifa, ujuzi,
maarifa na uzoefu wa kushika nafasi ya kuhukumu chini ya utaratibu wa sheria za Kiislamu.
Maoni hayo, ya Waislam, kupitia
jumuiya na taasisi zao Kumi na Moja, yalidhihirisha dosari kubwa kwenye muswada
huo kwenye maeneo yanayohusu, kutokuwepo kwa kifungu kinacho anzisha na/au
kuitambua Mahakama ya Kadhi; kutokuwepo muundo wa mahakama ya kadhi
inayokusudiwa; kutoelezwa sifa za kadhi; upungufu kwenye utaratibu wa uteuzi wa
makadhi; kukosekana maelezo ya ajira na usalama wa ajira ya makadhi; mapungufu
yanayoambatana na kuweka mamlaka ya kutengeneza kanuni za mahakama ya kadhi kwa
‘Mufti’ na ya kukazia hukumu kwa Waziri; kukosekana kwa utaratibu wa kudhibiti
nidhamu, mwenendo na maadili ya makadhi; mapungufu kwenye uwigo wa mamlaka wa
mahakama; hiyari kwa mdaawa Muislamu kufungua shauri lake la sheria ya Kiislamu
katika Mahakama ya Kadhi; upungufu wa dhana ya Mahakama ya Kadhi
kujiendesha; mamlaka ya Waziri kutoa
matamko ya sheria za Kiislamu; na ulazima wa Mahakama ya Kadhi kutajwa kwenye
Katiba.
Kwa hoja hizo, Waislamu kupitia
taasisi zao hizo Kumi na Moja, walishauri kwa kupendekeza muswada mbadala
kwamba serikali iuondoe muswada huo ili uboreshwe kabla ya kuwasilishwa bungeni
kwa mjadala.
Upotoshaji Uliofanywa na
Matamko Yaliyotolewa
Upotoshwaji
wa maoni ya waislamu yaliyotolewa kupitia taasisi zao kumi na moja, uliofanywa
na matamko yaliyotolewa na taasisi mbalimbali, watu binafsi, viongozi wa serikali
na magezeti, umejikita kwenye maeneo haya ya fuatayo: (i) Kuwa taasisi 11
zilizowasilisha maoni ya Waislamu juu ya muswada wa mahakama ya kadhi zinawakilisha
wachache; (ii) Kuwa asasi hizo 11 ni za Wahabi na hivyo maoni yao hayawakilishi
waislamu wote; (iii) Kuwa Mufti ndiye kiongozi mkuu wa Waislamu; (iv) Kuwa
Mufti ndiye anastahiki kuteua makadhi; (v) Kuwa BAKWATA ndiyo taasisi baba,
nyingine watoto wake; na (vi) Kuwa Mahakama ya Kadhi italeta hukumu za kukata
mikono, kuhukumu wasio kuwa Waislamu, na kubagua wasio kuwa Waislamu. Matamko
ambayo yamebeba upotoshaji huu yametolewa kwa makusudi kwa lengo la hadaa kwa Waislamu,
wananchi na serikali kwa jumla ili wasitilie maanani maoni yaliyotolewa na
taasisi hizo Kumi na Moja ambayo kama yatafanyiwa kazi na Serikali yatawezesha
kupatikana kwa Mahakama ya Kadhi inayokidhi matakwa ya sheria za Kiislamu na
wajibu wake kama mamlaka ya kutoa na kutenda haki.
Tamko Letu Dhidi ya Upotoshaji Uliotolewa
Hivyo
basi, kwa lengo la kuweka sahihi kumbukumbu na kuondosha uwezekano wa
upotoshaji huu kuchukuliwa kuwa ni kweli, ni vyema tukabainisha ukweli kama
ifuatavyo:
1.
JJumla ya taasisi
kumi na moja (11) ziliwasilisha maoni ya Waislamu juu ya muswada wa Mahakama ya Kadhi. Hizi ni pamoja na taasisi ambazo zinatambulika, zimesajiliwa na zenye uwakilishi
na mtandao wa kitaifa. Baadhi ya taasisi hizo ni Baraza Kuu, TAMPRO, BASUTA,
JASUTA, IPC, HAIYAT ULAMAA, Umoja wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania; na
Shura ya Maimam Tanzania. Maoni juu ya muswada wa Mahakama ya Kadhi
yalipatikana baada ya mchakato uliohusisha wanachama na wawakilishi wa asasi
hizo Tanzania nzima. Hivyo, siyo kweli kuwa asasi hizi Kumi na Moja (11)
zinawakilisha maoni ya wachache. Ni wazi pia kuwa upotoshaji huu unadhihirisha
kuwa waliotoa kauli za upotoshaji huu wanaona uzito wa umoja huu wa asasi za Kiislamu
na maoni yao kweye suala hili la mahakama ya kadhi.
Hawa
wanaosema taasisi hizi zinawakilisha maoni ya wachache na ya wahabi,
hawatuambii kuwa maoni yao yanawakilisha taasisi ngapi za Kiislamu na ya
madhehebu yepi. Ukweli ni kwamba hoja hii inadhihirisha hofu ya mshikamano wa
asasi za Kiislamu katika kukabiliana na suala hili la Mahakama ya Kadhi. Ndiyo
maana badala ya kujibu hoja na mapendekezo yaliyotolewa na asasi hizi, matamko
hayo yamejikita kwenye kushambulia taasisi husika kwa hoja ambazo zina misingi
ya kuwagawa Waislamu.
2. Madai kuwa
Mufti ndiye kiongozi mkuu wa Waislamu hapa Tanzania na kwamba ndiye anaye
stahili kuteua makadhi nchini siyo sahihi. Inawezekana kwa taasisi kuwa na
muundo wa uongozi ambao unamfanya Mufti kuwa kiongozi mkuu wa Waislamu wa taasisi
hiyo na hapa huyo Mufti atakuwa mkuu wa taasisi husika na siyo Waislamu wote wa
Tanzania. Mfano wa taasisi ambazo kiongozi wake mkuu ni Mufti ni BAKWATA. Hii
haina maana kuwa kiongozi huyo ndiye kiongozi wa Waislamu wote nchi nzima. Tulieleza
kwenye kamati ya Bunge kama tunavyoeleza hapa kuwa zipo taasisi nyingi za Kiislamu
zilizoandikishwa na mamlaka mbalimbali za uandikishaji wa asasi huru na vyama
vya kijamii (NGOs) zenye maafisa wenye cheo cha Mufti. Kwa hivyo, siyo vyema
sheria kuweka mamlaka yoyote inayohusu
mahakama ya kadhi (mfano uteuzi wa makadhi) kwa Mufti wa taasisi binafsi kwa
kuwa kunaweza kukatokea mgongano na mgogoro mkubwa kwa kila asasi kutaka kutumia
mufti wake kuteua makadhi.
3. Madai
haya kwamba Mufti ndiye kiongozi mkuu wa Waislam na anaye stahili kuteua
makadhi yanalenga kupotosha hoja ya msingi kwamba siyo sahihi kwa sheria kumpa
Mufti mamlaka yeyote yahayohusu mahakama ya kadhi kwa kuwa mufti huyu, ama wa
BAKWATA au wa taasisi nyingine yeyote,
siyo chombo kinachoundwa na sheria yoyote (bali katiba ya taasis husika)
na wala hakuna sheria inayounda ofisi ya Mufti. Mahakama ya Kadhi kuwekwa chini ya Mufti ni
kuifanya mamlaka hiyo muhimu ya kutoa haki kuwa chombo kilicho chini ya Taasisi
binafsi, jambo ambalo ni kinyume cha sheria. Kwa mfano, siyo kila Muislamu wa
Tanzania Bara ni mwanachama wa BAKWATA na yuko chini ya Mufti wa BAKWATA. Ibara ya 20 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania inatoa uhuru wa kujumuika na kujiunga katika jumuiya
mbalimbali. Kuwalazimisha Waislamu wawe chini ya Mufti wa BAKWATA au Mufti wa
taasisi nyingine yeyote ni kuvunja Katiba ya nchi. Hivyo basi si sahihi mamlaka
ya kutoa haki kuhusishwa na MUFTI anayetokana na Katiba ya Taasisi binafsi.
4. Kama
tulivyokwisha eleza kwenye maoni yetu tuliyowasilisha kwenye kamati ya Bunge
juu ya muswada wa mahakama ya kadhi, kwa istilahi ya Kiislamu “Mufti”
maana yake ni alim (msomi) mwenye upeo mkubwa wa elimu ya dini na sheria. Ni
mtu aliyebobea katika taaluma za dini na sheria. Si afisa wa Serikali wala hana
dhima ya utawala au uongozi. Alim hutambuliwa kuwa Mufti na maulamaa wenzake wa
eneo husika kwa kutambua upeo wake mkubwa katika fani za elimu ya dini na
sheria. Alim akitambuliwa na kupewa hadhi ya mufti huchukuliwa kuwa ni marejeo
kwa ajili ya kutolea ufafanuzi masuala ya elimu ya dini na sheria. Kwa hiyo Mufti
jukumu lake ni kufutu mas’ala ya dini na sheria. Si kuwa mtawala au mpangaji wa
masuala ya utawala. Ni dhahiri kuwa madai yaliyotolewa kuwa Mufti ndiye kiongozi
Mkuu wa Waislam hayana mashiko kilugha wala kiistilahi.
5. Hatuamini
hata kidogo kuwa wanaotoa madai haya na upotoshaji huu hawajui nafasi ya Mufti
katika mfumo wa sheria za Kiislam na kilugha. Tunashawishika kuamini kuwa
wanafahamu ukweli kama tulivyouweka hapo juu, bali wanapotosha kwa malengo
mahsusi kwa sababu baadhi yao ni wasomi wenye shahada mpaka shahada za juu
katika fani mbalimbali za dini ya Kiislamu.
6. Madai
kuwa BAKWATA ndiyo taasisi baba na taasisi nyingine ni watoto wake hayana mashiko yeyote ndiyo maana hata Kamati
ya Bunge haikutoa mualiko kwa BAKWATA pekee bali kwa taasisi nyingi za Kiislamu
ikiwemo BAKWATA. Ifahamike kuwa BAKWATA ni taasisi ya kidini kama zilivyo taasisi
nyingine lakini pia BAKWATA ni taasisi dhaifu na iliyopoteza imani kwa Waislamu
wengi nchini. Jina la taasisi hiyo haliifanyi taasisi hiyo kuwa ndiyo kubwa na
yenye hadhi kuliko taasisi zingine za Kiislamu. Hata hivyo, kimuundo na
kiuwakilishi, taasisi hii haina sifa ya kuwa ni taasisi kubwa na yenye mamlaka
dhidi ya taasisi nyingine za Kiislamu kwa sababu zifuatazo;(i) BAKWATA haina
wanachama tofauti na taasisi zingine ambazo zina wanachama; (ii) mara kadhaa BAKWATA imetoa matamko kuwa haiwakilishi Waislamu
wote wa Tanzania; (iii) Asili yake BAKWATA haijaundwa na Waislamu kwa umoja
wao. Ndiyo maana uhalali wa BAKWATA kuwa
ndicho chombo kikuu cha uongozi wa Waislamu nchini umehojiwa na Waislamu mara
nyingi.
7. Kama
tulivyoeleza kwenye maoni yetu juu ya muswada wa Mahakama ya Kadhi, tunarudia
kusema tena kuwa iwapo Serikali itafuata upotoshaji huo kuwa BAKWATA ndiyo
chombo kikuu kinachowakilisha Waislamu wote na hivyo kuipa BAKWATA nafasi ya kuwawekea Waislamu Mahakama ya Kadhi itahesabiwa
na Waislamu kuwa ni hila ya Serikali kutaka kulazimisha mamlaka ya BAKWATA juu
ya Waislamu hata wale wasioikubali taasisi hiyo. Jambo ambalo litakuwa limekiuka haki ya
msingi ya kila Mtanzania kujumuika kwa uhuru bila kutezwa nguvu au kushinikizwa.
Inasikitisha kwamba, wakati mchakato wa maoni juu ya muswada wa Mahakama ya Kadhi unaendelea, baadhi ya viongozi wa juu wa serikali wametoa kauli ambazo
zinaoana na hoja dhaifu kuwa BAKWATA ndicho chombo cha uwakilishi cha Waislamu na
kwamba serikali imeuandaa mchakato wa Mahakama ya Kadhi kwa kuishirikisha
BAKWATA kwa karibu kama chombo kinachowakilisha Waislamu wote. Hili ni kosa
kubwa kwa kuwa BAKWATA siyo chombo cha Waislamu wote nchini..
8. Kuna matamko
yametolewa na taasisi na watu binafsi ambao wanatumia muswada huu wa mahakama
ya kadhi kuleta hoja zinazokusudia kuleta faraka za kimadhehebu kwa propaganda
ambazo hazina msingi au ukweli wowote katika dini ya Kiislamu hasa suala la
kupinga Mufti kuwa ndiye mteuzi wa makadhi na utengenezaji wa kanuni za Mahakama
ya Kadhi. Tunaotoa udhaifu wa kumpa madaraka hayo Mufti tumezingatia hoja za
kisheria, kidini na kimantiki. Hivyo si kweli kuwa tunapinga Mufti kupewa
madaraka hayo kutokana na tofauti za madhehebu ndani ya Uislamu. .
9. Kadhalika,
wapo viongozi wa dini ambao si Waislamu (mfano maaskofu) wametoa matamko ya
kupinga Mahakama ya Kadhi kwa hoja kuwa italeta hukumu za kukata mikono,
kuhukumu wasio kuwa waislamu, kubagua wasio kuwa waislamu nk. Hoja hizo zote siyo
za kweli na watoaji wa hoja hizo wanajua ukweli kuwa mahakama ya kadhi
inayokusudiwa ni mahakama itakayotumia sheria za Kiislamu ambazo zinatumika kwenye
mahakama za kawaida toka enzi za ukoloni mpaka leo. Inajulikana wazi kuwa
mahakama ya kadhi itashughulika na mambo binafsi ya watu kwa mujibu wa sheria
za Kiislamu ambazo ni sehemu ya sheria halali zinazotumika hapa nchini, mfano
mambo kama ndoa, talaka mirathi, wakfu na malezi ya watoto. Kinachofanywa na
viongozi hao wa dini wasiokuwa waislamu ni kuivunjia heshima jamii ya Kiislamu
na kupotosha ukweli ambao uko wazi.
…………………………………………………………………………
Sheikh Suleiman A. Kilemile
Mwenyekiti wa Hay Atul -Ulamaa
03/02/2015
No comments:
Post a Comment