Tuesday, 17 February 2015

MAREHEMU SHEIKH ILUNGA HASSAN KAPUNGU MAKALA YAKE KUHUSU VITA VYA MAJI MAJI

ALI SONGEA MBANO
JEMADARI WA VITA VYA MAJI MAJI



Nje kidogo ya mji wa Songea kuna kitongoji kinaitwa Mahenge, hapo kuna sehemu ya kumbukumbu ya vita vya Majimaji. Jambo kubwa  la mahala hapo ni kaburi kubwa la halaiki ambamo askari zaidi ya sitini na… (sitini na saba) walizikwa kwa pamoja. Na kando ya kaburi hilo la pamoja kuna kaburi la Ally Songea Mbano ambae yeye alizikwa peke yake.

Kwa mara ya kwanza nilitembelea makumbusho hayo mwishoni mwaka 2007. Baada ya kusaini kitabu cha wageni na kulipa ada ya kituo muhudumu wa kituo hicho alitupa karatasi yenye orodha ya majina ya wale wote walionyongwa na kuzikwa hapo. Ukiitazama orodha hiyo na hasa ukiwa Mwislam jambo moja litakustuwa. Robo tatu ya walionyongwa na kuzikwa hapo ni Waislaam. Linaanza jina lake la Kiiislam, kisha kwenye mabano kuna jina la Kikristo na mwishoni linaishia jina la kiasili, mfano Abdulrahman [Dominic] Mputa Gama.

Muhudumu akatueleza  kuwa hawa mashujaa wa vita vya Maji Maji kabla ya kunyongwa alikuwako padri ambae aliwabatiza na kuwapa majina ya Kikristo na baadae kunyongwa, wengi walibatizwa kwa hadaa kuwa wakibatizwa wataachiwa huru, wote katika hao walionyongwa walikuwa ni Waislam. Uzuri ni kwamba katika orodha hiyo kulikuwa na jina na  sahihi ya yule padri aliyewabatiza, na kwa mkono wake [huyo padri] aliiyaandika hayo majina. Karatasi yenyewe ilihifadhiwa vizuri kwenye fremu ngumu ya kioo. Tuliomba kwa nguvu zote kupatiwa hiyo karatasi ya  majina hata kwa kununua lakini haikuwezekana pamoja na kuwaona na kuwaona wakubwa wa kituo hicho.  Niliporudi kwa mara ya pili mwezi July 2009 nilipata mstuko.

Karatasi iliyohifadhiwa kwenye fremu ngumu ya kioo, iliyokuwa na majina ya  Kiislaam ya mashujaa wa vita vya Maji Maji, haikuwapo,na badala yake imewekwa karatasi nyingine ombayo ndani ya karatasi hiyo majina ya Kiislaam ya mashujaa hao wa vita vya Maji Maji yameondolewa na kuachwa majina ya ubatizo na yale ya kiasili tu, jina la padri, sahihi yake na wadhifa wake katika Kanisa Katoliki pia vimeondolewa na karatasi yenyewe haikuwa kwenye fremu ya kioo na ilikuwa katika fotokopi tu.

Nilimuuliza muhudu kulikoni? Akasema, “Songea pana mzee mmoja maarufu sana katika historia ya TANU na historia ya kuasisiwa Bakwata anaitwa kwa kifupi M. S. Mzee huyu ana binti yake ambaye ameolewa na Mzungu wa Kijerumani. Binti huyu na na mumewe wa Kijerumani walikuja hapa Songea matembezi. Hivyo kwa shinikizo la huyu mzee M.S. karatasi hiyo alipewa huyu Mzungu kwa ahadi kwamba anaipeleka Ujerumani na atairudisha. Hivyo ndivyo karatasi ile asilia ilivyotoweka. Kubwa katika karatasi ile ni ule ushahidi wa majina kuwa wote katika wale walionyongwa na kuzikwa hapo ni Waislaam, wengi katika hao walihadaiwa kuachwa huru hivyo wakabatzwa ispokuwa wachahe sana waligoma kama shujaa Abdulrauf Songea Mbano. Huyu kwa ushujaa wake wa kupambana na Wajerumani aligoma na akasumbua sana kiasi akanyongwa siku yake na peke yake na ndio sababu akazikwa peke yake.

Ukiingia ndani ya kinyumba cha ghorofa, unaanza kuona picha za mashujaa wa Maji Maji wakiwa wamevaa mavazi ya vita mithili ya mahujaji wanavyovaa Ihraam wakati wa hija. Kinachoongezeka kwao ni vilemba kichwani. Chini ya kila picha kuna jina la aliyekuwa kwenye picha ile. Ukipanda gorofani utaona silaha za kiajadi kama mikuki, pinde, ngao n.k. Kinachosisimua zaidi ni mavazi ya vita. Mavazi ya vita ya askari wa Maji Maji wengi walivaa kanzu za Kiislaam na vilemba. Jambo jingine linalosisimua ni kile ambacho watu wa  kituo hicho wameandika ”rosary” hili ni  jina la Kikristo, hasa la Kikatoliki, ni zile shanga ambazo huning’inia msalaba lakini unapotazama hicho kilichoitwa “rosary” utaona si “rosary,” bali ni tasbihi hasa ya Kiislaam yenye kupangika hasa shanga zake, 33, 33, 34. Maneno yaliyoandikwa kuelezea “rosary” hizo ambazo ni tasbihi ni:

“Hizi ni rosary ambazo wapiganaji wa majimaji walikuwa wakitumia KUTAMBIKA kabla ya kwenda vitani kwa kuamini kwamba zitawakinga na risasi.”

Ukweli ni kwamba hawa askari wa Maji Maji wengi walikuwa ni Waislaam hivyo hawakuwa WAKITAMBIKA bali walikuwa wakitumia tasbihi hizo kufanya dhikri kwa Allah kabla ya kwenda vitani. Midhali sisi Waislaam hatujawa tayari kuandika historia yetu kama Waislaam wanaotuandikia watapotosha na kupindisha na kutuzulia wanavyotaka. Hapo gorofani kuna jambo jingine la kusisimua. Kuna magudulia na makopo. Wameandika kuwa, haya ndio makopo ambayo askari wa Maji Maji walikuwa wakiyatumia KUNAWA kabla ya kwenda vitani [kushika udhu na sio kunawa] pia kwa kuamini kuwa maji hayo yatawakinga. Muhudumu alitueleza kuwa kumbukumbu nzuri na za kuaminika ziko Jimbo Kuu la Wakatoliki Peramiho.

Tulikwenda jimboni lakini hatufanikiwa kwa sababu za ki-urasimu tu.T ulitakiwa tupate kibali cha Askofu Mkuu. Hatukukipata. Kwa yale tuliyoyaona na kuyashudia yafuatayo:

Vita vya Maji Maji havikuwa ni vita vya kizalendo, kwamba wazalendo walikuwa wakipigania nchi yao. La. Vilikuwa ni vita vya Waislaam wakipigana na Wakristo wa Kijerumani waliovamia maeneo asilia ya Waislaam kwa lengo la kuuwa Uislam na kusimamisha Kanisa kwani mazingira yote utayoyaona ya mashujaa wa vita vya Maji Maji ni mazingira ya Kiislaam, kingine ni kwamba hukuti mahala yalipo makaburi ya askari wa Kijerumani ila katika miji ya Waislaam kama Kilwa, Bagamoyo n.k. Kwa nini wauliwe maeneo ya Waislaam tu? Walifuata nini huko?

Kuna upotoshaji mkubwa sana wa historia ya vita vya Maji Maji. Vinaoneshwa kama ni vita vya wazalendo wakipigana na wakoloni wa Kijerumani, wakati ukweli si hivyo. Ukweli ni kwamba vita vya Maji Maji vilikuwa ni vita baina ya Waislaam na Wakrito wa Kijerumani, Waafrika Wakristo wa Songea walijiunga na Wakristo wenzao wa Kijerumani  dhidi ya Waafrika wenzao wa Kiislam.

Wakristo wameitafiti hakika hii na wakaijua kisha wameificha kwa maslahi yao.

Kuna haja  ya wasomi wetu wa Kiislaam kufanya juhudi za makusudi za utafiti wa historia yetu ili kukifanya kizazi hiki cha Kiislaam kujitambua zaidi na kujenga ujasiri. Taasisi za Kiislaam na watu binafsi [matajiri] wawawezeshe kiuchumi wasomi hawa kufanya kazi hii.



Mwaka 2008 nimetembelea Kilwa Kisiwani, huko nikamkuta Mzungu wa Kifaransa akiandika historia ya Kilwa Kisiwani akiitwa Thiery, ameweka kambi na majenereta ya umeme, solar power na makompyuta. Kazi nyingine kubwa alokuwa akifanya ni kukarabati yale magofu ambayo mengi ni misikiti na majumba ya mawe ya wafalme wa kale. Kilwa Kisiwani ni moja kati ya dola kubwa za Kiislaam katika mwambao wa Afrika Mashariki, ndio dola ya mwanzo kuwa na  sarafu yake ambayo iliandikwa jina la Allah. Tuliposoma kazi ile ya Yule Thiery Mfaransa tayari alikwisha ipotosha kwa kiasi kikubwa. Sikuwa na la kumfanya. Kizazi cha vijana wa Kiislaam hakitopata historia ya kweli ya Kiislaam kama tutawaacha akina Thiery waandike na hivyo vijana wetu hawatajitambua na hawatokuwa na ujasiri katika Uislam wao.

Ilunga Hassan Kapungu
Jumanne 19 Oktoba 2010







No comments: