

TAREHE: 18 MACHI 2015
PRESS RELEASE
TAMKO LA TAASISI YA MASHEIKH NA
WANAZUONI WA KIISLAMU TANZANIA
KUFUATIA TAMKO LA JUKWAA LA WAKRISTO TANZANIA KUHUSU MAHAKAMA YA KADHI
Assalaam Alaykum,
1.
Madhumuni ya Tamko la
Taasisi ya Masheikh na Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania
Kufuatia Tamko la Maaskofu la tarehe 10
Machi 2015, liliotolewa kwa kutumia “mwamvuli” wa Jukwaa la Wakristo Tanzania
(T.C.F) kuhusu Katiba inayopendekezwa, Mahakama ya Kadhi na Hali ya Usalama na
Amani ya Nchi, Taasisi ya Masheikh na Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania ilifanya
kikao chake jana Jumanne tarehe 17 Machi 2015 kwa lengo la kulitafakari tamko
hilo.
2.
Muhtasari wa Yaliyojitoleza
Katika Tamko la Maaskofu
Taasisi imezipitia kwa kina nukta zote nne
za Tamko hilo pamoja na hitimisho lake na
kubaini yafuatayo:
(a)
Maaskofu “wamejisahau” kwamba wao ni
viongozi wa kiimani na kiroho ambao wanatakiwa wawe tayari kumpokea yeyote na
kumpa neno la hekima lililojazwa faraja, bila hata ya kujali itikadi au chama
chake cha siasa. Badala yake wameamua kutoa faraja kwa waumini wao kwa
kuzingatia utashi wa kisiasa.
(b)
Maaskofu wameamua kutumia msukumo wa kiimani
pamoja na kuzitumia nyumba zao za ibada ili kuwazuilia Waislamu wasipate haki yao ya kuwa na Mahakama
ya Kadhi na kutoa madai ya “Waislamu kupewa rushwa” ili kufanikisha mchakato wa
Katiba inayopendekezwa.
(c)
Maaskofu wameamua kuanzisha utamaduni mpya
wa kuyaendea mambo ya kisiasa kwa misingi ya kiimani na hivyo kutoa tishio la
kuwagawa Watanzania kwa misingi hiyo.
3.
Nasaha za Taasisi
ya Masheikh na Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania
Baada ya Taasisi ya Masheikh na Wanazuoni
wa Kiislamu Tanzania kujiridhisha
na yaliyomo katika Tamko hilo la Maaskofu chini
ya mwamvuli wa Jukwaa la Wakristo Tanzania (T.C.F), imeona itoe
“nasaha” zifuatazo:
(a)
Kwa
kuwa Serikali ina vyombo makini vyenye wataalamu wenye uwezo wa kufahamu na
kuelewa uvunjifu wa Katiba na Umoja wa Kitaifa, tunaiomba Serikali ilipuuze
tamko hilo la Maaskofu na iendelee na mchakato wa Mahakama ya Kadhi na Maaskofu
wawe wavumilivu kwani Serikali hii ni ya Watanzania wote.
(b)
Taasisi
ya Masheikh na Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania
imesikitishwa sana
na Tamko la Maaskofu lililowadhalilisha Waislamu kwa kudai kuwa wamepewa
“rushwa ya Mahakama ya Kadhi”. Madai haya yanaonesha dharau, kiburi na
kutowaheshimu Waislamu, jambo ambalo lina athari mbaya kwa mahusiano baina ya
Waislamu na Wakristo nchini.
(c)
Suala
la Mahakama ya Kadhi ni haki ya Waislamu na haliwahusu wala halihitaji ridhaa
ya wasiokuwa Waislamu kama ambavyo waislamu hawajapata kuombwa ridhaa yao katika yale ambayo Serikali imekuwa ikiwafanyia
wakristo na makanisa yao .
(d) Taasisi ya Masheikh
na Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania inapinga kwa nguvu zote madai ya Maaskofu
kuwa Waislamu kuwa na mahakama ya kadhi ni uvunjifu wa Katiba, kwani Sheria za
Kiislamu ni moja ya vyanzo vya Sheria ya Tanzania kama ilivyo kwa “Common Law
of England” na ndio maana Mahakama za Tanzania zimekuwa zikizitumia sheria hizo
kuhukumu kesi za Waislamu kuhusu Ndoa, Talaka, Mirathi na kadhalika toka mwaka
1963 ilipopitishwa Sheria ya Mahakama za Mahakimu (Magistrates Courts Act) ya
mwaka 1963, kufuatiwa na Sheria ya Tamko la Sheria ya Kiislamu ya mwaka 1964
(The Islamic Law(Restatement) Act of 1964) na kuhitimishwa na Sheria ya Ndoa ya
mwaka 1971. Jambo la msingi hapa ni kuwa kesi hizo zinahukumiwa na Mahakimu
wasio na elimu wala ujuzi na sifa za kuwa Makadhi kwa mujibu wa Sheria za Kiislam na ndio msingi wa Waislamu kudai
uwepo wa Mahakama ya Kadhi Tanzania Bara.
(e)
Taasisi
ya Masheikh na Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania inawakumbusha Maaskofu
kuzingatia kuwa madhara ya kuwagawa Watanzania kwa misingi ya kiimani, dhambi
yake haitoishia kwenye kadhia ya Mahakama ya Kadhi wala Katiba Inayopendekezwa,
bali itaendelea kukita mizizi yake katika kila jambo linalowahusu Watanzania.
(f)
Taasisi
ya Masheikh na Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania inawasisitizia Watanzania kwa
ujumla wao kuwa wapate elimu ya Katiba Inayopendekezwa kwa kuisoma kwa makini na
kuielewa vilivyo ili wawe na uwezo na uhuru wa kuchagua kile wanachikiona kina
manufaa kwao bila kuwepo shinikizo la kiimani.
(g)
Taasisi
ya Masheikh na Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania
inawanasihi Watanzania wote kuendelea kudumisha udugu wao kama
Watanzania bila ya kujali rangi, dini, kabila na itikadi za kisiasa, na
tumkemee yeyote yule anayetaka kutugawa kwa kutumia misingi ya kidini,
kikabila, kisiasa, kiuchumi na kadhalika.
(h)
Kuhusu
hali ya usalama wa nchi, viashiria vya ugaidi na mauaji ya Albino, Taasisi ya
Masheikh na Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania inawakumbusha Watanzania
kuwa suala la kulinda na kudumisha Amani na utulivu nchini ni wajibu wa kila
mtanzania. Hivyo inawaomba Watanzania wote kutoa ushirikiano kwa vyombo vya
ulinzi na usalama katika kuzikabili changamoto hizo.
(i)
Ifahamike
kwamba mauaji ya Albino, tishio la ugaidi na uhalifu mwengine, kamwe havitoweza
kukomeshwa kama hatujengi utamaduni wa kutoa
ushirikiano kwa vyombo vya ulinzi na usalama nchini.
Ahsanteni sana .
_________________________________
SHEIKH KHAMIS SAID MATAKA
KATIBU MKUU
No comments:
Post a Comment