Friday, 17 July 2015

ZAKATUL FITR NA FUNGA YA SIKU SITA NA BEN RIJAL




Zakatul-Fitri na Funga ya Siku Sita
Na Ben Rijal
            Zakatul-fitri ni Zakka ambayo inamlazimu Muislamu bada ya kufunga Ramadhan. Zakkatul-fitri inamlazimu kila Muislamu mkubwa na mdogo, mwanamume na mwanamke alio huru na mtumwa.

            Maana ya Zakat-Fitr ni Sadaqa ya utakaso kwa yule ambaye amefunga mwezi mtukufu wa Ramadhani. Zakka hio hutolewa pale mwezi unapoandama mpaka pale inapomalizika kusaliwa sala ya Eid.

Maana ya Zakka
            Maana ya Zakka kilugha ni kukuwa, kuzidi na kujitakasa kwa upande wa Kisheria Zakka ni kutoa kiwango maalumu kwa mali iliyopitiwa na mwaka na kuwapa khasa khasa masikini na mafakiri.

Hekima ya kutoa Zakatul-Fitri
            Hekima ya kutoa Zakatul-fitri ni kuwatakasa wale waliofunga kwa kuweza kuzisafisha sawmu zao kutokana na makosa ya hapa na pale, aidha Zakatul-fitri ni kuwalisha Waislamu maskini na wao wawe kwenye furaha kwa siku ya Eid.

            Wamepokea Bukhari na Muslim katika vitabu vyao vilivyo sahihi kutokana na Ibn Umar RA amesema: “Amefaradhisha Mtume SAW Zakatul Fitri pishi ya tende au pishi ya shairi kwa Mtumwa na muungwana mwanamume na mwanamke na mdogo na mkubwa wa katika waislamu.” Aidha imepokewa tena na Ibn Umar amesema: “Hukmu Za Zakatul Fitri Katika Sunna iliyotakaswa.” Aidha imepokewa na Ibn Abass RA “Mtume SAW amefaradhisha Zakatul Fitri kwa ajili ya kumsafisha mwenye kufunga kutokana na maneno yake machafu na ya upuuzi, na kwa ajili ya kuwalisha maskini.”

 Utowaji
            Alivyokuwa akifanya Mtume SAW na Masahaba zake ni kutoa kwa njia ya chakula.  Abu Sa'id al-Khudri RA:  "Katika wakati wa Mtume SAW tulikuwa tukitoa Zakatul-fitri  Sa' moja ya chakula, Sa' moja ya Shayiri, Sa' moja ya Tende, Sa' moja ya Aqit (maziwa makavu), au Sa' moja ya Zabibu kavu. Wakati huo chakula chetu cha kawaida kilikuwa ni Shayiri, Zabibu kavu, Aqit  na Tende.
             Wanazuwoni wanatafautiana kuna wanaosema kuwa nikutoa chakula na kuna wengine wanaoelezea kuwa unaweza kutoa chakula au thamani ya chakula, hawa wa kauli ya pili wanafahamisha kuwa ikiwa kila mtu atampelekea chakula na mtu huyo anahitajia vitu vyengine kuweza kupika kile ulichompelekea ndipo walipoeleza kuwa unaweza kutoa thamani.
             Anayoongoza familia ndio inayomlazimu kutoa, kwa kujitolea yeye na wale wote waliokuwa chini ya mamlaka yake ambao wanamtegemea pamoja na mfanya kazi wa nyumbani, aidha ikiwa anawangalia wazee wake na wao bado wapo hai itamlazimu aidha nao kuwalipia.

 Viwango na namna ya kutoa
            Sa’ ni sawa na pishi na pishi ipo Kilo 2.75, Pishi ni kiwango ambacho kilikuwa kinatumika huko nyuma na kwasasa pishi sio kiwango ambacho kinatumika lakini imefanyiwa kazi na kujulikana kiwango chake.

            Imepatikana ikhtilafu baina ya wanavyuoni kuhusu neno "twa'am" (chakula) lililotajwa kwenye riwaya iliyotangulia hapo juu. 
Vilevile ni rahisi kutambua yakuwa neno hilo limehusu nafaka na aina nyengine ya chakula kinachoweza kupimwa kwa chombo. Jambo hilo limedhihirishwa na baadhi ya riwaya kutoka kwa maswahaba. Kwa mfano Ibn Abbas  RA amesema: "Sadaka ya Ramadhan ni Sa' moja ya chakula, kwa hivyo yule atakaeleta ngano, atakubaliwa nayo, kwa yule atakaeleta shayiri, atakubaliwa nayo; kwa yule atakaeleta tende, atakubaliwa nayo; kwa yule atakaeleta nafaka (kama ngano) atakubaliwa nayo; kwa yule atakaeleta zabibu kavu, atakubaliwa nayo."

             Sa’ ni kilo kuna wanayoielezea kuwa ni sawa na 2.5 Kg au 2.75 Kg na wengine nikuona awla bora kutoa kilo 3Kg kamili.

 Namna ya kutoa
            Vyema kutumia Formula ambayo itakuelekeza namna ya kutoa.
N=namba ya watu waliokulazimu, P=Pishi, B=Bei ya chakula hicho kinacholiwa katika mji.
             Tutoe mfano familia ya watu 5 na uchukulie pishi ni 2.5 na gharama ya chakula ni shillingi 2,000. Kwahio ni sawasawa na Zakatul Fitri : 5 x 2.5 x 2,000=25,000
Mtu mmoja : 1 x 2.5 x 2,000=5,000.

Jadwedi iliopo hapo chini itakusaidia katika kufanya mahesabu yako
Idadi, N=Watu
Pishi (2.75)
Gharama ya Chakula
Jumla yote (N*P*B)
2
2.75
2,000
2 x 2.75 x 2,000=11,000
4
2.75
2,000
4 x 2.75 x 2,000=22,000
2
2.75
4,000
2 x 2.75 x 4,000=22,000
2
2.75
4,000
2 x 2.75 x 4,000=44,000
       
Sawmu ya Siku sita baada ya Ramadhani
            Tumeelezwa kuwa funga zetu kuwa zitakuwa zinaninginia baina ya mbingu na ardhi na hazitofika kukubaliwa mpaka kwa kuzitolea Zakatul-fitri, ni vyema tukaelewa wajibu huu kuwa tulikaa kwa mwezi mzima tukafunga kwa kuwa na matarajio ya kupata mafanikio, itakuwaje sisi ya malipo ukaja kujikuta kuwa hukuwa na malipo yoyote katika funga zako, ikiwa sawa na mwanafunzi aliofanya mtihani wa kuingia darasa jengine na kujenga matumaini kafanya vizuri katika mtihani aje kujikuta mwisho wa siku kuwa kaaunguka na kila somo ana sufuri, mwanafunzi huyo atakuwaje?

            Anasema Sheikh Sayed Sabiq katika kitabu chake kiitwacho ‘Fiq -hi Sunnah’ kwamba wamesimulia Maimam wote wa Hadithi isipokuwa Bukhari kuwa; Ameelezea Abu Ayoub Al Ansari  (Radhiya Llahu anhu) kwamba Mtume  SAW "Atakeyefunga Mwezi wa Ramadhani kisha akafuatilia (kufunga) siku sita katika mwezi wa Shawaal, (anakuwa) kama aliyefunga maisha yake yote,” na mapokezi mengine yanasema ni kama aliyefunga mwaka.

            Wengine wamepiga mahesabu kusema kuwa tumeelezwa kuwa kila jema tulifanyalo huongezwa ujira wake kwa mara kumi, kwa hio mwezi wa Ramadhani unasiku 30 ukizidisha mara kumi unapata 360 na siku 6 za mwezi wa mfungo mosi ukafunga siku 6 ukizizidisha mara 10 utapata 60 kwa hio 300 ukiongeza 60 ni sawa na 360 ikiwa ni siku za mwaka. 

Hesabu: 30 x 10= 300 na 6 x 10=60 ukijumlisha 300+60=360
            Waislamu tuzingatie masomo tulioyapata katika mwezi wa Ramadhani na tuzikamilishe Sawm zetu kwa kutoa Zakatu-fitri pamoja na kufunga siku Sita za mfungo mosi tuzidi kupata mafanikio.

            Natanguliza kutoa mkono wa Eid kwa Waislamu wote, Eid Said, Wakulu Aum Wa Antum Bil Kheir.

No comments: