Assalam Alaykum Sheikh Mohamed,
Miaka saba iliyopita niliwahi kununua kitabu ulichokipa
jina ‘’Maisha na Nyakati za Abdulwahid Sykes.’’
Kwa wakati ule
nilikuwa nimezongwa sana nikakosa utulivu wa kukisoma kitabu kile, bahati
mbaya au nzuri akatokea swahib wangu ambaye ni mwanaharakati katika dawaa na
khatibu katika misikiti mbali mbali Zanzibar akaniomba nimuazime.
Bila hiyana nilifanya hivyo nikiamini kupitia kwake
watafaidika Waislamu wengi zaidi. Nikampa sikuwa nimekisoma kitabu kile.
Ni kama mwezi mmoja uliopita nikaranda katika maduka
yanayouzwa vitabu nikijiandaa kwa ajili ya watoto wangu kuanza mwaka mpya
katika madarasa mapya, nikasadifu kukikuta tena kitabu hiki.
Nikakinunua.
Katika wakati Alhamdullilah nimepata wasaa wa kusafiri nacho
nikiwa India ndani ya wiki tatu nimeweza kukiosoma mara mbili.
Kwa hakika nimefaidika na mengi, kitabu
kimeniwezesha kujibu masuala niliyokuwa nikijiuliza siku zote hasa nilipokuwa
chuoni nikifanya BA, Edn (History).
Masuala yaliyokuwa yakinitanza ni harakati za uhuru
Tanganyika kabla ya jina la Nyerere kutajwa ziliongozwa na nani ambao hawatajwi
tena katika historia ya nchi hii?
Pili kupitia taarifa tofauti tunajifunza kuwa Waislamu walikuwa
mstari wa mbele katika kupigania uhuru, kipi kiliwasibu baadaye mpaka
wakapotea.
Haya yote nimepata majibu vizuri.
Pia wakati nasoma chuoni nilikuwa nikibishana sana na
Mwalimu wangu Dr. Mayanja Kiwanuka leo namkuta humu, sawa nimeelewa
kwanini tulikuwa tukibishana.
Sheikh Mohamed,
Kitabu kimejaa mafunzo si tu kwa watafiti na wanahistoria lakini zaidi kwa Waislamu wenyewe wa Tanzania.
Kitabu kimejaa mafunzo si tu kwa watafiti na wanahistoria lakini zaidi kwa Waislamu wenyewe wa Tanzania.
Kuna sehemu zinahuzunisha sana zimenitoa machozi hasa ninapokutana
na aina ya Waislamu kama kina Adam Nasibu.
Inasikitisha kuona
namna Waislamu tulivyorahisi kutumika na kumalizana wenyewe kwa wenyewe.
Inasikitisha zaidi kuona kuwa hali ya Waislamu wa leo
matokeo yaliyochangiwa kwa kiasi kikubwa na Waislamu wenyewe.
Sheikh Mohamed, sitaki nikuchoshe kwa maelezo
marefu, kwa ufupi nikupe pongezi zangu za dhati kwa namna unavyojitolea
kusimamia UKWELI na UADILIFU katika maandishi yako.
Nakuombea Mungu akulipe kila la kheir na kwa maandishi
yako haya iwe nj sababu ya kukufutia madhambi yako na kukuingiza katika pepo
yake.
Nduguyo katika Uislamu,
Kwasasa nipo India ila mastakimu yangu ni Zanzibar.
Jina langu si geni katika masikio wala macho ya dada hapo
(Ahli wako) Mhe Riziki.
Naomba nisalimie.
Nikutakie
kila kheir.
Wakatabah
Issa Kheir Hussein
![]() |
| Wakwanza kulia ni Dk, Mayanja Kiwanuka |
![]() |
| Toleo la kwanza kwa Kiingereza 1998 |


No comments:
Post a Comment