Jamal Yassin |
Barua ya Uthibitisho Kutoka BAKWATA |
Mwandishi akizungumza na Jamal Yassin na Ali Mbaruk Seboy Katibu wa Kamati ya Maafa Shura ya Maimam Tanzania |
Kushoto Mwandishi akizungumza na Jamal Yassin kulia na Ali Mbaruk |
''Jina langu ni Jamal
Yassin na ni mtu wa Pemba, Ole Kiyanga ambako nilizaliwa mwaka wa 1978.
Shughuli zangu za kujiendeshea maisha ni mfanyabiashara wa dagaa ninazotoa
Pemba kuzileta Dar es Salaam kwa usafiri wa majahazi. Nimefanya biashara hii
kwa karibu miaka mitano sasa. Mwezi Juni 2015 nikiwa natoka kuwatembelea wateja
wangu nikirejea nyumbani Kigamboni nilipanda daladala Mbagala Rangi Tatu ambako
nilikuwa nimesali sala ya L’Asr. Nilishuka BP Kurasini karibu na daraja na
mzunguko wa barabara ya kuelekea Kariakoo na nyingine Posta. Nilikuwa na abiria
wenzangu wawili wote akina mama. Tulipokaribia ule mzunguko tukakuta gari ya polisi Landrover Defender imeegeshwa
pale. Mara wakatokea askari wawili wakiwa na silaha na kutuambia kuwa tuko
chini ya ulinzi.
Tukakalishwa chini na palepale askari akanikanyaga began a buti
za polisi alizovaa. Nilikuwa nimevaa kanzu na kichwani nimepiga kilemba. Haya
ndiyo mavazi yangu ya kawaida siku zote. Hapo tukaanza kuulizwa dini zetu. Wale
akina mama mmoja akasema yeye ni Msabato na akaachiwa aendelee na safari yake.
Mwenzake akasema yeye ni Muanglikana nay eye pia akaachiwa. Mimi nikasema ni
Muislam na kwahakika hapakuwa na haja ya kujitambulisha hivyo mwonekano wangu
ulikuwa dhahiri unanitambulisha mimi dini gani. Jibu lililotoka kwa askari ni
kuwa, ’’Huyo mwenye ndevu ndiye tunaemtaka.
Hapo hapo nikaanza kurushwa
kichurachura kuvuka barabara huku nikipigwa. Baada ya kuvuka barabara
nikafungwa pingu. Hapo nikaingizwa ndani ya gari ile ya polisi hadi Central
Police. Nikiwa nje ya jingo nikavuliwa nguo zote nikabaki na chupi. Nikalazwa
kifudifudi pembeni ya barabara wakisema wananipekua kuangalia kama nina mabomu.
Wakati wakifanya upekuzi wakawa wanakoki silaha na kuulizana kama wanimalize au
vipi. Hapo hapo nikamuelekea Allah na kutoa shahada kumpwekesha Mola wangu na
kushuhudia kuwa Mtume Muhammad ni Mjumbe Wake. Wale askari wakawa wanaambizana
wenyewe kwa wenyewe kuwa, ‘’Hawa Waislam ni magaidi tu tummalize huyu.’’
Akatokea afande mmoja
anaitwa Mohamed. Huyu akauliza mbona wale wengine mmewaachia? Mwingine akajibu akasema,
‘’Hawa wenye ndevu si wakuachia hawa wanavunja vituo vya polisi.’’ Kiza
kilikuwa kjmeingia nikaingizwa ndani ya jingo la Central Police ilikuwa kama
mida ya saa mbili usiku hivi. Wakati nilipokuwa nasulubiwa pale nje ya jingo wapiti
njia wote walikimbia sehemu ile pakawa
patupu huoni mtu. Sasa nikafungwa pingu kwa nyuma na nilipofika ndani nikafungwa
mnyororo kiunoni na miguuni. Askari
mmoja akaleta ‘’tape measure’’ akawa anapima kanzu yangu hadi ilipoishia na akapima
pale ilipoishia kanzu hadi unyayoni. Nikaulizwa kwanini navaa kilemba na kuweka
ndevu. Mimi niajibu kuwa hayo ni mafundisho ya dini ya Kiislam kama
alivyofundisha kiongozi wetu Muhammad (SAW) yeye katunasihi tujifananishe na yeye.
Majibu haya yangu wakawa wanayaandika. Wakaleta kiti wakaniweka kisha
wakaniamrisha kunyanyuka na nikaingizwa kwenye chumba kidogo wakafungua maji
wakaanza kunimwagia. Maji yale yalikuwa yakitoka katika ‘’pressure’’ kali na ya baridi na yalikuwa yanawasha.
Askari walikuwa nje ya
kichumba hiki wananiangalia. Haya maji yaliniumiza sana. Ngozi yangu ikaanza kuvimba.
Haukupita muda nikawa hoi nguvu zimekwisha na akili yangu naihisi inapotea.
Wkati wote huu mimi nilikuwa uchi. Walipoacha kunitesa wakaanza kunihoji na
wakanambia kuwa nikikubali yale wanayotaka. Wkasema kuwa kuwa kwangu na ndevu
na kanzu fupi kwao wao ni kiashiria kuwa mimi Al Qeda. Wakanambia kuwa mimi ndiye
niliyeongoza mashambulizi ya Sitakishari. Wakaniuliza zile bunduki nimezipeka
wapi? Wakataka niwaeleze nani nilishirikiana nao katika shambulio lile.
Wakanambia kuwa mimi lengo langu ni kutaka kuweka sheria za Kiislam Tanzania. Wakambia niwaonyeshe wapi
nimezificha wakazichukue. Wakasema kuwa nikiwaeleza wapi silaha zilipo hawatanifanya
chochote kwa kuwa rafiki yao. Wakaniahidi kunijengea nyumba Oysterbay na kunipa
gari. Nikaanza kuwajibu kuwa sijaiba silaha wala sijavamia kituo chochote cha
polisi mahala popote. Hapo wakaanza kunipiga makofi, mateke, ngumi na kunipiga shoti
za umeme. Nilipoteza fahamu. Nilipozinduka ilikuwa tayari kumekucha.
In Shaallah itaendelea...
In Shaallah itaendelea...
Kushoto: Sheikh Ali Mbaruk na Jamal Yassin |
Nilipozinduka ndipo
wakanipekeka shimoni. Panaitwa shimoni kwa sababu hizo seli zipo chini ya jengo
hilo na hata magari yanapopita nje barabarani unayasikia kwa juu. Hapo shimoni
nilikuta Waislam wengi na baadhi yao nikawafamu. Nilimkuta Abubakar ambae
tulijuana kwa ajili ya kuwa pamoja katika shughuli za Uislam. Walikuwapo
vilevile Kudra Same na Ismail Abubakar. Nilikakaa shimoni nikiuguza majeraha niliyopata
mgongoni, ubavuni, miguuni na kifuani kutokana na vipigo nilivyopata. Sikuweza
kulala kwa masiku. Baadae nikapelekwa kituo cha polisi cha Shitakishari, Buguruni
na Msimbazi pamoja na wenzangu niliowakuta shimoni tukiwa tukihamishwa siku
baada ya siku. Baadae tukarudishwa shimoni pale tulipotoka Central Police. Kutoka
hapo sasa ndipo tukapelekwa Oyster Bay kwa mahojiano na Task Force ambacho ni
kitengo maalum kwa jaili ya ugaidi. Walionihoji hapo Task Force waliniambia
kuwa mateso niliyokwishapata huko nilikotoka ni madogo, hapo nitapata mateso makubwa
zaidi. Wakanitahadharisha kuwa itabidi nionyeshe silaha ziko wapi kabla hawajanishughulikia
zaidi.
Maswali yakawa ni yale
yale na nikaanza kupigwa safari hii miguuni baada ya kufungwa katika kitu kama
pipa ambacho kinashikilia miguu. Nilipigwa hadi nikawa siwezi kusimama. Adhabu
zikawa zinaeendelea maswali ni kuhusu silaha. Majibu yangu yakawa ni yale yale
kuwa sihusiki na mambo hayo. Kutoka hapo sasa nikapelekwa Mikese, Morogoro.
Wakati napelekwa huko nilikuwa nimefungwa kitambaa cheusi usoni. Hapo Mikese ni
sehemu ya wazi hatukuwa ndani ya majengo. Hapo panaitwa ‘’gereji,’’ kwa kuwa
hapo ni sehemu makhsusi ya kuwashughulikia Waislam. Hapo nilionyeshwa kaburi na
nikaambiwa kuwa katika kaburi lile amezikwa mvaa kanzu fupi, kilemba na mfuga ndevu
kama mimi. Nilivuliwa nguo na kuanza kupigwa bakora nyingi sana huku mahojiano
yakiendelea na mimi nikiwa uchi. Waliniambia nikiri kuwa mimi ni gaidi. Mimi
nilikataa.
Kuna mwenzetu alivunjwa
mkono katika mahojiano na baada ya kuvunjwa mkono kwa ajili ya maumivu yale
alikiri kuwa yeye ni gaidi. Alinieleza kuwa yeye hakuwa anahusika na
yaliyotokea Sitakishari lakini aliambiwa kuwa asipokiri atavunjwa mkono wa pili
na baba na mama yake watakamatwa na kuteswa kama alivyoteswa yeye. Kwa ajili ya
kuwanusuru waazazi wake aliona bora awakubalie wanalolitaka. Hapa tulikuwa kama
watu 18 kisha wakaletwa wanawake watatu. Siwezi kueleza yaliyowafika hawa
wanawake. Nilipigwa sindano ambayo kwa kweli sijui ya nini na kuanzia hapo
nilipoteza fahamu. Nilipozinduka niliambiwa na walioniokota kuwa walinikuta
Mbezi Barabara ya Morogoro na walidhani ni maiti. Hivi sasa mimi ni mgonjwa kwa
ajili ya kipigo kile. Natokwa na damu katika sehemu zangu mbili za siri.
Nimewaona mara mbili watesaji
wangu mara ya kwanza Msikiti wa Mtambani na mara ya pili Msikiti wa Buguruni.
Tulitazamana uso kwa macho na walijua kuwa nimewatambua. Ningeliweza kupiga
kelele pale msikitini kuwa hawa hapa watesaji wa Waislam lakini Allah
alinielekeza kwenye busara. Laiti ningelifanya vile na kwa kuwa mkasa wangu
unafahamika na ndugu zangu Waislam wale askari nina hakika wangeuliwa mle
msikitini. Nilijizuia nikabaki kimya nikawa nawaangalia wakitoka nje ya msikiti
kwa haraka na kukimbia. Kama ungeliwaona wakiwa katika himaya yao usingeamini
kuwa wale walikuwa waoga wanaogopa kukabiliana na Waislam. Sihitaji kulipiza
kisasi kwa dhulma niliyofanyiwa mimi na Waislam wengine. Sihitaji kulipiza
kisasi ingawa kisasi ni haki yangu. Allah anatosha kwani yeye ni hakimu
muadilifu.''
Jamal Yassin akiwa amefuatana na Sheikh Ali Mbaruk ameonana na Mufti wa BAKWATA Sheikh Abubakar Zubeir na kumfahamisha yote aliyoshuhudia wakifanyiwa Waislam mikononi mwa polisi na yaliyomfika yeye kwa ajili ya Uislam. Mufti Zubeir ameahidi kulifikisha suala hili kwenye vyombo husika.
Jamal Yassin akiwa amefuatana na Sheikh Ali Mbaruk ameonana na Mufti wa BAKWATA Sheikh Abubakar Zubeir na kumfahamisha yote aliyoshuhudia wakifanyiwa Waislam mikononi mwa polisi na yaliyomfika yeye kwa ajili ya Uislam. Mufti Zubeir ameahidi kulifikisha suala hili kwenye vyombo husika.
No comments:
Post a Comment