Thursday, 17 March 2016

SHEIKH MUHAMMAD IDDI AMZUNGUMZA RAIS JOHN MAGUFULI


Sheikh Muhammad Iddi

MAGUFULI ANATEUA HATUMBUWI
Msamiati wa utumubaji wa majipu umepata umaarufu mkubwa haswa katika awamu ya tano ya Mheshimiwa Rais, Dokta John Pombe Magufuli. Msamiati huo kama tungekuwa tumemsikiliza vyema mwenyewe Mheshimiwa Rais Magufuli, tungejua ni wapi unafaa kutumia na ni wapi haufai kutumia.

Watanzania tunayo tabia pindi msamiati mpya ukienea katika jamii huwa tunautumia bila hata ya kuangalia kama ni sahihi au sio sahihi hapo tunapounasibisha. Mheshimiwa Rais John Magufuli anapotamka msamiati wa kutumbua majipu anachokusudia ni kumfukuza au kumuwajibisha yule mtendaji ambaye amehusika moja kwa moja na ubadhirifu katika nafasi husika.

Lakini pia kwa mujibu wa utendaji wa Serikali inayoheshimu misingi ya sheria na utawala bora, bado chombo kikuu chenye mamlaka ya kumtia mtuhumiwa hatiani ni Mahakama na si vyenginevyo.
Kwa bahati mbaya sana katika uongozi wa awamu ya tano chini ya Mheshimiwa Rais, Dokta John Pombe Magufuli, kila mabaye uteuzi wake unatenguliwa au anastaafishwa basi jamii inaaminishwa kwamba huyo alikuwa ‘jipu’ na sasa ametumbuliwa. Jambo hili linavunja heshima waliyojiwekea watendaji Serikalini kwa miaka kadhaa na kibaya zaidi ni kwamba wanahojiwa huku tayari wameshahukumiwa.

Ipo mifano kadhaa amabayo kwa kweli ni muhimu sana kuitazama kwa jicho la ndani zaidi kwani kama hatutokuwa makini Mheshimiwa Rais John Magufuli pamoja na kazi njema yenye nia njema kwa nchi yake anaweza kuweka historia ya kuwa Rais wa kwanza Afrika kupendwa mwanzoni na hatimaye kuchukiwa sana mwishoni.

Tukiyaangalia matukio ya tngu Mheshimiwa Rais John Magufuli aingie madarakani tutaona wazi kwamba yapo matukio matatu yaliyoshudiwa na kupokewa kwa hisia kubwa sana na wananchi.

(a) Lipo tukio la Mheshimiwa Rais John Magufuli kuwawajibisha baadhi ya wafanyakazi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na hatimaye watendaji hao kufikishwa mahakamani. Lakini mtendaji mkuu (Kamishna) wa mamlaka hiyo uteuzi wake ulitenguliwa. Kwa kuwa huyu hakufikishwa mahakamani, msamiati wa kutumbuliwa ‘jipu’ kwake ni uonevu kwani yapo matukio kadhaa ambayo ni vigumu kuyahusisha na yeye moja kwa moja haswa ukilinganisha yaliyokuwa yakiri na mfumo wa kuyahusisha kwake.

Lakini kutokana na mfumo tulio nao, utaona yakitajwa hayo yanayoitwa ‘majipu’ maneno yanajirudia rudia kwa kila ambaye kwa sasa ameondolewa katika nafasi yake ya kiutendaji Serikalini au katika Mashirika ya Umma.

(b) Tumeshuhudia tukio la Mkurugenzi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) akifanyiwa kama ya Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kwa kuitwa ‘jipu’ kwa sababu tu ametenguliwa wadhifa wake aliokuwa nao. Jambo baya zaidi ni tukio la hivi karibuni la uteuzi wa Wakuu wa Mikoa Wapya. 

Baada ya kuteuliwa Wakuu hao wa Mikoa, kutajiwa vituo vya kazi na hatimaye kuapishwa tayari, kwa kuwa ndio mtindo ulio mashuhuri kwa sasa tayari wapo wanaowaona wale wote ambao wameachwa na hawakupewa kuendelea na nafasi zao kwamba hao ni ‘majipu’.
Hapo ndipo tunapoona Watanzania tukumbushane kwamba Mheshimiwa Rais John Magufuli anateua, hatumbuwi ‘majipu’.

Amma hii dhana nzima ya utumbuaji wa majipu inahitaji ufafanuzi au urekebishwaji mkubwa sana. Mfanyakazi aliyeitumikia Serikali au Shirika la Umma kwa muda mrefu, kibinaadamu anayo mafanikio na pia anazo changamoto kadhaa. Anaposimamishwa kazi kwa ghafla kwa ubadhirifu alioufanya, huo ni upande mmoja wa shilingi. Lakini kwa upande wa pili wa shilingi ni vizuri kuchunguza pia kwa miaka yote hiyo ameiingizia Serikali au Shirika kiwango gani cha mafanikio.
Tunawaona watendaji wa Serikali wakipigwa mapicha katika vyombo vya habari na huku wakipewa majina ya uhalifu, hilo linaweza kupunguza ari ya watendaji waliopo kwani haiwezekani aliyetumikia miaka takriban thelathini kazini halafu leo hii mema yake yote yasahauliwe na yakumbukwe mapungufu tu tena ambayo bado hayajathibitishwa na vyombo husika.

Ni vizuri dhana hii ya utumbuaji wa majipu tukaiunga mkono kwani inaonyesha ina dhamira njema, lakini ni muhimu pia kuuangalia mfumo mzima wa utumbuaji ili jamii ibakie salama pamoja na kuwalindia watendaji hao heshima zao walizojiwekea kwa miaka mingi katika uongozi.

Kwa kuanzia, katika zile nafasi ambazo Mheshimiwa Rais John Magufuli anaonekana anao uwezo wa kutengua uteuzi na kumteua mwengine, falsafa ya jipu hapo isipewe nafasi kwani kumteua mtendaji na kumuacha mwengine ni jambo la kawaida. Na yule anayeachwa wala haimaanishi kwamba ni ‘mchafu’ sana bali ni utaratibu katika uongozi kupokezana vijiti katika nafasi.
Nihitimishe Kalamu yangu wiki hii kwa kumpa nasaha Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa John Pombe Magufuli, kwamba:

  1. Kiongozi bora hapimwi kwa umahiri wa kuwaadhibu waliokosea katika uongozi uliopita kwani yapo baadhi ya makosa yanamlazimu mtawala kuyaachia kutokana na mazingira ya wakati husika. Fikra ya ‘kuchimbua’ makosa yote yaliyotokea na kufanywa katika uongozi uliopita ili wakosaji waadhibwe inaweza kukosa nia njema au mwisho mwema. Katika uungwana na ustaarabu wa utawala bora ni kuheshimu mema ya mtangulizi wako na kuufungulia mlango wa dharura kwa yale ambayo yanaonekana ni makosa. Kuendelea ‘kuchimbua’ yote yanayoonekana yamekosewa kutazalisha mfumo mpya wa uongozi katika nchi yetu wa kutoheshimu mazuri ya mtangulizi wako. Aidha, uchambuzi huo unaweza kufikia katika wizara ambazo wewe Rais wetu uliziongoza na hatimaye kutuletea vurugu nchini kwa wanachi kutaka ‘ujitumbue’ mwenyewe wakati sisi bado tunakuhitajia sana.
  2. Kwa siasa za Kitanzania zilivyo kila tukio unaloendelea nalo imma linaleta wingi wa kura au linapunguza idadi ya kura katika Uchaguzi Mkuu ujao mwaka 2020. Ingawa wewe ni Rais wa Watanzania wote bila ya kujali vyama, lakini umeletwa kwenye uwanja wa kura kupitia chama chako. Kwa muktadha huo, ni vyema sana kutaka ushauri kwa viongozi wa chama chako ili ‘mruke’ pamoja.
  3. Watanzania wanayo tabia ya kumpenda mtu kwa ‘mkupuo’ (bila ya sababu) na pia kumchukia mtu kwa ‘mkupuo’. Tayari mapenzi ya Watanzania umeyaona, hiyvo ni vizuri pia ukajiandaa kupokea watakavyokuchukia.

Ukweli ni lazima usemwe! Mheshimiwa Rais John Magufuli ameteua katika maeneo mengi tu na kamwe dhana ya utumbuaji majipu haipo.
Naomba kuwasilisha.
 Mwandishi wa makala haya ni Mwenyekiti wa ARRISAALAH ISLAMIC FOUNDATION.
Unaweza kuwasiliana naye kwa namba: +255 754 299 749, +255 784 299 749.


No comments: