Thursday 18 August 2016

TAAZIA: ABOUD JUMBE MWINYI 1920 - 2016



TAAZIA
ABOUD JUMBE 1920 - 2016


Mzee Aboud Jumbe na Mwandishi

George Githii alikuwa Mhariri Mkuu wa gazeti la Nation. Githii aliandika taazia ya Jomo Kenyatta wakati Kenyatta yu hai hajafa. Bahati mbaya sana kwa Githii, Kenyatta akapata taarifa kuwa kaandikiwa taazia mapema inamsubiri afe tu Githii aichape. Kenyatta hakufurahishwa na habari ile hata kidogo na inasemekana alimwita Githii Gatundu kwa ‘’mazungumzo.’’ Kenyatta hakupendezwa na kitendo kile kwa kuwa yeye akiogopa kifo na akiogopa kukutana na malaika wa mauti, hakutaka mtu amkumbushe kifo.

Aboud Jumbe alikuwa na yakini ya kukutana na Mola wake na hakusubiri mtu kumkumbusha hilo. Aboud Jumbe alijikumbushs mwenyewe kifo na akaandika kwa mkono wake mwenyewe usia wake na vipi angependa mazishi yake yawe. Hii ndiyo tofauti kubwa kati ya viongozi hawa wawili. Aboud Jumbe alikitegemea kifo muda wowote na akajitayarisha na siku atakayokutana na Mola wake. Usia wa Jumbe vipi azikwe umewashtua wengi katika serikali ya Tanzania kwani alikataa kuzikwa nje ya taratibu za Kiislam. Kwa ajili  hii basi Aboud Jumbe alizikwa kama Uislam ulivyofundisha na kuwa kiongozi wa kwanza wa juu katika historia ya Tanzania kuhitimishwa nje ya utaratibu uiiozoeleka wa ‘’sherehe.’’

Nimejuana na Mzee Jumbe katika takriban miaka ishirini na tano ya mwisho wa maisha yake. Huu usia ambao umezunguka sana katika mitandao ya jamii na kuzungumzwa sana mara tu ulipotolewa hadharani, mimi na wenzangu tuliusikia kutoka kinywani kwake mwenyewe. Mimi na wenzangu tulikuwa nyumbani kwake Mji Mwema na Mzee Jumbe akawa anatukumbusha sisi kama wanae hatari ya mja kutekwa na dunia akaisahau akhera kama vile iko mbali sana. Hiyo ndiyo siku alipotueleza kuhusu usia huu. Alituambia kuwa baada ya kuandika usia wake akamwita kiongozi mmoja wa juu katika Serikali ya Muungano kumfahamisha kuhusu usia ule na vipi angelipenda azikwe umauti utakapomfika. Alimweleza kuwa yeye angependa kuzikwa kama wanavyozikwa Waislam kwa mujibu wa sharia na akamsisitizia kuwa asingependa afanyiwe yale yaliyoko nje ya Uislam, mojawapo likiwa jeneza lake kufunikwa bendera. Mzee Jumbe akatueleza kuwa jibu alilotoa yule kiongozi lilimshangaza. Anasema yule kiongozi alimwambia Mzee Jumbe kuwa asiwe na hofu yote aliyoagiza katika usia wake watatekeleza. Mzee Jumbe akasema kwa masikitiko kuwa yeye hakutegemea jibu hili peke yake bali alitegema kuwa na yeye kwa kuwa ni Muislam angemuunga mkono na kusema kuwa hata yeye angependa kuzikwa kama Mtume (SAW) alivyofundisha. Hili kiongozi yule hakulisema. Msisitizo wake ulikuwa kwenye utekelezaji wa usia wa Mzee Jumbe, yeye atazikwa kwa, ‘’sherehe’’ na bendera juu ya jeneza lake. Hivi ndivyo iliyotokea miaka michache baadae. Kiongozi huyu alifariki ghafla na akazikwa kwa, ‘’sherehe,’’ na jeneza lake likafunikwa bendera ya CCM. Bahati mbaya sana kwake usia wa Mzee Jumbe haukumzindua.

Kenyatta alisoma taazia yake mwenyewe yungali hai akaghadhibika akamuita George Githii Gatundu kwa makemeo. Kiongozi huyu aliusoma usia wa Mzee Jumbe lakini yeye aliona haumuhusu. Hivi ndivyo Mzee Jumbe alivyokuwa, tofauti mno na viongozi wenzake. Kuna mwandishi mmoja katika taazia aliyomwandikia Mzee Jumbe, kwa kutoelewa maisha ya Mzee Jumbe kawapa wasomaji wake picha ya kuwa Mzee Jumbe amekufa akiwa ‘’mpweke.’’ Hii si kweli watu walikuwa hawapungui nyumbani kwake Mji Mwema. Nimekuwa nikienda nyumbani kwa Mzee Jumbe mimi na wenzangu mara ambazo hata siwezi kuzihesabu na sikupata hisia hata kidogo kama kuwa Mzee Jumbe alikuwa mpweke. Geti lake lilikuwa wazi ingawa kulikuwa na askari na silaha wakilinda pale. Ukiwa pale nyumbani kwake muda wote utawaona majirani zake wakiingia na kutoka ndoo kichwani wakija kuteka maji, akina mama na watoto mgongoni na wengine wakiwa na watoto wadogo wamewatangulia au wako nyuma yao. Askari walinzi wakiwaachia waingie na kutoka kama watu wa nyumbani. Nyumba ya Mzee Jumbe haikuwa nyumba iliyojiinamia. Sikuenda kwa Mzee Jumbe nikakuta lile geti limefungwa hata siku moja. Nyumba ilizidi uchangamfu kwa wavuvi kuingia na kutoka kuja kufata barafu kwani Mzee Jumbe alikuwa na mtambo wa kisasa kabisa wa kutengenzeza vinoo vya barufu kwa ajili ya uvuvi. Wakati wote wavuvi walikuwa wakipita nyumbani kwake kuja kununua barafu. Siku moja katika mazungumzo Mzee Jumbe katika hulka yake ya kutuchekesha alituambia kuwa yeye hakutaka kuwa tegemezi akae kusubiri hundi ya pensheni maana alisema huenda siku bwana fedha akasahau kukutumbukizia hundi yako. Yeye kwa ajili hii akaamua ajishughulishe kidogo na ndiyo akaleta mtambo wa barafu. Mzee Jumbe akatumalizia kwa kusema alichagua biashara ile ya barafu kwa sababu alijua itawasaidia sana nduguze wavuvi. Si wengi wenye kulijia hili lakini ukweli ni kuwa babu yake mkuu Mzee Othman Kitamaguru aliondoka Mji Mwema na kuhamia Chukwani Zanzibar kuendeleza shughuli zake za uvuvi.

Aboud Jumbe hakuwamo katika mpango wa mapinduzi. Huenda hili likawashangaza watu wengi. Labda kwake yeye hii ni kheri kubwa sana na ilimpa utulivu wa nafsi kwani wale wachache kutoka Zanzibar na Tanganyika waliohusika na mipango ya mapinduzi, hawakutaka baada ya mapinduzi majina yao yanasibishwe na mapinduzi yale. Kwani ni muda mfupi tu baada ya mapinduzi, mauaji na unyama uliofanyika Zanzibar ukajulikana dunia nzima. Kulikuwa na kambi Kipumbwi, nje kidogo ya Tanga ambapo kuliwekwa mamluki wengi wao Wamakonde kutoka mashamba ya mkonge ya Sakura. Hawa ndiyo waliovushwa na kuingia Zanzibar kusaidia mapinduzi na inasemekana kuwa hawa Wamakonde waliua watu wengi sana hasa Waarabu.  Kila Mzanzibari kiongozi niliyezungumzanae kuhusu mamluki hawa au hata kuwapo kambi yao Kipumbwi alisema hana taarifa hizo. Lakini kwa sasa hii si siri tena kwani kitabu cha Dr. Harith Ghassany, ‘’Kwaheri Ukoloni Kwaheri Uhuru,’’ kimeeleza kila kitu. Aboud Jumbe bila shaka alishukuru kuwa hakuwa na mkono katika mpango huu kwani imeshadhihirika hivi sasa kuwa mauaji yale yalikuwa mauaji ya kimbari.

Swali ambalo litakuja ni kuwa nani aliidhinisha kuwepo kwa kambi hii katika ardhi ya Tanganyika? Baada ya swali hili kujibiwa ndipo yatafuata maswali mengine ambayo historia ya Zanzibar na Aboud Jumbe akiwa mmoja wa walioandika historia hii ataweza kutupa majibu. Hivi ni kweli Mwalimu Nyerere alisaidia kuipindua serikali ya Waziri Mkuu Mohamed Shamte kwa kuwa ilikuwa serikali dhalim au kulikuwa na sababu nyingine ambayo wanamapinduzi hawakuijua?

Inajulikana wazi kuwa mgongano wa Nyerere na Aboud Jumbe umetokana na Jumbe kuhoji muungano. Hiki ni kisa maarufu. Bahati mbaya hakuna mwandishi aliyekwenda zaidi ya hapo na kueleza kwa nini suala la Zanzibar kuwa na uhuru lau kidogo wa kujiamulia mambo yake likawa jambo kubwa sana kwa Nyerere? Suala la Zanzibar kuwa huru lilikuwa jambo zito kwa Nyerere kwa sababu ikiwa Zanzibar itatoka mikononi kwake itakuwa yeye alifanya kazi ya bure kusaidia mapinduzi ya Zanzibar. Kwa Aboud Jumbe kuitaka iwe huru pawepo na serikali tatu hii ilikuwa vita ya wazi dhidi ya Nyerere. Lakini muhimu kujiuliza Aboud Jumbe alifika vipi katika hali ile ya kuidai Zanzibar kutoka kwa Nyerere? Katika kitabu chake Dr. Harith Ghassany anaeleza Ali Muhsin anavyoieleza Zanzibar kama Ngome ya Kusini ya Uislam ambayo maadui wa Uislam walidhani wakiiangusha ngome hiyo basi na Uislam nao utaanguka. Ilimchukua muda gani kwa Aboud Jumbe na yeye kuliona hili ambalo wale waliopinduliwa waliliona zamani? Ni kweli kuwa Zanzibar ile kabla ya mapinduzi si Zanzibar hii ya mapinduzi.

Ili kumwelewa Aboud Jumbe hadi kufikia pale ambapo aligongana na Nyerere ni vyema kwanza ijulikane kuwa Aboud Jumbe aliupenda Uislam wake kama vile Nyerere alivyokuwa anaupenda Ukatoliki wake ila tofauti kati yao ilikuwa moja tu. Wakati Nyerere alifanya mipango yake ya kusaidia dini yake kwa usiri wa hali ya juu, Jumbe yeye alifanya juhudi zake waziwazi bila ya kificho. Aboud Jumbe alisaidia kuanzishwa kwa Baraza la Misikiti Tanzania (BAMITA) mwaka wa 1984. Hii ni miaka 12 baada yeye kuwa rais wa Zanzibar na Makamu wa Rais wa Tanzania. Historia ya Nyerere inaonyesha kuwa hapajatokea kiongozi katika serikali yake akajinasibisha na Uislam na Waislam akanusurika. Aboud Jumbe kwa kule kujinasibisha na Uislam alikuwa tayari kwa fikra ya Nyerere kamtangazia vita. Nyerere alitoa, ‘’Presidential Notice,’’ akionya kuhusu viongozi wa serikali kufanya shughuli za dini.

Kwa hakika haikuwa ‘’viongozi wa serikali,’’ onyo lile lilikuwa kwa Makamu wa Rais Aboud Jumbe moja kwa moja. Uislam lilikuwa suala nyeti sana kwa Nyerere na alitumia nguvu za dola kuwamaliza wote walijaribu kuutia nguvu Uislam Tanzania. Sheikh Hassan bin Amir, Tewa Said Tewa, Bi. Titi Mohamed, Abubakar Mwilima na Prof. Kighoma Malima wote hawa walishughulikiwa barabara na wote wakajikuta nje ya siasa za Tanzania, achilia mbali wale waliowekwa kizuizini. Uislm lilikuwa jambo linalotisha na hakuna kiongozi aliyekuwa na ujasiri wa kuleta agenda hiyo mezani.

Aboud Jumbe alikuwako katika kikao cha Kamati Kuu ya CCM siku Abubakar Mwilima alivyomkabili Nyerere uso kwa macho kama Rais wa Tanzania na mwenyekiti wa CCM na kumuuliza imekuwaje Waislam wako nyuma wakati wenzao wanasongambele. Nyerere alikuwa kimya. Ukumbi mzima vilevile ulikuwa kimya. Wajumbe walikuwa wameshika roho zao mkononi. Swali hilo hakuna aliyekuwa hajui kuwa ni mwiko mkubwa kuulizwa. Kwa sekunde chache ilikuwa kama vile dunia imesimama, haizunguki, imetuwama mahali pamoja. Nyerere aliahirisha kikao wajumbe wakanywe chai. Aboud Jumbe alikuwako na alishuhudia jinsi wajumbe wa mkutano walivyomkimbia Mwilima. Hakuna aliyetaka kumkaribia wala kuongea na yeye. Mwilima alikaa mezani akinywa chai peke yake. Wenzake wote hata wale marafiki zake wa siku zote walimkalia mbali. Waliporudi kikaoni Nyerere aliendelea na mkutano kama vile hakuna kilichopitika. Nyerere hakutaka kulijibu swali la Sheikh Mwilima.

Haukupita muda Sheikh Abubakar Mwilima aliitwa kuhojiwa kuhusu kuuza dola za Kimarekani kinyemela. Haukupita muda na yeye kama wenzake waliomtangulia akajikuta yuko nje.

Siku moja Mzee Jumbe alitupa kisa cha, ‘’The Long Letter.’’ Hii barua ndefu ilikuwa ile barua iliyotayarishwa na Bashir Swanzy Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar ndani yake yakiwa mashtaka dhidi ya Muungano kuhoji uhalali wa wa Muungano. Barua hii ilikuwa  imekusudiwa iwasilishwe kwenye Mahakama Maalum ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano. Mzee Jumbe alikuwa akitualika mara kwa mara nyumbani kwake na yeye akipenda sana kuandalia. Mzee Jumbe akikualika nyumbani kwake kula, inabidi ujitayarishe vyema kwani alikuwa akichafua uwanja. Ilikuwa katika moja ya barza zetu kama hizi ndipo siku hiyo akatuhadithia yale yaliyotokea Dodoma kati yake na Nyerere kupelekea yeye kujiuzulu nyadhifa zake zote. Mzee Jumbe alikuwa ana namna ya kuhadithia jambo hata liwe zito vipi, wewe msikilizaji likakufikia kwa wepesi na wakati mwingine katika njia ya kukufanya ucheke. Alikuwa keshatuhadithia jinsi mashtaka yale yalivyokuwa yametayarishwa na hapo ndipo alipokuja na jina hilo la, ‘’The Long Letter,’’ na sisi ikawa huo waraka tunauita, ‘’Long Letter,’’ kama yeye mwenyewe, katika njia ya utani alivyopenda kuita.

Mzee Jumbe alipokuwa anaeleza kupotea kwa waraka ule na ukaibuka mikononi kwa Nyerere Dodoma, Mzee Jumbe alikuwa akituchekesha alivyokuwa akitueleza jinsi Nyerere alivyoinga’nga’nia, ‘’The Long Letter,’’ na akawa anasoma vipande alivyovipenda yeye na Jumbe akimwambia endelea na soma na mahali pengine, Nyerere alivyokuwa hataki akishikilia hapo hapo kama mtoto mdogo aliyepewa pipi na sasa anahisi anataka kunyang’ang’anywa. Huku tukishusha biryani na juisi baridi, hakika ilikuwa ni burdani ya aina yake. Mzee Jumbe akicheka na sisi wasikilizaji tukicheka pia. Mzee Jumbe Uislam na kukubali qadar ya Allah kulikuwa kumemweka pazuri sana.  Mzee Jumbe hakuwa mtu aliyejuta kutoka katika uongozi kiasi alikuwa sasa anatushekesha kuhusu madhila ya uongozi. Akawa siku zote tukiizungumza na yeye kuhusu, ‘’The Long Letter,’’ masikitiko yake ni kuwa kuikosa, ‘’The Long Letter,’’ hawezi kuandika kitabu kuhusu matatizo ya Muungano.

Siku zikenda na miaka ikapita. Siku moja tuko kwake akatuangushia bomu lililotuacha midomo wazi. Mzee Jumbe akatuambia kuwa, ‘’The Long Letter,’’ kaiona nyumbani kwake Migombani kwenye, ‘’Study Room,’’ yake. Tulimuuliza Mzee Jumbe kaiona vipi? Yeye akatujibu kuwa na yeye amepigwa na mshangao kama tulivyopigwa sisi. Akatuambia kuwa na keshaanza kuandika kitabu. Siku zile Mzee Jumbe tayari alikuwa keshaanza kupoteza nuru ya macho na akiandika na kusoma kwa msaada wa ‘’lens.’’ Iko siku mimi na mwenzangu sasa tukihariri mswada wa kitabu cha Mzee Jumbe kilichokuja kujulikana kama, ‘’The Partner-ship: Tanganyika-Zanzibar Union 30 Turbulent Years.’’  alitualika nyumbani kwake Zanzibar Migombani na tulisafiri meli moja. Siku ile alituingiza katika ‘’Study Room,’’ yake na akatuonyesha ‘’desk,’’ alipoikuta, ‘’The Long Letter,’’ikimsubiri, imerejeshwa kama ilivyoibiwa ofsini kwake Ikulu Zanzibar. Kwangu mimi binafsi ilikuwa furaha ya pekee. Nakumbuka wakati tumekaa tunajiuliza ni nani aliyeirudisha, ‘’The Long Letter,’’ nyumbani kwa Mzee Jumbe na asionekane na mtu. Hakika kilikuwa kitendawili. Mzee Jumbe alikuwa mtu wa kupenda kuandalia chakula kama nilivyosema hapo awali. Wakati sote tumeinamisha vichwa tunamsikiliza jinsi alivyoiona, ‘’The Long Letter,'' ghafla  wakaingia watu wa ‘’catering,’’ na mavazi yao meupe wamebeba sahani za vyakula wanatuandalia. Ilikuwa kiasi cha saa kumi na moja jioni.

Kile ambacho Aboud Jumbe hakupewa nafasi kukisema Dodoma Allah akamuwezesha kukisema miaka kumi baadae kupitia kitabu chake, ‘’The Partner-ship: Tanganyika-Zanzibar Union 30 Turbulent Years.’’ Mzee Jumbe alikuwa mtu wa vichekesho sana. Tulikuwa tunachagua picha za kitabu sasa tukawa tunaangalia picha moja Karume na Nyerere wamepanda gari la wazi. Mmoja wetu akamuuliza Mzee Jumbe, ‘’Hii picha tuweke, ‘’caption gani?’’ Mzee Jumbe mara moja hapo kwa hapo akajibu, ‘’Karume being taken for a ride by Nyerere.’’ Sote tuliangua kicheko.

Nadhani hapa tulipofika panatosha. Huwezi mtu ukammaliza Mzee Jumbe. Nina mengi ningeweza kueleza kuhusu Aboud Jumbe na juhudi zake za kuwasaidia Waislam khasa wa Bara. Mzee Jumbe alikuwa karibu sana na viongozi wa Waislam Bara na alijitahidi sana kuwasaidia kwa hali na mali akifanya mambo yake kimya kimya. Darul Iman walipofanyiwa hujuma wasijenge shule ya ufundi Kibaha. Darul Iman walifunga virago na fedha zile wakataka kuzipeleka Somalia. Mzee Jumbe hakukubali aliwaambia kuwa ikiwa watafanya hivyo watakuwa wamewadhulumu Waislam wa Tanzania kwani hizo fedha zimetolewa kwao. Mzee Jumbe akawaambia kuwa Tanzania ni nchi mbili, ikiwa bara Waislam wanazuiliwa kujengewa hiyo shule hizo fedha zipelekwe Zanzibar na yeye atahakikisha kuwa ardhi inapatikana na shule inajengwa. Mzee Jumbe alipotuambia kuwa kanifanikiwa kuzirejesha fedha za Darul Iman na shule itajengwa Zanzibar, tulimshauri kuwa itakuwa bora badala ya shule kijengwe Chuo Kikuu. Hivi ndivyo ilivyokuja kujengwa Zanzibar University, Tunguu.

Allah tunakuomba umsamehe dhambi zake mzee wetu huyu na umweke mahali pema peponi.


No comments: