Thursday 15 September 2016

WAJA WA KHERI: SHEIKH ROCKET, MZEE SAID NA WENGINEO - HAMZA RIJAL


Sheikh Rocket na bendera yake katika khitma ya Saigon Club 2010

Kuna watu wawili Tanzania maarufu walikuwa kila mwaka wakenda Hijja kwa miguu, Sheikh Rocket na mwengine nimemsahau jina lake nikilikumbuka nitakuambieni. 

Huyu wa Unguja alikuwa ni msafisha msikiti wa pale karibu na Ofisi ya Utawala Bora.

Mzee huyu akiondoka kwa meli bure, akarukia mabasi hadi anaingia Sudan na Misri, kisha hupata usafiri wa meli kuingia Makka.

Alichokuwa nacho mkononi ni mkoba wake wa ukindu tu.

Rocket yeye alizidi, yeye kote alichonacho ni bendera yake, na siku zote alikuwa wa mwanzo kufika kuliko ma group ya Watanzania.

Bahati mbaya zama zao hakukuwa na mitandao ya kijamii kuweza kuzungumzwa.


Nimelipata jina la mzee wa Zanzibar jina lake ni Mzee Zaidi, akisafisha Msikiti kwa kufyegia, kutia maji ya kunywa kwenye mtungi na kupaka rangi Msikiti, alikuwa na yeye akitizamwa na watu wa kheri wasiokuwa wakitaka kujulikana.

Katika mwambao huu wetu iwe Unguja, Pemba, Bagamoyo, Mafia, Lamu, Tanga n.k. wametokea Masheikhe wakubwa aidha wametokea waja wa kheri kama kina Mzee Zaidi na Sheikh Rocket. 

Katika miaka ya 70 safari mmoja nilimshuhudia Rocket amekuja Msikiti Jibril, mtu tuliokuwa tunamsikia tu, tukaambiwa alipofika siku yake ya kurudi Mrima, bandarini alipita tu na hakuna aliyemuuliza kwii, tiketi iko wapi na pasi ya kusafiria iko wapi.

Waja wa Kheir huwezi kuwaelezea, kuna mtu alipewa salamu kutoka Saudi kumpa Sheikh Rocket aliojiuliza huyo mtu amejuana naye vipi na wakizungumza lugha gani?

Waja kama hawa huwezi kujua daraja zao kwa Allah kwa namna walivyoiweka Akhera mbele na Dunia nyuma ya migongo yao...

Kuna sheikhe wetu mkubwa tu aliwahi kutuambia kuwa wao wamesoma na kujuwa lakini Ucha Mungu upo kwa watu wa kawadia akatuambia kuna watu wanafunga Sunna ya Mtume Ayoub, siku kufunga siku kula, siku takriban chini ya 172 kwa kuzingatia mwaka wa Kiislamu kuwa na siku 354.

Watu hao ni wa kawaida tu, nao hutoa sadaka kupindukia, ukimjaalia pesa na yeye hatokaa nayo ataigawa, watu hao ni wa kawaida kabisa wapo lakini hatuna macho ya kuwajua na wao walivyokuwa watu wa kawaida utajua ni mtu wa kawaida, ndipo marehemu Maalim Aboud Maalim alipoambiwa asome dua na kupiga fatha alikataa akamuambia mzee mmoja ambaye ni mtu wa kawaida akionekana mnyonge, mzee alikataa Maalim akasema hatosoma dua mbele yake, aliposoma dua watu walistaajabu alivyokuwa anateremka na kushusha vitu.

Kuna Mzee Rajab wa mtaa wa Funguni hivi sasa ndipo ilipokuwepo Hoteli ya Bwawani, alisikia kuwa mwenye kuadhini Miongo mitatu pasi kukosa kipindi pepo ndio itakuwa makazi yake, hakika nafahamishwa kuwa watoto wadogo wa Mtaa wa Funguni wanaanza kufungua macho na kuingia akili wakimsikia ana adhini kila kipindi, kazi zake zilikuwa hapo hapo, akijua wakati wa Sala umeingia anakimbilia kuadhini, na kufa kwake alifia msikitini baada ya kusali sala ya asubuhi.

Kikwajuni mtaa wetu alikuwepo Babu Haji kazi yake ilikuwa ni kuli, akiwacha mizigo na kukimbilia kuadhini Msikiti wa Wireless. 

Babu Haji alikuwa na hima ya kuadhini na pindipo akifika msikitini ikawa kachelewa na kumeadhiniwa huwa mnyonge laysal kiyas. Babu Haji inawezekana kuwa kaadhini kati ya miaka 40 au na zaidi.

Waja hawa wa kheri kwa walivyokuwa watu wa kawaida basi nyakati zao walikuwa hawazungumziki ila sasa ndio tunawzungumza Allah awajaalie pepo zenye mabustani mazuri mazuri na mito inayoizunguka hizo Bustani. 
Ameen.




Sheikh Rocket kwa heshima na taadhima akipokelewa viatu vyake katika
khitma ya Saigon Club 2010


No comments: