Sunday 30 July 2017

KUTOKA FB: HUENDA LIKAWA PAMBANO LA KARNE SPIKA WA BUNGE, MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA NA MKURUGENZI WA TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI WATAKAPOSIMAMA KIZIMBANI


Muhammad Ali bingwa wa masumbwi aliandika kitabu cha maisha yake, ‘’The Greatest My Own Story,’’ ambamo ndani yake ameeleza pigano lake na George Foreman kwa kirefu sana. Huyu George Foreman alipigananae mwaka wa 1974 na katika maisha yake yote katika masumbwi hapakutokea mpiganaji dhidi yake ambae watu waliona kuwa safari hii Ali atapigwa ila huyu Foreman.

Sababu kubwa ya watu na washabiki wa Ali kuona kuwa safari hii Ali hatovuka kiunzi ni kuwa Foreman alimpiga mpinzani mkubwa wa Ali, Joe Frazier katika raundi ya tatu na Frazier akiangushwa chini mara tatu katika raundi moja. Kila aliyepigana na Foreman alikuwa hakatizi raundi ya tatu anakuwa yuko chini hoi. Wengi wakadhani kuwa na Alii ataishia chini kama waliomtangulia kupigana na Foreman.

Katika hiki kitabu chake Ali aliweka sura akaipa jina, ‘’Bossman Comes,’’ katika sura hii ndimo alimoeleza pigano lake na Foreman kwa kirefu sana. Bossman ni jina la mpiganaji masumbwi wa uzito wa juu, pandikizi la jitu na alikuwa ndiyo, ‘’sparring partner, yaani mfanya mazoezi ya kupigana. Huyu Bosman ndiye Foreman akifanyanae mazoezi.

Ali katika mkakati wake wa mazoezi alitaka kujua kila kitu na mbinu zote za Foreman aliyekuwa na sifa za kuwamaliza wapinzani wake chini ya raundi ya tatu. Kwa ajili hii basi alimuajiri Bossman kama, ‘’sparring partner,’’ wake ili amfunze mbinu na kumpa siri za mpinzani wake Foreman ulingoni.

Ali alikuwa anafanya mazoezi ya raundi 30 kila siku akijitayarisha kwa pambano hilo.
Lakini Bossman alimuambia Ali bila kumficha kitu kuwa hatoweza kumpiga Foreman na akamueleza sababu zake kwa nini Ali atapigwa. Alimwambia Ali kuwa Foreman ana ngumi nzito na nguvu nyingi atakuwa anamsukuma nyuma kama karatasi. Ali alimuuliza Foreman, ‘’Niambie, Foreman anaweza kujitolea kufa ili ashinde abaki na taji?’’
Wakati ule Foreman ndiye alikuwa anashikilia taji la dunia la uzito wa juu.
Hapa Ali alitaka kujua ujasiri wa Foreman. Bossman alitingisha kichwa kuonyesha shaka. Katika pigano lile ilipofika raundi ya tatu Ali alikuwa bado yuko wima na akimrushia Foreman makonde ya uhakika.

Ali anasema alijua Foreman atachoka haraka na atampiga kwa sababu ngumi zake nyingi zilikuwa hazimpati zikiishia hewani na katika mchezo wa ngumi Ali anasema, hiyo ni dalili mbaya kwani mpiganaji anajichosha mwenyewe akimwacha mpinzani na nguvu zake.
Katika pigano lile Foreman alipigwa kwa, ‘’knockout.’’
Wataalamu wa masumbwi wanasema kilichomfanya Foreman apigwe ni kitu kimoja tu nacho ni kutegemea ushindi wa haraka wa raundi tatu. Foreman hakuwa amejitayarisha kwa safari ndefu ya jasho na damu. Ali alikuwa akifanya mazoezi ya raundi 30 ilhali masumbwi ni raundi 15.
Nimekileta kisa hiki cha Ali na Foreman kutaka kuwafikirisha wasomaji wangu. Nilikuwa nasoma hapa FB jinsi baadhi ya watu wanaomuunga mkono Prof. Lipumba walivyokuwa wamefurahishwa na kufukuzwa kwa wabunge 8 wa CUF na Spika wa Bunge kwa kasi ya ajabu kuwafuta ubunge na Tume ya Uchaguzi kupokea majina ya wabunge wapya walioteuliwa.

Lakini kilichonishangaza zaidi ni pale nilipoona katika TV jinsi baadhi ya hao "wabunge," walioteuliwa walivyokuwa wakijibu maswali na kufurahi na kuona kuwa tayari wameshakuwa washindi na weshaapishwa na kuwa wabunge. Nikawa najiuliza, ‘’Inakuwaje watu wetu wakawa na uwezo mdogo wa kutafakari mambo kiasi hiki kufikia kushindwa kuona kuwa hivi ni vita vikubwa na sasa vilikuwa vinaingia katika kipindi muhimu na kigumu kitakachoacha katika sakafu damu nyingi sana, inawezekanaje?’’

Ndipo kiliponijia hiki kisa cha Muhammad Ali na mipango yake ya kupigana pambano la muda mrefu na kwa mkakati huu akaibuka mshindi.
Mgogoro wa CUF sasa uko katika kipindi muhimu sana na Tanzania inaandika historia mpya. Wabunge 8 waliofukuzwa na Prof. Lipumba wamekwenda mahakamani na kwa mara ya kwanza Spika, Msajili wa Vyama Vya Siasa, Mkurugezi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi na hao ‘’Wabunge,’’ waliochaguliwa na Prof. Lipumba watasimama mahakamani kujibu mashtaka kama washitakiwa. Haya si waliyotegemea hasa kwa hawa ‘’Wabunge,’’ watarajiwa, hawa hawakutegemea kabisa kushtakiwa.

Hivi sasa sakata hili linaingia katika safari ndefu ya nenda rudi, panda shuka ya mahakama. CUF wana uzoefu wa kutembea safari ndefu zenye shida, mihangaiko na damu na hii ndiyo silaha yao kubwa iliyowawezesha kuwapo hadi leo na kubaki wakiwa na nguvu kubwa juu ya shida zote walizopitia.

Kuanzia juzi naona hali imebadilika kwa upande waliokuwa wakifurahi kwa kupata ‘’Wabunge,’’ wapya. Ukweli wa hali halisi taratibu unazama na kueleweka uzito wake kuwa hii si safari ya raundi tatu alizotegemea Foreman bali hii sasa ni safari ya raundi 30 alizokuwa anazisubiri Ali na akawa amejitayarisha kwa safari ya mwendo mrefu. Ali alimuuliza Bossman ikiwa Foreman yuko tayari kufa kupata ushindi. Je, hawa wanaopelekwa makahamani bila ya khiyari zao wako tayari kubeba zigo hili zito ambalo hawakujitayarisha wala kutegemea?


Kwa kuhitimisha ningependa ieleweke kuwa pambano hili la Ali na Foreman la mwaka wa 1974 juu ya umaarufu wake si, ‘’Pambano la Karne,’’ kamwe. Pambano la Karne ni lile Ali alipopigana na Joe Frazier mwaka wa 1971 na Ali akashindwa kwa, ‘’points.’’


Ukifika Madison Square Garden, New York ambako ndipo walipopigana Ali na Frazier katika, ‘Pambano la Karne,’’ nje liko bango kubwa sana la wanamasumbwi hawa.

Naingia maktaba kutafuta picha ya bango hili nikiiipata nitaiweka hapa jamvini.
Top of Form
LikeShow more reactions
Bottom of Form


No comments: