HABIB OMAR
BIN AHMAD BIN ABUBAKAR BIN SUMEYT
1303 – 1396
1886 - 1976
Jina lake
Habib Omar bin Ahmad bin Abubakar bin Sumeyt
Aal-Baalawy, nasabu yake inapita kwa Sayyid Alwy bin Muhammad (Sahibul Mirbat)
ami yake Imam Muhammad (Faqihul Muqadam) bin Ali bin Muhammad (Sahibul Mirbat).
Ukoo huu wa Aal Baalawy ni wajukuu wa Mtume Muhammad (Rehma na amani ziwe juu
yake) kupitia kwa Sayyidna Husein bin Ali bin Abi Talib.
Wazee wake
Babu yake Habib Abubakar
ndie mzee wake wa mwanzo alietokea
Hadhramout na kufikia
Ngazija na akafariki huko Ngazija mwaka 1290Hiria na baba yake Habib Ahmad ndie
aliyehamia Zanzibar na akafariki Zanzibar mwaka 1343 Hijria na kuzikwa mbele ya
Msikiti wa Ijumaa wa Malindi.
Kuzaliwa na kulelewa kwake
Habib
Omar alizaliwa siku ya Alkhamisi mwishoni mwa Dhulhijja mwaka 1303 AH sawa na
Septemba 1886AD katika mji wa Itsandaa uliopo Ngazija (Comoro). Alilelewa
malezi mazuri na mama yake aliyekuwa mchamungu Bibi Fatma bint Maalim Shanziy
ambaye alipomzaa baba yake Habib Ahmad bin Sumeyt alikuwa Istanbul (Uturuki)
wakati huo.
Habib
Omar alipofika umri wa miaka sita alilelewa na baba yake Habib Ahmad visiwani
Zanzibar, hapo akapata malezi mazuri chini ya uangalizi wa baba yake ambaye
alikuwa Mwanachuoni mkubwa wa Afrika Mashariki na Ulimwengu mzima.
Kusoma kwake
Habib
Omar alipofika umri wa miaka minane alipelekwa na baba yake Hadhramout kwa
ajili ya kusoma kwa Wanavyuoni wachamungu waliojaa katika miji mbalimbali ya
Hadhramout.
Alimuweka
katika mji wa Shibam nyumbani kwa Mwanachuoni mkubwa Habib Tahir bin Abdalla
bin Sumeyt, ambaye ni ami yake Habib Ahmad bin Sumeyt na akawa chini ya malezi
yake na uangalizi wa mwanawe Habib Abdallah bin Tahir bin Sumeyt.
Habib
Omar baada ya kushiba elimu ya Shibam akapewa idhini ya kwenda kuchota elimu
zaidi kwa Wanavyuoni waliokuwepo katika miji ya Hadhramout iliyokuwa maarufu
kwa Elimu na Wachamungu. Alienda kusoma katika miji ya Hawta, Seyun, Tareem na
kwengineko na akasoma fani tofauti na kwa kiasi kikubwa mpaka kuwapita wenzake
wa rika moja.
Habib
Omar alisoma Hadhramout mpaka ujajani mwake akiwa anakwenda na kurudi Zanzibar
kila baada ya muda. Alipomaliza masomo yake alirudi Zanzibar na akaongeza elimu
nyingi kwa baba yake Habib Ahmad bin Sumeyt na Sheikh Abdallah Bakathir mpaka
akafikia upeo mkubwa kwa fani tofauti.
Habib
Omar alibobea katika fani nyingi zikiwemo Tafsiri ya Qur-an, Hadithi, Fiqhi,
Usulul Fiqhi, fani za Lugha,Tasawwuf na nyenginezo.
Mashekhe zake
Habib
Omar alipata fursa ya kusoma kwa Mashekhe wengi sana, kila aendapo huchota
kutoka kwa Wanavyuoni wa eneo hilo, Mashekhe wake wengi walitokea Zanzibar na
Hadhramout.
Baadhi ya Mashekhe zake wa Zanzibar
1. Habib Ahmad bin Abubakar bin Sumeyt
(baba yake mzazi).
2. Sheikh Abdalla bin Muhammad Bakathir.
3. Sheikh Said bin Muhammad bin Abdalla
bin Dahman.
Baadhi ya Mashekhe zake wa Hadhramout.
1.
Habib
Aidarous bin Omar Alhabshy.
2.
Habib
Ali bin Muhammad Alhabshy.
3.
Habib
Abdalla bin Hasan bin Saleh Albahr.
4.
Habib
Ahmad bin Hasan Al-Attas.
5.
Habib
Omar bin Muhammad Alhaddad.
6.
Habib
Tahir bin Abdalla bin Sumeyt.
7.
Habib
Abdalla bin Tahir bin Sumeyt.
8.
Habib
Ubeydillah bin Muhsin Assaggaf.
9.
Habib
Ahmad bin AbdulRahman ASsaggaf.
10. Habib Abdalla bin Ali bin Shihab.
11. Habib Hasan bin Muhammad Balfaqiih.
12. Habib AbdulRahman bin Muhammad
AlMash-hur.
13. Habib Abdalla bin Omar Asshatiry.
14. Habib Salim bin Hafiidh Al Shekh
Abubakar bin Salim.
15. Habib Mustafa bin Ahmad AlMihdhaar.
Baadhi ya Mashekhe wake wa Hijaaz
(Makka na Madina)
1. Sheikh Omar bin Abubakar BaaJuneyd.
2. Sheikh Omar Hamdan AlMahrusy.
3. Habib Husein bin Muhammad Alhabshy.
Hao ni
baadhi ya Mashekhe zake ambao wengine alisoma kwa kupiga goti na wengine kwa
kupewa Ijaza na kutabaruku nao.
Madhehebu yake
Habib Omar bin Sumeyt
alikuwa Sunni katika Akida, akifuata
Madhehebu ya Kishaafii
katika Fiqhi na alikuwa na Tariqa ya wazee wake Al-Baalawy katika Tasawuf. Pia
alipata ijaza za Tariqa tofauti na kuhudhuria baadhi ya hadhara zao mfano wa
Tariqa ya Shadhiliya na Qadiriya.
Kusomesha kwake
Habib Omar baada ya kumaliza kusoma kwa
Mashekhe zake wa Zanzibar alionelea vyema arejee Ngazija alikozaliwa akaanze
kuwanufaisha watu kwa kuwasomesha na kuwaongoza katika kheri. Akarudi Ngazija
na kusomesha wanafunzi wengi sana na watu wa Ngazija walimpenda na kumheshimu
sana, pia alisomesha sana Zanzibar alipohamia mnamo mwaka 1355 Hijria baada ya
kuteuliwa awe Kadhi na na Mfalme wa Zanzibar Sayyid Khalifa bin Harub.
Alikuwa na darasa baada ya Sala ya Laasiri katika msikiti wa Ijumaa
wa Malindi, alikuwa akisomesha kitabu cha Fiqhi “Fat-hul Muiin” na vyenginevyo,
wakihudhuria watu wengi wa kila tabaka na kila rika wakiwemo Mashekhe, watu wa
kheri, vijana, wazee, wafanya biashara, na wengineo.
Aidha alikuwa na darasa nyumbani kwake kwa nyakati tofauti khasa
baada ya kujiuzulu Ukadhi, ikawa wanafunzi wanafurika kujichotea kila aina za
elimu.
Wanafunzi wake
Habib Omar alikuwa na wanafunzi wengi katika maeneo mbalimbali na
wengi wao walikuwa ni Wanavyuoni wakubwa katika zama zao.
Miongoni mwa wanafunzi wake wakubwa
wa Afrika Mashariki (Zanzibar na Kenya) ni:
1.
Sheikh
Suleiman bin Muhammad Al-Alawy.
2.
Habib
Ahmad bin Husein bin Sheikh Abibakar bin Salim.
3.
Sheikh
Ilyas bin Ali bin Ilyas Assinesry.
4.
Sheikh
Salim bin Abdalla bin Wad-aan.
5.
Sayyid
Ali bin Jaafar Al-Waht Saggaf.
6.
Sheikh
Burhan Muhammad Mkele.
7.
Sayyid
Abal-Hasan bin Ahmad Jamali-Leyl.
8.
Habib
Ahmad Mashhur bin Taha AlHaddad (wa Kenya).
9.
Sheikh
Ali bin Muhammad Baaqashmar.
10. Sheikh Abdalla Saleh Farsy.
11. Sayyid Muhammad bin Alwy Jamali-Leyl.
12. Sayyid Alwy bin AbdulWahhab
Jamali-Leyl.
13. Sayyid Omar bin Abdalla Aal Sheikh
(Mwenye Baraka).
14. Sheikh Abdalla bin Ahmad Baafadhil.
15. Sayyid Ali bin Ahmad Badawy
Jamali-Leyl (wa Lamu).
16. Sayyid Abdurahman Khitamy (wa Lamu).
17. Sayyid Abubakar (Shibli) bin Omar
Qullatein.
18. Sayyid Said bin Abdalla Albiidh (wa
Mambrui).
19. Ustadh Muhammad bin Sharif Said
Albiidh (wa Mambrui).
20. Sayyid Muhammad bin Alwy Bunamay.
21. Sayyid Mustafa bin Alwy Bunamay.
22. Sayyid Muhammad bin Adnan Aydid (wa
Dar es Salaam).
23. Sayyid AbdulQadir bin AbdulRahman
Al-Juneyd (wa Dar es Salaam). Na wengi wengine tusiowataja
waliokuwa wametawanyika katika kila pembe ya dunia.
Wahudumu wake
Habib Omar alikuwa bwana mkubwa
katika elimu na uchamungu, baadhi ya wanafunzi wake walijitolea kumtumikia
katika hali zake za kila siku hata anapokuwa safarini.
Miongoni mwa waliowahi kumhudumia:
1.
Sheikh Said Al-Khusty, alianza kumhudumia tokea Ngazija,
Madagaska na hadi alipohamia Unguja na akafariki Unguja.
2.
Sayyid Muhammad Alwy Bunamay, alipata bahati kubwa ya kuwa khadimu
wa Habib Omar hadi kumuoa mjukuu wa Habib Omar kwa upande wa binti yake.
3.
Sayyid Mustafa Alwy Bunamay, ambae alisogezwa na kaka yake Sayyid
Muhammad.
4.
Watoto wa nyumbani, walikuwepo watoto nyumbani kwa Habib
Omar nao walipata bahati
ya kumhudumia, miongoni mwao ni Ali Amour
Bubahy, Rashid M. Seif,
Sayyid Mahsen, Shee Hamadi, Sayyid
Muhammad Ahmed
Al-Hindwani, Sheikh Abdallah Said Azzan na Said Ali Aboud.
Kazi alizozifanya
Habib Omar bin Sumeyt baada ya kusoma Hadhramout alirejea
Ngazija mji aliozaliwa.
Alisomesha watu wengi huko Ngazija, Madagaska, Zanzibar na kwengineko, alifanya
biashara mbalimbali ikiwemo ya kuuza mafuta mazuri (uturi).
Alisilimisha watu wengi Madagaska kupitia Daawa yake, alijenga
misikiti, alichimbisha visima na kujenga mahodhi khasa Ngazija ambapo walikuwa
wakitegemea zaidi maji ya mvua kwa kunywa na kupikia, visima alivyovichimba
vimewanufaisha watu wengi na vyengine vinatowa maji hadi sasa vikiwa na khabari
nyingi za maajabu.
Habib Omar alikuwa Kadhi wa Zanzibar, alihukumu
kwa uadilifu mkubwa, vile vile alikuwa ni marejeo katika Fatwa kwa ukanda mzima
wa Afrika Mashariki hadi nchini Afrika ya Kusini.
Kuchaguliwa
kwake kuwa Kadhi
Ilipofika mwaka 1355 Hijria (1936 AD) aliyekuwa Mfalme wa Zanzibar
Sayyid Khalifa alimteuwa Habib Omar bin Sumeyt kuwa Kadhi wa Pemba na ndio
ikawa sababu ya kuhamia Zanzibar kutoka Ngazija, kisha akamchaguwa kuwa Kadhi
wa Unguja mnamo mwaka 1357 Hijria. Ilipofika mwaka 1362 Hijria (1942 AD)
Sayyid Khalifa alimchaguwa Habib Omar kuwa Kadhi Mkuu wa Zanzibar wadhifa ambao
alidumu nao hadi alipojiuzulu katika mwaka 1379 Hijria (1959 AD).
Habib Omar ni mzalendo katika Ukadhi wa Unguja
kwani baba yake na babu yake wote walikuwa Makadhi wa Unguja.
Mambo muhimu
aliyoyafanya akiwa Kadhi Mkuu Zanzibar
Habib Omar alikubali wadhifa wa Ukadhi pamoja na uzito wa wadhifa
huo kutokana na haja ya Waislamu kuwa na Kadhi katika kila nchi na kwa Zanzibar
yeye ndie aliyekuwa anaestahiki zaidi kuwa Kadhi.
Alikuwa muadilifu wa hali ya juu, kesi zake nyingi huzimalizia kwa
suluhu bila ya kutowa hukumu, na alikuwa hawakubalii mawakili kila walisemalo bali
alihukumu kulingana na Elimu aliyonayo.
Katika mambo makubwa aliyoyafanya Zanzibar ni kushauri kuwekwa mfumo
mzuri wa kusimamia Mali za Wakfu. Mali nyingi za Wakfu zilikuwa hazitekelezwi
manufaa yake yaliyokusudiwa, na Wakfu nyengine zilikuwa chini ya Serikali
zikitumika kinyume na makusudio ya waweka Wakfu na Misikiti mingi ilikosa Mali
za kuisimamia.
Akashauri kuwekwe utaratibu mzuri wa
kuinufaisha Misikiti iliyokosa Mali za Wakfu ili Misikiti yote ipate kutumikiwa
kama Wakfu mmoja.
Tabia zake
Habib Omar bin Sumeyt alisifika na sifa nyingi
zilizokuwa njema, alikuwa mkarimu sana, mwenye huruma, mvumilivu, msamahevu kwa
wale waliomkosea, aliwapenda wanafunzi na akiwasaidia, hapendi dhuhuri, hasemi
sana, alikuwa amejipangizia nidhamu maalumu katika maisha yake kwa kila jambo,
alikuwa maridadi, na alisifika na sifa nyingi nyenginezo.
Hadhi yake na
heshima aliyokuwa nayo
Habib Omar alikuwa Mwanachuoni Mchamungu wa kupigiwa mfano katika
zama zake, kila aliyemuona hakuwacha kumsifu kwa sifa ya UchaMungu. Alipendwa
na Wanavyuoni waliomsomesha na kumtanguliza katika Majlis tofauti. Wanafunzi
wake walikuwa wakimuheshimu upeo wa kumheshimu, viongozi wa Kidunia walimtukuza
na kumfanya katika washauri wa mambo yao hadi kutumika picha yake katika noti
ya elfu kumi (10,000) ya visiwa vya Komoro.
Safari zake
muhimu
Habib Omar alisafiri kwenda Hadhramout, Hijaz,
Misri, Ngazija, Madagaska, Kenya, Somalia, Mauritius, Tanganyika na nchi
nyenginezo. Alikwenda Hadhramout (mbali na safari yake ya kusoma) mara kwa
mara mji wa wazee wake na Mashekhe zake kwa ajili ya kuwaunga na kutabaruku nao
kama ilivyokuwa ada ya WachaMungu ya kutembeleana. Habib
Omar ameziandika baadhi ya safari zake za Hadhramout na Hijaz, ameziandika kwa
ukamilifu kila sehemu alizozuru na Mabwana aliokutana nao, Ijaza walizopeana
pamoja na kuelezea matukio muhimu. Safari moja ameiita “Annafhatu-Shadhiyya”
alipokwenda Hadhramout tu, pia ameiandika safari ya Hijazi na Hadhramout na
kuiita “Talbiyatu- Sawt”, tungo hizo mbili zimechapishwa katika kitabu kimoja
na sasa kipo mikononi mwa watu wa kheri.
Pia imeandikwa safari yake nyengine ya
Hadhramout na mwanafunzi wake Sheikh Muhammad Jubran ambayo imeitwa “Arrihlatu-
Sumaytiyyah
fil-Araadhil Hadhramiyyah” nayo imechapwa karibuni kama alivyokusanya na
kuiandika safari ya Habib Omar ya Misri ambayo bado haikuchapishwa.
Vitabu
alivyotunga
Habib Omar alitunga baadhi ya vitabu ambavyo
vimesheheni elimu pamoja na kushughulika na kazi ya Ukadhi ambayo ilimnyima
muda wa kutosha wa kufaraghika na uandishi.
Miongoni mwa vitabu vyake:
1. “Hadiyyatul-Ikhwan” sherehe ya
Aqidatul-Iman.
2. “Annafahatul-Shadhiyyah”, Safari yake
ya Hadhramout.
3. “Talbiyatu Sawt”, safari yake ya
Hijaaz na Hadhramout.
4. Tarekhe ya baba yake Habib Ahmad bin
Sumeyt na Shekhe wake
Sheikh Abdallah Bakathir, vyote vimechapwa pamoja na kitabu cha Habib
Ahmad bin Sumeyt kiitwacho “Al-Ibtihaj fiy bayanil Istilahil Minhaj” 5. “Shadhiyul Azhaar”, ziara ya Habib Salim bin Hafiidh Unguja.
6. Diwani ya mashairi, bado haijachapishwa.
Mkusanyiko wa maneno yake ya hikma
“Majmuu Kalam”.
“Majmuu kalaam” ni moja ya aina ya Utunzi maarufu kwa Wanavyuoni wa
Tasawwuf khassa Aal-Baalawy.
Ni mkusanyiko wa matukio mbalimbali na maneno ya hikma aliyoyatowa
mhusika katika hali mbalimbali. Mkusanyiko huo huandikwa na wale waliomlazimu
na kuishi nae na huwa kwa utungo mzuri wenye kumvutia msomaji kiasi ya kujihisi
yupo katika matukio.
Habib Omar ametungiwa “Majmuu Kalaam” yake na watu tofauti ambayo
yameandikwa kwa khatti za mkono na nyakati tofauti kila mmoja na sehemu
alipokutana nae.
Miongoni mwa walioandika “Majmuu
Kalaam” yake ni wafuatao:
1.
Sheikh
Ubeid bin Said Damis Bajubeir, alipokuwa akiishi Zanzibar.
2.
Sayyid
Hadi bin Ahmad Alhaddar, alipokuwa anaishi Unguja na Pemba. 3. Sheikh Fadhil bin Muhammad bin Awadh Bafadhil alipomzuru
Habib Omar Zanzibar.
4. Sheikh Omar bin Hassan bin Muhammad Arfan Barajaa, wakati
Habib Omar alipokuwa Kenya, Aden, Shihr na Zanzibar.
Zote hizo zipo mbalimbali, kisha zikakusanywa katika tungo moja na
Sayyid Abdul-Qadir bin Abdul-Rahman Al-Juneyd.
Zanzibar katika zama za Habib Omar
bin Sumeyt
Zanzibar ilikuwa ni kitovu cha elimu
ya dini ya Kiislamu katika miaka iliyopita na ilinawiri sana wakati wa Habib
Omar bin Sumeyt. Wanavyuoni wengi waliokuwa baada yake walisoma kwake, watu wa
kawaida walifurahishwa na mwenendo wake na wakimpa heshima kubwa. Habib Omar
alikuwa na bustani yake huko Sharif Msa nje ya mji wa Zanzibar aliyoiita
“Aniisah” kama Shekhe wake Habib Ali Habshy alivyokuwa nayo bustani kwa jina
hilo huko Seyun Hadhramout. Kila siku ya Jumapili walimiminika Sharif Msa
Wanavyuoni wa Zanzibar pamoja na wanafunzi wao pamoja na wapenzi wake kwenda
kumsalimia Habib Omar na kusoma baadhi ya vitabu pamoja na kutabaruku nae, nae
akiwakirimu wale waliokuwa wakimzuru.
Zanzibar katika wakati wa Habib Omar ilitembelewa na Wanavyuoni
wachaMungu wakubwa sana wa Hadhramout wa zama hizo na wote walizuru Zanzibar
kutokana na kuwepo kwake, ziara hizo zilikatika mara tu baada ya Habib Omar
kuhamia Shihri.
Miongoni mwa Wanavyuoni waliozuru
Zanzibar zama za Habib Omar ni:
1. Habib Abdalla bin Tahir bin Sumeyt
(aliyekuwa mlezi wake Shibam).
2. Habib Salim bin Hafiidh Ibni Sheikh
Abibakar bin Salim.
3. Habib AbdulRahman bin Ubaydillah
Saggaf.
4. Habib Muhammad bin Salim bin Hafiidh.
5. Habib AbdulQadir bin Muhammad bin Ali
Alhabshy.
6. Sheikh Fadhl bin Muhammad bin Awadh
Bafadhl.
7. Habib Ali bin Hassan Al-Attas.
8. Habib Abubakar bin Tahir Al-Haddad.
Maneno yake ya Hekima
Habib Omar alikuwa na maneno mingi ya Hekima kwa tungo za mashairi
na za kawaida. Wameyapokea wanafunzi wake maneno hayo na mengi yamo katika
“Majmuu Kalam” zilizokusanywa.
Miongoni mwa maneno yake ya Hekima:
• Unapotaka raha ya kweli ya Akhera
basi wacha raha za kidunia.
• Baalawy hawapendi dhuhuri tofauti na
watu wengine, wanaona hilo sio ukamilifu wa mtu isipokuwa kwa yule aliyepewa
idhini.
• Kulingania kwa ajili ya Allah
hakuhitaji elimu kubwa wala ufasaha bali kunahitaji upole na tabia njema, na
anapokumbusha mkumbushaji (anapotowa mawaidha) akamuona yule anaemnasihi ni
bora kuliko yeye basi maneno huwa yanatoka moyoni na huathiri, ama akijiona
yeye bora kuliko anaowanasihi basi maneno hutoka katika nafsi na yanakosa
kuathiri wasikilizaji.
Kuhama kwake Zanzibar
Baada ya Mapinduzi ya Zanzibar mwaka 1964 Habib Omar alipendelea kuishi
Shihr moja ya miji maarufu ya Hadhramout
na akahamia mwaka 1385 Hijria (1965 AD), akaishi huko kwa kipindi akinufaisha
watu kwa elimu yake.
Habib Omar
aliombwa na Maraisi wawili wa visiwa vya Komoro ahamie Ngazija alikozaliwa na
walipo jamaa zake wengi nae akaamua kuhamia visiwa vya Komoro na ndipo
alipomalizia uhai wake wa duniani.
Kufariki
kwake
Habib Omar alifia katika visiwa vya Ngazija katika mji aliozaliwa
Itsandaa usiku wa kuamkia Jumanne tarehe 9 Safar mwaka 1396 Hijria sawa na
tarehe 10/2/1976 akiwa na miaka tisiini na tatu takiriban.
Ilikuwa ni
siku ya huzuni kubwa kwa Waislamu wote wa Ngazija na Afrika ya Mashariki.
Maziko yake yalihudhuriwa
na umma wa watu kutoka kila pembe ya Afrika
Mashariki na akasaliwa na kuzikwa na watu wa kheri akiwemo Sayyid AbdulQadir bin AbdulRahman Al-Juneyd ambae
alishiriki kushuka kaburini.
Familia yake
Habib Omar hakuwa na watoto wa kiume, kizazi
chake kimeendelea kupitia kwa Sayyid Muhammad Bunamay aliyemuoa mjukuu wake kwa
upande wa bint yake. Habib Omar alikuwa na ndugu wa kiume anaeitwa Habib
Abubakar aliyefariki Unguja, pia alikuwa na ndugu wa kike.
Hizi ni
miongoni mwa khabari za Bwana huyu mtukufu, na amesifiwa na kutajwa kwa kheri
na Wanavyuoni wengi wa kila pembe ya Dunia, tumeyakusanya haya kwa ufupi
kuepuka kumchosha msomaji.
Rejea:
1. Kitabu “Baadhi ya Wanavyuoni wa Mashariki ya Afrika” cha Sheikh Abdallah
Saleh Farsi.
2. Kitabu cha maisha ya Habib Omar “Nubdhah min hayatil Imam Al-
Allamah Habib Omar bin Sumeyt” cha
Sayyid AbdulQadir AlJuneyd.
3. Kitabu “Uqudul-Jaaizah” cha Sayyid AbdulQadir AlJuneyd
4. Kurasa alizoandika Sayyid Abubakar (Shibli) Qullatein kuhusu Habib Omar.
5. Majmuu kalaam za Habib Omar alizozikusanya Sayyid AbdulQadir Al-Juneyd
kutoka kwa watunzi wanne.
Aliyesimama Nyuma ya Masheikh ni Abbas Sykes na Waliokaa Kulia ni
Sheikh Omar bin Sumeit na Kushoto ni Sheikh Ahmed bin Hussein
Wakati hii miaka ya mwanzoni 1960 Abbas Sykes Alikuwa Regional Commissioner
wa Jimbo la Mashariki
Maahad Juneyd Islamiy

+255 777 878 047 – Zanzibar
No comments:
Post a Comment