Utangulizi
![]() |
Sheikh Abdulrazak Mussa Simai (Kwacha) |
Mwandishi
wa makala haya ya Sheikh Kwacha (jina nimelihifadhi) mie humuusudu sana na huwa
sipiti wala sithubutu kufanya hivyo ninapoona makala zake. Kalamu yake kaitia
barafu, maneno baridi lakini yanatia ganzi. Msome hapo chini anavyomweleza
Maalim Sheikh Abdulrazak Musa Simai, mwanasiasa wa Hizbu, bingwa wa tajwid
lakini ikafika wakati akiwa jukwaani akiambiwa asome Qur’an anasema, ‘’Haya hii
Qur’an nasoma, ‘’Alif, Be, Te, The…Wasalaam.’’ Walioijua ilm yake wakabaki
wameinamisha vichwa huku wakivitingisha. Msikilize Sheikh Kwacha wa leo hapo
chini na msome mwandishi baridi anavyomweleza katika wakati wake.
Kwacha
ana tarekhe ya namna yake ambayo inamuweka mtu kuona namna mtu anavyokuwa
anabadilika kutokana na zama na kushindwa baadhi yao kutanabahi kuwa wakati sio
wauuendekeza ila akhera ndio ya mtu kuiweka usoni.
Jina
la Kwacha kamili ni Abdulrazak Mussa Simai mzaliwa wa Paje, amebahatika kwa
zama za katika miaka 50 na mwanzo ya 60 kuweza kusoma elimu ya dini na dunia.
Kwacha
alikuwa katika wenye kupenda kusikilizwa anaposimama kwenye jukwaa na
kuzifasili siaza za Hizbul Watan-ZNP.
Akipanda jukwaani atatoa mwito, ‘’Kwaacha.’’ Hujibiwa,
‘’Kweupe,’’ yaani kumeshakuchaa!
Wasikilizani humjibu Kweupee yaani sasa walikuwa
wanataka uhuru.
Vigogo
vya ZNP wakati huo ni Abdulrahman Mohammed Babu na Ali Muhsin Barwany ukitaka
kuyajua hayo mbali ya kuhadithiwa jitupe kwenye Ofisi ya Nyaraka (Archives)
kisha nenda moja kwa moja kwenye sehemu ya magazeti yaliopita uombe, ‘’Mwongozi,’’
ya 1950 kisha mtafute Babu halafu Ali Muhsin, Babu msome, ‘’Fikra za Mwanadamu,’’
na Sheikh Ali Muhsin msome, ‘’Barua kutoka Cairo,’’ hapo kama mwaka wa 1958
utapowasoma ukawaona namna afkar zao zilivyokuwa na hoja nzito walizonazo
unaona hata hawa wanasiasa wetu wa leo na kuwa na mitandao hawakaribii hata
shubiri.
Kila
kitu huandikwa, wazee wetu wakipenda kusema ‘’aaah, Maktoub,’’ yameandikwa
hayo.
Nini
kilichotokea?
Kilichotokea
ni pale shetani alipoingia Babu kuja na hoja Kwacha aje Mjini kugombania kiti
kwa ZNP na Sheikh Ali Muhsin aende Ng’ambo hapo ndipo sawtafaham kubwa ambayo
ilikuwa na sababu nyuma ya pazia, na nyenginezo kama kina Ali Sultan kuwekewa
makartasi na mengineo.
Umma Party ikabidi iundwe, katika kipindi hiki ilihitajika nasaha watu kuja pamoja badala ya kufarikiana kwani hapo ndipo paliporaruka Zanzibar hadi leo kuwa hapashoneki.
Umma Party ikabidi iundwe, katika kipindi hiki ilihitajika nasaha watu kuja pamoja badala ya kufarikiana kwani hapo ndipo paliporaruka Zanzibar hadi leo kuwa hapashoneki.
Chama
cha ZNP kilikuwa ni tishio kubwa kwa wakoloni na Afrika, kilikuwa ni Chama cha
Kizalendo ambacho kikiunga mkono harakati za Mau Mau Kenya, FNL Algeria na kuwa
wapo mstari wa mebele katika masuala mazima ya Pan Africanism, wakati huku ASP
washapewa Land Rover kutoka Jeresulem na wao wapo na Siasa ya Gozi Zuia.
ZNP
ilikuwa ndio yenye kutaka kuleta uhuru na kuunganisha Waafrika na suala zima la
Pan Africanism, fitna na Muingereza akayasuka yake kuuparaganya umoja wa kikweli
wa Wazanzibari ambao kina Mzee Vuai Kitoweo, Maalim Mandowa, Shaalabi wahadimu
wa asili walipompa Uongozi Ali Muhsin hao waliitakia Zanzibar iwe ya umoja na
iwe ya watu wote ingawa kila mmoja anayake ya kuyaelezea.
Kwacha
akawa Umma Party sasa, Mapinduzi yakaja akapata mpaka U-Regeional Commisioner,
akawa alivyokuwa kama walivyokuwa wengine bada ya Mapinduzi na vishindo vya
Kimapinduzi.
Paa!
72 imefika Karume kauliwa Tarehe 7 April, 1972 Macomrade wakaanza kukamatwa
mmoja bada ya mwengine na Kwacha akawemo kama wakati huo wenyewe ASP wakisema, ‘’Aliomo
yumo asiokuwemo hayumo.’’
Abeid Amani Karume
Yeye
akakuwemo akafungwa na akaja kutolewa akiwa mnyonge kabisa, akaamua kurejea
Paje na kusomesha Qur’an na Darsa kwa misingi aliopita kwa wazee wake.
Kwacha
akaonekana siasa kamwe hatoitaka tena, lakini dunia sio mgando bali ni mtiririko,
(It is not static but is dynamic) akaja mwanawe wa kike akifaya kazi Manispaa
(Zanzibar Municipal Council) akiwa mshika fedha pakatokea matatizo kazini kwake
yakawa bimdogo huyo hana njia ya kutoka, hapo Kwacha akategwa kuwa yaeshe kwa
mwanawe aje kwenye Chama tawala na apande kwenye majukwaa arushe cheche na
fashfashi na fataki akama alivyokuwa akizivurumisha wakati wa Hizbu, naam
akaitikia wito, heeehe ukajiuliza huyu Kwacha aliotulia na kurudi kwa Mungu au
aliokuja tena kuwa Firauni?
Kwani
maneno yake yakawa ya Kifirauni, baadhi ya watu wakamhama msikitini kwa kuona
kichakuwa burtangi amekwenda arijojo.
Nasita
hapa, kisha nitarudia kuyaeleza ninayoyajua, nilioyasikia na niliyoyasoma.
Nionavyo
sivyo uonavyo na haina maana sote tuone sawa sawa, ila wazee huja wakasema hizo
nilizozimwaga ni tarahambi, mimi naona
kama mzee Al Marhum Amani Thani alivyosema kwenye kitabu chake, ‘’Ukweli ni Huu,’’
aliposema, ''Mie naandika kama nisemavyo, hizo kanuni za uandishi sinazo.''
Naibwaga
nanga hapa bada ya safari iliokuwa shwari bila ya mawimbi ya aina yoyote ile.
No comments:
Post a Comment