Sunday 25 February 2018

HAIDAR MWINYIMVUA (1905 - 1987) ALIUZA NYUMBA KUIKOMBOA TANGANYIKA NA ALHAJ ABDALLAH TAMBAZA

SHAJARA YA MWANA MZIZIMA:
MZEE HAIDAR MWINYIMVUA
(1905 - 1987)
ALIUZA NYUMBA KUIKOMBOA TANGANYIKA
Alhaji Abdallah Tambaza
Hidar Mwinyimvua
(1905 - 1987)

Raia Mwema Februari 26 - 27, 2018


AWALI ya yote napenda kuwashukuru wale wote ambao wametokea kuipenda safu hii ya Shajara ya Mwana Mzizima, hususan wale ambao wamekuwa wakinipigia simu za pongezi mara kwa mara au kutuma ujumbe wa sms.
Jumatatu ya leo, Shajara inamwangazia mmoja wa wanaharakati za kupigania Uhuru aliyekuwa mstari wa mbele kabisa, lakini jina lake limesahaulika kabisa baada ya nchi na watu wake kukombolewa kwenye mikono michafu ya ukoloni wa Kiingereza. Jina lake ni Sheikh Haidar Mwinyimvua.
Ni bahati mbaya sana, watu wetu wa leo hawayafahamu vizuri madhila na mateso ya utawala wa Kiingereza, wakidhani kwamba walikuwa wema na wazuri kama vile zilivyo nzuri timu zao za mpira za Liverpool, Manchester, Arsenal na Chelsea ambazo watu huzishabikia kiwendawazimu kabisa, huku wakisema; sisi Arsenal, sisi Manchester, sisi Liverpool.
Walitugawa vipande vipande hapa ili iwe rahisi kwao kututesa watakavyo. Ingawa wenyeji hapa kwetu Mzizima hatukuwa na ubaguzi kwa ndugu zetu waliotoka mikoani, Wangereza walileta mpango wa kila kabila kuwa na kiongozi wao atakayekuwa akipokea amri  kutoka bomani na kuzifikisha kwa wengine.
Wamanyema walikuwa na mkuu wao; Wanyamwezi walikuwa na mkuu wao; Waluguru walikuwa na mkuu wao; Wangindo walikuwa na mkuu wao; Wamwera walikuwa na mkuu wao na hata wenyeji Wazaramo na Wamashomvi nao walikuwa na wakuu wao pia. Hapo nyuma, Watanganyika, pamoja na makabila yetu haya kuwa nayo, lakini tulikuwa wamoja tukicheka na kutaniana kwenye utani wa asili wa kikabila, pamoja na ule wa Sunderland na Yanga.
Wakristo na Waislamu tuliishi tu kidugu bila tabu tukila na kuzungumza pamoja na kila mtu akifuata dini yake; na inapotokea Mkristo anataka kuchinja kuku, basi humwendea jirani yake Mwislamu amchinjie ili isije kuwa taabu kwa watoto kula pamoja. Kwenye misiba, harusi na sherehe mbalimbali tulijumuika pamoja kama jamii moja tu.
Mtawala Mwingireza, ambaye ni mkuu wa Kanisa lake la Kianglikana duniani, alisema hapana; akaagiza maeneo ya Misheni Kota ndiyo wakae Wakristo huko. Wakristo wengi wa Kianglikana hapa jijini waliishi huko na barabara zikapewa majina ya wanakotoka kama Ndanda, Magila, Muheza na Masasi.
Misikiti ya Waislamu nayo pia ikatengwa kwa misingi ya kikabila. Upo Msikiti wa Manyema, Warufiji, Wayao, Wazaramo, Wamakonde, Wangazija, Ibadhi n.k. Tokea zamani watu hawakupenda hali hii ya kubaguana kwenye ibada, hivyo walikuwa wakienda kusali popote pale wakati na muda wa sala unapomkuta. Ilikuwa haishangazi kumwona Imam Mmakonde, akienda Msikiti wa Manyema, akawatania na kuingia kwenye mihrabu kuswalisha. Hakuna sala ya Kimakonde peke yao wala Kimanyema peke yao, lakini ndio ujinga wa kutawaliwa huo jambo likaenda hivyo.
Pale karibu na soko la Kariakoo kuna Msikiti wa Mtoro. Mtoro ni jina la muasisi wa msikiti huo huko nyuma. Kamwe hapaitwi Msikiti wa Kwa Mtoro, kama ndugu zetu wa Kirangi wanavyodhani ni Msikiti wa kutoka kwao ‘Kwa Mtoro’ kule Kondoa; na hivyo kujinasibisha nao visivyo kabisa kama nao ni Msikiti wa Warangi.
Mzee Haidar Mwinyimvua alitokea maeneo ya Winde,  Bagamoyo na aliishi eneo la Kisutu hapa Dar es Salaam. Nyumba yake ilikuwapo pale Kisutu Mivinjeni, mita chache tu kutoka kwenye uzio wa makaburi ya Kisutu, kwenye Barabara iliyojulikana kama Wadigo Street. Wadigo Street namba 5, ndiyo nyumba alimokulia mwandishi huyu iliyomilikiwa na baba yake mkubwa hayati Mzee Abdallah Saleh Diwan Tambaza, aliyekuwa Jumbe wa Kisutu. Wadigo Str. Namba 7 ilikuwa mali ya Jumbe Abdallah pia.
Mzee Haidar Mwinyimvua alijiunga na TANU mapema kabisa akiwa mwenyekiti wake eneo la Kisutu, lakini tawi lilikuwa mtaa wa Mvita, Kariakoo. Mvita Branch ndiyo lililokuwa tawi lenye nguvu kabisa jijini na nchi nzima kwa wakati huo. Uzinduzi wa tawi la Mvita umeweka historia mpaka leo, kwani walihudhuria watu wengi mashuhuri kutoka ndani na nje ya nchi akiwamo na Bwana PC pia. Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wakati huo, Sheikh Suleiman Takadir kutokana na kumpenda Nyerere kupindukia, ndipo kwa mara ya kwanza alipomfananisha Nyerere kama ni ‘nabii wa watu weusi’ kutoka kwa Mola wao— Inna Lillah Wainna Ilayhi Rajuun!
Kutokana na ushupavu na mapenzi yake kwenye mapambano, Mzee Haidar haraka haraka, akaingizwa kwenye Baraza lenye nguvu la Wazee wa TANU na pia Halmashauri Kuu ya TANU pale Makao Makuu. Huko aliungana na viongozi wengine waandamizi wakati huo kama vile John Rupia, Julius Nyerere, Zuberi Mtemvu, Jumbe Tambaza, Suleiman Takadir, Oscar Kambona, Bhoke Munanka na wengineo wakawa wanashughulikia ukombozi wa nchi yetu kwa karibu kabisa wakitoa nguvu na mali zao.
Kuwemo ndani ya Baraza la Wazee au Halmashauri Kuu ya TANU siku zile, kamwe haikuwa nafasi ya wewe kwenda kujitengenezea posho za vikao au safari za nje upate pesa za kujikimu—hapana. Ni nafasi adhimu ya kuonyesha ni kwa kiasi gani wewe utaweza kuitumikia nchi yako kuliko kungojea nchi ikutumikie wewe (Rejea maneno mashuhuri ya aliyepata kuwa Rais wa Marekani John Kennedy ‘...ask not what your country can do for you; but what you can do for your country)—tafsiri ya maneno hayo ni kwamba; usiulize nini nchi yako itakufanyia, bali wewe useme kwanza nini utaifanyia nchi yako.
Mzee Mwinyimvua, aliifanyia nchi yake mengi sana wakati ule wa ukombozi. Alizunguka na kina Nyerere, Titi na wengineo nchi nzima hii kuelezea mustakabali wa kudai uhuru. Wao wenyewe wakijigharimia kula, kunywa, kulala na usafiri wa kwenda na kurudi. Alhamdullilah, nchi yetu si ndogo kwa mapana na marefu, sasa pimia mwenyewe watu wale walijinyima kiasi gani kwa ajili yetu.
Mzee Haidar Mwinyimvua alikuwamo kwenye ujumbe wa kutoka Jimbo la Mashariki na Makao Makuu ya TANU wakati huo, kwenye mkutano ule mashuhuri wa ‘Kura Tatu’ kule Tabora; mkutano ambao nusura ukisambaratishe chama kwa kutoelewana kuhusu kushiriki au kususia Uchaguzi Mkuu wa mwaka wa 1958. Kazi waliofanya kina Mzee Mwinyimvua na wenzake kwa kufikia kile kilichoitwa ‘Uamuzi wa Busara’, kule mkutanoni ndicho kilichotufikisha hapa leo tuko ‘huru huria’.
Moja ya masharti magumu ya uchaguzi ule ni kwamba ili mtu aingie kwenye Baraza la Kutunga Sheria, ilibidi lazima awe na kiwango fulani cha elimu, ambayo wengi wa viongozi waandamizi wa chama cha Tanu wakati ule hawakuwa nayo. Kina Mzee Haidar na wenzake wakaondoa mawazo ya kuwa wajumbe katika Baraza la Kutunga Sheria (LEGCO)—Legislative Council of Tanganyika—sawa na Bunge kwa sasa. Waliwapisha wasomi ambao hawakuwamo mwanzoni kwenye mapambano. (Angalia kitabu Mohammed Said, Maisha na Nyakati za Abdulwahid Sykes,uk. 266/274).
Kitendo cha kuwaingiza mapandikizi mapya katika harakati, tena wengi wao wakiwa ni wa kutoka upande wa pili wa dini nyengine, ambao mwanzoni hawakushabikia mapambano yale kwa kuhofia kupoteza ajira zao serikali, kilimsononesha sana Sheikh Suleiman Takadir, ambaye ndiye aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa TANU lenye nguvu zote.
Mzee Haidar Mwinyimvua, ambaye alikuwa rafiki mkubwa wa Sheikh Takadir anaelezea tukio la kihistoria lilotokea mwaka 1958 Makao Makuu ya Chama:
“Ilikuwa katika ofisi ya zamani ya TANU tukisubiri kufanya mkutano wa Halmashauri Kuu ya Taifa. Ghafla tu Sheikh Takadir alisimama wima akishikilia fimbo yake ya kutembelea akimuelekea Nyerere huku akisema “Huyu mtu katu hatakuja kutujali sisi bali atawajali ndugu zake. Usipoziba ufa utajenga ukuta”. …sisi sote katika chumba tulipigwa na butwaa na maneneo yale …nilimwona Nyerere akilia na akatugeukia sisi na kutuuliza, ‘ je, Sheikh Suleiman amesema maneno yale kwa niaba yenu?’. Tulijibu kwa pamoja kuwa hatukuwa na habari na shauri lile; na mkutano ulivunjika hapo hapo.” (Angalia Mohamed Said, uk. 274).     
Katika kukisaidia chama na harakati zake pale zilipokwama, habari zinasema kwamba Mzee Haidar Mwinyimvua, baba wa watoto kadhaa mashuhuri hapa nchini, akiwamo Imam Mkuu wa Msikiti wa Mwinyikheri Akida, Kisutu, Dar es Salaam, Sheikh Ahmed Haidar, aliuza moja ya nyumba zake na kupeleka pesa zote katika mapambano dhidi ya mkoloni! Mungu wangu; ni uzalendo wa hali ya juu huo.
Wanao wana njaa; wake zako wana njaa; mama mzazi ana njaa; nguo zenu matambaratambara; humiliki hata baiskeli mbovu ya kutembelea; unauza nyumba unapeleka fedha kusaidia ukombozi wa taifa lako— Mh! Mh! Mh! Taifa lenyewe kiziwi; taifa lenyewe bubu; taifa lenyewe kipofu, leo halina ahsante wala shukrani ya kukumbuka mchango mkubwa kama ule.
Mzee wetu huyu, Mungu amrehemu huko alipo, amghufirie madhambi yake na, naam, ampe pepo siku ya hesabu; aliamini sana katika malezi na maadili mema miongoni mwa wanafamilia yake. Alijitahidi katika hali hiyo duni ya Kiafrika siku hizo, kuhakikisha wanawe wamepata elimu bora.
Sheikh Ahmed Haidar Mwinyimvua, ni mtoto mkubwa wa Mzee Haidar;  ana shahada tatu za juu katika elimu ya dini ya Kiislamu kutoka Al Azhar Shariff kule Cairo, Misri. Amekuwa mwalimu kule nchini Yemen, Chuo cha Kiislamu cha Markaz, Chang’ombe na Chuo Kikuu cha Mzumbe, Morogoro.
Mwanawe mwengine, Twahir Haidar (ameshatangulia mbele ya Haki), alibobea katika sheria akiwa na degree yake kutoka Urusi, alikopelekwa na chama cha TANU. Kwa miaka mingi sana alifanya kazi katika Ofisi ya Kabidhi Wasii (sasa Rita), kama mtaalamu wa masuala ya sheria za vyama na NGOs.
Serikali ya Tanzania ilipotaka kurejesha Mahakama ya Kadhi nchini, Twahir Haidar ndiye aliyepewa kazi ya kutembelea nchi mbalimbali na kuangalia namna gani wanavyoendesha Mahakama hizo nchini mwao, akilinganisha na zile za hapa wakati wa ukoloni.
Ripoti yake ndefu kuhusu suala hilo, ndiyo aliyoitumia Waziri Bernard Membe, pale alipolihakikishia Bunge kwamba ni bora Tanzania ikaridhia kuruhusu Mahakama ya Kadhi kwa Waislamu na kujiunga na OIC.  Katika uhai wake Twahir Haidar ndiye aliyekuwa tegemeo kubwa la Waislamu pale walipokuwa wakikusudia kuanzisha taasisi au kutengeneza katiba zao za misikiti kabla kupeleka RITA.
Mtoto mwengine wa Mzee Mwinyimvua, ni Adam Haidar, aliyewahi kufanya kazi katika Ofisi za ‘Interline’ kwenye Shirika la Ndege la Afrika Mashariki ya zamani EAAC na baadaye akafanya kazi pia kwenye Shirika la Ndege la Tanzania – ATCL. Yuko pale anaishi maisha ya kustaafu kwenye maeneo ya Biafra, Kinondoni, Dar es Salaam.
Watanzania tuamke na tutafute habari za watu wa namna hii, ili nasi angalau leo tuseme ahsante kwa watoto wao basi! Kwani watoto wale walikosa sehemu fulani ya malezi ambayo baba zao waliilekeza kwenye taifa zima.

Kaburi la Sheikh Haidar Mwinyimvu Kisutu kaburi hili lipo jirani sana na walipozikwa
Abdul na Ally Sykes na hawa wote walikuwa wazalendo waliopigania uhuru wa Tanganyika

Simu: 0715808864   

        

No comments: