Wednesday 21 March 2018

BABA WA TAIFA NA WAZEE WA DAR ES SALAAM WALIOMUUNGA MKONO WAKATI WA KUPIGANIA UHURU

Utangulizi

Francis Daudi ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu Ulaya ambae akimaliza masomo yake atakuja kuwa mwalimu wa historia. Tumejuana na tunabadilisha mawazo katika historia ya Tanzania. Ameniletea hii hotuba hapo chini nami nimempa fikra zangu.

HOTUBA YA MWALIMU NYERERE YA KUAGA TAIFA TAREHE 5 NOVEMBA, 1985 KABLA HAJASTAAFU URAIS ALIYOITOA MBELE YA WAZEE WA DAR ES SALAAM

Baraza la Wazee wa TANU 1955
(Picha kwa hisani ya Msakala Mohamed Tambaza)

[9:10 AM, 3/20/2018] Francis Daud:
‘"Mimi nimeanza siasa na wazee wa Dar es Salaam; na wazee wa Tanzania. Nimeanza nao mapema sana; mapema kweli. Nilirudi kutoka masomoni, Uingereza Oktoba 1952 – miaka 33 nyuma. Wakati huo nikiwa kijana mdogo wa miaka thelathini na kidogo hivi. 
MS

Niliporudi nikakubaliana na wamisionari hapo Pugu (sekondari), nifundishe shuleni kwao. Lakini nikiwa shuleni – Chuo Kikuu – nilijua. Niliishaamua kwamba maisha yangu yatakuwa ya siasa. Niliamua hivyo: Nitafundisha kwa muda wa miaka mitatu, nione hali inavyokwenda na kuzoeana na wenzangu kabla ya kuanza maisha ya siasa.

Niliporejea nchini hapo Oktoba, nikaenda Butiama. Januari nikarudi Dar es Salaam. Nikaanza kazi. Nikataka kujua habari za African Association. Mzee Mwangosi anakumbuka. Yeye ndiye aliniambia habari za African Association. Aliisha niambia habari hizo tangu nikiwa Makerere – Chuo Kikuu – nikiwa mwanafunzi.

Pale, mimi na wanafunzi wenzangu tulikuwa tumeanzisha chama kinachoitwa Tanganyika African Welfare Association (TAWA) cha wanafunzi wa Tanganyika; mimi nikiwa katibu wao. Hapa tukaona mambo yanakwenda vizuri kidogo. 

Tukaona kwanini TAWA iwe ya wanafunzi peke yao na siyo Tanganyika nzima. Kwa hiyo nikawaandikia baadhi ya watu Tanganyika. Nikasema, jamani ee, tumeanzisha chama, kwanini msianzishe huko matawi ya chama hicho?

Ndugu Mwangosi akapata barua hiyo. Alikuwa miongoni mwa waliopata barua hiyo. Akaniandikia – nikiwa Makerere – akasema: wewe kwanini unataka kuanzisha chama kipya? Kipo chama. Kipo chama cha TAA (Tanganyika African Association). 

Kwa hiyo la maana siyo kuanzisha matawi, maana chama kipo na matawi yameenea; la maana ni kwamba hicho chama chenu mfute, na muanzishe tawi la Tanganyika African Association.

KUVUNJWA KWA TAWA
Hivyo ndivyo tulivyofanya. Kwa hiyo mimi nikawa katibu wa katawi ka TAA hapo Makerere. Niliporudi Tabora na kuanza kufundisha pale St. Marys (sasa inaitwa Sekondari ya Milambo), nikachaguliwa katibu wa TAA wa jimbo ambalo makao yake makuu yalikuwa Tabora. Ulipofanyika mkutano wa TAA mjini Dar es Salaam, nilihudhuria nikiwa mjumbe kutoka Tabora.

Kwa hiyo nilikuwa naijua Tanganyika African Association. Nilipokuwa ninaondoka kwenda Ulaya kusoma, nilikuwa nimeishaonja shughuli za TAA. Sasa niliporudi, baada ya kukaa Pugu siku chache, nikaja mjini Dar es Salaam. Nikauliza nani wanaongoza TAA?Nikaambiwa kuna jamaa mmoja anaitwa Abdul Sykes. Sasa ni marehemu. Abdul ndiye alikuwa katibu wakati huo. 

Nilipelekwa na Kasela Bantu - ambaye naye aliteleza-teleza na hatunaye hapa (kwenye mkutano). Kasela Bantu alikuwa mwalimu mwenzangu. Tulifundisha pamoja Milambo. Nilipokuja Dar es Salaam, nikakuta anafanya kazi Redio (Tanganyika Broadcasting Corporation). Ni Kasela Bantu aliyenipeleka kwa Sykes.

Wakati huo mambo yalikuwa yanasinzia kidogo. Kwa muda mfupi mwaka ule, tukafufua-fufua, hasa kutoka Januari. Kufika Aprili, TAA ikafufuka. Tukafanya mkutano hapo Anautouglou. Kwenye mkutano huu wakanichagua…''

UCHAMBUZI WA HOTUBA YA MUAGO YA BABA WA TAIFA MWALIMU JULIUS KAMBARAGE NYERERE
Francis,

Hotuba hii mimi inanishangaza kwa jinsi Mwalimu Nyerere alivyoacha kutaja majina ya hao wazee anaowashukuru. Huwezi kuwaadhimisha watu wasio na majina, maana yake na tafsiri yake ni kuwa huwajui au umesahau majina yao. Hawa wazee wanafahamika na kila mtu alichangia kwa namna yake kiasi Mwalimu Nyerere hawezi hata kidogo kuwasahau. Wapo aliojuananao kwa shughuli za TANU na siasa tu na kuna wale aliojuananao zaidi katika udugu kwa kuwa wao ndiyo waliompokea kama mgeni wao na akawa sehemu ya ndugu katika ukoo. Hapa sitawataja akina Sykes kwa kuwa historia yao na Baba wa Taifa sasa ni mashuhuri inafahamika. Lakini kuna watu kama Shariff Abdallah Attas na mkewe Bi. Chiku Kikusa, mama yake Maalim Sakina na Maalim Fatna Baba wa Taifa alionekana zaidi kama ndugu. Maalim Sakina na Maalim Fatna ndugu hawa wawili wote walikuwa walimu katika shule ya Al Jamiatul Islamiyya Fi Tanganyika.  Shariff Attas alijuana na Nyerere si zaidi katika siasa bali kama mgeni wa Abdul Sykes.

Shariff Abdallah Attas

Shariff Attas alikuwa akifanya kazi Soko la Kariakoo ambako Nyerere alianza kufika pale 1952 kila akija mjini kutoka Pugu mwisho wa juma. Abdul Sykes alikuwa ndiye Market Master na Shariff Attas akiwa Dalali Mkuu wa Soko. Kupitia kwa Abdul Sykes ndipo Nyerere akajuana na Shariff Attas na watu wa nyumbani kwa Shariff na jamaa zake wote kama Maalim Fatna, Bi. Chiku Kisusa mama yao mzazi Maalim Sakina na Maalim Fatna. Lakini hawa wote niliowataja ndiyo wakajakuwa wanachama wa kwanza wa TANU mjini Dar es Salaam. Hata ukiangalia picha hiyo hapo chini huyu mama utamuona yuko na Baba wa Taifa Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam akimsindikiza Mwalimu Nyerere safari yake ya kwanza UNO, 1955.

Kulia Mzee Mshume Kiyate, Julius Nyerere, Mzee Max Mbwana na
Mzee Mwinjuma Mwinyikambi

Kulia ni Bi, Tatu bint Mzee, Bi, Titi Mohamed, wa nne Julius Nyerere
na wa mwisho ni Bi. Chiku Kisusa


Hapo sokoni Karikakoo ndipo Mwalimu Nyerere akajuana na Mzee Mshume Kiyate. Sasa huyu Mzee Mshume Kiyate wakajuana zaidi katika siasa na udugu ukaja baadae. Mzee Mshume alikuwa mmoja wa wajumbe katika Baraza la Wazee wa TANU na alikuwa mmoja wa wafadhili wakubwa wa chama hadi uhuru ulipopatikana na hili hakuna asiyelijua. Haiyumkini ikawa mtu kama Mzee Mshume KIyate akatajwa kwa ujumla wa ‘’wazee,’’ pasi na kulitaja jina lake. Katika hotuba hii Mwalimu Nyerere kamtaja Sheikh Mohamed Ramiyya lakini hakueleza alimjua vipi Sheikh Ramiyya kwani yeye hakuwa mkazi wa Dar es Salaam. Sheikh Ramiyya alikuwa akiishi Bagamoyo na waliomchukua Baba wa Taifa kumpeleka Bagamoyo kumjulisha kwa Sheikh Ramiyya walikuwa Mzee Idd Tosiri na Mzee Idd Faiz Mafungo na wote hawa watatu, Sheikh Ramiyya, Tosiri na Faiz ni ndugu Wamanyema na wazee wao walitokea Belgian Congo. Hawa walitoa mchango mkubwa katika TANU. Ilistahili siku ile Baba wa Taifa awataje kwa majina yao.  Hii mosi.
Pili, tuje kwa Abdul Sykes.

Kulia Idd Faiz Mafungo, Sheikh Mohamed Ramia, Julius Nyerere
na Haruna Taratibu

Abdul alikuwa wakati ule Nyerere alipopelekwa kwake kukutananae, Abdul alikuwa Kaimu Rais na Katibu wa TAA. Rais alikuwa Dr. Vedasto Kyaruzi lakini kwa sababu ya uongozi huu wa Abdul na Dr. Kyauzi kuiingiza TAA katika masula mazito ya siasa walipoingia madarakani 1950, Dr. Kyaruzi akapewa uhamisho akapelekwa Kingolwira Prison akawe daktari wa wafungwa na ilipoonekana kuwa uhamisho ule haukumzuia kuja Dar es Salaam mwisho wa juma kuja kuonana na Abdul Sykes kendeleza harakati za TAA, Dr. Kyaruzi akahamishiwa Nzega. Hii ndiyo ikafanya sasa nafasi ya rais iwe wazi haina mtendaji na Abdul akakaimu nafasi ile kwa miaka takriban mitatu bila ya kuitisha uchaguzi. Ulipofika mwaka wa 1953 ulipofanyika uchaguzi wa mwaka Nyerere na Abdul wakagombea nafasi ya urais. Hili si Nyerere wala wanahistoria wetu wamelieleza popote.

Nyerere katika hotuba yake hii kwa Wazee wa Dar es Salaam anasema,’’ Tukafanya mkutano hapo Anautouglou. Kwenye mkutano huu wakanichagua…’’ Katika hotuba hii Mwalimu Nyerere kamtaja Abdul Sykes kuwa ni mmoja wa vijana wenzake waliokuwa katika siasa mwingine akisa Dossa Aziz lakini hakusema kuwa aligombea na Abdul Sykes nafasi ya urais wa TAA katika uchaguzi wa mwaka wa taehe 17 April 1953 pale Ukumbi wa Arnautoglo. Wala hakusema kuwa alishinda uchaguzi ule kwa kura chache sana. Hii ni muhimu sana kwani In Shaa Allah nitaeleza huko mbele kuwa hii ilikuja kuwa ndiyo sababu TAA ilikufa baada ya  yeye kuchukua uongozi.

Kushoto Dossa Aziz, Julius Nyerere, Abdul Sykes na Lawi
Sijaona, Ukumbi wa Arnautoglo katika tafrija ya kumaga Nyerere
safari ya pili UNO 1957

Tatu, si kweli kuwa TAA ilikuwa imesinzia kwa sababu 1950 ilikuwa imeunda TAA Political Subcommittee ikiwa na wajumbe hawa wafuatao: Mufti Sheikh Hassan bin Ameir, Sheikh Said Chaurembo, Hamza Mwapachu, Stephen Mhando, John Rupia, Dr. Vedasto Kyaruzi na Abdul Sykes. Kamati hii ilitengeneza mapendekezo ya katiba kwa Gavana Edward Twinning. Haya mapendelezo ndiyo Mwalimu Nyerere aliyasoma katika hotuba yake UNO mwaka wa 1955. Haiwi chama kilichosinzia kikaja na mapendelezo mazito kama haya ambayo yalifika hadi UNO. Licha ya hili mapendekezo haya ndiyo yalijadiliwa katika mkutano uliounda TANU na wanakamati wake wawili Abdul Sykes na John Rupia wakiwa kati ya wajumbe 17 wa mkutano ulioasisi TANU mwaka wa 1954.

Kulia Sheikh Said Chaurembo na Liwali Ahmed Saleh,
1956

Lakini ukweli ni kuwa chama kilisinzia Mwalimu Nyerere alipochaguliwa kuwa Rais wa TAA na ikabidi zifanyike jitihada ili kukihuisha upya chama. Muhimu ieleweke kuwa TAA haikudorora kwa kuwa kiongozi alikuwa hana uwezo, la hasha, TAA ilidorora kwa kuwa Nyerere alikuwa hafahamiki hili la kwanza la pili ni kuwa kwa wakati ule Nyerere hakuweza kutia katika chama kile ambacho Abdul alikuwa akifanya kwa muda wote alipokuwa kiongozi wa juu. Ukweli ni kuwa ikiwa halmashari ya TAA itakutana nyumbani kwake basi kikao kitamalizika vizuri kwa pengine kula na kunywa pale nyumbani au Princess Hotel. Hulka hii iliendelea hadi wakati wa TANU. Mwalimu Nyerere alikuwa mgeni Dar es Salaam na hakuwa na fedha wala na nyumba ambayo angeliweza kufanya haya. Nyumba ya Abdul ambayo kabla yake ilikuwa nyumba ya baba yake, Kleist Sykes, ilikuwa kituo cha harakati dhidi ya ukoloni. Toka miaka ya 1920.

Nne, mwaka wa 1952 TAA ikishirikiana na Meru Citizens Union ilifanikisha kumpeleka Japhet Kirilo na Earle Seaton UNO katika "petition" ya Mgogoro wa Ardhi ya Wameru na ilikuwa Abdul Sykes akiwa Katibu na Kaimu Rais wa TAA ndiye aliyemwomba Earle Seaton asaidie kutoa ushauri kwa Meru Citizens Union katika mgogoro ule kwani Seaton alisaidia sana TAA Political Subcommittee  katika kuandika mapendekezo ya katiba yaliyokwenda kwa Gavana Twinning 1950, mapendekezo ambayo kama ilivyoelezwa huko juu, ndiyo yaliyotengeneza hotuba ya Mwalimu Nyerere UNO 1955.

Kushoto Earle Seaton na Julius Nyerere baada ya uhuru Seaton
akiwa mfanyakazi wa serikali

Tano, si kweli kuwa hawa wazee walikuwa hawajui nafasi ya Waingereza katika Tanganyika kwani Visiting Mission za UNO zilikuwa zikipita Tanganyika na TAA ikishiriki katika mazungumzo na taarifa zao zikiandikwa katika gazeti la Zuhra lililokuwa likiendeshwa na Ramadhani Mashado Plantan kama mhariri. Hii ndiyo ilikuwa sauti ya Waafrika wa Tanganyika. Nyerere mwenyewe kaandikwa kwa mara ya kwanza jina lake na habari zake  ndani ya gazeti hili mwaka wa 1953. Haiwezekani katika hali ya siasa kama hii ikawa kuwa wazee hawakujua waanzie wapi kudai uhuru. Ukiachia TAA Political Subcommittee 1950 ambamo walikuwa watu wazima kama Mufti Sheikh Hassan bin Ameir, Sheikh Said Chaurembo na John Rupia, zipo pia barua za 1933 walizoandikiana Rais wa African Association Mzee bin Sudi na Katibu, Kleist Sykes zikizungumza kuhusu uhuru wa Tanganyika.

Kwa ajili hii basi si kweli kuwa watu hawakujua namna ya kutaka kujitawala. Abdul Sykes alianza harakati za kuunda TANU akiwa Burma katika Vita Vya Pili Vya Dunia (1938 -1945) na msingi wa kuasisi TANU aliujenga kupitia 6th Battalion ya King African Rifles (KAR) Burma Infantry. Shajara ya Abdul Sykes inaonyesha kuwa mazungumzo ya mwisho ya azma ya kuunda chama cha siasa yaliyafanywa Kalieni Camp India tarehe 25 Desemba 1945 mkesha wa Xmas wakisubiri meli kurejeshwa Tanganyika baada ya kumalizika vita.

Mimi naamini hotuba ya Baba wa Taifa ilitolewa akiwa yeye mwenyewe hajui mengi kabla ya wakati wake. Naamini kabisa kuwa yawezekana pia Mwalimu Nyerere hakuwa anamjua Abdul Sykes vizuri na historia ya baba yake Kleist, katika siasa za ukombozi wa Tanganyika na kuundwa kwa African Association 1929 lau kama aliishi na watoto wake, Abdul, Ally na Abbas kwa karibu sana hadi uhuru ulipopatikana mwaka wa 1961. Lakini vilevile utafiti umeonyesha pia kuwa baada ya uhuru ziliingia sababu nyingine zilizofanya historia ya TANU ielezwe kwa namna alivyoieleza Baba wa Taifa ikiwaweka pembeni baadhi ya wazalendo. Itoshe tu kwa kuhitimisha kusema kuwa hata hao wazee ambao Mwalimu Nyerere hakuwataja kwa majina, alijulishwa kwao na Abdul Sykes na Dossa Aziz. Iwe iwavyo si rahisi kusahau kuwa Msajili wa Vyama Vya Siasa alikataa kuiandikisha TANU kwa kuwa chama hakikuwa na wanachama Nyerere alipofikisha maombi ya TANU kwake. Si wengi wanajua hili lakini Ilikuwa Mzee Said Chamwenyewe ndiye aliyetumwa Rufiji na Abdul Sykes akaandikishe wanachama wa mwanzo wa TANU ambao Baba wa Taifa alifikisha orodha yao ile kwa Msajili wa Vyama Vya Siasa na TANU ikaandikishwa.

Hatujachelewa lau kama miaka mingi imepita bado iko nafasi ya kuwaadhimisha Wazee wa Dar es Salaam na kwengineko waliomuunga mkono  katika kuijenBaba wa Taifa katika kuijenga TANU na kupigania uhuru wa Tanganyika.

No comments: