Tuesday 17 April 2018

PETER MHANDO MUASISI WA TANU TANGA, 1955

PETER MHANDO 
MUASISI WA TANU TANGA
1955
 
Peter Mhando
(Picha kutoka kitabu cha Saadan Abdul Kandoro
''Mwito wa Uhuru''
Utangulizi
Historia hii ya vipi TANU iliundwa Tanga nimeiandika kutokana na mazungumzo niliyofanya na Mohamed Kajembe, Ngamiani Tanga ndani ya duka lake. Mzee kajembe alinionyesha kijitabu cha mwaka 1955 kilichoandikwa kwa penseli ambamo ndani yake aliandika tarehe za mikutano na majina ya wanachama waasisi wa TANU. Mzee Kajembe alifariki Juni, 1996.

***
Jimbo la Tanga lilibarikiwa na kuwa na Waafrika walioelimika sana. Waafrika hawa walikuwa kutoka kabila la Wabondei. UMCA ilikuwa imehama kutoka Zanzibar kwenda Magila katika Jimbo la Tanga mwaka 1875. Ukristo ulianzishwa na kustawi katika nchi ya Wabondei, na vivyo hivyo nafasi za elimu kwa watoto wa Wabondei. Katika lile wimbi la kuwania nafasi za elimu, watoto wengi wa Kiislamu walibatizwa. Ni jambo la kawaida miongoni mwa Wabondei kukuta majina kama Peter Saidi au John Ramadhani. Huu ni ukumbusho wa damu ya Kiislam katika Wabondei. Wabondei wengi walikwenda Makerere College na siasa za kizalendo zilipoanza baada ya Vita Kuu ya Pili (1938 – 1945), Wabondei walikuwa wamejaa katika utumishi wa serikali ya kikoloni. Gurudumu la historia ya Tanganyika likizungushwa na baadhi ya Wabondei, maarufu miongoni mwao wakiwa watu kama Martin Kayamba aliyejikomba sana kwa wakoloni, George Magembe mtu ambae huku hayuko kule hayuko, hujui kama yupo na wazalendo au na wakoloni, Stephen Mhando; mzalendo mwenye msimamo mkali na mdogo wake Peter ambae alikuja kufanya makubwa katika harakati za kuunda TANU na kupigania uhuru wa Tanganyika lakini alifariki akiwa kijana sana kabla ya uhuru kupatikana.

Wabondei walikuwa ndiyo walimu, makarani, wakalimani mahakamani na maofisa wa ustawi wa jamii katika serikali ya kikoloni. Hili lilikuwa tabaka maalum la Waafrika, waliosomeshwa na wamishonari kuitumikia serikali ya kikoloni na katika kufanya hivyo kulitumikia Kanisa na Ukristo, uhusiano ambao ulikuwa wenye manufaa kwa pande zote mbili zilizokuwa  zikishirikiana. Ilikuwa vigumu sana kwa Wabondei kutokana  na upendeleo huo wasifikirie kwamba wana uhusiano maalum na Kanisa na serikali ya kikoloni. Hawa Waafrika wasomi kutoka shule za misheni na Makerere walikuwa watiifu kwa taasisi mbili zanye nguvu nchini, yaani serikali ya kikoloni na Kanisa. Kwa ajili hii basi, ilibakia kwa Wadigo Waislam wasiokuwa na elimu kama elimu ilivyokuwa ikiitikadiwa, kuunda TANU na kuongoza harakati za kudai uhuru.

TANU iliasisiwa Tanga mwaka 1955 kukabiliana na serikali ya kikoloni kupitia juhudi binafsi za kikundi cha wafanyabiashara wadogo wadogo katika soko la Ngamiani. Kikundi hiki kiliongozwa na kijana mdogo Peter Mhando, ambae kabla ya hapo katika siku za nyuma alikuwa katibu wa kikundi cha majadiliano cha wasomi wa Kibondei kilichojulikana kama Discussion Group. Peter Mhando alikuwa akifanya kazi kama mhandisi katika Noran Industries- wanunuzi wa nazi na watengenezaji sabuni pale Tanga. TAA ilikuwapo mjini hapo lakini ilikosa umoja baina ya wakazi wa mji kwa kubaguana kwa dini, kabila, rangi na kiwango cha elimu. Discssion Group na vyama hivi vilikuwa vimeshikwa na Wabondei wasomi wengi wao wakiwa Wakristo. Hali hii iliviza juhudi za kuunda TANU. Vikundi hivi vya majadiliano, vilitarajiwa kutojihusisha na siasa na vilitiwa nguvu na serikali vikihimizwa kufanya mijadala na kusoma vitabu. Katika muda wote wa uhai wa vikundi hivyo hawa wasomi wa Kibondei walikuwa chini ya usimamizi wa afisa Mzungu.

Akikiongoza kikundi hiki cha wafanya biashara wa Soko la Ngamiani, alikuwa baharia mstaafu, Hamis Heri Ayemba. Hamis Heri alikuwa Mmanyema kutoka kabila la Wakusu wazee wake wakitokea Belgian Congo. Hamisi Heri alikuwa na umri wa katikati na katika ujana wake alikuwa baharia na alipata kusafiri chombo kimoja na Abeid Amani Karume, ambae baadae alikuja kuwa rais wa Zanzibar. Baada ya Vita Kuu ya Pili, Hamisi Heri alirudi kwao Tanga ili aanze biashara. Hamiri Heri alikuwa mtu aliyejikuza na kujielimisha mwenyewe; na alikuwa amesafiri sana. Hamisi Heri alizungumza vizuri sana Kiingereza na Kiarabu. Katika miaka yake ya mwanzo katika biashara, alikuwa dalali. Heri aliwashangaza wateja wake kwa uhodari wake wa lugha mbali mbali, akinadi bei kwa Kihindi au Kiarabu, kutegemea utaifa wa watu waliokuwepo pale mnadani.

Harakati za kudai uhuru zilipoanza Heri alikuwa ametajirika na mmoja wa Waafrika wenye kuheshimiwa sana mjini Tanga. Peter Mhando alipochoshwa na kile kikundi cha majadiliano, alijiunga na Hamisi Heri na kikundi cha wafanya biashara wa Ngamiani pale mjni ambao walikuwa wakijitahidi sana kuunda tawi la TANU. Wakati huo mwanasiasa mwenye uzoefu mkubwa kuliko wote mjini Tanga alikuwa Mwalimu Kihere.Lakini siasa za mapambano baina  ya ule uongozi wa TAA na kikundi cha majadiliano zilimzuia kutoa mchango wowote wa maana. Mwalimu Kihere alikuwa amehudhuria mikutano kadhaa ya African Association tangu mwaka 1946. Wakati wa uongozi wa Abdulwahid Sykes katika TAA Mwalimu Kihere alikuwa amedumisha uhusiano mkubwa sana baina yake yeye mwenyewe binafsi, Abdulwahid na Dossa Aziz. Hii ilifanya vilevile adumishe mawasiliano ya karibu sana na makao makuu ya TAA. Lakini kwa sababu ya mizozo katika siasa hapo Tanga, ule mkutano mkuu wa kuasisiwa TANU uliofanyika Dar es Salaam mwaka wa 1954 ulipita bila ya Tanga kupeleka mjumbe.

Kile kikundi cha wafanyabiashara wadogo wadogo katika soko la Ngamiani kiliitisha mkutano katika Ukumbi wa Tangamano tarehe 5 Septemba, 1955. Waliohudhuria mkutano huo walikuwa Hamis Heri, Peter Mhando, Mohamed Kajembe,Tuwa Abdallah, Dhili Mgunya, Abdallah Rashid Sembe, Victor Mkello, Mohamed Sadik, Hassan, Peter Ramadhani Jembe na Ali Mohamed. Peter Ramadhani tayari alikuwa mwanachama wa TANU huko Arusha na alikaribishwa mkutanoni ili waasisi wa TANU wanufaike kutokana na uzoefu wake. Wasomi wa Makerere, uongozi wa TAA chini ya Waarabu na Mwalimu Kihere hawakuwepo kwenye mkutano huu muhimu. Mkutano ulifunguliwa na Hamis Heri saa tisa adhuhuri na ulifungwa saa mbili baadae kwa uamuzi kuwa mkutano mwingine wa kuchagua viongozi wa chama ufanyike tarehe 23 Oktoba. Mkutano uliamua vilevile kuwa juhudi zifanyike kupata waanachama wengi iwezekanavyo. Kiasi kidogo cha fedha kilikusanywa na Harir Omari Siagi alipewa aende makao makuu ya TANU, Dar es Salaam kununua kadi 70  za TANU.

Tarehe 23 Oktoba, wanachama wa mwanzo wa TANU huko Tanga walikutana kuchagua uongozi wao chama. Hamisi Heri alichaguliwa kuwa mwenyekiti na Peter Mhando katibu. Jumla ya watu arobaini na tano walihudhuria mkutano huo na wakapewa kadi za TANU. Mwalimu Kihere alihudhuria mkutano ule lakini hakuchaguliwa katika nafasi yoyote ya uongozi. Kamati ya wanachama iliundwa kutokana na wale wanachama kumi na moja waasisi waliokutana katika ule mkutano wa kwanza mwezi uliopita. Kamati hiyo ilikuwa na wajumbe wafuatao: Abdallah Rashid Sembe, Mohamed Kajembe, Victor Mkello, Dhili Mgunya, Ali Mohamed, Abdallah Mohamed na Mohamed Sadik. Peter Mhando alijitolea nyumba yake kuwa ofisi ya kwanza ya tawi la TANU mjini Tanga. Mara tu baada ya mkutano huu wazee wa Tanga wakiongozwa na Makoko Rashid, mwanachama wa zamani wa TAA walianza kufanya kampeni kwa ajili ya TANU. Chama kilipata msukumo mwingine na kuongezeka nguvu wakati Sadik Ali Patwa Muasia tajiri alipoingia TANU.

Patwa alikuwa Muislam wa madhehebu ya Shia. Patwa alikuwa amehamia Tanganyika kutoka Zanzibar mwaka 1918 baada ya kumalizika kwa Vita Kuu ya Kwanza. Pale Tanga Patwa alianzisha kiwanda cha soda na akatajirika. Wakati huo wa zama za ukoloni wakati Waasia wenzake walikuwa wakiwabagua Waafrika, Patwa alikuwa akikaa na Waafrika wa rika lake akinywa nao kahawa. Halikadhalika watoto wake wakawa wanacheza kandanda na vijana wenzao wa Kiafrika katika vilabu vya Tanga. Hili lilikuwa jambo geni na lisilokuwa la kawaida kutoka kwa familia ya Kiasia wakati wa ukoloni. Patwa alisaidia harakati za kudai uhuru kwa hali na mali, na akaifanyia kampeni TANU miongoni mwa jamii yake mwenyewe ya Kiasia. Wakati wa harakati Nyerere alikuwa akifanyiana maskhara na  Patwa akimwambia, ‘’Mzee Patwa baada ya kupata uhuru nadhani tukuteuwe uwe balozi wetu India.’’ Lakini Patwa hakuiona Tanganyika huru, alifariki kabla ya uhuru kupatikana.

Baada ya kufungua tawi la TANU mjini Tanga, uongozi wa chama ulimwalika Julius Nyerere, Bibi Titi Mohamed, John Rupia na Mbutta Milando kufanya ziara Tanga. Nyerere alifikia nyumbani kwa Hamisi Heri. Ujumbe huu kutoka makao makuu ya TANU ulipata makaribisho makubwa yaliyoandaliwa na vyama vya lelemama ambavyo kwa kawaida vilikuwa vingi sana katika pwani ya Afrika ya Mashariki kutoka Mombasa nchini Kenya hadi Mikindani, Tanganyika. Kiongozi wa akina mama hawa mjini Tanga aliyesaidia kuieneza TANU alikuwa Bibi Mwanamwema bint Sultan, ndugu wa mbali wa mwenyekiti wa TANU Tanga, Hamisi Heri.

Matokeo ya ziara ya Nyerere Tanga ilikuwa ni kumrudisha Mwalimu Kihere katika siasa. Baada ya kushindwa kupata nafasi yoyote katika chama, Mwalimu Kihere alipoteza shauku ya siasa. Nyerere alipokuja Tanga kuifanyia kampeni TANU ndipo Mwalimu Kihere alikaribishwa kujiunga na chama. Mwalimu Kihere alifahamiana na Nyerere mwaka 1946 walipokutana Dar es Salaam katika mkutano wa mwaka wa African Association. Nyerere alipozuru Tanga Mwalimu Kihere alitaka kufanya dhifa nyumbani kwake kwa heshima yake. Uongozi wa TANU, hususan Hamisi Heri na Mzee Makoko walikataa kumruhusu Nyerere kuhudhuria dhifa hiyo kwa sababu Mwalimu Kihere alikuwa hajaonesha nia ya kuiunga mkono TANU. Nyerere akitambua utu uzima wa Mwalimu Kihere, uzoefu na sifa yake ya uongozi katika African Association, alishauri uongozi wa TANU Tanga usiache fursa ile ipite bure. Nyerere alitoa hoja kuwa, ilikuwa muhimu kukubali mwaliko wa Mwalimu Kihere na kutumia fursa hiyo kumuomba arudi kwenye harakati kwa kuwa TANU ingefaidika kutokana na uzoefu wake alioupata katika African Association. Kwa ajili ya nasaa hiyo TANU ilikubali mwaliko wa Mwalimu Kihere na Nyerere alihudhuria dhifa ile nyumbani kwa Mwalimu Kihere pamoja na wanachama wengine.

Mwalimu Kihere alikuwa mwanasiasa wa msimamo wa wastani, alikuwa mbali na msimamo mkali dhidi ya serikali. Kwa ajili hii Mwalimu Kihere alielewana vizuri na utawala wa kikoloni. Hii ilikuwa kinyume kabisa na wazalendo wengine kama Mzee Makoko Rashid ambaye kwa miaka mingi alijulikana kwa chuki yake dhidi ya Waingereza. Inasadikiwa kwamba watu wawili wataingia katika historia kwa chuki zao mahsusi dhidi ya Waingereza, mtu wa kwanza ni Abdillah Schneider Plantan na wa pili ni Mzee Makoko Rashid. Wote wawili walifungwa gerezani kwa sababu ya msimamo wao dhidi ya serikali ya kikoloni. PC na DC wake wote wawili walikukubali mwaliko wa Mwalimu Kihere. Mwalimu Kihere alimtambulisha Nyerere kwa wageni mashuhuri na alimuomba azungumze maneno machache. Nyerere kwa kipaji chake cha ufasaha wa kuzungumza alitoa hotuba kuhusu lengo la TANU na kanuni za kidemokrasia kama zilivyoelezwa na Umoja wa Mataifa. P.C. alisimama baada ya Nyerere kuzungumza na akatoa hotuba kwa niaba ya serikali. P.C. alimsifu Nyerere kuwa ni mwanasiasa mzuri kinyume na vile alivyosikia kabla ya kukutana naye. Hapo hapo alitoa ruhusa kwa Nyerere na TANU kufanya mikutano ya hadhara katika wilaya zote za jimbo hilo. Lakini uhusiano huu haukudumu, serkali iliyapiga marufuku matawi kadhaa ya TANU Tanga mara tu baada ya kuundwa kwa United Tanganyika Party (UTP).

Siku iliyofuata mabingwa wa hotuba wa TANU, Julius Nyerere na Bibi Titi Mohamed walihutubia mkutano wa hadhara kwenye uwanja wa Tangamano. Hii ilikuwa hatua kubwa sana kwa TANU, na kwa harakati dhidi ya ukoloni pale Tanga.  Ilikuwa muda mrefu umepita tangu zile siku za zile siasa za wasomi katika Discussion Group, kikundi cha majadiliano; na ile mizozo baina yao na ule uongozi uliokuwa katika TAA. Baada ya hapo, Mwalimu Kihere alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa TANU Tanga badala ya Hamisi Heri na Amos Kissenge alichaguliwa katibu. Abdallah Rashid Sembe mmoja wa wanachama waasisi wa mwanzo kabisa wa TANU alichaguliwa kuwa mjumbe wa Kamati Kuu ya Taifa ya TANU akiwakilisha Jimbo la Tanga. Haukupita muda mrerfu mpangaji mikakati mzuri Peter Mhando akahamishiwa Makao Makuu ya TANU Dar es Salaam na kutoka hapo alipelekwa Tabora ambako kulikuwa na matatizo.

Tabora TANU ilichelewa kuundwa na mara tu chama kilipoundwa kukazuka ugomvi baina ya ofisi ya wilaya na ile ya jimbo. Ilipoingia mwaka 1956, matawi ya TANU yalikuwa yamefunguliwa katika wilaya zote nane za Tabora kwa nguvu za uongozi wa wilaya. Mwaka 1957 malalamiko yaliyokuwa yakitoka ofisi ya wilaya mjini Tabora iliyokuwa chini ya uongozi wa Wamanyema ilikuwa kwamba ofisi ya jimbo chini ya Germano Pacha haikuwa imara kwa hiyo ulitaka uchaguzi ufanywe ili kuchagua katibu na mwenyekiti mpya wa jimbo na kumng’oa Pacha toka kwenye uongozi. Katika jimbo pale Tabora mjini TANU kwa hakika haikuwa na ofisi yake yenyewe na hii iliathiri sana utendaji kazi wa Pacha. Ijapokuwa kulikuwa na ukweli kidogo katika zile tuhuma, Pacha aliyachukulia matokeo yote haya mapya kama ni kisingizio na juhudi za makusudi za kumtoa yeye madarakani.

Mzee Fundi Mhindi, mwanasiasa mkongwe na mwanachama muasisi wa African Association mwaka 1945 na mmoja wa waasisi wa TANU mwaka wa 1955 katika Jimbo la Magharibi na sasa akiwa Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa TANU Tabora, alitumwa kwenda makao makuu ya TANU Dar es Salaam kujadili tatizo la uchaguzi katika Jimbo la Magharibi.  Mzee Fundi Mhindi alifanya majadiliano na Julius Nyerere na John Rupia. Makao makuu ya TANU yaliamua kumtuma Peter Mhando kwenda Tabora kufanya uchunguzi na kuandika taarifa ambayo ingetoa msingi wa ufumbuzi wa kudumu kuhusu matatizo yanayoisibu TANU pale Tabora. Wakati ule Peter Mhando alikuwa kijana wa kiasi cha miaka ishirini hivi. Peter Mhando aliifanya kazi ile akishirikiana na vijana wengine kama Bilal Rehani Waikela, Ramadhani Abdallah Singo, Abdallah Saidi Kassongo na vijana wengineo. Peter Mhando alikamilisha taarifa ya mgogoro wa TANU Jimbo la Magharibi na kuituma makao makuu. Makuu makuu ya TANU ilichukua hatua kutokana na ile taarifa ya Mhando na kumpeleka Said Ali Maswaya Tabora kutoka Shinyanga kuwa katibu wa mkoa badala ya Pacha. Katika taarifa yake kwa makao makuu ya TANU, Peter Mhando alipendekeza kuwa mkutano mkuu wa mwaka wa 1958 wa TANU uliokuwa unakaribia, ufanyike Tabora ili kukipa chama nguvu zaidi katika Jimbo la Magharibi. Hivi ndivyo Tabora ilivyokuja kuandaa na kuwa mwenyeji wa ule mkutano muhimu wa TANU uliojadili kura tatu. Hii ilikuwa ndiyo kazi ya mwisho ya Mhando kuifanyia TANU kwani alifariki kwa ugonjwa wa kisukari mara tu baada ya kutayarisha na kutuma taarifa yake makao makuu ya TANU.

No comments: