Monday 14 May 2018

WAJUE WANA SAIGON CLUB WA MZIZIMA - NA ALHAJ ABDALLAH TAMBAZA


Shajara ya Mwana Mzizima:
WAJUE WANA SAIGON CLUB WA MZIZIMA
Na Alhaji Abdallah Tambaza

Saigon Khitma  Jumapili 13 May 2018
Raia Mwema 14 - 15 May 2018

JUMA hili, shajara imeonelea ichepuke kidogo kutoka kwenye siasa na kuangalia mambo ya kijamii kidogo ili wasomaji wasichoshwe na historia ya siasa peke yake;   leo tutaangazia habari nyengine kutoka katika jamii tunamoishi.

Vijijini kule tunakotoka, ukitaja neno ‘klabu’ au klabuni, basi moja kwa moja hiyo inamaanisha kwamba umekusudia mahala ambapo watu – wanawake kwa wanaume—watakuwa wamejazana wakinywa ‘mapombe’ yale ya kienyeji yaliyovunda na kutoa harufu mbaya kabisa.

Mijini hali kadhalika, ukisema ‘nakwenda klabu’ maana yake ni kwamba unakusudia klabu cha usiku (Night Club), ili pia ukalewe na, au kukesha huko ukicheza muziki na mambo mengine ya anasa kama kucheza kamari na kuvinjari na warembo wa mjini hapo. Klabu pia inaweza kuwa kama vile klabu za mpira za Simba, Azam na Yanga ili kwenda kujumuika na wapenzi na marafiki mzungumzie masuala ya soka na michezo mengine kama tenisi na gofu (Gymkhana) na Leaders Club (Klabu ya Viongozi pale Barabara ya Ali Hassan Mwinyi), siasa na biashara—basi hakuna zaidi.

Jijini Dar es Salaam, hususan maeneo ya katikati ya Kariakoo, inapatikana klabu moja mashuhuri sana inayojulikana kama Saigon Club, yenye maskani yake pale Mtaa wa Narung’ombe na Livingstone. Ni klabu kongwe ambayo umaarufu wake umezagaa kila pembe, ambapo hakuna mwenyeji wa jiji hili, atasema haijui au hajawahi kuisikia. Saigon kabla ya kuhamia Mtaa wa Narung’ombe na Livingstone ilikuwa Mtaa wa Sikukuu na Narung’ombe.

Madhumuni ya klabu hiyo—‘raison d’etre’— ni tofauti kabisa na vilabu vingine vyote tulivyovizoea katika maisha ya kawaida. Hapo hapachezwi mpira (ingawa wanachama wake labda kwa kiasi fulani ni wapenzi wa mpira), wala mchezo wa aina yoyote ile kama karata, drafti na dhumna. Hii siyo kusema kuwa Saigon haikuwa klabu ya mpira. Saigon ilianza kama klub ya mpira ya watoto wadogo wa shule za msingi na wakakua nayo hadi ukubwani na walipokuwa sasa hawawezi tena kucheza mpira Saigon ikabaki kama barza, mahali wanakutana kwa mazungumzo.

Klabu hii ya kupigiwa mfano au yenye mfano wa kuigwa, ni mahala ambapo watu huenda jioni na kuzungumza mambo mbali mbali ya kijamii na namna ya kuyatafutia ufumbuzi wa haraka kwa mustakabali wa jiji la Dar es Salaam na watu wake.

Orodha ya wanachama wake imekusanya watu kutoka katika kada mbalimbali wakiwamo kwanza hao wanamichezo, wapenzi wa michezo, masheikh, maimamu, walimu wa skuli na madrassa; pamoja na wanasiasa waandamizi wakiwamo mpaka marais, mawaziri, wabunge na madiwani.

Wamo pia wanajeshi la Ulinzi, Polisi, Usalama wa Taifa, Madaktari na wafanyabiashara wakubwa na wadogo wa mjini Dar es Salaam wa jinsia zote.

Klabu ya Saigon ina madhumuni tofauti na vilabu vyengine na mambo yanayofanyika pale ni aghlabu kuyakuta kwenye vilabu vya kawaida tulivyovielezea hapo awali.

Kwanza, uanachama wake hauangalii umri, jinsia, dini, kabila, itikadi ya vyama vya siasa, cheo, na mambo kama hayo. Utanzania wako ndiyo kigezo kikuu cha kuwa mwanachama ingawa klabu ni ya watu wa Dar es Salaam.

Katika kalenda yake ya mwaka, Klabu ya Saigon huadhimisha mambo makubwa  matatu hivi.



Kwanza, ni kuandaa shughuli kubwa siku chache kabla ya kuingia mwezi mtukufu wa Ramadhani kwa kuwaalika watu mashuhuri kuja kujumuika na jamii ya kawaida kuja kuwaombea dua wanachama wa klabu hiyo waliotangulia mbele ya haki, pamoja na wakazi wa jiji hili ambao maisha na matendo yao walipokuwa hai, yaliacha athari na kumbukumbu kwa watu wa jiji hili.

Kushoto Brigadier General Mstaafu Simba Waziri, Mwinyi Mangara
na Boi Risasi katika futari ya mwaka wa 2010
Hao ni pamoja na wasanii wa fani mbalimbali; mashekhe na walimu wakubwa; wazee mashuhuri pamoja na viongozi waliopata kushika nyadhifa mbalimbali jijini Dar es Salaam na kugusa nyoyo za watu.
 
Katikati Abdallah Tambaza mwandishi wa makala hii na kulia
Mussa Shagow na kushoto ni Mwinyikhamis Mwinyimadi

Shughuli hiyo ya khitma, husababisha kufungwa kwa matumizi ya kawaida, barabara yote ya Narung’ombe kuanzia Sikukuu mpaka ile ya Livingstone. Idadi ya wahudhuriaji huwa zaidi ya watu elfu 4000 mpaka 5000. Vyakula vya aina mbalimbali hupikwa kwa wingi sana siku hiyo na vinywaji baridi na matunda hutolewa kwa wageni.

Sherehe hii, ambayo huwa si ya kukosa kuhudhuria kwa wenyeji, hufana sana maana huwa imepangiliwa kwa ustadi mkubwa kuanzia madua na visomo mbalimbali, pamoja na wazungumzaji wa kutoa nasaha zenye mazingatio kwa waalikwa.

Kila mwaka huwa inaushinda mwaka uliotangulia kwa ubora. Huwa ni hadhara ya aina yake iliyojaa vicheko, utani na vitimbi mbalimbali vya Usimba na Uyanga kwa watu kupigana vijembe vya upendo.

Pili, ni kuandaa futari maalumu katika siku moja ya Ramadhani na kufuturisha watu wa jiji hili bila ubaguzi, hata kama mtu hukufunga au si Mwislamu huwa anakaribishwa kujumuika. Kitendo hicho, si tu kinajenga udugu miongoni mwa wanachama, bali hutoa fursa kwa watu mbalimbali kukutana na kula pamoja futari hiyo katika hali ya furaha na upendo.

Daima kwenye futari hizo za kimrima, waandaaji huhakikisha vile vitu vyote vizuri vinakuwamo sahanini, siniani na vyanoni—iwe ndizi mzuzu na mihogo kwa papa; tambi, kaiamati na maandazi; mikate ya kusukuma na ya kumimina; bajia, sambusa na kachori pia huwamo. Uji wa pilipili manga na ‘chai za zatari’ huhanikiza kwa harufu nzuri mahala hapo. Waandaji huweka pia makombe (mabakuli makubwa) ya michuzi ya kuku, maini na mbuzi pia. Vitu huwa vimekamilika kisawasawa vyenye kutamanisha machoni na mdomoni!    

Wazalendo hawa wa Saigon huwa hawaishii hapo, bali pia huandaa sherehe ya usiku mmoja ya kasida za Mtume Muhammad, kwa ajili ya mahujaji wa jijini ambao walibahatika kwenda kufanya Ibada ya Hija na kurejea salama. Hii nayo hupendeza kwelikweli, maana hutoa fursa kwa mahujaji, wakiwa kwenye kanzu zao nzuri zenye kumeremeta, kuja kuelezea waliyoyaona na kuyadiriki walipokuwa kule kwenye miji mitukufu ya Makkah na Madina katika Hijja na Umra kwa kuwaburudisha kwa kasida zinazoimbwa na kughaniwa kwa sauti nyororo.

Hii huwa ni nafasi nzuri kwa wasiobahatika kuwenda Hijja ya kuombewa dua na watu wale watukufu siku za mwanzo kabisa, kwani imesemwa kwamba dua za mahujaji kabla ya siku 40 kwisha huwa mustajaba (hukubaliwa na anayeombwa).

Saigon Sports Club, hapo mwanzoni iliundwa na vijana wadogo wa skuli za Mchikichini na Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam, mwaka 1966, ikiwa kama klabu ya mtaani kwa madhumuni ya kucheza mpira na watoto wenzao wa mitaa mingine.

Kwa mujibu wa Alhaji Mussa Mohammed Shaggow, mwanachama mwandamizi, waanzilishi wachache wa mwanzo wa klabu hii wakati huo ikijulikana kama Everton ni pamoja na Mussa Shaggow mwenyewe, Harudiki Kabunju, Yaakub Mbamba, Atika Kombo, Abdu Shiba, Dachi na Salum Khalil akiwa Golikipa wa mwanzo klabuni.


Kulia Atika Kombo, Harudiki Kabunju na Sunday Kayuni
wakijikinga mvua katika khiyma ya mwaka wa 2017

Kushoto Abdu Shiba na Mohamed Said

Timu nyingine za watoto wa mitaani siku hizo hapa Kariakoo, ni pamoja na iliyokuwa jirani yao, Cuba Rovers, New Take Time, New Port (mwandishi huyu alikuwa mwanachama), Dundee, Young Kenya na Young Boys. Zote hizo ziliundwa na vijana wadogo wa umri wa wastani wa miaka 14 wa maeneo ya Kariakoo, ili kutoa ushindani wa kimpira.

Sasa kadri miaka ilivyokuwa inakwenda mbele na vijana wale kuondoka kutoka utoto na kwenda ukubwani, wakabadilisha madhumuni ya klabu yao na kuwa haya sasa ili kudumisha udugu wao pamoja na kuwapokea wanachama wapya wakiwamo wanawake na wazee pia.

Kwa sasa, Saigon mpya yenye malengo mapya na maono mapya, inaongozwa na Mahmoud Mbarak kama Mwenyekiti, akisaidiwa na Juma Abeid ‘Spencer’. Boi Juma ni Katibu wa Klabu akisaidiwa na Mohammed Msitu na Alhaji Mussa Shaggow Mweka Hazina akisaidiana na Abdul Risasi. Kwenye orodha ya wajumbe yumo Muharram Mkamba, Mohammed Tall, R. Sultan na wanawake Hamida Simba na Awena Kitama.

Iddi Simba, mwanasiasa mkongwe na aliyewahi kugombea urais wa nchi hii, kupitia CCM ndiye mlezi wa Saigon ambaye kila mara amekuwa mstari wa mbele kuitetea na kuihami pale inapotaka kutetereka au kwenda kombo, kwani klabu hii ni kioo cha uzalendo uliotutuka kwa kufanya mambo makubwa ambayo wengi wamejaribu kuyaiga lakini wameshindwa vibaya.

Dr. Gharib Bilal akitoa nasaha katika Khitma ya Saigon
Kushoto Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi na mwisho kulia Idd Simba

Wamo pia katika wanachama na wapenzi wakubwa wa Klabu ya Saigon, Rais mstaafu wa Awamu ya Nne Jakaya Mrisho Kikwete na Makamu wake Dk. Mohammed Gharib Bilal. Wengine ni Mwanasiasa mashuhuri wa nchi hii hayati Ali Sykes na nduguye Balozi Abbas Sykes pamoja na watoto wao Kleist Sykes (sasa marehemu), Abraham na Ayoub Sykes. Yumo pia Mussa Azzan Zungu, Mbunge wa Ilala, na marehemu Balozi Abdul Cisco Mtiro na ACP Kamanda Mohammed Chico (sasa marehemu).


Kulia Ally Sykes, Sheikh Issa ''Smart Boy'' Ausi, mwisho
kushoto Juma ''Spencer'' Abeid

Kulia marehemu Balozi Cisco Mtiro, Mrehemu Sheikh Hussein, Sheikh
Shomari na Abraham Sykes katika Khitma ya Saigon
   
Mheshimiwa Mussa Zungu katikati akifuturu

Madhumuni mapya ya uwepo wa Klabu hiyo, pamoja na hayo niliyaeleza hapo juu ni pamoja na kusaidiana kwa shida; kufa na kuzikana. Saigon pia imekuwa kimbilio kubwa la wanasiasa wakubwa na wadogo wanaowania nafasi za uongozi katika ngazi mbali mbali hapa nchini ili kupata kuungwa (endorsement).

Hivyo basi kutokana na kuwa na wanachama wa rika na kada mbalimbali inakuwa rahisi kwa mgombea kukubalika jijini kama watu wa Saigon watamridhia na ‘kumpigia debe’ tiketi yake. Hiyo imethibitika mara nyingi na hivyo kuwa na ulazima wa kujitambulisha mapema kwa wana Saigon pale mgombea anapotangaza nia. Cha ajabu ni kwamba, hiyo si kwa wanasiasa peke yao bali hata wale wanaogombea kwenye vilabu vya mpira vya Simba na Yanga na kwenye ofisi za TFF za Taifa—Saigon wana mkono mrefu na nguvu kote huko. Fitna za siasa na mpira wanajua kuzicheza.

Lakini basi pamoja na mafanikio yote hayo mazuri, klabu ya Saigon imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo zimesababisha kuwepo na makundi mawili hasimu yasiyoiva pamoja. Jitihada mbalimbali zimefanywa kuwarudisha pamoja kwa faida ya watu wa Dar es Salaam, mpaka leo hazijazaa matunda. Hivyo ni jukumu letu kuzidi kumwomba Allah (SWT) aipeperushe fitna hii kwa mbali na amani nzuri irejee pale Saigon ili Dar es Salaam yetu iendelee kustawi. Wahenga walisema; ‘wengi huitwa wale na mmoja huitwa yule!’

Hiyo ndiyo Saigon Club, yenye kuunganisha watu kwa namna ya kipekee ambayo haijapata kufanywa, kuwepo au kutokea mfano wake hapa Tanzania katika huu umri wa miaka 60 wa kujitawala.

Jana tarehe 13 May 2018 Saigon walifanya khitma ambayo juu ya kuwa ilinyesha mvua kubwa wengi walihudhuria.
Alamsiki!
Simu: 0715808864
atambaza@yahoo.com

No comments: