Tuesday, 3 June 2014

TAAZIA: KIFO CHA SHEIKH MANZI BIN SAID BIN MANZI AMIR NA IMAM WA MSIKITI WA MWINYIMKUU MAGOMENI MAPIPA


TAAZIA: SHEIKH MANZI BIN SAID BIN MANZI
AMIR NA IMAM WA MASJID MWINYIMKUU AMEFARIKI
Sheikh Manzi bin Said bin Manzi
Masjid Mwinyimkuu
Siku mbili zilizopita tulitangaziwa msikitini petu Masjid Nur Magomeni Mapipa ugonjwa wa Sheikh Manzi. Leo tarehe 4 Shaaban 1435 sawa na 3 Juni 2014 baada ya sala ya Alfajr tukatangaziwa kifo cha sheikh wetu. Si zaidi ya juma moja nimekutana na Sheikh Manzi Magomeni Mapipa nyakati za asubuhi. Kama kawaida yake yeye alikuwa mtu wa kutabasamu nyakati zote. Akanisasalimia kwa bashasha yake niliyoizoea kisha akaniambai kwa njia ya maskhara, ''Sheikh Mohamed nakusoma.'' Akacheka sana huku anatingisha kichwa. Ajabu kwa watu wenye ilm kama ya Sheikh Manzi kutunyanyua watu kama sisi kwa cheo adhim cha usheikh. Sheikh Manzi mimi ni mzungumzaji wangu sana tukikutana kama kawaida lazima nimuulize ujenzi wa Msikiti wa Mwinyimkuu ambao amekuwa akiusimamia kwa muda sasa. Akanifahamisha kuwa msikiti unakwenda vyema. Si kama huu msikiti siujui.

Msikiti wa Mwinyimkuu ni jirani yangu sana na hupita hapo mara kwa mara na nikiona ghorofa zinavyopanda nami hushukuru. Siku hii Sheikh Manzi akaniambia kitu ambacho nilikuwa mie sikijui. Katika mazungumzo yetu pale nikamtaja Sheikh Hassan bin Amir. Sheikh Manzi akanishika mkono akanambia, ''Sheikh Mohamed, Sheikh Hassan bin Amir ndiyo mwalimu wangu.'' Nilipigwa na butwaa. Nikamjibu Sheikh Manzi nikamwambia, ''Sheikh Manzi sasa nimekufahamu zaidi. Nilimsikia Sheikh Abdallah Iddi Chaurembo akisema tena katika darsa Msikiti wa Mtoro kuwa, ''Mwanafunzi mwenye akili ya kawaida hendi kusoma kwa Sheikh Hassan, ukiona mwanafunzi kabeba kitabu anakwenda kusoma kwa Sheikh Hassan bin Amir basi jua huyo akili yake si ya kawaida.''

Kama kawaida kwa adab ya watu alim akaninilalamikia kunituliza kuwa yeye alikuwa mwanafunzi mtoto wa kawaida tu. Lakini kwa yule aliyepata kumsikia Sheikh Manzi akiwaidh utajua kwa hakika amesoma vizuri. Tulipoagana nikawa sasa naendelea na safari yangu nikawa nawaza ndani ya nafsi yangu, ‘’Kumbe ndiyo maana katika khitma ya Sheikh Ali bin Abbas miezi michache iliyopoita alipoombwa amzungumze Sheikh Ali bin Abbas alimzungumza kwa undani kabisa, kumbe katika miaka ile wote walikuwa wanafunzi watoto kwa Sheikh Hassan bin Amir.’’

Majuma machache yaliyopita mie na wenzangu wa Masjid Nur tulikuwa tunazungumza kuhusu mwezi mtukufu wa Ramadhani na matayarisho yake. Yakanijia mazungungumzo niliyofanya mwaka jana na rafiki yetu mmoja ambae mimi ndiye aliyenijulisha kwa Sheikh Manzi nikawa nasema, ''Mnajua jamani kwa nini Sheikh Manzi yeye kila mwaka anatushinda katika kugawa futari kule mtaani kwake? Ni kwa sababu yeye kwa miaka mingi ametengeneza ''data bank,'' ya wajane, yatima, wazee na wengineo wanaohitaji futari. Sasa mimi mkinituma kwa yule rafiki yetu kweli anatupa lakini hatupati kwa wingi kwa kuwa hatuna hesabu iliyokamilika kwa hiyo mwaka huu kama tutakwenda tena na mikono mitupu tutapata kama kawaida lakini Sheikh Manzi atatushinda tena yeye mipango yake itakuwa imesimama vizuri kila mwaka.'' Ikawa sasa sote tumepwelewa hatujui tuanzie wapi kuitengeneza hiyo ‘’data bank.’’ Ikawa tunasema, ''Hapa la kufanya ni kumwendea Sheikh Manzi atufundishe namna ya kujenga, ''data base'' kama yake aliyotengeneza pale Msikiti wa Mwinyimkuu.'' Kufikia umuzi huu ikawa sasa kila mtu anasema lake kuwa kwa mwaka huu tumechelewa lakini hili tulifanyeni ni jambo zuri. Ndani ya nafsi yangu nikawa najisemea mwenyewe, ''Lo! Mwaka huu tena Sheikh Manzi katushinda yule rafiki yetu sijui atatuonaje maana mwaka jana tulilia ngoa, ''Bwana mbona  Sheikh Manzi unamjazia na sisi tunataka kama yeye au tumshinde.'' Rafiki yetu akawa anacheka akajibu, ''Sheikh Manzi ana orodha kamili nyinyi mnayo? Sisi ukweli wa mambo tulikuwa tumeliendea jambo lile bila ya mipango kamili ya kisanyansi tunategemea uzoefu tu wa mpata mpatae hatuna orodha kamili ya wahitaji. Sisi tunaomba bila kujua nani na nani tunataka futari iwafikie, lakini Alhamdulilah hakututoa mikono mitupu nasi tukakabidhiwa futari. Misikiti yetu ipo jirani kwa hiyo futari ikishuka Msikiti wa Mwinyimkuu mara moja tushapata taarifa.  

Kifo cha Sheikh Manzi kimewasikitisha wengi khasa sisi tuliyekuwa tunaishi nae Magomeni. Sheikh Manzi amesimamia ujenzi wa msikiti wa Mwinyimkuu kwa mfanikio makubwa sana na kila ukienda kuswali pale utaona ubao wake ambao anaeleza mapato na matumizi na maendeleo ya ujenzi. Kwa kweli mtu unasikia raha. Unaona kazi inavyokwenda na jinsi msikiti unavyopendeza. Dar es Salaam imefiwa. Shughuli gani utamkosa Sheikh Manzi na akiombwa azungumze kila mtu atatoka pale si kama alivyokuja. Allah aiweke roho ya ndugu yetu mahali pema peponi. 

Amin.

Sheikh Manzi bin Said bin Manzi

Waliokaa wa Mwisho Kulia Sheikh Manzi Bin Said bin Manzi
Katika Maulid ya Mwinyimkuu 29 Mfungo Sita 1435
31 Januari 2014


Maulid Masjid Mwinyimkuu

No comments: