Wednesday, 25 March 2015

MCHANGO WA WAISLAM KATIKA MAENDELEO YA DUNIA - IBN BATTUTA



Mchango wa Waislamu Katika Maendeleo ya Dunia
Ibn Battuta
(2)
na Ben Rijal
Makala hii itamuangalia mweledi wa safari Ibn Battuta na mchango wake katika maendeleo ya Sayari yetu hii. Ninani Ibn Battuta? Jina hili katika uga wa elimu ya Jiografia lilihitajika lizungumzwe kwa mapana na marefu kwa nchi za Kiafrika na hata katika ulingo wa historia Ibn Battuta ana mchango wake alioutoa. Kinyume chake jina la Ibn Battuta linaonekana haliingii katika mizani kwasababu za wanalolikataa wanazijua wenywe, aidha kinachosikitisha nikuwa hata katika nchi za Kiislamu na za Kiarabu katika mitaala yao hawamzungumzi na wale wanaomzungumza hawamzungumzi anavyo stahiki.

Ibn Battuta jina lake khasa ni Abu Abdullah Muhammad Ibn Battuta mzaliwa wa Morocco alizaliwa tarehe 24 Februari mwaka wa 703 Hijria (1304 CE) wakati wa utawala uliokuwa ukijulikana kama Marinid, akifahamika zaidi kwa jina la Shams -ad-Din. Wazazi wake ni wakabila la Kiberber na walikuwa na utamaduni wa kabila hilo kufanya kazi za uhakimu. Baada ya kupata elimu nyumbani  kwao Morocco katika fani ya Sheria ya Kiislamu akaamua kuondoka na kuanza safari kiguu na njia ili kuweza kuujua ulimwengu, alianza safari zake hizo akiwa kijana mwenye umri wa miaka 21.

Safari yake ya mwanzo kutoka Morocco ilikuwa kuelekea Makka na kupata fursa ya kutimiza nguzo ya Hijja hata hivyo safari hio ilikuwa ni refu kwani  ilimchukua miezi 16 kutoka Morocco hadi Makka, baada ya kukamilisha Hijja akaamua kutorudi nyumbani na ilimchukua muda wa maiaka 24 kuizunguka sehemu ya dunia mpaka kurudi kwao Morocco. 

Baada ya kuondoka Makka alisafiri katika maeneo mbalimbali ikiwa baadhi ya nchi za Kaskazini mwa Afrika akaendelea na safari zake hadi Afrika ya Magaharibi, Kusini mwa Ulaya, Ulaya ya Mashariki kwa upande wa Magharibi, Mashariki ya Kati, sehemu za India, Kusini Mashariki ya Asia na China kwa upande wa Mashariki, safari zake hizo inaaminika kuwa hakuna kati ya watangulizi wake ambaye aliwahi kupita kote huko alikopita. Ibn Battuta alisafiri kukamilisha masafa zaidi ya maili 75,000 kumpita mvumbuzi Marco Polo. Baada ya kusafiri nchi zote hizo inaelezwa kuwa mwishoni alirudi nchini Morocco na kuyaelezea yale yote aliyoyaona na kuyashuhudia kwa Ibn Juzay.

Ibn Battuta aliweza kusafiri takribana katika nchi zote zile ambazo zikikaliwa na Waislamu kwa wingi katika wakati wake. Katika safari zake akipendelea zaidi kusafiri kwa kupitia njia za nchi kavu koliko njia za baharini kwa kuchelea kuhujumiwa na maharamia ambao walikuwa wakitamba katika maeneo ya baharini, alikuwa akipendelea kujiunga na misafara ya wafanya biashara.

Alipofika katika mji wa Sfax alipiga chuo na kubakia hapo kwa muda, katika mji huo wa Sfax aliponea chupuchupu kuweza kupoteza maisha yake pale jahazi alilosafiria kuzama na alipofanikiwa kufika nchi kavu ikawa ule msemo usemao kutoka kikangoni kuangukia motoni, alikuta mapambano yaliopamba moto vikiwa ni  vita vya wenyewe kwa wenyewe alifanikiwa kuokoka.


http://i5.photobucket.com/albums/y186/secretdubai/ibnbattuta_head.jpg
Mvumbuzi wa nchi mbalimbali Ibn Battuta
Baada ya kukaa Sfax kwa muda aliendelea na safari zake kuujuwa ulimwengu, safari hii  alifanikiwa kuwasili katika maeneo ya Mashariki ya kati, akateremkia Bahari Nyekundu (Red sea) kupitia mji mtakatifu wa Makka, kisha akalivuka jangwa la Uarabuni na kuendelea na safari zake zilizomfikisha nchi za Iran na Iraq.

Ulipofika mwaka wa 1330 akapita kwa mara nyengine tena katika Bahari Nyekundu hadi kufika visiwa vya Zanzibar ambapo katika maandishi yake alielezea kuwa alikutana na watu wa kisiwa hicho wakiwa ni Waislamu watu walio wakarimu na akazungumza nao kwa Kiarabu akasali nao, aidha aliyasifu maji ya hapo kwa utamu wake. Kutoka Unguja akaelekea Kilwa nako huko hakupata tabu kuwasiliana na watu wa Kilwa, aliwasiliana nao kwa lugha ya Kiarabu na alivutiwa kukuta kuwa watu wake wana ustaarabu na wanaishi katika nyumba za mbao zilizoezekwa  mapaa yake kwa makuti. Alibahatika kukutana na Mtawala wa Kilwa  Sultan al-Hasan ibn Sulaiman akiwa ni katika kizazi cha Ali ibn al-Hassan Shirazi, alivutiwa na mpango wa majenzi ya Kilwa yalivyokuwa ya kimpangilio na kuelezea kama ni mji uliokuwa na maendeleo. Aliuelezea Msikiti Mkuu wa Kilwa, Msikiti uliokuwa mkubwa wenye kuvutia uliojengwa kwa mawe ya matumbawe.

Ulipofika mwaka wa 1332 aliendelea na safari zake kuelekea India ambapo ilimchukua miaka 8 kuweza kufika huko India bada ya kutoka maeneo ya Afrika ya Mashariki. India alipokelewa kwa mikono miwili na Sultan wa India, baada ya kustakimu hapo kwa muda akamua  kuendelea na safari zake zilizoweza kumfikisha China, katika mwaka wa 1352 mshipa wa kurudi nyumbani ulimpiga akarudia hata katika maeneo ya Bahari Nyekundu na kuelekea Magharibi ya Afrika katika nchi ya Mali  nchi ambayo ina urithi mkubwa wa utamaduni wa Kiislamu, alikaa katika mji wa Timbuktu akaitumia maktaba kubwa ya Timbuktu kujiongezea taaluma. Mji wa Timbuktu unaringia kazi kubwa iliofanywa na Mfalme Mansa Mussa ambaye ndio aliowapeleka walimu kutoka Misri kwenda kusomesha watu dini na kuandika vitabu mbalimbali. (Mansa Mussa ana makala zake 2 siku za mbele nitamuelezea).
 
Ramani inayoonyesha njia alizopita Ibn Battuta
Anapozungumzwa Ibn Battuta huzungumzwa zaidi juu ya safari zake bila ya kutajwa utaalamu wa masuala ya kidunia. Mbali ya taaluma ya Jiografia alikuwa mtaalamu wa fani ya Sayansi ya mimea (Botany) aidha alibobea katika elimu ya Sayansi ya jamii. Tunafaidika pakubwa na kazi za Ibn Battuta kutokana na maandishi yake mengi aliyoyaandika. Fani ya uandishi kwa wasomi wa Kislamu imepotea, waliopita waliandika sana na maandishi yao yalitoa mchango mkubwa katika maendeleo ya sayari yetu hii.

Maandishi ya Ibn Battuta

Maandishi yake
Baadhi ya maandishi yake unapoyasoma unapata ladha namna alivyokuwa anazielezea jamii za Kiislamu zilivyokuwa zinaishi na ustaarabu waliokuwa nao, nitadokowa mawili matatu juu ya hayo.

Alipokuwa nchini Syria aliona mambo yaliomvutia kabisa, Syria iliojaa utamaduni na huruma, Syria yaleo inavurugwa na kupotezewa alama zote za athari za Kiislamu, Ibn Battuta aliandika yafawtayo: “Utapojumlisha matumizi ambayo serikali katika nchi ya Syria yakifanyika katika karne ya 14 yalikuwa hayana kifani. Kukitengwa fungu la kuwasaidia wale wote wasiokuwa na uwezo wa kwenda Kuhiji Makka sio tu kusaidiwa kufika huko bali na matumizi yao ya kula na mambo madogo madogo, aidha wakisaidiwa wale ambao hawana pesa za mahari ya kuolea, aidha  kukitengwa fedha za kuwapa familia ya bibi harusi waliokuwa wanyonge hawana vitu vya kumpa bi harusi, vilevile  kukitengwa fedha kuwasaidia wasafari walioishiwa kwa kuwasaidia chakula na nguo na usafiri wakuwafikisha makwao. Kulikuwa na fungu la kuwaweka huru wafungwa na kuwasaidia maisha yao bada yakutoka gerezani, aidha kukitengwa fungu la kuweka taa za barabarani na kuimarisha njia ya wapitao kwa miguu na vipando.”

Alipofika Iraq aliandika haya: Kisha tukawasili Baghdad mji mkuu wa Iraq ikiwa ni mwahali paliokua na amani  mji kati ya miji ya Kiislamu. Tulizikabili daraja mbili kama Hilla, ikiwa daraja hizo watu wanazipita usiku na mchana, kike kwa kiume. Sehemu za kukogea zilijaa watu pomoni, sehemu hizo zilijengwa kwa kiufundi kabisa na kupakwa rangi za kupendeza na kuta zake zikiwa za mramar nyeusi. Maeneo hayo yakukogea yalikuwa yanamaji ambayo yakitokea Kufa na Basra saa zote na siku zote maji hayo yakiwa yakitiririka. Sehemu hizo za  kukogea zilikuwa zikimilikiwa na watu binafsi, unapokwenda kukoga unapewa taula za kujifutia maji tatu, mmoja ikiwa ya kujifunga kiunoni unapoingia kukoga na nyengine ya kujifutia maji na nyengine kuvaa kiunoni unapotoka kukoga.”

Vilevile aliandika mambo aliyoyayaona Uturuki, Mongolia na visiwa vya Maldives. Aliyoyaona Uturuki na Mongolia yalimsataajabisha kuona jamii ya watu wa hapo  kuwapa uhuru ulio mkubwa wanawake, aidha kilichomvutia katika kisiwa cha Maldives ni kuona wanawake vivazi vyao ni nguo za ming’aro.

Baada ya safari zake za miaka mingi kwa kipindi cha miaka 24 kuwa nje ya nyumbani mshipa wa kurudi nyumbani ulianza kumpiga na ulipofika mwaka wa 1355 aliwasili Morocco  katika mji wa Tangier sehemu ambayo ndio alipofia na kuzikwa katika mwaka wa 1368 na kaburi lake limewekwa kuwa alama ya mvumbuzi huyu na wengi hulizuru kama tunavyotakiwa kuzuru waliokufa na kuomba dua.

Wataalamu wa Kimagharibi hawaamini kuwa Ibn Battuta alifanya safari hizi bali wakionacho nikuwa alinukuu kazi za watu wengine, hio yote ni kuwa kila kinachohusiana na taaluma na maendeleo ni cha mzungu, hutajwa mvumbuzi Vasco Dagama bila ya kudhukuriwa Tiro aliokuwa mjuzi wa kuongoza safari za baharini, Tiro alikuwa mtu mweusi.

Eneo aliozikwa Ibn Battuta sehemu ya Tangier
 Makala ijayo tutamuelezea Ibn Rushd na mchango wake katika maendeleo ya Sayari yetu hii.


No comments: